Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Mufano wa Talanta Unatufundisha Nini?

Mufano wa Talanta Unatufundisha Nini?

‘Akamupa mumoja talanta tano, mwingine mbili, na mwingine moja.’MT. 25:15.

1, 2. Sababu gani Yesu alitoa mufano wa talanta?

KATIKA mufano wa talanta, Yesu anaonyesha wazi daraka la wafuasi wake watiwa-mafuta. Ni lazima tuelewe maana ya mufano huo kwa sababu unawahusu Wakristo wote wa kweli, iwe wataenda mbinguni ao wataishi hapa duniani.

2 Yesu alitoa mufano wa talanta katika jibu lenye alipatia wanafunzi wake kuhusu ‘ishara [alama] ya kuwapo kwake na ya umalizio wa mufumo wa mambo.’ (Mt. 24:3) Kwa hiyo, mufano wa Yesu unatimia katika siku zetu na ni sehemu ya alama yenye kuonyesha kuwapo kwa Yesu katika mamlaka ya Ufalme.

3. Ni mambo gani inakaziwa katika mifano yenye kuzungumuziwa katika Mathayo sura ya 24 na 25?

3 Mufano wa talanta, ni moja kati mifano ine yenye Yesu alizungumuzia katika Mathayo 24:45 mupaka 25:46. Yesu alizungumuzia mufano wa mutumwa mwaminifu na mwenye busara, mufano wa mabikira kumi, na mufano wa kondoo na mbuzi. Yesu alitoa pia mifano hiyo tatu katika jibu lenye aliwapatia wanafunzi wake juu ya ulizo lenye kuhusu alama ya kuwapo kwake. Katika mifano yote ine, Yesu alikazia alama zenye zingewatambulisha wafuasi wake wa kweli katika siku hizi za mwisho. Yesu alitoa mufano wa mutumwa mwaminifu, mabikira, na talanta ili kuzungumuzia wafuasi wake watiwa-mafuta. Katika mufano wake wa mutumwa mwaminifu, Yesu anakazia kwamba kikundi kidogo cha Wakristo watiwa-mafuta wenye wamepewa kazi ya kulisha watumishi wake wa nyumbani katika siku za mwisho, wanapaswa kuonyesha uaminifu na busara. Katika mufano wa mabikira, Yesu anakazia kwamba wafuasi wake wote watiwa-mafuta wanapaswa kuwa tayari na wenye kukesha, kwa sababu hawajue siku wala saa ya kuja kwake. Katika mufano wa talanta, Yesu anaonyesha kwamba watiwa-mafuta wanapaswa kutimiza madaraka yao ya Kikristo kwa bidii. Yesu anatoa mufano wa mwisho, ni kusema, mufano wa kondoo na mbuzi kwa ajili ya wale wenye kuwa na tumaini la kuishi hapa duniani. Katika mufano huo, Yesu anakazia kwamba wanapaswa kuwa waaminifu na kutegemeza kabisa ndugu zake watiwa-mafuta. * Tuzungumuzie sasa mufano wa talanta.

BWANA ANAWAPATIA WATUMWA WAKE FEZA NYINGI SANA

4, 5. Mwanaume, ao bwana huyo, anafananisha nani, na iliomba mutu akuwe na dinari ngapi ili apate talanta moja?

4 Soma Mathayo 25:14-30. Tangu zamani, vichapo vyetu vimekuwa vikifasiria kwamba mwanaume huyo, ao bwana mwenye kuzungumuziwa katika mufano huo ni Yesu na kwamba alisafiri kwenda ngambo (ao inchi ingine) wakati alienda mbinguni katika mwaka wa 33. Mbele atoe mufano huo, Yesu alikuwa ametoa mufano mwengine wenye kuonyesha kusudi la safari hiyo. Alisema kwamba bwana huyo alisafiri ili “ajipatie mamlaka ya kifalme kwa ajili yake mwenyewe.” (Lu. 19:12) Wakati Yesu alienda mbinguni, hakupewa mamlaka ya Kifalme mara moja. * Lakini, ‘alikaa kwenye mukono wa kuume wa Mungu, tangu wakati huo na kuendelea akingojea mupaka adui zake wawekwe kuwa kiti cha miguu yake.’—Ebr. 10:12, 13.

5 Mwanaume mwenye kuzungumuziwa katika mufano huo, alikuwa na talanta munane; hizo zilikuwa feza nyingi sana wakati huo. * Mbele ya kusafiri katika inchi ingine, aliwapatia watumwa wake talanta. Alipenda watumwa hao watumikishe talanta hizo ili kufanya biashara wakati yeye atakuwa amesafiri. Kama mwanaume huyo, Yesu alikuwa na kitu cha bei kubwa sana mbele aende mbinguni. Ni kitu gani hicho? Ni kazi yenye alikuwa anafanya wakati alikuwa hapa duniani.

6, 7. Talanta zinafananisha nini?

6 Yesu aliona kazi yake ya kuhubiri na kufundisha kuwa ya lazima sana. (Soma Luka 4:43.) Kupitia kazi hiyo, alilima shamba lenye lingezaa matunda mengi sana. Ndiyo sababu aliwaambia wanafunzi wake hivi: ‘Muinue macho yenu mutazame mashamba, kwamba ni meupe kwa ajili ya kuvunwa.’ (Yoh. 4:35-38) Alikuwa anafikiria kazi ya kukusanya watu wengine wengi wenye kustahili ambao wangekuwa wanafunzi wake. Kama vile mulimaji muzuri, Yesu hangeachilia shamba lenye lilikuwa tayari kwa ajili ya kuvunwa. Kwa hiyo, muda mufupi kisha kufufuliwa kwake na mbele aende mbinguni, Yesu aliwapatia wanafunzi wake kazi kubwa. Aliwaambia hivi: ‘Kwa hiyo muende mufanye wanafunzi.’ (Mt. 28:18-20) Wakati aliwaambia maneno hayo, Yesu aliwapatia wanafunzi wake hazina yenye bei kubwa sana, ni kusema, kazi ya kuhubiri.—2 Kor. 4:7.

7 Kwa hiyo, tuseme nini basi? Wakati Yesu aliwapatia wafuasi wake kazi ya kufanya wanafunzi, ni kama vile ‘aliwapatia mali zake,’ ni kusema, talanta zake. (Mt. 25:14) Kwa kifupi, tunaweza kusema kwamba talanta hizo ni kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi.

8. Hata kama watumwa wote hawakupewa hesabu ileile ya talanta, bwana wao alipenda wafanye nini?

8 Mufano wa talanta unaonyesha kwamba bwana huyo alipatia mutumwa mumoja talanta tano, mwengine talanta mbili, na wa mwisho talanta moja tu. (Mt. 25:15) Hata kama watumwa hao hawakupewa hesabu ileile ya talanta, bwana wao alipenda wote watumikishe talanta hizo kwa bidii, ni kusema, wafanye kazi ya kuhubiri kulingana na uwezo wao wote. (Mt. 22:37; Kol. 3:23) Wakati wa mitume, wafuasi wa Kristo walianza kutumikisha talanta hizo ili kufanya biashara tangu Pentekoste ya mwaka 33. Bidii na kazi yao ya kufanya wanafunzi inazungumuziwa katika kitabu cha Biblia cha Matendo ya Mitume. *Mdo. 6:7; 12:24; 19:20.

WANATUMIKISHA TALANTA KATIKA SIKU ZA MWISHO

9. (a) Watumwa waaminifu walifanya nini na talanta zenye walipewa, na hilo linaonyesha nini? (b) “Kondoo wengine” wanafanya kazi gani?

9 Katika siku za mwisho, zaidi sana kuanzia mwaka wa 1919 na kuendelea, watumwa watiwa-mafuta waaminifu wa Kristo wenye kuwa hapa duniani, wameendelea kutumikisha talanta za Bwana wao. Kama vile wale watumwa wawili wa kwanza, ndugu na dada watiwa-mafuta wamefanya kazi yao kulingana na uwezo wao wote. Hakuna lazima ya kuwazia-wazia ni nani kati yao walipewa talanta tano na nani walipewa talanta mbili. Katika mufano wa Yesu, watumwa wote wawili walizidisha mara mbili talanta zenye bwana wao aliwapatia. Kwa hiyo, wote wawili walitumika kwa bidii. Wakristo wenye kuwa na tumaini la kuishi hapa duniani, wao pia, wanahusika katika kazi hiyo? Ndiyo! Yesu anaonyesha katika mufano wake wa kondoo na mbuzi kwamba, wale wenye kuwa na tumaini la kuishi duniani wako na pendeleo la kutegemeza kwa uaminifu ndugu watiwa-mafuta wa Kristo katika kazi ya kuhubiri na kufundisha. Katika siku hizi za mwisho zenye kuwa hatari, vikundi vyote viwili vinatumika pamoja kama “kundi moja” kwa kufanya kwa bidii kazi ya kufanya wanafunzi.—Yoh. 10:16.

10. Ni sehemu gani ya maana sana ya alama yenye kuonyesha kwamba Yesu ni Mufalme mwenye kutawala?

10 Bwana anatazamia kupata faida. Kama vile tumezungumuzia katika habari hii, wanafunzi waaminifu wa wakati wa mitume, waliongeza mali ya Bwana. Tuseme nini sasa kuhusu wakati huu wa mwisho, wakati ambao mufano wa Yesu juu ya talanta unatimia? Katika historia ya wanadamu, watumishi waaminifu na wenye bidii wa Yesu wametimiza sana kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi. Vikundi hivyo viwili vimetumika pamoja kwa bidii, na maelfu ya wanafunzi wapya wanajiunga na wahubiri wa Ufalme kila mwaka. Kwa hiyo, kazi ya kuhubiri imekuwa sehemu ya maana sana ya alama yenye kuonyesha kwamba Yesu ni Mufalme mwenye kutawala. Bila shaka, Bwana wao anafurahia sana kazi yao!

Kristo aliwapatia watumishi wake kitu cha bei, ni kusema, kazi ya kuhubiri(Ona fungu la 10)

BWANA ATAKUJA KUFANYA HESABU WAKATI GANI?

11. Sababu gani tunasema kwamba Yesu atakuja kufanya hesabu wakati wa ziki kubwa?

11 Yesu atakuja kufanya hesabu pamoja na watumwa wake mbele ziki kubwa imalizike. Sababu gani tunasema hivyo? Katika unabii wenye kuzungumuziwa katika Mathayo sura ya 24 na 25, Yesu alitumia kila mara neno kuja ao kufika kwake. Wakati alizungumuzia hukumu yenye itafanyika wakati wa ziki kubwa, Yesu alisema kwamba watu ‘watamuona Mwana wa binadamu akija juu ya mawingu ya mbinguni.’ Alishauria wafuasi wake wenye kuishi katika siku za mwisho kwamba wanapaswa kukesha. Alisema hivi: ‘Hamujue ni siku gani Bwana yenu atakuja’ na ‘Mwana wa binadamu atakuja katika saa musiyofikiria.’ (Mt. 24:30, 42, 44) Kwa hiyo, wakati Yesu alisema kwamba “bwana wa watumwa hao alikuja na kufanya hesabu,” alikuwa anafikiria wakati atakuja kuleta hukumu juu ya ulimwengu huu wa Shetani. *Mt. 25:19.

12, 13. (a) Bwana anawaambia nini wale watumwa wawili wa kwanza, na sababu gani? (b) Wakristo watiwa-mafuta watatiwa muhuri kwa mara ya mwisho wakati gani? (Ona kisanduku “ Wanatoa Hesabu Wakati wa Kifo.”) (c) Wale wenye wataonwa kuwa kondoo watapewa pendeleo gani?

12 Katika mufano huo, wakati bwana anakuja, anakuta wale watumwa wawili wa kwanza wamezidisha mara mbili talanta zao. Kwa hiyo, walikuwa waaminifu. Bwana huyo anawaambia watumwa wote wawili maneno haya: ‘Vema, mutumwa mwema na mwaminifu! Ulikuwa mwaminifu juu ya mambo machache. Nitakuweka juu ya mambo mengi.’ (Mt. 25:21, 23) Bwana, Yesu mwenye utukufu, atafanya nini wakati atakuja kuleta hukumu?

13 Wale wenye kufananishwa na watumwa wawili wa kwanza, ni kusema, wanafunzi watiwa-mafuta wenye bidii, watakuwa wametiwa muhuri kwa mara ya mwisho mbele ziki kubwa ianze. (Ufu. 7:1-3) Mbele vita ya Har-magedoni ianze, Yesu atawapatia zawadi yao ya kuenda mbinguni. Wale wenye kuwa na tumaini la kuishi duniani na ambao walitegemeza ndugu za Kristo katika kazi ya kuhubiri, wataonwa kuwa kondoo na watapewa pendeleo la kuishi katika dunia yenye kutawaliwa na Ufalme wa Mungu.—Mt. 25:34.

MUTUMWA MUOVU NA GOIGOI

14, 15. Yesu alimaanisha kwamba ndugu zake wengi watiwa-mafuta watakuwa waovu na wavivu? Fasiria.

14 Katika mufano wa talanta, mutumwa wa mwisho alizika talanta yenye alipewa, kuliko kuitumikisha ao kuitia kwa watunza-hazina. Mutumwa huyo, alionyesha roho mubaya, kwa sababu alikataa kimakusudi kufanya sawasawa na vile bwana wake alipenda. Bwana wake alikuwa na sababu ya kumuita ‘mutumwa muovu na goigoi [muvivu].’ Alimunyanganya talanta hiyo na kuipatia ule mwenye alikuwa na talanta kumi. Kisha, mutumwa huyo muovu alitupwa ‘inje katika giza.’ Na ‘huko ndiko angelia na kusaga meno yake.’—Mt. 25:24-30; Lu. 19:22, 23.

15 Mutumwa mumoja kati ya watumwa hao watatu alificha talanta yenye alipewa; je, Yesu alikuwa anamaanisha kwamba sehemu fulani ya wafuasi wake watiwa-mafuta watakuwa waovu na wavivu? Hapana. Tufikirie mifano mbili yenye tumezungumuzia. Katika mufano wa mutumwa mwaminifu na mwenye busara, Yesu alizungumuzia mutumwa muovu mwenye anapiga watumwa wenzake. Yesu hakumaanisha kwamba kungetokea kikundi cha mutumwa muovu. Lakini, alikuwa anamuonya mutumwa mwaminifu asigeuke na kuwa mutumwa muovu. Vilevile, katika mufano wa mabikira kumi, Yesu hakumaanisha kwamba nusu ya wafuasi wake watiwa-mafuta watakuwa kama wale mabikira wapumbavu. Lakini, alikuwa anawaonya ndugu zake wa kiroho juu ya mambo yenye ingewapata ikiwa hawangeendelea kukesha na kuwa tayari. * Kwa hiyo, tunaweza kusema kwamba katika mufano wa talanta, Yesu hakumaanisha kwamba ndugu zake wengi watiwa-mafuta watakuwa waovu na wavivu katika siku za mwisho. Lakini, Yesu alikuwa anaonya wafuasi wake watiwa-mafuta waendelee kuwa na bidii, ni kusema, “kufanya biashara” na talanta zenye wamepewa, na waepuke kuwa kama mutumwa muovu.—Mt. 25:16.

16. (a) Tumejifunza mambo gani katika mufano wa talanta? (b) Habari hii imetutolea mafasirio gani mapya kuhusu mufano wa talanta? (Ona kisanduku “ Tuelewe Mufano wa Talanta.”)

16 Tunajifunza mambo gani mawili katika mufano wa talanta? Jambo la kwanza, Bwana aliwapatia watumwa wake watiwa-mafuta kitu fulani chenye bei kubwa, ni kusema, kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi. Jambo la pili, Kristo anatazamia kila mumoja wetu afanye kazi ya kuhubiri kwa bidii. Tunaweza kuwa hakika kwamba ikiwa tunafanya hivyo, Bwana atatubariki kwa sababu tumeonyesha imani, tumekesha, na tumebaki waaminifu.—Mt. 25:21, 23, 34.

^ fu. 3 Munara wa Mulinzi wa tarehe 15 Mwezi wa 7, 2013, ukurasa wa 21-22, fungu la 8-10, unaonyesha ni nani ndiye mutumwa mwaminifu na mwenye busara. Katika gazeti hili, habari yenye ilitangulia ilifasiria ni nani ndio mabikira. Mufano wa kondoo na mbuzi unazungumuziwa katika Munara wa Mulinzi wa tarehe 15 Mwezi wa 10, 1995, ukurasa wa 23-28 na katika gazeti hili katika habari yenye kufuata.

^ fu. 5 Katika siku za Yesu, iliomba mutu akuwe na dinari 6000 hivi ili apate talanta moja. Ili kupata talanta moja, mufanyakazi wa kawaida mwenye alikuwa anapokea dinari moja kwa siku, alipaswa kutumika miaka 20.

^ fu. 8 Kisha kifo cha mitume, Shetani alianzisha uasi-imani, na uasi-imani huo, uliendelea kwa muda wa miaka mingi. Katika kipindi hicho, kazi ya kufanya wanafunzi wa kweli wa Kristo ilifanyika kwa kiasi kidogo sana. Lakini mambo ingebadilika katika kipindi cha “mavuno,” ni kusema, katika siku za mwisho. (Mt. 13:24-30, 36-43) Ona Munara wa Mulinzi wa tarehe 15 Mwezi wa 7, 2013, ukurasa wa 9-12.

^ fu. 11 Ona Munara wa Mulinzi wa tarehe 15 Mwezi wa 7, 2013, ukurasa wa 7-8, fungu la 14-18.

^ fu. 15 Ona fungu la 13 la habari yenye kichwa “Utaendelea Kukesha”? katika gazeti hili.