Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuwaunga Mkono kwa Ushikamanifu Ndugu za Kristo

Kuwaunga Mkono kwa Ushikamanifu Ndugu za Kristo

“Kwa kadiri ambayo mlimtendea hilo mmoja wa walio wadogo zaidi wa ndugu zangu hawa, mlinitendea mimi.”—MT. 25:40.

1, 2. (a) Yesu aliwasimulia rafiki zake mifano gani? (Tazama picha kwenye ukurasa huu.) (b) Tunahitaji kujua nini kuhusu mfano wa kondoo na mbuzi?

YESU amekuwa akizungumza na rafiki zake wa karibu Petro, Andrea, Yakobo, na Yohana. Amewasimulia mfano wa mtumwa mwaminifu na mwenye busara, mfano wa mabikira kumi, na mfano wa talanta. Yesu anamalizia mazungumzo yake kwa kuwasimulia mfano mwingine. Anaeleza kuhusu wakati ambapo “Mwana wa binadamu” atahukumu “mataifa yote.” Bila shaka, mfano huo uliwavutia sana wanafunzi wake! Katika mfano huo, Yesu anakazia fikira vikundi viwili, kimoja kinafananishwa na kondoo na kingine kinafananishwa na mbuzi. Naye anataja kikundi cha tatu muhimu anachokiita “ndugu” za “mfalme.”—Soma Mathayo 25:31-46.

2 Kwa muda mrefu watu wa Yehova wamependezwa na mfano huo kwa sababu Yesu anaonyesha kwamba uhai wa watu unahusika. Anafunua kwa nini baadhi yao watapokea uzima wa milele na wengine kuangamizwa milele. Uhai wetu unategemea kuelewa na kutenda kupatana na kweli ambazo Yesu alifundisha. Kwa kuwa mengi yanahusika, tunapaswa kujiuliza hivi: Yehova ameboreshaje hatua kwa hatua uelewaji wetu kuhusu mfano huo? Kwa nini tunaweza kusema kwamba mfano huo unakazia umuhimu wa kazi ya kuhubiri? Ni nani anayekabidhiwa kazi ya kuhubiri? Na kwa nini huu ndio wakati wa kuwa washikamanifu kwa “mfalme,” na kwa wale ambao Yesu anawaita ‘ndugu zake’?

UELEWAJI WETU UMEBORESHWAJE?

3, 4. (a) Ni lazima tujue mambo gani muhimu ili tuelewe mfano wa kondoo na mbuzi? (b) Katika mwaka wa 1881, gazeti la Zion’s Watch Tower lilifafanuaje mfano huo?

3 Ili kuelewa vizuri mfano wa kondoo na mbuzi, tunahitaji kujua mambo matatu muhimu katika mfano huo: utambulisho wa watu wanaotajwa, wakati wa hukumu, na sababu ya watu kuhesabiwa kuwa kondoo au mbuzi.

4 Katika mwaka wa 1881, gazeti la Zion’s Watch Tower lilimtambulisha Yesu kuwa “Mwana wa binadamu,” ambaye pia anaitwa “Mfalme.” Wanafunzi wa awali wa Biblia walielewa kwamba maneno “ndugu zangu” yanawahusu wale watakaotawala na Kristo, na pia wanadamu wote baada ya kurudishwa kwenye ukamilifu duniani. Walifikiri kwamba kondoo watatenganishwa na mbuzi wakati wa ile Miaka Elfu Moja ya Utawala wa Kristo. Na waliamini kwamba watu watahesabiwa kuwa kondoo kwa sababu waliishi kupatana na sheria ya Mungu ya upendo.

5. Uelewaji wetu uliboreshwaje katika miaka ya 1920?

5 Mwanzoni mwa miaka ya 1920, Yehova aliwasaidia watu wake kuboresha uelewaji wao kuhusu mfano huo. Gazeti Mnara wa Mlinzi la Oktoba 15, 1923, lilithibitisha kwamba Yesu ndiye “Mwana wa binadamu.” Hata hivyo, gazeti hilo lilitaja sababu za Kimaandiko ambazo ziliwatambulisha ndugu za Kristo kuwa ni wale tu ambao wangetawala naye mbinguni, na pia lilisema kwamba kondoo ni wale wanaotumaini kuishi duniani chini ya utawala wa Ufalme wa Kristo. Vipi kuhusu wakati wa kutenganisha kondoo na mbuzi? Kulingana na makala hiyo, wale walio na tumaini la kuishi duniani hawangeweza kuwasaidia au kuwapuuza ndugu za Kristo wakati wa Utawala wake wa Miaka Elfu Moja, kwa sababu ndugu za Kristo wangekuwa mbinguni wakitawala naye wakati huo. Kwa hiyo, kondoo wangetenganishwa na mbuzi kabla ya Utawala wa Kristo wa Miaka Elfu Moja. Makala hiyo ilisema kwamba sababu ya watu kuhesabiwa kuwa kondoo ni kukiri kwamba Yesu ni Bwana, na kutumaini kwamba Ufalme utaleta hali bora.

6. Maoni yetu yaliboreshwaje katika miaka ya 1990?

6 Kwa sababu ya uelewaji huo uliorekebishwa, watumishi wa Yehova walifikiri kwamba watu walikuwa wakihukumiwa kuwa mbuzi au kondoo katika kipindi chote cha umalizio wa mfumo wa mambo, ikitegemea jinsi wanavyoitikia ujumbe wa Ufalme. Hata hivyo, katikati ya miaka ya 1990, maoni yetu yaliboreshwa. Makala mbili za gazeti Mnara wa Mlinzi la Oktoba 15, 1995, zililinganisha maneno ya Yesu katika Mathayo 24:29-31 (soma) na yale yaliyo kwenye Mathayo 25:31, 32. (Soma.) * Makala hizo zilifikia mkataa gani? Makala ya kwanza ilisema hivi: “Kutoa hukumu juu ya kondoo na mbuzi ni kwa wakati ujao.” Wakati gani hasa? Kutenganishwa huko “kutatokea baada ya ‘dhiki’ inayotajwa katika Mathayo 24:29, 30 kufyatuka na Mwana wa binadamu ‘kufika katika utukufu wake.’ . . . Ndipo, mfumo huu wote ukiwa umefikia mwisho wao, Yesu atafanya mahakama na kutoa na kutekeleza hukumu.”

7. Leo tunaelewa vizuri mfano gani?

7 Leo, tunaelewa vizuri maana ya mfano wa kondoo na mbuzi. Kuhusu utambulisho wa wale wanaotajwa katika mfano huo, tunajua kwamba Yesu ndiye “Mwana wa binadamu,” au Mfalme. Wale anaowaita “ndugu zangu” ni wanaume na wanawake watiwa-mafuta watakaotawala na Kristo mbinguni. (Rom. 8:16, 17) “Kondoo” na “mbuzi” wanafananisha watu wa mataifa yote. Watu hao hawajatiwa mafuta kwa roho takatifu. Namna gani kuhusu wakati wa hukumu? Hukumu hiyo itatekelezwa kabla tu ya kumalizika kwa dhiki kuu itakayoanza hivi karibuni. Na watu watahukumiwa kuwa kondoo au mbuzi kwa sababu gani? Matokeo yanategemea jinsi ambavyo wamewatendea ndugu watiwa-mafuta wa Kristo walio duniani. Kwa kuwa mwisho wa mfumo huu unakaribia sana, tunamshukuru Yehova kwa kuangaza hatua kwa hatua nuru kuhusu mfano huo na mifano mingine inayotajwa katika Mathayo sura ya 24 na 25.

MFANO HUO UNAKAZIAJE UMUHIMU WA KAZI YA KUHUBIRI?

8, 9. Kwa nini kondoo wanaitwa “waadilifu”?

8 Katika mfano wa kondoo na mbuzi, Yesu hataji moja kwa moja kazi ya kuhubiri. Basi kwa nini tunaweza kusema kwamba mfano huo unakazia umuhimu wa kuhubiri?

9 Kwanza, kumbuka kwamba Yesu anatumia mfano kufundisha. Bila shaka, hazungumzii kutenganishwa kwa kondoo na mbuzi halisi. Vivyo hivyo, hamaanishi kwamba kila mtu anayeonwa kuwa kondoo ni lazima amlishe, amvishe, amtunze, au kumtembelea kihalisi gerezani mmoja wa ndugu za Yesu. Badala yake, anatumia mfano kueleza mtazamo wa watu walio kama kondoo kuelekea ndugu zake. Anawaita “waadilifu” kwa sababu wanatambua kwamba Kristo ana kikundi cha ndugu watiwa-mafuta ambao wako duniani, na kondoo hao huwaunga mkono kwa ushikamanifu watiwa-mafuta katika siku hizi za mwisho ambazo ni hatari.—Mt. 10:40-42; 25:40, 46; 2 Tim. 3:1-5.

10. Kondoo wanaweza kuwaonyeshaje fadhili ndugu za Kristo?

10 Pili, fikiria muktadha wa maneno ya Yesu. Anazungumzia ishara ya kuwapo kwake na ya umalizio wa mfumo wa mambo. (Mt. 24:3) Mwanzoni mwa mazungumzo yake, Yesu alionyesha kuwa ishara hiyo ingetia ndani kazi ya pekee sana. Alisema kwamba habari njema ya Ufalme “itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa.” (Mt. 24:14) Kabla tu ya kuzungumza kuhusu kondoo na mbuzi, alisimulia mfano wa talanta. Kama ilivyoelezwa katika makala iliyotangulia, Yesu alitumia mfano huo kukazia kwamba lazima wanafunzi wake waliotiwa mafuta kwa roho, yaani, “ndugu” zake, wahubiri kwa bidii. Hata hivyo, idadi ndogo ya watiwa-mafuta ambao wangali duniani wakati wa kuwapo kwa Yesu wana kazi kubwa sana ya kuhubiri “kwa mataifa yote” kabla ya mwisho kuja. Mfano wa kondoo na mbuzi unaonyesha kwamba watiwa-mafuta wangesaidiwa kuhubiri. Kwa hiyo, njia moja ya msingi ambayo wale wanaoonwa kuwa kondoo wanawaonyesha fadhili ndugu za Kristo ni kuwaunga mkono katika kazi ya kuhubiri. Hata hivyo, kuwaunga mkono kunahusisha nini? Je, kunahusisha tu kuwasaidia kifedha na kuwatia moyo, au mengi zaidi yanahusika?

NI NANI WANAOPASWA KUHUBIRI?

11. Huenda watu fulani wakauliza swali gani, na kwa nini?

11 Leo, idadi kubwa sana kati ya wanafunzi milioni nane wa Yesu hawajatiwa mafuta kwa roho. Hawajapokea talanta ambazo Yesu aliwapa watumwa wake watiwa-mafuta. (Mt. 25:14-18) Kwa hiyo, huenda watu fulani wakauliza: ‘Je, kweli kazi ya kuhubiri inawahusu wale ambao hawajatiwa mafuta kwa roho takatifu?’ Ndiyo. Acheni tuone kwa nini tunasema hivyo.

12. Tunajifunza nini kutokana na maneno ya Yesu katika Mathayo 28:19, 20?

12 Yesu aliwaagiza wanafunzi wake wote wahubiri. Baada ya kufufuliwa, Yesu aliwaambia wafuasi wake wafanye wanafunzi na kuwafundisha kushika “mambo yote” ambayo aliwaamuru. Kazi ya kuhubiri ilikuwa miongoni mwa mambo aliyowaamuru. (Soma Mathayo 28:19, 20.) Kwa hiyo, wanafunzi wote wa Kristo wanapaswa kuhubiri, iwe wana tumaini la kutawala mbinguni au kuishi duniani.—Mdo. 10:42.

13. Maono ya Yohana yanaonyesha nini, na kwa nini?

13 Kitabu cha Ufunuo kinaonyesha kwamba kazi ya kuhubiri ingefanywa na watiwa-mafuta na watu wengine. Yesu alimwonyesha mtume Yohana maono ya “bibi-arusi,” yaani, wanadamu 144,000 waliotiwa mafuta ambao watatawala na Kristo mbinguni, wakiwaalika watu ‘wachukue maji ya uzima bure.’ (Ufu. 14:1, 3; 22:17) Maji hayo ya mfano yanafananisha maandalizi ya Yehova ya kuwaokoa wanadamu kutoka katika dhambi na kifo kwa msingi wa dhabihu ya fidia ya Kristo. (Mt. 20:28; Yoh. 3:16; 1 Yoh. 4:9, 10) Fidia ni sehemu muhimu sana ya ujumbe tunaohubiri, na watiwa-mafuta wanaongoza katika kuwasaidia watu wajifunze na kunufaishwa na fidia. (1 Kor. 1:23) Lakini katika maono, Yohana anaona watu wengine ambao si wa jamii ya bibi-arusi. Wao pia wanaambiwa waseme, “Njoo!” Wanatii na kuwaalika wengine wachukue maji ya uzima. Kikundi hicho cha pili ni wale wenye tumaini la kuishi duniani. Kwa hiyo, maono hayo yanaonyesha wazi kwamba wote wanaokubali mwaliko huo, wana wajibu wa kuwahubiria wengine.

14. Kutii “sheria ya Kristo” kunahusisha nini?

14 Wote walio chini ya “sheria ya Kristo” lazima wahubiri. (Gal. 6:2) Yehova anatarajia waabudu wake wote wafuate viwango vilevile. Kwa mfano, aliwaambia Waisraeli hivi: “Sheria moja itakuwapo kwa ajili ya mwenyeji na kwa ajili ya mkaaji mgeni anayekaa akiwa mgeni katikati yenu.” (Kut. 12:49; Law. 24:22) Wakristo hawako chini ya Sheria ya Musa. Lakini sisi sote, iwe ni watiwa-mafuta au la, tuko chini ya “sheria ya Kristo.” Sheria hiyo inahusisha mambo yote ambayo Yesu alifundisha. Mojawapo ya mambo muhimu zaidi ambayo Yesu alifundisha ni kwamba wafuasi wake wanapaswa kupendana. (Yoh. 13:35; Yak. 2:8) Njia moja ya msingi tunayoonyesha kwamba tunampenda Mungu, Kristo, na jirani zetu ni kuhubiri habari njema ya Ufalme.—Yoh. 15:10; Mdo. 1:8.

15. Kwa nini tunaweza kusema kwamba amri ya Yesu inawahusu wafuasi wake wote?

15 Maneno ambayo Yesu aliwaambia wanafunzi wake wachache yanaweza kuwahusu wanafunzi wengi. Kwa mfano, Yesu alifanya agano la Ufalme na wanafunzi 11 tu, lakini agano hilo kwa kweli linawahusu watiwa-mafuta wote 144,000. (Luka 22:29, 30; Ufu. 5:10; 7:4-8) Vivyo hivyo, Yesu aliwaamuru wafuasi wake wachache tu wahubiri, yaani, wale aliowatokea baada ya kufufuliwa. (Mdo. 10:40-42; 1 Kor. 15:6) Lakini wanafunzi wake wote waaminifu katika karne ya kwanza walitambua kwamba amri hiyo iliwahusu, hata ingawa wao binafsi hawakumsikia Yesu akitoa amri hiyo. (Mdo. 8:4; 1 Pet. 1:8) Leo pia, Yesu hajaongea na yeyote kati ya wahubiri milioni nane wa Ufalme wenye bidii. Lakini wote wanatambua kwamba wana wajibu wa kumwamini Kristo na kuonyesha imani hiyo kwa kuhubiri.—Yak. 2:18.

HUU NDIO WAKATI WA KUWA WASHIKAMANIFU

16-18. Tunaweza kuwaungaje mkono kwa ushikamanifu ndugu za Kristo, na kwa nini tunapaswa kufanya hivyo sasa?

16 Shetani anapigana vita dhidi ya ndugu za Kristo waliotiwa mafuta kwa roho walio duniani, na atazidisha mashambulizi yake kadiri ‘kipindi chake kifupi cha wakati’ kinavyokaribia kwisha. (Ufu. 12:9, 12, 17) Licha ya majaribu makali, watiwa-mafuta wanaongoza kampeni kubwa zaidi ya kuhubiri katika historia. Hapana shaka yoyote kwamba Yesu yuko pamoja nao, akiwaongoza katika jitihada zao.—Mt. 28:20.

17 Idadi inayoongezeka ya watu wanaotumaini kuwa kondoo wanaona kuwa ni pendeleo kuwaunga mkono ndugu za Kristo katika kazi ya kuhubiri, na katika njia nyingine. Kwa mfano, wanachangia fedha na kusaidia kujenga Majumba ya Ufalme, Majumba ya Kusanyiko, na ofisi za tawi, nao wanawatii kwa ushikamanifu wale waliowekwa rasmi na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” ili kuongoza.—Mt. 24:45-47; Ebr. 13:17.

Watu walio kama kondoo huwaunga mkono ndugu za Kristo kwa njia mbalimbali (Tazama fungu la 17)

18 Hivi karibuni malaika wataachilia zile pepo za uharibifu za dhiki kuu. Hilo litatukia baada ya ndugu wote wa Kristo walio duniani kutiwa muhuri wa mwisho. (Ufu. 7:1-3) Kabla ya Har–Magedoni kuanza, watiwa-mafuta watachukuliwa kwenda mbinguni. (Mt. 13:41-43) Kwa hiyo, huu ndio wakati wa wale wanaotumaini kuhukumiwa kuwa kondoo kuwaunga mkono kwa ushikamanifu ndugu za Kristo.

^ fu. 6 Kwa habari zaidi kuhusu mfano huo, tazama makala yenye kichwa “Utasimamaje Mbele ya Kiti cha Hukumu?” na “Kuna Wakati Ujao Gani kwa Kondoo na Mbuzi?” katika gazeti Mnara wa Mlinzi la Oktoba 15, 1995.