Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Amri ya Kuoa au Kuolewa “Katika Bwana Tu”—Je, Imepitwa na Wakati?

Amri ya Kuoa au Kuolewa “Katika Bwana Tu”—Je, Imepitwa na Wakati?

“Sijapata mwenzi kutanikoni, na ninaogopa kuzeeka peke yangu.”

“Wanaume fulani ambao si Mashahidi ni wenye fadhili, wana upendo, na wanajali. Hawaipingi dini yangu, na wanaonekana wanavutia zaidi kuliko baadhi ya ndugu.”

Baadhi ya watumishi wa Mungu wamekuwa na maoni kama hayo kuhusiana na kutafuta mwenzi wa ndoa. Hata hivyo, wanajua vizuri kwamba Yehova anataka watumishi wake waoe au kuolewa “katika Bwana tu,” yaani, kuoa au kuolewa na Wakristo wa kweli tu. (1 Kor. 7:39) Kwa nini basi wana maoni hayo?

KWA NINI WENGINE WANA SHAKA?

Huenda wale walio na maoni hayo wanahisi kwamba idadi ya dada waseja ni kubwa kuliko ndugu waseja. Kwa kweli, hivyo ndivyo ilivyo katika nchi nyingi. Fikiria mifano miwili: Nchini Korea, kati ya Mashahidi 100 waseja, 57 ni akina dada na 43 ni akina ndugu. Nchini Kolombia asilimia 66 ya Mashahidi ni akina dada, na asilimia 34 ni akina ndugu.

Katika nchi fulani, wazazi ambao si Mashahidi hudai kiasi kikubwa cha mahari, na hivyo kufanya iwe vigumu kwa akina ndugu wenye kipato cha chini kuoa. Kwa hiyo, huenda dada akafikiri kwamba haiwezekani kuolewa “katika Bwana.” Hivyo huenda akajiuliza hivi, “Je, kweli inawezekana kupata mwenzi anayenifaa kati ya Wakristo wenzangu?” *

NI MUHIMU KUMTEGEMEA YEHOVA

Iwapo umewahi kufikiria hivyo, uwe na hakika kwamba Yehova anaelewa hali yako. Kwa kweli, anajua jinsi unavyohisi kuhusu jambo hilo.—2 Nya. 6:29, 30.

Hata hivyo, Yehova ametoa mwongozo katika Neno lake kwamba tunapaswa kuoa au kuolewa katika Bwana tu. Kwa nini? Kwa sababu anajua jambo linalowafaa watu wake. Yehova huwalinda watumishi wake ili wasipate maumivu yanayotokana na kufuata njia isiyofaa, na anataka pia wawe na furaha. Katika siku za Nehemia, Wayahudi wengi walipofunga ndoa na watu wa mataifa ambao hawakumwabudu Yehova, Nehemia aliwakumbusha mfano mbaya wa Sulemani. Ingawa Sulemani “alipendwa na Mungu wake, . . . wake wa kigeni walimfanya hata yeye atende dhambi.” (Neh. 13:23-26) Hivyo, Mungu ametupatia mwongozo wa kuoa au kuolewa na waabudu wa kweli tu kwa faida yetu wenyewe. (Zab. 19:7-10; Isa. 48:17, 18) Wakristo wa kweli wanamshukuru sana Mungu kwa sababu anawajali, nao wanategemea mwongozo wake. Kwa kujitiisha chini ya utawala wake wanaonyesha kwamba wanamtambua yeye kuwa Mwenye Enzi Kuu.—Met. 1:5.

Bila shaka, usingependa “kufungwa nira” na mtu yeyote ambaye atakufanya umwache Mungu. (2 Kor. 6:14) Wakristo wengi wametii mwongozo unaofaa wa Mungu ambao umethibitika kuwa ulinzi na wametambua kwamba wamefanya uamuzi wa hekima. Hata hivyo, wengine wamefanya uamuzi tofauti.

BADO NI MWONGOZO UNAOFAA

Maggy, * dada anayeishi Australia, anaeleza kilichotokea alipoanzisha urafiki wa kimapenzi na mwanaume asiye mwamini: “Nilikosa mikutano mingi ili tu niwe pamoja naye. Hali yangu ya kiroho iliporomoka.” Ratana kutoka India alianzisha uhusiano wa kimahaba na mwanafunzi mwenzake ambaye alianza kujifunza Biblia. Hata hivyo, baada ya muda mwanafunzi huyo alionyesha kwamba nia yake ilikuwa kuanzisha uhusiano wa kimahaba pamoja naye. Hatimaye, Ratana aliacha kweli na kujiunga na dini nyingine ili aolewe.

Mfano mwingine ni Ndenguè anayeishi Kamerun. Aliolewa akiwa na umri wa miaka 19. Mchumba wake alimwahidi kwamba angemruhusu aendelee kushirikiana na dini yake. Hata hivyo, majuma mawili baada ya harusi yao, mume wake alimkataza kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Anasema hivi: “Nililia na nilikuwa mpweke sana. Nilitambua kwamba sikuwa na uhuru tena. Kila siku nilijihisi mwenye hatia.”

Bila shaka, si wenzi wote wasio Mashahidi ambao hubadilika na kuwa wakatili na wasiokubali sababu. Hata ingawa hujapatwa na hali hizo ngumu kwa sababu ya kuolewa na mtu asiye mwamini, uamuzi huo umeathirije uhusiano wako pamoja na Baba yako wa mbinguni mwenye upendo? Unahisije kujua kwamba hukufuata mwongozo wake unaofaa ambao aliandaa kwa faida yako? Na jambo muhimu zaidi, anahisije kuhusu uamuzi wako?—Met. 1:33.

Ndugu na dada ulimwenguni pote wanaweza kuthibitisha kwamba kuoa au kuolewa “katika Bwana tu” ndiyo uamuzi bora zaidi. Ndugu na dada waseja wameazimia kuufurahisha moyo wa Mungu kwa kuwa tayari kuoa au kuolewa tu na mwenzi anayewafaa kati ya waabudu wake. Michiko anayeishi Japani, alishawishiwa na watu wake wa ukoo afunge ndoa na mtu asiye mwamini. Zaidi ya hilo, Michiko aliumia zaidi alipoona rafiki zake wakipata wenzi katika kutaniko la Kikristo. Anasema hivi: “Sikuzote nilijikumbusha kwamba Yehova ni ‘Mungu mwenye furaha,’ kwa hiyo furaha yetu haitegemei ikiwa tumefunga ndoa au la. Pia, ninaamini kwamba yeye hututimizia tamaa za moyo wetu. Hivyo, ikiwa tungependa kuolewa lakini hatupati mwenzi wa ndoa, ni afadhali kubaki waseja kwa muda.” (1 Tim. 1:11) Mwishowe, Michiko aliolewa na ndugu mwenye sifa nzuri, na anafurahi kwamba alisubiri.

Ndugu wengine pia wamesubiri ili wapate mwenzi anayewafaa. Bill anayeishi Australia ni miongoni mwao. Anakiri kwamba kuna nyakati ambazo alivutiwa na wanawake wasio Mashahidi. Hata hivyo, aliepuka kabisa kuwa na urafiki wa karibu pamoja nao. Kwa nini? Kwa sababu hakutaka kuchukua hatua ya kwanza ambayo ingemwongoza ‘afungwe nira isivyo sawa’ na mtu asiye mwamini. Kwa miaka mingi alivutiwa na dada kadhaa lakini wao hawakuvutiwa naye. Bill alisubiri kwa miaka 30 ndipo alipompata dada waliyefaana. Bill anasema hivi: “Sijuti hata kidogo.” Anaeleza: “Ninahisi kwamba nimebarikiwa kwa sababu tunahubiri pamoja, tunajifunza pamoja, na kuabudu pamoja. Ninafurahi kuwajua na kushirikiana na rafiki za mke wangu kwa sababu wote ni waabudu wa Yehova. Tunaimarisha ndoa yetu kwa kutumia kanuni za Biblia.”

UNAPOENDELEA KUMNGOJEA YEHOVA

Utafanya nini unaposubiri na kuendelea kufuata mwongozo wa Yehova? Jambo moja ni kufikiria kwa nini hujafunga ndoa. Ikiwa sababu kuu ni kutii mwongozo wa Biblia wa kuoa au kuolewa “katika Bwana tu,” basi unastahili kupongezwa kwa kutii amri hiyo ya Mungu. Uwe na hakika kwamba Yehova anafurahishwa sana na msimamo wako thabiti wa kutii Neno lake. (1 Sam. 15:22; Met. 27:11) Endelea ‘kuumimina moyo wako’ kwa Mungu kupitia sala. (Zab. 62:8) Kadiri unavyoendelea kumwomba kwa bidii na bila kukoma, ndivyo utakavyobaki imara licha ya ushawishi wowote. Uhusiano wako pamoja na Mungu utaimarika siku baada ya siku. Uwe na hakika kwamba yule Aliye Juu Zaidi anapendezwa na watumishi wake wote waaminifu na kwamba una thamani machoni pake. Anaelewa mahitaji yako na tamaa zako. Yehova hatoi ahadi ya kumpa mtu yeyote mwenzi wa ndoa. Hata hivyo, ikiwa kwa kweli unahitaji mwenzi wa ndoa, Mungu anajua njia bora zaidi ya kutosheleza tamaa zako zinazofaa.—Zab. 145:16; Mt. 6:32.

Huenda nyakati nyingine ukahisi kama mtunga zaburi Daudi, aliyesema hivi: “Ufanye haraka, unijibu, Ee Yehova; roho yangu imefikia mwisho. Usiufiche uso wako mbali nami.” (Zab. 143:5-7, 10) Nyakati kama hizo, mpe Baba yako wa mbinguni nafasi ya kukuonyesha mambo anayotaka ufanye. Unaweza kufanya hivyo kwa kusoma Neno lake na kutafakari yale unayosoma. Utaelewa amri zake na kuona jinsi alivyowasaidia watu wake wakati uliopita. Kwa kumsikiliza, utaweza kumtii.

Waseja wanathaminiwa sana kutanikoni, mara nyingi huwasaidia watoto na familia

Ni nini kingine kitakufanya uwe na furaha, na mengi ya kufanya wakati wa useja? Tumia miaka ya useja kusitawisha utambuzi, ukarimu, bidii, urafiki, ujitoaji-kimungu, kwani hizo ni sifa muhimu ili kuwa na familia yenye furaha. (Mwa. 24:16-21; Rut. 1:16, 17; 2:6, 7, 11; Met. 31:10-27) Tafuta kwanza Ufalme kwa kushiriki kikamili katika kazi ya kuhubiri na utendaji mwingine wa Kikristo; kufanya hivyo kutakulinda. Bill, aliyetajwa mwanzoni, anasema hivi kuhusu miaka ambayo alitamani kuoa: “Ilipita haraka sana! Nilitumia wakati huo kumtumikia Yehova nikiwa painia.”

Naam, amri ya kuoa au kuolewa “katika Bwana tu” haijapitwa na wakati. Kutii amri hiyo kunaweza kukusaidia kumheshimu Yehova na kuridhika maishani. Biblia inasema: “Mwenye furaha ni mtu anayemwogopa Yehova, ambaye amependezwa sana na amri zake. Vitu vyenye thamani na utajiri vimo nyumbani mwake, nao uadilifu wake unasimama milele.” (Zab. 112:1, 3) Hivyo, azimia kuendelea kushika amri ya Mungu ya kuoa au kuolewa “katika Bwana tu.”

^ fu. 7 Katika makala hii, tutachunguza jambo hili kwa kufikiria maoni ya akina dada, ingawa kanuni zinazozungumziwa zinawafaa akina ndugu pia.

^ fu. 13 Majina mengine yamebadilishwa.