Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kristo—Nguvu za Mungu

Kristo—Nguvu za Mungu

“Kristo ni nguvu za Mungu.”—1 KOR. 1:24.

1. Kwa nini Paulo alisema kwamba “Kristo ni nguvu za Mungu”?

YEHOVA alionyesha nguvu zake kupitia Yesu kwa njia za pekee sana. Vitabu vinne vya Injili vinaeleza mambo yenye kuimarisha imani kuhusu miujiza ambayo Kristo alifanya. Inaelekea alifanya miujiza mingine mingi. (Mt. 9:35; Luka 9:11) Naam, Mungu alionyesha nguvu zake kupitia Yesu. Hiyo ndiyo sababu Paulo angeweza kusema: “Kristo ni nguvu za Mungu.” (1 Kor. 1:24) Hata hivyo, miujiza ya Yesu inatufundisha nini?

2. Miujiza ya Yesu inatufundisha nini?

2 Mtume Petro alisema kwamba Yesu alifanya miujiza, au “mambo ya ajabu.” (Mdo. 2:22) Kazi zenye nguvu ambazo Yesu alifanya alipokuwa duniani zilikuwa kionjo cha baraka nyingi zaidi zitakazoletwa na utawala wake. Zilikuwa kivuli cha miujiza ambayo Yesu atafanya kwa kiwango kikubwa katika ulimwengu mpya wa Mungu! Miujiza hiyo inatusaidia pia kuelewa vizuri utu wake na wa Baba yake. Acheni tuchunguze baadhi ya miujiza ya Yesu na kujifunza mambo yatakayotusaidia katika maisha yetu sasa na wakati ujao.

MUUJIZA UNAOTUFUNDISHA UKARIMU

3. (a) Eleza hali zilizopelekea Yesu afanye muujiza wake wa kwanza. (b) Yesu alionyeshaje ukarimu huko Kana?

3 Yesu alifanya muujiza wake wa kwanza katika karamu ya harusi huko Kana ya Galilaya. Hakukuwa na divai ya kutosha kwa ajili ya wageni waalikwa. Maria, mama ya Yesu, alikuwepo katika karamu hiyo. Je, alimwomba Yesu asaidie akiamini kuwa ana nguvu za kufanya miujiza? Bila shaka alitafakari kwa miaka mingi unabii uliomhusu mwana wake, ambaye alijua angeitwa “Mwana wa Aliye Juu Zaidi.” (Luka 1:30-32; 2:52) Ni wazi kwamba Maria na Yesu waliwahurumia maharusi hao na walitaka kuwasaidia ili wasiaibike. Yesu alitaka kuonyesha ukarimu. Hivyo, alifanya muujiza kwa kubadili lita 380 za maji kuwa “divai nzuri.” (Soma Yohana 2:3, 6-11.) Je, ilikuwa lazima Yesu afanye muujiza huo? Hapana. Alifanya hivyo kwa sababu aliwajali watu na alimwiga Baba yake wa mbinguni kwa kuwa mkarimu.

4, 5. (a) Muujiza wa kwanza wa Yesu unatufundisha nini? (b) Muujiza wa Kana unatufundisha nini kuhusu wakati ujao?

4 Yesu aliandaa divai nyingi kimuujiza. Muujiza huo unatufundisha nini? Utayari wa Yesu wa kufanya muujiza huo unatuhakikishia kwamba yeye na Baba yake wanajali sana hisia za watu. Baba na Mwana si wachoyo. Hebu wazia jinsi Yehova atakavyotumia nguvu zake katika ulimwengu mpya kuandaa karamu ya vyakula vinono kwa “vikundi vyote vya watu” duniani kote!—Soma Isaya 25:6.

5 Wazia hili! Wakati ujao Yehova atatosheleza mahitaji na tamaa zetu zote zinazofaa. Kwa mfano, kila mtu atapata chakula chenye lishe na nyumba nzuri. Tunafurahi sana tunapofikiria mambo mazuri ambayo Yehova atatuandalia katika Paradiso duniani.

Tunaiga ukarimu wa Yesu tunapotumia wakati wetu kuwasaidia wengine (Tazama fungu la 6)

6. Yesu alitumia nguvu zake za kufanya miujiza kwa ajili ya nani, na tunawezaje kumwiga?

6 Yesu alikataa aliposhawishiwa na Shetani ageuze mawe yawe mkate; hakutaka kutumia nguvu zake za kufanya miujiza kwa manufaa yake. (Mt. 4:2-4) Lakini alitumia nguvu zake kutosheleza mahitaji ya wengine. Tunawezaje kuiga ukarimu wake? Yesu alisema hivi: “Muwe na mazoea ya kuwapa watu.” (Luka 6:38) Tunaweza kuonyesha ukarimu kwa kuwaalika wengine nyumbani kwetu kwa ajili ya chakula na karamu ya kiroho. Pia, tunaweza kutumia muda wetu baada ya mkutano kumsaidia mtu mwenye uhitaji, kama vile kumsikiliza ndugu anapofanya mazoezi ya hotuba yake. Au tunaweza kuwasaidia na kuwazoeza wengine katika huduma. Tunaonyesha kwamba tunaiga ukarimu wa Yesu tunapowasaidia wengine kimwili na kiroho kadiri tuwezavyo.

“WOTE WAKALA WAKASHIBA”

7. Tatizo gani litaendelea kuwepo maadamu mfumo huu upo?

7 Umaskini si jambo jipya. Yehova aliliambia taifa la kale la Israeli kwamba hakutakosa kuwa na maskini katika nchi. (Kum. 15:11) Karne kadhaa baadaye, Yesu alisema hivi: “Mna maskini pamoja nanyi sikuzote.” (Mt. 26:11) Je, Yesu alimaanisha kwamba daima kutakuwa na maskini duniani? Hapana. Alimaanisha kwamba kutakuwa na maskini maadamu mfumo huu mwovu wa mambo upo. Kwa hiyo, inatia moyo sana kujua kwamba miujiza ya Yesu ilikuwa ishara ya maisha bora ya wakati ujao chini ya utawala wa Ufalme. Kila mtu atakuwa na chakula cha kutosha.

8, 9. (a) Kwa nini Yesu aliwalisha maelfu ya watu kimuujiza? (b) Unahisije kuhusu muujiza huo?

8 Mtunga-zaburi alisema hivi kumhusu Yehova: “Unaufumbua mkono wako na kutosheleza tamaa ya kila kitu kilicho hai.” (Zab. 145:16) ‘Kristo, nguvu za Mungu,’ alimwiga Baba yake, hivyo mara kwa mara aliufumbua mkono wake na kutosheleza mahitaji ya wafuasi wake. Hakufanya hivyo ili tu kuonyesha nguvu zake. Bali aliwajali watu kikweli. Acheni tuzungumzie andiko la Mathayo 14:14-21. (Soma.) Wanafunzi wa Yesu walimkaribia ili kuzungumzia kuhusu chakula. Huenda walikuwa na njaa, lakini waliwahangaikia zaidi watu waliowafuata kwa miguu kutoka majijini. Watu hao walikuwa wamechoka na walikuwa na njaa. (Mt. 14:13) Yesu angefanya nini?

9 Akitumia mikate mitano na samaki wawili, Yesu aliwalisha wanaume 5,000, na vilevile wanawake na watoto! Je, huvutiwi na jinsi Yesu alivyotumia nguvu zake za kufanya miujiza kutosheleza mahitaji ya watu, kutia ndani watoto? Watu “wote wakala, wakashiba.” Hilo linaonyesha kwamba kulikuwa na chakula kingi. Yesu hakuandaa kipande kidogo tu cha mkate, bali mlo wa kutosha ambao ungewapa watu nguvu za kutembea safari ndefu kurudi nyumbani. (Luka 9:10-17) Mabaki ya chakula yalijaza vikapu kumi na viwili!

10. Ni mabadiliko gani kuhusu umaskini yatakayotokea hivi karibuni?

10 Leo, mahitaji ya msingi ya mamilioni ya watu hayatoshelezwi kwa sababu ya ufisadi wa serikali za wanadamu. Hata mahitaji ya msingi ya baadhi ya ndugu zetu hayatoshelezwi kikamili. Hata hivyo, karibuni wanadamu watiifu watafurahia ulimwengu usio na ufisadi wala umaskini. Ikiwa ungekuwa na uwezo, je, ungetosheleza mahitaji ya wanadamu? Mungu Mweza-Yote ana uwezo, anatamani, na atafanya hivyo hivi karibuni. Naam, kitulizo kinakaribia sana!—Soma Zaburi 72:16.

11. Kwa nini una uhakika kwamba hivi karibuni Yesu atatumia nguvu zake kuwanufaisha wanadamu? Na hilo linakuchochea kufanya nini?

11 Alipokuwa duniani, Yesu alifanya kazi zake katika eneo dogo kwa muda wa miaka mitatu na nusu. (Mt. 15:24) Akiwa Mfalme aliyetukuzwa, Yesu atawasaidia wanadamu duniani kote. (Zab. 72:8) Miujiza ya Yesu inatuhakikishia kwamba ana uwezo na anatamani kutusaidia, na hivi karibuni atatumia mamlaka yake kwa faida yetu. Hatuwezi kufanya miujiza, lakini tunaweza kuwafundisha watu kwa shauku Neno la Mungu lililoongozwa na roho. Biblia ina unabii mwingi unaotuhakikishia kwamba wakati ujao hali zitakuwa bora. Ukiwa Shahidi wa Yehova mwenye ujuzi huo wenye thamani kuhusu wakati ujao, je, huhisi kwamba una deni? (Rom. 1:14, 15) Kutafakari jambo hilo na kutuchochee kuwaambia wengine habari njema ya Ufalme wa Mungu!—Zab. 45:1; 49:3.

KUDHIBITI NGUVU ZA ASILI

12. Kwa nini tuna uhakika kwamba Yesu anaelewa kikamili mifumo ya asili ya dunia?

12 Mungu alipoumba dunia na vitu vilivyomo, Mwana wake mzaliwa-pekee alikuwa kando yake akiwa “stadi wa kazi.” (Met. 8:22, 30, 31; Kol. 1:15-17) Hivyo, Yesu anaelewa kikamili mifumo ya asili ya dunia. Anajua jinsi ya kutumia, kusimamia, na kugawanya maliasili za dunia kwa njia inayofaa.

Kwa nini unavutiwa na jinsi Yesu alivyotumia nguvu zake za kufanya miujiza? (Tazama fungu la 13, 14)

13, 14. Toa mfano unaoonyesha uwezo wa Yesu wa kudhibiti nguvu za asili.

13 Alipokuwa duniani, Yesu alionyesha kwamba yeye ni “nguvu za Mungu” kwa kudhibiti nguvu za asili. Fikiria jinsi Yesu alivyodhibiti dhoruba iliyohatarisha uhai wa wanafunzi wake. (Soma Marko 4:37-39.) Msomi mmoja wa Biblia anasema hivi: “Neno la Kigiriki [linalotafsiriwa “dhoruba” kwenye Marko 4:37] linamaanisha tufani kubwa au kimbunga. Si dhoruba ya ghafla tu inayopita mara moja . . . bali ni dhoruba inayoambatana na radi na mvua kali, na kusababisha uharibifu mkubwa.” Simulizi la Mathayo linafafanua dhoruba hiyo kuwa “msukosuko mkubwa.”—Mt. 8:24.

14 Wazia hali iliyokuwepo: Mawimbi yanaipiga mashua na maji yanaingia ndani. Hata hivyo, licha ya kelele za dhoruba na kuyumbayumba kwa mashua, Yesu amelala usingizi. Alihitaji kupumzika kwa sababu alikuwa amechoka kutokana na huduma yake yenye mambo mengi. Wakiwa wamejaa woga, wanafunzi wake wanamwamsha na kumwambia: “Tuko karibu kuangamia!” (Mt. 8:25) Yesu anaamka na kuuamrisha upepo na bahari kwa kusema: “Nyamaza, utulie!” na upepo mkali unatoweka. (Marko 4:39) Yesu aliuamrisha upepo na bahari itulie. Matokeo yakawa nini? “Kukawa utulivu mkubwa.” Naam, alionyesha nguvu kwa njia yenye kustaajabisha sana!

15. Mungu Mweza-Yote ameonyeshaje uwezo wake wa kudhibiti nguvu za asili?

15 Nguvu za Yesu zilitoka kwa Yehova, hivyo tuna kila sababu ya kuamini kwamba Mungu Mweza-Yote ana uwezo wa kudhibiti kikamili nguvu za asili. Fikiria mifano kadhaa. Yehova alisema hivi kabla ya Gharika: “Baada ya siku 7 nitanyesha mvua duniani siku 40 mchana na usiku.” (Mwa. 7:4) Vivyo hivyo, tunasoma hivi kwenye Kutoka 14:21: “Yehova akaanza kuifanya bahari irudi nyuma kwa upepo wenye nguvu wa mashariki.” Vilevile, andiko la Yona 1:4 linasema hivi: “Yehova mwenyewe akavumisha upepo mkubwa baharini, kukawa na tufani kubwa baharini; nayo meli ikawa karibu kuvunjika.” Inatia moyo kujua kwamba Yehova anaweza kudhibiti nguvu za asili. Bila shaka, atahakikisha kuwa dunia itakuwa salama wakati ujao.

16. Kwa nini inafariji kujua kwamba Yehova na Mwana wake wanaweza kudhibiti nguvu za asili?

16 Inafariji sana kutafakari kuhusu nguvu zenye kustaajabisha za Muumba wetu na ‘stadi wake wa kazi.’ Wakati wa Miaka Elfu Moja ya Utawala wa Kristo, kila mtu atakuwa salama. Nguvu za asili zenye kutisha zitakuwa kati ya mambo ya zamani. Katika ulimwengu mpya, hakuna atakayeogopa vimbunga, tsunami, volkano, au matetemeko. Inapendeza sana kufikiria wakati ambapo nguvu za asili hazitamuua au kumjeruhi yeyote, kwa maana “hema la Mungu [litakuwa] pamoja na wanadamu”! (Ufu. 21:3, 4) Tunaweza kuwa na uhakika kwamba Mungu atamtumia Yesu kudhibiti nguvu za asili wakati wa Utawala wake wa Miaka Elfu Moja.

MWIGE MUNGU NA YESU

17. Tunawezaje kumwiga Mungu na Kristo?

17 Hatuwezi kudhibiti nguvu za asili, lakini tuna uwezo kwa kadiri fulani. Tunaweza kuutumiaje? Njia moja ni kutumia andiko la Methali 3:27. (Soma.) Ndugu zetu wanapokabili hali ngumu, tunaweza kuwafariji na kuwategemeza kimwili, kihisia, na kiroho. (Met. 17:17) Kwa mfano, tunaweza kuwasaidia wanapopatwa na majanga ya asili. Mjane mmoja ambaye nyumba yake iliharibiwa na kimbunga alisema hivi: “Ninafurahia sana kuwa kwenye tengenezo la Yehova, kwa sababu linatusaidia kiroho na kimwili pia.” Dada mwingine mseja alikata tamaa na kupigwa na butwaa baada ya nyumba yake kuharibiwa na dhoruba. Alisema hivi baada ya kupokea msaada: “Sijui nisemeje! Nashindwa kueleza kikamili jinsi ninavyohisi . . . Asante Yehova!” Tuna shangwe kwa sababu ndugu na dada zetu wanatujali kikweli. Jambo muhimu zaidi ni kwamba Yehova na Yesu Kristo wanatujali sana.

18. Ni nini kinachokuvutia kuhusu nia ya Yesu?

18 Katika huduma yake, Yesu alithibitisha kwamba yeye ni “nguvu za Mungu.” Lakini alikuwa na nia gani? Hakutumia kamwe nguvu zake kujionyesha au kujinufaisha. Kwa kweli, miujiza aliyofanya inathibitisha kwamba anawapenda wanadamu. Tutazungumzia jambo hilo katika makala inayofuata.