Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ishi Kupatana na Sala ya Mfano—Sehemu ya Kwanza

Ishi Kupatana na Sala ya Mfano—Sehemu ya Kwanza

“Jina lako na litakaswe.”—MT. 6:9.

1. Tunaweza kuitumiaje sala iliyoandikwa kwenye Mathayo 6:9-13 katika huduma?

WATU wengi wameikariri Sala ya Bwana. Tunapokuwa katika huduma ya shambani, mara nyingi tunaitumia sala hiyo kumsaidia mwenye nyumba aelewe kwamba Ufalme wa Mungu ni serikali halisi itakayoleta mabadiliko mazuri duniani. Au tunaweza kutumia ombi la kwanza katika sala hiyo kuthibitisha kwamba Mungu ana jina, ambalo linapaswa kutakaswa.—Mt. 6:9.

2. Je, Yesu alimaanisha kwamba tunapaswa kurudia-rudia maneno ya sala ya mfano kila tunaposali? Eleza.

2 Je, Yesu alimaanisha kwamba tunapaswa kurudia-rudia maneno ya sala hiyo kila tunaposali, kama makanisa fulani ya Kikristo yanavyofanya? Hapana. Kabla tu ya kufundisha sala hiyo ya mfano, Yesu alisema hivi: “Mnaposali, msiseme mambo yaleyale tena na tena.” (Mt. 6:7) Baadaye, Yesu aliirudia sala hiyo kwa kutumia maneno tofauti. (Luka 11:1-4) Hivyo, Yesu alitusaidia kujua mambo tunayopaswa kuomba, na ni yapi yanapaswa kuchukua nafasi ya kwanza katika sala zetu. Ndiyo sababu inaitwa sala ya mfano.

3. Tunaweza kujiuliza maswali gani tunapozungumzia sala ya mfano?

3 Katika makala hii na inayofuata, tutazungumzia sala hiyo ya mfano. Tunapofanya hivyo, jiulize hivi, ‘Sala hii inaweza kunisaidiaje kuboresha sala zangu? Na je, ninaishi kupatana na sala hii?’

“BABA YETU ULIYE MBINGUNI”

4. Maneno “Baba yetu” yanatukumbusha nini? Ni katika maana gani Wakristo wenye tumaini la kuishi duniani wanamwona Yehova kuwa “Baba”?

4 Maneno “Baba yetu,” na si “Baba yangu,” yanatukumbusha kwamba sisi ni sehemu ya “ushirika mzima wa akina ndugu” ambao wanapendana kikweli. (1 Pet. 2:17) Hiyo ni baraka iliyoje! Yehova amewachagua Wakristo watiwa-mafuta wakaishi mbinguni na amewafanya kuwa wana Wake, hivyo wanamwona Yehova kuwa “Baba” yao katika maana kamili. (Rom. 8:15-17) Wakristo wenye tumaini la kuishi duniani wanaweza pia kumwona Yehova kuwa “Baba” yao. Yeye ndiye huwapa uhai na kutosheleza mahitaji ya waabudu wake wa kweli. Wale wenye tumaini la kuishi duniani watakuwa watoto wa Mungu kikamili watakapofikia ukamilifu na kuendelea kuwa waaminifu baada ya jaribu la mwisho.—Rom. 8:21; Ufu. 20:7, 8.

5, 6. Ni zawadi gani nzuri ambayo wazazi wanaweza kuwapa watoto wao, na kila mtoto ana wajibu gani? (Tazama picha kwenye ukurasa wa 20.)

5 Wazazi huwapa watoto wao zawadi nzuri sana wanapowafundisha kusali na kuwasaidia wamwone Yehova kuwa Baba yao wa mbinguni anayewajali. Mwangalizi wa mzunguko kutoka Afrika Kusini anakumbuka hivi: “Tangu binti zetu walipozaliwa, nilisali nao kila usiku isipokuwa wakati nilipokuwa safarini. Mara nyingi binti zetu wanasema kwamba hawakumbuki maneno ya sala hizo. Hata hivyo, wanakumbuka hali ya utulivu na usalama pamoja na utakatifu wa kuwasiliana na Baba yetu, Yehova. Walipokua, niliwatia moyo wasali kwa sauti ili niwasikie wanavyomweleza Yehova mawazo na hisia zao. Hiyo ilikuwa nafasi nzuri sana ya kujua mambo yaliyokuwa moyoni mwao. Kisha, hatua kwa hatua niliwafundisha kutaja mambo muhimu yaliyo kwenye sala ya mfano ili wasali kwa njia inayofaa.”

6 Mabinti wa ndugu huyo walifanya maendeleo ya kiroho. Sasa kila mmoja wao ana ndoa yenye furaha, na wote wanamtumikia Yehova katika utumishi wa wakati wote pamoja na waume zao. Zawadi nzuri zaidi ambayo wazazi wanaweza kuwapa watoto wao ni kuwasaidia wasitawishe uhusiano wa karibu sana na Yehova. Bila shaka, kila mtu ana wajibu wa kudumisha uhusiano wake na Yehova. Kufanya hivyo kunahusisha kulipenda, na kuliheshimu sana jina la Mungu.—Zab. 5:11, 12; 91:14.

“JINA LAKO NA LITAKASWE”

7. Watu wa Mungu wamepewa heshima gani, lakini tunapaswa kufanya nini?

7 Ni heshima kubwa sana kwetu kulijua jina la Mungu na kuitwa “watu kwa ajili ya jina lake.” (Mdo. 15:14; Isa. 43:10) Tunasali hivi kwa Baba yetu wa mbinguni: “Jina lako na litakaswe.” Kufanya hivyo kutatuchochea tumwombe Yehova atusaidie kuepuka maneno au matendo yanayoweza kulivunjia heshima jina lake takatifu. Hatupaswi kuwa kama watu fulani katika karne ya kwanza ambao walitenda kinyume cha mambo waliyohubiri. Mtume Paulo aliandika hivi kuwahusu: “Jina la Mungu linafanyiwa makufuru katikati ya mataifa kwa sababu yenu.”—Rom. 2:21-24.

8, 9. Toa mfano unaoonyesha jinsi ambavyo Yehova huwabariki wale wanaotaka kulitakasa jina lake.

8 Tunataka kulitakasa jina la Mungu. Dada mmoja nchini Norway ambaye mume wake alikufa mvulana wao alipokuwa na umri wa miaka miwili, anaeleza hivi: “Ulikuwa wakati mgumu sana maishani mwangu. Nilisali kila siku, karibu kila saa, nikimwomba Yehova anisaidie kuwa mtulivu ili nisifanye uamuzi wowote usiofaa au kuvunja uaminifu wangu, na hivyo kumpa Shetani sababu ya kumdhihaki Yehova. Nilitaka kulitakasa jina la Yehova, na nilitaka mwanangu amwone tena baba yake katika Paradiso.”—Met. 27:11.

9 Je, Yehova alijibu sala za dada huyo? Bila shaka! Waamini wenzake walimtia moyo kwa kuwa alishirikiana nao kwa ukawaida. Miaka mitano baadaye aliolewa na mzee wa kutaniko. Leo mtoto wake ambaye ana umri wa miaka 20, ni ndugu aliyebatizwa. Anasema hivi: “Nina furaha sana, kwa kuwa mume wangu alinisaidia kumlea.”

10. Yehova atafanya nini ili kulitakasa jina lake?

10 Ni nini kinahitaji kufanywa ili jina la Mungu litakaswe na kuondolewa shutuma kabisa? Ni lazima Yehova awaondoe wale wote wanaopinga kimakusudi enzi yake kuu. (Soma Ezekieli 38:22, 23.) Halafu, hatua kwa hatua wanadamu watafanywa kuwa wakamilifu. Tunatazamia kwa hamu wakati huo ambapo viumbe wote wenye akili watalitakasa jina la Yehova! Hatimaye, Baba yetu wa mbinguni atakuwa “vitu vyote kwa kila mtu.”—1 Kor. 15:28.

“UFALME WAKO NA UJE”

11, 12. Yehova aliwasaidia watu wake kujua jambo gani katika mwaka wa 1876?

11 Kabla Yesu hajarudi mbinguni, mitume wake walimuuliza hivi: “Bwana, je, unarudishia Israeli ufalme wakati huu?” Jibu la Yesu lilionyesha kwamba haukuwa wakati wao kujua Ufalme wa Mungu ungeanza kutawala lini. Aliwaambia wanafunzi wake wakazie fikira kazi muhimu ambayo walipaswa kuifanya, yaani, kutoa ushahidi. (Soma Matendo 1:6-8.) Hata hivyo, Yesu aliwafundisha wafuasi wake watazamie kuja kwa Ufalme wa Mungu. Hivyo tangu siku za mitume, Wakristo wamekuwa wakisali Ufalme huo uje.

12 Muda ulipokaribia, Yehova aliwasaidia watu wake kujua mwaka hususa ambao Yesu angeanza kutawala mbinguni akiwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu. Mwaka wa 1876, Charles Taze Russell alichapisha makala yenye kichwa, “Nyakati za Mataifa: Zakoma Wakati Gani?” kwenye gazeti Bible Examiner. Makala hiyo iliutaja 1914 kuwa mwaka muhimu. Ilisema kuwa “nyakati saba” zinazotajwa katika unabii wa Danieli ni sawa na zile “nyakati zilizowekwa za mataifa” zilizotajwa na Yesu. *Dan. 4:16; Luka 21:24.

13. Ni nini kilichotokea mwaka wa 1914, na tangu wakati huo matukio ya ulimwengu yanathibitisha nini?

13 Mwaka wa 1914, vita vilianza kupiganwa katika mataifa ya Ulaya, na baada ya muda mfupi vilienea duniani kote. Vita hivyo, ambavyo viliisha mwaka wa 1918, vilisababisha upungufu mkubwa sana wa chakula. Kisha kukatokea mafua makali sana ambayo yaliua watu wengi zaidi kuliko vita hivyo. Huo ukawa mwanzo wa utimizo wa ile “ishara” ambayo Yesu aliitoa ili kuonyesha kuwapo kwake akiwa Mfalme mpya wa dunia. (Mt. 24:3-8; Luka 21:10, 11) Mambo mengi yanathibitisha kwamba Bwana Yesu Kristo ‘alipewa taji’ mwaka wa 1914. Naye “akaenda akishinda na kukamilisha ushindi wake.” (Ufu. 6:2) Yesu alisafisha mbingu kwa kumtupa Shetani na roho wake waovu kwenye ujirani wa dunia. Tangu wakati huo wanadamu wamejionea ukweli wa maneno haya: “Ole wa dunia na wa bahari, kwa sababu Ibilisi ameshuka kwenu, akiwa na hasira kali, akijua kwamba ana kipindi kifupi cha wakati.”—Ufu. 12:7-12.

14. (a) Kwa nini bado ni muhimu tuombe Ufalme wa Mungu uje? (b) Ni kazi gani muhimu tunayopaswa kufanya?

14 Unabii ulioandikwa kwenye Ufunuo 12:7-12, unatusaidia kuelewa kwa nini wanadamu wamekuwa wakipatwa na matukio mabaya sana tangu Ufalme wa Mungu ulipoanza kutawala. Ingawa Yesu, Mfalme wa Ufalme wa Mungu, alianza kutawala mbinguni, bado Shetani anatawala dunia. Hata hivyo, hivi karibuni Yesu atakamilisha ushindi wake kwa kuondoa kabisa uovu duniani. Kabla wakati huo haujafika, tutaendelea kusali Ufalme wa Mungu na uje. Wakati huohuo, tunapaswa kuishi kupatana na sala zetu kwa kushiriki kutimiza mojawapo ya sehemu muhimu ya ile “ishara.” Yesu alitabiri hivi: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.”—Mt. 24:14.

“MAPENZI YAKO NA YATENDEKE DUNIANI”

15, 16. Tunawezaje kuishi kupatana na sala yetu ya kuomba mapenzi ya Mungu yatendeke duniani?

15 Karibu miaka 6,000 iliyopita, mapenzi ya Mungu yalikuwa yakifanywa kwa ukamili duniani. Ndiyo sababu Yehova alipotazama mwanzo mzuri wa mwanadamu alisema kwamba kila kitu “kilikuwa chema sana.” (Mwa. 1:31) Baada ya Shetani kuasi, wanadamu wachache sana wamekuwa wakifanya mapenzi ya Mungu duniani. Hata hivyo, leo tunafurahi sana kuwa miongoni mwa Mashahidi milioni nane hivi, ambao wanasali mapenzi ya Mungu yatendeke duniani na wanajitahidi kuishi kupatana na sala hiyo. Wanafanya hivyo kwa kuishi maisha yanayomfurahisha Yehova na kuwa wenye bidii ya kuwafundisha watu kuhusu Ufalme wa Mungu.

Je, unawasaidia watoto wako waombe mapenzi ya Mungu yatendeke duniani na kuishi kupatana na ombi hilo? (Tazama fungu la 16)

16 Kwa mfano, dada mmoja aliyebatizwa mwaka wa 1948, na kutumikia akiwa mmishonari barani Afrika anasema hivi: “Sikuzote ninasali ili watu ambao ni kama kondoo wafikiwe na kusaidiwa kumjua Yehova kabla haijawa kuchelewa sana. Pia, kabla ya kuanza kumhubiria mtu, huwa ninamwomba Yehova anipe hekima ili niufikie moyo wa mtu huyo. Kuhusiana na wale walio kama kondoo ambao tayari wamepatikana, ninasali kwa Yehova atubariki tunapoendelea kujitahidi kuwatunza.” Haishangazi kwamba dada huyu mwenye umri wa miaka 80 amefanikiwa kuwasaidia watu wengi wawe Mashahidi wa Yehova. Bila shaka, unaweza kutafakari mifano mingine mizuri ya wale ambao wana bidii ya kufanya mapenzi ya Mungu licha ya uzee.—Soma Wafilipi 2:17.

17. Unahisije unapofikiria mambo ambayo Yehova atawafanyia wanadamu ili kutimiza mapenzi yake duniani?

17 Tutaendelea kusali mapenzi ya Mungu na yatendeke duniani, hadi maadui wote wa Ufalme wa Mungu watakapoondolewa. Kisha, tutaona mapenzi ya Mungu yakitendeka kikamili mabilioni ya wafu watakapofufuliwa katika paradiso duniani. Yesu alisema hivi: “Msistaajabie jambo hili, kwa sababu saa inakuja ambayo wale wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti [yangu] na kutoka.” (Yoh. 5:28, 29) Hebu wazia shangwe tutakayopata tunapowakaribisha wapendwa wetu waliokufa! Mungu “atafuta kila chozi kutoka katika macho [yetu].” (Ufu. 21:4) Watu wengi watakaofufuliwa ni wale “wasio waadilifu,” yaani, wale ambao hawakuwahi kamwe kujifunza kweli kumhusu Yehova Mungu na Mwana wake. Itakuwa shangwe iliyoje kuwafundisha mapenzi ya Mungu na kusudi lake, na hivyo kuwasaidia wastahili kupata “uzima wa milele.”—Mdo. 24:15; Yoh. 17:3.

18. Mwanadamu ana mahitaji gani muhimu zaidi?

18 Ufalme wa Mungu utalitakasa jina la Yehova na kuleta amani na umoja ulimwengu pote. Hivyo, Mungu atatosheleza mahitaji muhimu zaidi ya wanadamu atakapojibu maombi matatu ya kwanza katika sala ya mfano. Katika makala inayofuata tutazungumzia mahitaji mengine muhimu ambayo Yesu alitufundisha tuombe.

^ fu. 12 Kwa maelezo zaidi kuhusiana na jinsi unabii huo ulivyotimizwa mwaka wa 1914 wakati Ufalme wa Mungu ulipoanza kutawala, tazama kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? ukurasa wa 215-218.