Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unakumbuka?

Je, Unakumbuka?

Je, umesoma kwa makini matoleo ya karibuni ya Mnara wa Mlinzi? Ona ikiwa unaweza kujibu maswali yafuatayo:

Je, Wakristo wanapaswa kusali kwa Yesu Kristo?

Hapana. Yesu alitufundisha tusali kwa Yehova, naye akaweka mfano mzuri kwa kusali kwa Baba yake. (Mt. 6:6-9; Yoh. 11:41; 16:23) Hivyo, wafuasi wake wa mapema walisali kwa Mungu na si kwa Yesu. (Mdo. 4:24, 30; Kol. 1:3)—1/1, ukurasa wa 14.

Tunapaswa kufanya nini kila mwaka tunapojitayarisha kuadhimisha kifo cha Yesu?

Jambo moja tunaloweza kufanya ni kwenda sambamba na ratiba ya usomaji wa Biblia unaohusiana na tukio hilo. Pia, tunaweza kujitahidi kuongeza huduma yetu wakati wa majira hayo. Pia, tunaweza kusali na kutafakari kuhusu tumaini ambalo Mungu ametupatia.—1/15, ukurasa wa 14-16.

Wale wafungwa wawili Wamisri waliomsimulia Yosefu ndoto zao walipata matokeo gani?

Yosefu alimwambia mnyweshaji wa Farao kwamba angerudishwa kwenye cheo chake cha awali. Lakini kwa mwokaji, ndoto yake ilimaanisha kuwa Farao angemuua na kumtundika juu ya mti. Maneno yote ya Yosefu yalitimia. (Mwa. 40:1-22)—2/1, ukurasa wa 12-14.

Akina ndugu wa Japani walipokea zawadi gani ambayo hawakuitarajia?

Walipokea kijitabu chenye Injili ya Mathayo iliyotolewa kwenye Tafsiri ya Ulimwengu Mpya. Kijitabu hicho kinatolewa katika huduma, na watu wengi ambao hawaijui vizuri Biblia wamekifurahia sana.—2/15, ukurasa wa 3.

Ni hali gani zilizosaidia kuenea kwa habari njema katika karne ya kwanza?

Hakukuwa na migogoro mingi kwa kuwa kulikuwa na Pax Romana au amani ya Roma. Wanafunzi wa mapema walisafiri kwenye barabara nzuri. Lugha ya Kigiriki ilizungumzwa kwa mapana na marefu, na hilo lilirahisisha kazi ya kuhubiri. Pia, Wayahudi walitawanyika katika milki yote ya Roma. Isitoshe, wanafunzi hao walitumia sheria za Roma kutetea habari njema.—2/15, ukurasa wa 20-23.

Kwa nini Wakristo wa kweli hawasherehekei Ista?

Yesu aliwaagiza wafuasi wake wakumbuke kifo chake na si ufufuo wake. (Luka 22:19, 20)—3/1, ukurasa wa 8.

Kwa nini katika miaka ya karibuni machapisho yetu yamezungumzia mara chache sana masimulizi ya Biblia ambayo yalikuwa kivuli na ufananisho?

Biblia inasema kwamba baadhi ya watu walifananisha jambo fulani kubwa zaidi. Mfano mmoja unapatikana kwenye Wagalatia 4:21-31. Lakini Biblia isipotaja chochote, ni afadhali kutowazia au kukata shauri kwamba mtu au kitu fulani ni kivuli au ufananisho wa kingine. Hata hivyo, tunaweza kujifunza mambo muhimu kutoka kwa watu na matukio yanayotajwa katika Biblia. (Rom. 15:4)—3/15, ukurasa wa 17-18.

Kwa nini tuvutiwe na kipande cha hati za mafunjo kilichovumbuliwa kwenye rundo la takataka huko Misri?

Hati fulani ilipatikana katika karne iliyopita ikiwa na visehemu vya Injili ya Yohana. Huenda iliandikwa karne chache baada ya Yohana kuandika kitabu chake, na mambo yaliyomo yanathibitisha usahihi wa maandishi tuliyonayo sasa, na hivyo kukazia kwamba habari tunayosoma katika Biblia ni yenye kutegemeka.—4/1, ukurasa wa 10-11.

Kwa nini ni mpango wenye upendo kumtenga na ushirika mkosaji asiyetubu?

Biblia inataja hatua hiyo nzito ya kutenga na ushirika, nayo inaweza kuwa na matokeo mazuri. (1 Kor. 5:11-13) Inalitukuza jina la Mungu, inalinda usafi wa kutaniko, na inaweza kumsaidia mkosaji arudiwe na fahamu.—4/15, ukurasa wa 29-30.