Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HABARI KUU | JINSI YA KUKABILIANA NA MAHANGAIKO

Mahangaiko Yako Kila Mahali!

Mahangaiko Yako Kila Mahali!

“Nilienda kununua chakula lakini nikapata tu biskuti iliyouzwa mara 10,000 zaidi ya bei ya kawaida! Siku iliyofuata, maduka yote hayakuwa na chakula.” —Paul, Zimbabwe.

“Mume wangu aliniambia kwamba ananiacha. Nitakabiliana jinsi gani na usaliti huo? Nitafanya nini na watoto wangu?”—Janet, Marekani.

“Ving’ora vinapolia na mabomu kuanza kulipuka, mimi hukimbia na kujificha. Hata baada ya saa kadhaa kupita, mikono yangu bado hutetemeka.”—Alona, Israeli.

Tunaishi katika kipindi chenye mahangaiko, yaani, “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1) Watu wengi wanakabili hali ngumu za kiuchumi, kuvunjika kwa familia, vita, milipuko ya magonjwa hatari, na misiba ya asili au ile inayosababishwa na wanadamu. Pia, kuna mahangaiko ya kibinafsi kama vile: ‘Je, uvimbe uliogunduliwa katika mwili wangu ni kansa?’ ‘Wajukuu wangu watalelewa katika ulimwengu wenye tabia gani?’

Si mahangaiko yote ambayo ni mabaya. Kwa kawaida, sisi hupatwa na mkazo kabla ya kufanya mtihani, kufanya jambo fulani mbele ya watu, au usahili wa kazi. Pia, woga unaofaa hutusaidia kuepuka hatari. Hata hivyo, mahangaiko yanayopita kiasi au yanayoendelea kwa muda mrefu yana madhara. Uchunguzi uliofanywa hivi karibuni uliohusisha watu zaidi ya 68,000, unaonyesha kwamba hata mahangaiko ya kiasi yanaweza kusababisha kifo cha mapema. Kwa sababu hiyo, Yesu aliuliza hivi: “Ni nani kati yenu kwa kuhangaika anaweza kuongeza kipimo cha mkono mmoja kwenye uhai wake?” Kwa kweli, mahangaiko hayamsaidii mtu kuwa na maisha marefu. Kisha, Yesu akashauri hivi: “Acheni kuhangaika.” (Mathayo 6:25, 27) Lakini, hilo linawezekanaje?

Jibu la swali hilo linatia ndani kutumia hekima, kusitawisha imani ya kweli kuelekea Mungu, na kujenga tumaini linalotegemeka la wakati ujao. Hata ikiwa sasa hatukabili hali ngumu, huenda tukakabili hali hizo wakati ujao. Hivyo, acheni tuone jinsi kufuata hatua hizo kulivyomsaidia Paul, Janet, na Alona kushughulika na mahangaiko.