Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HABARI KUU | JINSI YA KUKABILIANA NA MAHANGAIKO

Mahangaiko Kuhusu Hatari

Mahangaiko Kuhusu Hatari

Alona, anasema hivi: “Ninaposikia mlio wa king’ora na milipuko ya mabomu, moyo wangu huenda mbio nami hukimbia ili kutafuta mahali pa kujificha. Hata hivyo, mimi huwa na wasiwasi hata ninapokuwa huko. Hali huwa mbaya hata zaidi ninapokuwa nje pasipo na mahali pa kujificha. Pindi fulani, nilipokuwa nikitembea mtaani nilianza kulia na nikashindwa kupumua. Ilinichukua saa kadhaa kutulia. Kisha, king’ora kikaanza kulia tena.”

Alona

Vita ni moja kati ya vyanzo vingi vya hatari. Kwa mfano, kujua kwamba wewe au mtu fulani unayempenda anakabili ugonjwa hatari, jambo hilo linaweza kushtua sana. Kwa wengine, hofu ya kitakachotokea wakati ujao inaweza kuwafanya wawe na mahangaiko. Huenda wakawaza hivi kwa wasiwasi: ‘Je, watoto wetu au wajukuu wetu, wataishi katika ulimwengu huu wenye vita, jeuri, uchafuzi, mabadiliko ya tabia ya nchi, na magonjwa ya mlipuko?’ Tunaweza kukabiliana jinsi gani na mahangaiko hayo?

Kujua kwamba mambo mabaya hutukia humsaidia, ‘mtu mwerevu ambaye ameuona msiba ajifiche.’ (Methali 27:12) Kama vile tunavyojitahidi kulinda afya yetu, tunaweza kuchukua hatua kulinda hali yetu ya kiakili na kihisia. Burudani zenye jeuri na ripoti za habari zilizojaa picha zinazotisha hutuongezea mahangaiko sisi na watoto wetu. Kuepuka mambo hayo hakumaanishi kwamba tunapuuza uhalisia wa mambo. Mungu hakuumba akili yetu ili kuwaza uovu. Badala yake, tunapaswa kujaza akili yetu “mambo yoyote yaliyo ya kweli,  . . .  uadilifu, . . . safi kiadili, . . . na ya kupendeka.” Tukifanya hivyo “Mungu wa amani” atatupa amani ya moyoni na akilini.—Wafilipi 4:8, 9.

UMUHIMU WA SALA

Imani ya kweli hutusaidia kukabiliana na mahangaiko. Biblia hutuhimiza “kukesha kuhusiana na sala.” (1 Petro 4:7) Tunaweza kumwomba Mungu msaada, hekima na ujasiri ili tuweze kukabiliana vizuri na hali zetu, tukiwa na uhakika kwamba “yeye hutusikia kwa habari ya jambo lolote tunaloomba.”—1 Yohana 5:15.

Pamoja na mume wake, Avi

Biblia inaeleza kwamba si Mungu, bali Shetani ndiye “mtawala wa ulimwengu huu” na kwamba “ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu.” (Yohana 12:31; 1 Yohana 5:19) Hii ndiyo sababu Yesu alitufundisha tusali hivi: “Utukomboe kutokana na yule mwovu.” (Mathayo 6:13) “Ninaposikia mlio wa king’ora, mimi humwomba Yehova anisaidie kudhibiti hisia zangu,” anasema Alona. “Pia, mume wangu mpendwa husali pamoja nami. Sala husaidia sana.” Ni kama tu Biblia inavyosema: “Yehova yuko karibu na wote wanaomwitia, wote wanaomwitia yeye katika ukweli.”—Zaburi 145:18.

TUMAINI LETU LA WAKATI UJAO

Katika Mahubiri yake ya Mlimani, Yesu aliwafundisha wafuasi wake kusali hivi: “Ufalme wako na uje.” (Mathayo 6:10) Ufalme wa Mungu utaondoa kabisa mahangaiko. Kupitia Yesu, “Mkuu wa Amani,” Mungu ‘atakomesha vita mpaka kwenye mwisho wa dunia.’ (Isaya 9:6; Zaburi 46:9) “Naye [Mungu] hakika atafanya hukumu kati ya vikundi vingi vya watu . . . Hawatainua upanga, taifa juu ya taifa, wala hawatajifunza vita tena. . . . Wala hakutakuwa na mtu yeyote anayewatetemesha.” (Mika 4:3, 4) Familia zenye furaha ‘zitajenga nyumba na kukaa ndani yake, na hakika zitapanda mashamba ya mizabibu na kula matunda yake.’ (Isaya 65:21) “Na hakuna mkaaji atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa’”—Isaya 33:24.

Leo, licha ya jitihada mbalimbali, si rahisi mara zote kuzuia “tukio lisilotazamiwa” au kuepuka kuwa mahali pasipofaa na wakati usiofaa. (Mhubiri 9:11) Kama ilivyo kwa karne nyingi, vita, jeuri, na magonjwa yameendelea kuua watu wema. Watu hao wanatumaini gani?

Mamilioni ya watu, walio katika kumbukumbu ya Mungu, watafufuliwa ili waishi tena. Kwa sasa, wako salama katika kumbukumbu kamilifu ya Mungu, mpaka siku ambayo ‘wale wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho watatoka.’ (Yohana 5:28, 29) Biblia inapozungumzia kuhusu ufufuo, hutuhakikishia hivi: “Tumaini hilo tunalo kama nanga ya nafsi, likiwa hakika na imara.” (Waebrania 6:19) Mungu “ametoa uhakikisho kamili kwa watu wote kwa kuwa amemfufua [Yesu] kutoka kwa wafu.”—Matendo 17:31.

Kwa sasa, hata wale ambao hujitahidi kumpendeza Mungu wanakabili mahangaiko. Kwa kuchukua hatua zinazofaa, kumkaribia Mungu kupitia sala, na kujenga imani yetu kuhusu wakati ujao kupitia Biblia, Paul, Janet, na Alona wote wamekabiliana na mahangaiko yao kwa mafanikio. Kama ilivyo katika kisa chao, “Mungu anayetoa tumaini na awajaze ninyi shangwe yote na amani kwa kuamini kwenu.”—Waroma 15:13.