Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jitahidi Kuboresha Paradiso ya Kiroho

Jitahidi Kuboresha Paradiso ya Kiroho

“Nitapatukuza mahali pangu pa miguu.”—ISA. 60:13.

NYIMBO: 102, 75

1, 2. Maneno “kiti cha miguu” yanaweza kumaanisha nini katika Maandiko ya Kiebrania?

YEHOVA MUNGU alitangaza hivi: “Mbingu ni kiti changu cha ufalme, na dunia ni kiti cha miguu yangu.” (Isa. 66:1) Pia alisema hivi kuhusu “kiti cha miguu” yake: “Nitapatukuza mahali pangu pa miguu.” (Isa. 60:13) Anafanya hivyo jinsi gani? Na jambo hilo linamaanisha nini kwetu sisi tunaoishi kwenye “kiti cha miguu” cha Mungu?

2 Maneno “kiti cha miguu,” yanatumika pia kwa njia ya mfano katika Maandiko ya Kiebrania kufafanua hekalu lililotumiwa na Waisraeli. (1 Nya. 28:2; Zab. 132:7) Hekalu lilikuwa kituo cha ibada ya kweli duniani. Kwa sababu hiyo, lilikuwa lenye kupendeza sana machoni pa Yehova na lilipatukuza mahali pake pa miguu.

3. Hekalu kubwa la kiroho la Mungu ni nini, na lilianza lini?

3 Leo, kitovu cha ibada ya kweli si hekalu halisi. Badala yake, kuna hekalu la kiroho linalomtukuza Yehova kuliko jengo lolote lile. Hekalu hilo ni mpango unaowawezesha wanadamu kupatanishwa na Mungu kwa msingi wa ukuhani na dhabihu ya Yesu Kristo. Mpango huo ulianza mwaka wa 29 W.K. Yesu alipobatizwa na kutiwa mafuta kuwa Kuhani Mkuu katika hekalu kubwa la kiroho la Yehova.—Ebr. 9:11, 12.

4, 5. (a) Zaburi ya 99 inafafanuaje tamaa kubwa ya waabudu wa kweli wa Yehova? (b) Tunapaswa kujiuliza swali gani?

4 Tunamshukuru sana Yehova kwa mpango wa hekalu la kiroho. Tunamsifu kwa kuwajulisha watu jina lake na tunamtukuza kwa sababu ya zawadi bora sana ya fidia. Inasisimua sana kuona Wakristo wa kweli zaidi ya milioni nane wakimtukuza Yehova! Tofauti na baadhi ya wanadini wanaofikiri kimakosa kwamba watamsifu Mungu baada ya kuondoka duniani na kwenda mbinguni, Mashahidi wa Yehova wanatambua kwamba wanahitaji kumsifu Mungu sasa, wakiwa hapa hapa duniani.

5 Tunafuata mfano wa watumishi waaminifu wa Yehova wanaotajwa kwenye Zaburi 99:1-3, 5-7. (Soma.) Kama zaburi hiyo inavyoonyesha, Musa, Haruni, na Samweli waliunga mkono kabisa mpango wa ibada ya kweli katika siku zao. Leo, watiwa-mafuta wanatumikia kwa uaminifu katika ua wa hekalu la kiroho duniani kabla ya kwenda mbinguni ili kutumikia wakiwa makuhani pamoja na Yesu. Mamilioni ya “kondoo wengine” wanawaunga mkono kwa ushikamanifu. (Yoh. 10:16) Ingawa wana matumaini tofauti, vikundi vyote viwili vinamwabudu Yehova kwa umoja katika kiti cha miguu cha Mungu. Hata hivyo, kila mmoja wetu anapaswa kujiuliza hivi, ‘Je, ninaunga mkono kabisa mpango wa Yehova wa ibada safi?’

NI NANI WANAOTUMIKIA KATIKA HEKALU LA KIROHO LA MUNGU?

6, 7. Wakristo wa mapema walikabili tatizo gani, na ni nini kilichotokea miaka mingi baadaye?

6 Baada ya miaka isiyozidi mia moja tangu kuanzishwa kwa kutaniko la Kikristo, uasi-imani uliotabiriwa ulianza kusitawi. (Mdo. 20:28-30; 2 The. 2:3, 4) Baadaye, ikawa vigumu sana kuwatambua wale wanaomtumikia Mungu kikweli katika hekalu lake la kiroho. Miaka mingi ilipita kabla ya Yehova kufunua mambo kupitia Mfalme mpya anayetawala, Yesu Kristo.

7 Kufikia mwaka wa 1919, wale waliokubaliwa na Yehova na kutumikia katika hekalu la kiroho walitambuliwa waziwazi. Walikuwa wamesafishwa kiroho ili wamtumikie Mungu kwa njia inayokubalika zaidi. (Isa. 4:2, 3; Mal. 3:1-4) Maono ambayo Paulo aliona karne nyingi zilizopita yalianza kutimia kwa kadiri fulani.

8, 9. “Paradiso” ambayo Paulo aliiona katika maono inaweza kumaanisha nini?

8 Maono ya Paulo yanapatikana kwenye 2 Wakorintho 12:1-4. (Soma.) Maono ambayo Paulo aliona yanaelezwa kuwa ni ufunuo. Yalihusu tukio la wakati ujao, si jambo lililokuwepo katika siku za Paulo. Paulo aliona “paradiso” gani ‘aliponyakuliwa mpaka kwenye mbingu ya tatu’? Paradiso ambayo Paulo aliizungumzia ingekuwa na utimizo halisi, wa kiroho, na wa kimbingu, na wote ungetimizwa katika kipindi kimoja wakati ujao. Paradiso hiyo inaweza kumaanisha Paradiso halisi tunayotarajia hapa duniani. (Luka 23:43) Pia, inaweza kumaanisha paradiso ya kiroho ambayo tutaifurahia kikamili katika ulimwengu mpya. Isitoshe, inaweza kumaanisha hali nzuri katika “paradiso ya Mungu” mbinguni.—Ufu. 2:7.

9 Hata hivyo, kwa nini Paulo alisema kwamba alisikia “maneno yasiyoweza kutamkwa ambayo si halali mtu kuyasema”? Huo haukuwa wakati wa kueleza kwa kina mambo ya ajabu aliyokuwa ameona katika maono hayo. Lakini sasa tunaweza kueleza baraka ambazo watu wa Mungu wanazifurahia!

10. Je, “paradiso ya kiroho” ni sawa na “hekalu la kiroho”? Eleza.

10 Maneno “paradiso ya kiroho” yamekuwa msemo wa kawaida wa kitheokrasi. Msemo huo unafafanua mazingira au hali ya pekee ya kiroho inayotuwezesha kufurahia amani pamoja na Mungu na waumini wenzetu. Hilo halimaanishi kwamba “paradiso ya kiroho” ni sawa na “hekalu la kiroho.” Hekalu la kiroho ni mpango wa Mungu kwa ajili ya ibada ya kweli. Paradiso ya kiroho ni hali inayowatambulisha watu wenye kibali cha Mungu ambao wanatumikia katika hekalu lake la kiroho.—Mal. 3:18.

11. Yehova ameturuhusu kufanya jambo gani la pekee?

11 Inasisimua sana kujua kwamba tangu mwaka wa 1919, Yehova amewaruhusu wanadamu wasio wakamilifu washirikiane naye kusitawisha, kuimarisha, na kupanua paradiso ya kiroho duniani! Je, unashiriki katika kazi hiyo yenye kustaajabisha? Je, unajitahidi kufanya kazi na Yehova katika kutukuza ‘kiti chake cha miguu’?

TENGENEZO LA YEHOVA LINAZIDI KUBORESHWA

12. Tuna uhakika gani kuhusu utimizo wa andiko la Isaya 60:17? (Tazama picha kwenye ukurasa wa 7.)

12 Nabii Isaya alitabiri kwamba kungekuwa na mabadiliko mengi mazuri katika tengenezo la Yehova kama inavyoonyeshwa kwenye Isaya 60:17. (Soma.) Wale ambao ni wachanga au wapya katika kweli wamesoma au kusikia kuhusu mabadiliko hayo. Lakini ndugu na dada wengi wamepata nafasi ya pekee ya kushuhudia mabadiliko hayo. Si ajabu kwamba watumishi hao waaminifu wanasadiki kuwa Yehova analiongoza na kulielekeza tengenezo lake kupitia Mfalme wake anayetawala! Uhakika wao unategemea msingi thabiti. Maelezo yao ya kutoka moyoni yataimarisha imani yako na kukuchochea kumtumaini zaidi Yehova.

13. Andiko la Zaburi 48:12-14 linatupatia wajibu gani?

13 Haidhuru tumekuwa katika kweli kwa muda gani, tunapaswa kuwaeleza wengine kuhusu tengenezo la Yehova. Kuwa na paradiso ya kiroho katika ulimwengu mwovu, wenye ufisadi, na usio na upendo ni muujiza! Tunapaswa kukisimulia “kizazi cha wakati ujao” kuhusu uzuri wa tengenezo la Yehova, au “Sayuni,” na vilevile ukweli kuhusu paradiso ya kiroho.—Soma Zaburi 48:12-14.

14, 15. Ni marekebisho gani yaliyofanywa katika miaka ya 1970, na yamekuwa na manufaa gani?

14 Wale wenye umri mkubwa wameshuhudia kwa miaka mingi marekebisho ambayo yameboresha sehemu ya duniani ya tengenezo la Yehova. Wanakumbuka wakati ambapo kulikuwa na mtumishi wa kutaniko badala ya baraza la wazee, mtumishi wa ofisi ya tawi badala ya Halmashauri ya Tawi, na miongozo ilipotolewa na msimamizi wa Watch Tower Society badala ya Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova. Ingawa ndugu hao walikuwa na wasaidizi waaminifu, mtu mmoja hasa ndiye aliyewajibika kutoa uamuzi kutanikoni, katika ofisi za tawi, na makao makuu. Mabadiliko yalifanywa katika miaka ya 1970, usimamizi ulipowekwa chini ya vikundi vya wazee badala ya mtu mmoja.

15 Je, marekebisho hayo yamekuwa na manufaa? Ndiyo, na yana mantiki. Kwa nini? Kwa sababu yalitegemea kuelewa vizuri zaidi mpango ulio katika Maandiko. Badala ya mtu mmoja kusimamia kila kitu, sifa nzuri za wote ambao ni “zawadi katika wanadamu” zinalinufaisha tengenezo.—Efe. 4:8; Met. 24:6.

Yehova anawapatia watu kila mahali mwongozo wanaohitaji (Tazama fungu la 16 na 17)

16, 17. Umevutiwa na marekebisho gani ya karibuni, na kwa nini?

16 Fikiria pia marekebisho ya hivi karibuni, kama vile mabadiliko ya mwonekano na mambo yaliyomo katika machapisho yetu, na vilevile njia za kugawanya machapisho hayo. Katika huduma, tunafurahia sana kuwapatia watu machapisho yenye kuvutia na yanayogusa mioyo yao. Pia, tunapotumia teknolojia kueneza kweli, kama vile kutumia tovuti ya jw.org, tunamwiga Yehova kwa kuwasaidia watu kila mahali wapate mwongozo wanaohitaji sana maishani.

17 Hatuwezi kusahau pia marekebisho yaliyofanywa ili kutuwezesha kuwa na Ibada ya Familia au kuwa na wakati mwingi zaidi wa funzo la kibinafsi. Isitoshe, tunafurahia sana mabadiliko ambayo yamefanywa katika programu za makusanyiko. Mara nyingi tunasema kwamba makusanyiko hayo yanazidi kuwa bora kila mwaka! Pia, tunafurahia sana mazoezi yanayotolewa katika shule mbalimbali za kitheokrasi. Marekebisho hayo yanaonyesha wazi kwamba Yehova analiongoza tengenezo lake na anaboresha hatua kwa hatua uzuri wa paradiso ya kiroho tunayoifurahia sasa.

MCHANGO WAKO KATIKA PARADISO YA KIROHO

18, 19. Tunawezaje kuchangia uzuri wa paradiso ya kiroho?

18 Ni heshima kubwa kuruhusiwa na Yehova kuchangia uzuri wa paradiso ya kiroho. Tunafanya hivyo tunapohubiri kwa bidii habari njema ya Ufalme na kuwafundisha watu. Kila mara tunapomsaidia mtu kuwa Mkristo aliyejiweka wakfu, tunachangia kupanua paradiso ya kiroho.—Isa. 26:15; 54:2.

19 Pia, tunaweza kuchangia uzuri wa paradiso ya kiroho kwa kujitahidi kuboresha utu wetu wa Kikristo. Hilo litafanya watazamaji wavutiwe zaidi na paradiso hiyo. Kwa kawaida si ujuzi wa Biblia pekee unaowavuta watu kwenye tengenezo kwa mara ya kwanza na kuwafanya wampende Mungu na Kristo. Mara nyingi watu huvutiwa na mwenendo wetu mzuri na wenye amani.

Unaweza kuchangia kupanua paradiso ya kiroho (Tazama fungu la 18 na 19)

20. Kulingana na Methali 14:35, tunapaswa kuwa na tamaa ya kufanya nini?

20 Bila shaka, Yehova na Yesu wanafurahi sana wanapoona uzuri wa paradiso ya kiroho leo! Furaha tunayopata kwa kuchangia uzuri wa paradiso hiyo ni kionjo tu cha furaha tutakayopata tutakaposhiriki kuigeuza dunia kuwa paradiso halisi wakati ujao. Sikuzote na tukumbuke maneno haya ya Methali 14:35: “Furaha ya mfalme imo katika mtumishi anayetenda kwa ufahamu.” Acheni tuendelee kutenda kwa ufahamu tunapojitahidi kuchangia uzuri wa paradiso ya kiroho!