Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Shikamana na Ufalme wa Mungu

Shikamana na Ufalme wa Mungu

“Wao si sehemu ya ulimwengu.”—YOH. 17:16.

NYIMBO: 63, 129

1, 2. (a) Kwa nini ni muhimu tuwe washikamanifu kwa Mungu? Na ushikamanifu unahusianaje na suala la kutounga mkono upande wowote? (Tazama picha kwenye ukurasa huu.) (b) Watu wanaonyesha ushikamanifu wa aina gani, na kumekuwa na matokeo gani?

SIKUZOTE suala la ushikamanifu na kutounga mkono upande wowote limekuwa changamoto kwa Wakristo wa kweli. Kwa nini? Kwa sababu wale wote waliojiweka wakfu kwa Yehova walimwahidi kumpenda, kumtii, na kuwa washikamanifu. (1 Yoh. 5:3) Tunatii viwango vya uadilifu vya Yehova mahali popote tunapoishi, haidhuru malezi, taifa, au utamaduni wetu. Tunashikamana na Yehova na Ufalme wake kuliko kitu kingine chochote. (Mt. 6:33) Hivyo, hatupaswi kuunga mkono upande wowote katika migogoro na mabishano ya ulimwengu huu.—Isa. 2:4; soma Yohana 17:11, 15, 16.

2 Watu ambao si Mashahidi wa Yehova wanaweza kuwa washikamanifu sana kwa nchi, kabila, utamaduni, au timu zao za taifa. Inasikitisha kwamba jambo hilo limesababisha mashindano, chuki, na katika visa fulani, limesababisha umwagaji wa damu na mauaji ya halaiki. Ingawa hatushiriki katika migogoro hiyo, inaweza kutuathiri sisi au familia zetu, na wakati mwingine huenda ikatusababishia madhara makubwa. Kwa kuwa Mungu ametuumba tukiwa na hisia za kupenda haki, huenda tukakasirika serikali za wanadamu zinapofanya maamuzi yasiyozingatia haki na usawa. (Mwa. 1:27; Kum. 32:4) Tutatendaje tunapokabili hali hiyo? Inaweza kuwa rahisi sana kuunga mkono upande fulani na kushiriki katika mabishano ya ulimwengu huu.

3, 4. (a) Kwa nini Wakristo hawaungi mkono upande wowote katika mabishano ya ulimwengu huu? (b) Tutachunguza nini katika makala hii?

3 Huenda mashirika ya kijamii yakawashawishi raia waunge mkono upande fulani migogoro inapozuka. Wakristo wa kweli hawaungi mkono upande wowote. Hatujihusishi katika mabishano ya kisiasa ya ulimwengu huu, wala hatuendi vitani. (Mt. 26:52) Hatuamini kwamba sehemu fulani ya ulimwengu wa Shetani ni bora zaidi kuliko nyingine. (2 Kor. 2:11) Kwa kutokuwa sehemu ya ulimwengu, tunajiepusha na migogoro ya ulimwengu huu.—Soma Yohana 15:18, 19.

4 Kwa kuwa sisi si wakamilifu, huenda baadhi yetu bado tunapambana ili kung’oa mitazamo tuliyokuwa nayo zamani ambayo inaweza kusababisha migawanyiko. (Yer. 17:9; Efe. 4:22-24) Hivyo, katika makala hii tutachunguza baadhi ya kanuni zinazoweza kutusaidia kushinda mitazamo hiyo. Pia, tutaona jinsi tunavyoweza kuzoeza akili na dhamiri yetu ili tuwe washikamanifu kwa Ufalme wa Mungu.

KWA NINI HATUUNGI MKONO UPANDE WOWOTE KATIKA MASUALA YA ULIMWENGU?

5, 6. Yesu alikuwa na maoni gani kuhusu tofauti za kijamii, na kwa nini?

5 Ikiwa nyakati fulani unaona ni vigumu kutounga mkono upande wowote katika hali fulani, inafaa ujiulize hivi, ‘Angekuwa Yesu angefanya nini?’ Yesu alizaliwa katika taifa lililokuwa na watu kutoka maeneo mbalimbali, kama vile Yudea, Galilaya, Samaria, na maeneo mengine. Masimulizi ya Biblia yanaonyesha kwamba kulikuwa na migogoro kati ya watu wa maeneo hayo. (Yoh. 4:9) Kulikuwa na migogoro kati ya Mafarisayo na Masadukayo (Mdo. 23:6-9), watu wa kawaida na wakusanya kodi (Mt. 9:11), wasomi wa Sheria na wale ambao hawakuwa na elimu hiyo. (Yoh. 7:49) Katika karne ya kwanza, Wayahudi waliwachukia sana Waroma. Yesu aliitetea kweli na alijua kuwa ukombozi ungetoka kwa Wayahudi. Hata hivyo, hakuwafundisha kamwe wanafunzi wake kwamba wao ni bora kuliko wengine. (Yoh. 4:22) Badala yake, aliwahimiza wawapende watu wote.—Luka 10:27.

6 Kwa nini Yesu hakuona kikundi kimoja cha watu kuwa bora kuliko kingine? Kwa sababu yeye na Baba yake hawaungi mkono upande wowote katika mabishano ya ulimwengu huu. Yehova alipomuumba mwanaume na mwanamke, alikusudia kwamba waijaze dunia. (Mwa. 1:27, 28) Mungu aliwaumba wanadamu kwa njia ambayo wangeweza kutokeza watu wa rangi tofauti-tofauti. Hivyo, Yehova na Yesu hawafikiri kwamba rangi, taifa, au lugha fulani ni bora kuliko nyingine. (Mdo. 10:34, 35; Ufu. 7:9, 13, 14) Tunapaswa kuiga mfano wao bora.—Mt. 5:43-48.

7, 8. (a) Wakristo wanapaswa kuunga mkono suala gani? (b) Wakristo wanapaswa kukumbuka nini kuhusu suluhisho la matatizo ya wanadamu?

7 Tunapaswa kuunga mkono enzi kuu ya Yehova kwa kuwa yeye ndiye Mtawala wetu. Matatizo yalianza katika bustani ya Edeni Shetani alipopinga utawala wa Yehova. Shetani alitaka watu waamini kwamba njia yake ya kufanya mambo ni nzuri zaidi kuliko ya Mungu. Yehova ametupa uhuru wa kuchagua. Je, unaunga mkono upande wa Yehova kwa kuchagua kutii sheria na viwango vyake badala ya kufanya mambo kwa njia yako? Je, unaamini kwamba Ufalme ndio suluhisho pekee la matatizo ya wanadamu? Au je, unaamini kwamba mwanadamu ana uwezo wa kujitawala?—Mwa. 3:4, 5.

8 Kwa mfano, ukiombwa utoe maoni kuhusu chama fulani cha siasa au kikundi fulani cha wanaharakati, utasema nini? Huenda baadhi ya vikundi hivyo vimejitahidi kwa unyofu kusuluhisha matatizo ya wanadamu. Hata hivyo, Wakristo wa kweli wanatambua kwamba Ufalme wa Mungu tu ndio unaweza kusuluhisha matatizo ya wanadamu na kuleta haki ya kweli. Tunapaswa kuacha mambo mikononi mwa Yehova. Isitoshe, ikiwa kila Mkristo angefanya jambo analofikiri kuwa ni bora, je, hilo halingesababisha migawanyiko katika makutaniko yetu?

9. Ni tatizo gani lilitokea katika kutaniko la Korintho, lakini mtume Paulo alipendekeza suluhisho gani?

9 Fikiria jinsi ambavyo Wakristo fulani katika karne ya kwanza walitenda mabishano yalipotokea ndani ya kutaniko la Korintho. Wakristo fulani walisema: “‘Mimi ni wa Paulo,’ ‘Lakini mimi ni wa Apolo,’ ‘Lakini mimi ni wa Kefa,’ ‘Lakini mimi ni wa Kristo.’” Jambo hilo lilimkasirisha sana mtume Paulo. Akawauliza hivi: Je, “Kristo amegawanyika”? Ni nini kingesuluhisha tatizo hilo lililohatarisha amani ya kutaniko? Paulo aliwahimiza hivi Wakristo wenzake: “Sasa nawahimiza ninyi, akina ndugu, kupitia jina la Bwana wetu Yesu Kristo kwamba nyote mseme kwa upatano, na kwamba kusiwe na migawanyiko katikati yenu, bali kwamba muunganishwe vema katika akili ileile na katika njia ileile ya kufikiri.” Vivyo hivyo, hakupaswi kuwa na migawanyiko yoyote katika kutaniko la Kikristo leo.—1 Kor. 1:10-13; soma Waroma 16:17, 18.

10. Mtume Paulo alitumia mfano gani ili kuwaonyesha Wakristo uhitaji wa kutounga mkono upande wowote?

10 Paulo aliwahimiza Wakristo watiwa-mafuta wakazie fikira uraia wao wa mbinguni badala ya vitu vilivyo duniani. (Flp. 3:17-20) * Walipaswa kutenda kama mabalozi wa Kristo. Mabalozi hawaingilii mambo ya ndani ya nchi walikotumwa. Wao ni washikamanifu kwa nchi zao. (2 Kor. 5:20) Wakristo wenye tumaini la kuishi duniani pia ni raia wa Ufalme wa Mungu, hivyo hawaungi mkono upande wowote katika migogoro ya ulimwengu huu.

JIZOEZE KUWA MSHIKAMANIFU KWA YEHOVA

11, 12. (a) Tunapaswa kuepuka mtazamo gani ili tuendelee kuwa washikamanifu kwa Ufalme wa Mungu? (b) Mkristo mmoja alikabili tatizo gani, naye alilishughulikiaje?

11 Katika sehemu mbalimbali duniani, watu wa jamii moja huunganishwa na historia, desturi, na lugha; nao hujivunia sana mambo hayo. Katika hali kama hizo, Wakristo wanapaswa kuzoeza akili na dhamiri zao ili watende kwa njia inayofaa masuala ya kuunga mkono upande fulani yanapozuka. Wanawezaje kufanya hivyo?

12 Kwa mfano, mfikirie Mirjeta * kutoka katika eneo ambalo zamani liliitwa Yugoslavia. Alilelewa kwenye eneo ambalo watu waliwachukia Waserbia. Alipojifunza kwamba Yehova hana ubaguzi, na Shetani ndiye chanzo cha matatizo ya kijamii, alijitahidi sana kung’oa hisia za uzalendo. Hata hivyo, machafuko ya kikabila yalipozuka katika eneo lao, hisia za chuki alizokuwa nazo awali ziliibuka tena. Ikawa vigumu kwake kuwahubiria Waserbia. Lakini alitambua kwamba hisia hizo mbaya hazingeondoka kimuujiza. Alimwomba Yehova amsaidie kushinda tatizo hilo na pia kuanza upainia wa kawaida. Anasema hivi: “Nimegundua kwamba kukazia fikira huduma ni msaada bora zaidi. Nikiwa katika huduma, najitahidi kuiga sifa nzuri za Yehova, na hilo limenisaidia kuondoa hisia zisizofaa.”

13. (a) Ni jambo gani halikumfurahisha Zoila, naye alitendaje? (b) Kisa cha Zoila kinatufundisha nini?

13 Mfikirie pia Zoila ambaye alizaliwa nchini Mexico lakini sasa anahudhuria mikutano katika kutaniko fulani barani Ulaya. Alitambua kwamba ndugu fulani kutanikoni ambao walitoka sehemu nyingine za Amerika walidhihaki utamaduni, muziki, na pia nchi aliyozaliwa. Ungekuwa wewe ungefanya nini? Jambo hilo halikumfurahisha Zoila. Inapendeza kwamba alimwomba Yehova amsaidie ili asikasirike. Ni kweli kwamba baadhi yetu bado tunapambana na tatizo kama hilo. Tusingependa kamwe kusema au kufanya jambo lolote linaloweza kuchochea migawanyiko au hisia za uzalendo miongoni mwa ndugu na dada zetu.—Rom. 14:19; 2 Kor. 6:3.

14. Wakristo wanawezaje kuzoeza akili na dhamiri yao ili waendelee kuwa washikamanifu kwa Yehova?

14 Je, mazingira au malezi yako yamekufanya uhisi kwamba sehemu au taifa fulani ni bora kuliko lingine? Je, bado una hisia kama hizo? Wakristo hawapaswi kuruhusu hisia za uzalendo ziathiri jinsi wanavyowaona wengine. Lakini namna gani ukitambua kwamba una maoni yasiyofaa kuelekea watu wa taifa, utamaduni, lugha, au rangi nyingine? Basi ni muhimu kutafakari maoni ya Yehova kuhusu uzalendo na ubaguzi. Unaweza kufanya utafiti kuhusu mambo hayo wakati wa funzo lako la kibinafsi au ibada ya familia. Kisha mwombe Yehova akusaidie uwe na maoni kama yake kuhusiana na mambo hayo.—Soma Waroma 12:2.

Tunahitaji kukabiliana na vitisho kwa uthabiti ili tuendelee kuwa washikamanifu kwa Yehova (Tazama fungu la 15 na 16)

15, 16. (a) Watu wengine hutendaje tunapokuwa na msimamo tofauti? (b) Wazazi wanaweza kuwasaidiaje watoto wao waendelee kuwa washikamanifu kwa Yehova?

15 Wakati wowote watumishi wa Yehova wanaweza kukabili hali itakayowalazimu kuwa na msimamo tofauti na wafanyakazi wenzao, wanafunzi, majirani, watu wa ukoo, au watu wengine. (1 Pet. 2:19) Hata hivyo, tunapaswa kuwa tofauti. Yesu alituonya kwamba ulimwengu ungetuchukia kwa sababu ya msimamo wetu. Kwa hiyo hatupaswi kushangaa jambo hilo linapotokea. Wapinzani wetu hawaelewi umuhimu wa masuala yanayohusika katika msimamo wa Kikristo wa kutounga mkono upande wowote. Lakini masuala hayo ni ya muhimu sana kwetu.

16 Tunahitaji kukabiliana na vitisho kwa uthabiti ili tuendelee kuwa washikamanifu kwa Yehova. (Dan. 3:16-18) Watu wa umri mbalimbali wanaweza kunaswa na mtego wa kuwaogopa wanadamu, lakini huenda ikawa vigumu zaidi kwa vijana kuwa tofauti na wengine. Ikiwa watoto wako wanakabili masuala kama vile kusalimu bendera au sherehe za kizalendo, usisite kuwasaidia. Tumia wakati wa Ibada ya Familia kuwasaidia watoto wako waelewe masuala yanayohusika ili waweze kukabiliana na matatizo hayo kwa ujasiri. Wafundishe jinsi ya kuitetea imani yao waziwazi na kwa heshima. (Rom. 1:16) Ikihitajika, wasaidie watoto wako kwa kuzungumza na walimu wao kuhusu mambo hayo.

FURAHIA UUMBAJI WOTE WA YEHOVA!

17. Tunapaswa kuepuka mtazamo gani, na kwa nini?

17 Ni jambo la kawaida kupenda chakula, utamaduni, lugha, na mahali tulipozaliwa. Hata hivyo, ni lazima tuepuke mtazamo wa “changu ni bora kuliko cha wengine.” Yehova ameumba vitu vya aina mbalimbali ili tuvifurahie. (Zab. 104:24; Ufu. 4:11) Basi kwa nini tusisitize kwamba njia moja ya kufanya mambo ni bora kuliko nyingine?

18. Kwa nini ni muhimu tuwaone wengine kama Yehova anavyowaona?

18 Mungu anataka watu wa namna zote wapate ujuzi sahihi na uzima wa milele. (Yoh. 3:16; 1 Tim. 2:3, 4) Tunafurahia maisha na kuendeleza umoja wa Kikristo tunapokuwa tayari kusikiliza maoni mazuri ya wengine na kuyakubali, hata kama yanatofautiana na maoni yetu. Ili tuendelee kuwa washikamanifu kwa Yehova ni lazima tuepuke kujihusisha katika mabishano ya ulimwengu huu. Migawanyiko haina nafasi katikati yetu. Tunamshukuru sana Yehova kwa kutuweka huru kutokana na roho ya migawanyiko, majivuno, na mashindano ambayo inatawala katika ulimwengu wa Shetani. Acheni tuazimie kusitawisha mtazamo wa amani kama ule unaotajwa na mtunga-zaburi: “Tazama! Jinsi ilivyo vyema na jinsi inavyopendeza ndugu kukaa pamoja kwa umoja!”—Zab. 133:1.

^ fu. 10 Jiji la Filipi lilikuwa koloni la Roma. Baadhi ya washiriki wa kutaniko huenda walikuwa na aina fulani ya uraia wa Roma ambao ungewawezesha kupata haki fulani kuliko ndugu zao.

^ fu. 12 Baadhi ya majina yamebadilishwa.