Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Hapa Ni Mahali Petu pa Ibada

Hapa Ni Mahali Petu pa Ibada

“Bidii kwa ajili ya nyumba yako itanila.”—YOH. 2:17.

NYIMBO: 127, 118

1, 2. (a) Zamani, watumishi wa Mungu walitumia mahali gani kumwabudu Yehova? (b) Yesu alikuwa na maoni gani kuelekea hekalu la Yerusalemu? (c) Tutazungumzia nini katika makala hii?

TANGU zamani, watumishi wa Mungu wamekuwa na mahali kwa ajili ya ibada safi. Inaelekea Abeli alijenga madhabahu alipomtolea Mungu dhabihu. (Mwa. 4:3, 4) Pia Noa, Abrahamu, Isaka, Yakobo, na Musa walijenga madhabahu. (Mwa. 8:20; 12:7; 26:25; 35:1; Kut. 17:15) Yehova aliwaagiza Waisraeli wajenge maskani. (Kut. 25:8) Baadaye, walijenga hekalu kwa ajili ya ibada ya Yehova. (1 Fal. 8:27, 29) Baada ya kurudi kutoka uhamishoni Babiloni, Wayahudi walikusanyika kwa ukawaida kwenye masinagogi. (Marko 6:2; Yoh. 18:20; Mdo. 15:21) Wakristo wa mapema walikutana kwenye nyumba za washiriki wa kutaniko. (Mdo. 12:12; 1 Kor. 16:19) Leo, watu wa Yehova wanakutana ili kuelimishwa na kuabudu kwenye maelfu ya Majumba ya Ufalme duniani kote.

2 Yesu alilipenda na kuliheshimu sana hekalu la Yehova lililokuwa Yerusalemu. Jambo hilo liliwakumbusha wanafunzi wake kuhusu maneno haya ya mtunga-zaburi: “Bidii nyingi kwa ajili ya nyumba yako imenila.” (Zab. 69:9; Yoh. 2:17) Hakuna Jumba la Ufalme linaloweza kuitwa “nyumba ya Yehova” katika maana ileile ambayo hekalu la Yerusalemu liliitwa. (2 Nya. 5:13; 33:4) Hata hivyo, Biblia ina kanuni zinazotuonyesha jinsi tunavyopaswa kutumia na kuheshimu mahali petu pa ibada. Katika makala hii, tutazungumzia kanuni za Biblia zinazotufundisha jinsi tunavyopaswa kujiendesha, kugharimia, na kudumisha Jumba letu la Ufalme. *

HESHIMU IBADA SAFI

3-5. Jumba la Ufalme ni nini, na tunapaswa kuwa na maoni gani kuhusiana na mikutano yetu?

3 Jumba la Ufalme ni kitovu cha ibada safi. Baadhi ya mambo ambayo Yehova hutumia kutulisha kiroho ni mikutano ya kila juma inayofanywa kwenye Jumba la Ufalme. Katika mikutano hiyo tunaburudishwa kiroho na kupata maagizo tunayohitaji. Wale wote wanaohudhuria mikutano hiyo wanaonyesha kwamba wamekubali mwaliko wa Yehova na Mwana wake. Hatupaswi kamwe kupuuza mwaliko wa kula katika “meza ya Yehova.”—1 Kor. 10:21.

4 Yehova anaona nafasi za kuabudu na kutiana moyo kuwa muhimu sana hivi kwamba alimwongoza mtume Paulo atuhimize tuendelee kukusanyika pamoja. (Soma Waebrania 10:24, 25.) Kwa kuwa tunamheshimu Yehova, hatutakosa mikutano ya Kikristo pasipo sababu ya msingi. Tunaweza kuonyesha kwamba tunamshukuru Yehova na kuthamini mikutano kwa kutayarisha na kushiriki kikamili.—Zab. 22:22.

5 Maoni yetu kuhusu Jumba la Ufalme, yaani, jengo lenyewe na shughuli za kiroho zinazofanywa hapo, yanapaswa kuonyesha kwamba tunaheshimu mahali hapo. Je, si kweli kwamba maoni yetu yanafunua hisia zetu kuelekea jina la Mungu, ambalo sikuzote linaonekana kwenye kibao cha Jumba la Ufalme?—Linganisha na 1 Wafalme 8:17.

6. Watu wamesema nini kuhusu Majumba yetu ya Ufalme na wale wanaohudhuria mikutano? (Tazama picha kwenye ukurasa wa 27.)

6 Watu ambao si Mashahidi wanaona tunapoheshimu mahali petu pa ibada. Kwa mfano, mwanaume mmoja nchini Uturuki alisema hivi: “Usafi na utaratibu nilioona kwenye Jumba la Ufalme ulinivutia sana. Watu walikuwa wamevaa vizuri, wenye tabasamu, na walinisalimia kwa shauku. Jambo hilo lilinivutia sana.” Mwanaume huyo alianza kuhudhuria mikutano kwa ukawaida, na baada ya muda akabatizwa. Katika jiji moja nchini Indonesia, kutaniko liliwaalika viongozi wa serikali na majirani ili waone Jumba lao jipya la Ufalme kabla halijawekwa wakfu. Meya wa eneo hilo alihudhuria. Alivutiwa sana na ubora wa jengo, ubunifu wake, na bustani maridadi. Alisema hivi: “Usafi wa jumba hili unaonyesha kwamba mna imani yenye nguvu.”

Matendo yetu yanaweza kuonyesha kwamba hatumheshimu Mungu (Tazama fungu la 7 na 8)

7, 8. Wale wanaohudhuria mikutano ya Kikristo wanapaswa kukumbuka mambo gani muhimu?

7 Tunaonyesha kwamba tunamheshimu Yehova aliyetualika katika mikutano ya Kikristo kwa kuvaa na kujipamba kwa njia inayofaa, na vilevile kuwa wenye adabu. Heshima inahusisha pia kuwa na kiasi. Imeonekana kwamba baadhi ya watu wana msimamo mkali kuhusu namna ya kujiendesha tunapohudhuria mikutano ya kutaniko huku wengine wakijiendesha kwa njia isiyofaa katika Jumba la Ufalme. Ni wazi kwamba Yehova anataka watumishi wake na wageni waalikwa wafurahie wanapokuwa Jumba la Ufalme. Hata hivyo, tusingependa kuonyesha utovu wa nidhamu kwa kuvaa nguo zisizofaa, kutuma ujumbe, kula na kunywa, au kuzungumza wakati wa mikutano. Wazazi wanapaswa kuwafundisha watoto wao kwamba Jumba la Ufalme si mahali pa kukimbia-kimbia au kucheza.—Mhu. 3:1.

8 Yesu alipoona watu wakifanya biashara katika hekalu la Mungu, alikasirika sana naye akawafukuza. (Yoh. 2:13-17) Vivyo hivyo, leo tunamwabudu Yehova na kuelimishwa mambo ya kiroho katika Majumba ya Ufalme. Hivyo basi, shughuli yoyote ya kibiashara haipaswi kufanywa hapo.—Linganisha na Nehemia 13:7, 8.

KUJENGA NA KUGHARIMIA MAJUMBA YA UFALME

9, 10. (a) Majumba ya Ufalme hujengwa na kugharimiwa jinsi gani? Na kumekuwa na matokeo gani?(b) Ni mpango gani ambao umeyasaidia makutaniko yasiyo na uwezo wa kujijengea Majumba ya Ufalme?

9 Tengenezo la Yehova limejitahidi sana kujenga na kugharimia Majumba ya Ufalme. Ubunifu, ujenzi, na ukarabati wa majengo hayo hufanywa na wajitoleaji. Kumekuwa na matokeo gani? Tangu Novemba 1, 1999, zaidi ya Majumba ya Ufalme 28,000 yamejengwa duniani kote. Hilo linamaanisha kwamba kwa wastani Majumba matano ya Ufalme yamejengwa kila siku ndani ya miaka 15 iliyopita.

10 Jitihada nyingi hufanywa ili kutegemeza ujenzi wa Majumba ya Ufalme mahali penye uhitaji. Mpango huo unategemea kanuni ya Maandiko inayoonyesha kwamba ziada ya watu fulani inaweza kujazia upungufu wa wengine ili “usawazisho uwepo.” (Soma 2 Wakorintho 8:13-15.) Kwa hiyo, vituo vya ibada safi vimejengwa kwa ajili ya makutaniko ambayo huenda hayangeweza kujijengea Majumba ya Ufalme.

11. Ndugu fulani walisema nini kuhusu Jumba lao jipya la Ufalme, na hilo linakufanya uhisije?

11 Kutaniko moja nchini Kosta Rika lililofaidika na mpango huo, liliandika hivi: “Tunaposimama mbele ya Jumba la Ufalme, tunahisi ni kama tuko ndotoni! Hatuamini macho yetu. Jumba letu maridadi lilikamilika kabisa ndani ya siku nane tu! Ujenzi huo uliwezekana kwa sababu ya baraka za Yehova, mipango ya tengenezo lake, na msaada wa ndugu zetu wapendwa. Kwa kweli, mahali hapa pa ibada ni zawadi yenye thamani sana kutoka kwa Yehova. Tunafurahia sana.” Je, hufurahi kusikia maelezo ya shukrani kama hayo kwa ajili ya Majumba mapya ya Ufalme, na kujua kwamba maelfu ya ndugu zetu ulimwenguni pote hupata shangwe ya aina hiyo? Hii ni kazi ya Yehova, ndiyo sababu watu wengi wenye tamaa ya kumjua Muumba wetu mwenye upendo, humiminika kwenye Majumba ya Ufalme mara tu majumba hayo yanapokamilika.—Zab. 127:1.

12. Unaweza kusaidiaje ujenzi wa Majumba ya Ufalme?

12 Ndugu na dada wengi wamepata shangwe kubwa kwa kushiriki katika ujenzi wa Majumba ya Ufalme. Iwe tunaweza kushiriki katika ujenzi au la, sisi sote tunaweza kutegemeza miradi hiyo kupitia michango yetu. Bidii kwa ajili ya ibada safi iliwachochea watu wa Mungu kuchangia miradi ya kitheokrasi katika nyakati za Biblia, na ndivyo ilivyo leo pia. Tunapofanya hivyo tunamtukuza Yehova.—Kut. 25:2; 2 Kor. 9:7.

USAFI WA JUMBA LA UFALME

13, 14. Ni kanuni gani za Biblia zinaonyesha kwamba tunapaswa kudumisha usafi na utaratibu wa Jumba la Ufalme?

13 Tunamwabudu Mungu msafi na mtakatifu ambaye anataka tuwe wenye utaratibu. Hivyo, tunapaswa kudumisha usafi na utaratibu wa Jumba letu la Ufalme. (Soma 1 Wakorintho 14:33, 40.) Katika Biblia, utakatifu na usafi wa kiroho unahusianishwa na usafi wa kimwili. (Ufu. 19:8) Hivyo, ikiwa watu wanatamani kupata kibali cha Yehova, ni lazima wadumishe usafi.

14 Kupatana na kanuni hizo, kudumisha usafi wa Jumba letu la Ufalme kunafanya tujivunie kuwakaribisha watu kwenye mikutano yetu. Wataona kuwa tunamwabudu Mungu mtakatifu ambaye hivi karibuni ataifanya dunia iwe paradiso maridadi.—Isa. 6:1-3; Ufu. 11:18.

15, 16. (a) Kwa nini inaweza kuwa vigumu kudumisha usafi wa Jumba la Ufalme? Lakini kwa nini usafi ni muhimu? (b) Kuna mipango gani ya usafi katika Jumba lenu la Ufalme, na kila mmoja wetu ana fursa gani?

15 Watu wana maoni tofauti kuhusu usafi. Kwa nini? Huenda ni kwa sababu ya malezi. Baadhi ya watu wanaishi kwenye maeneo yenye vumbi au barabara mbaya na zenye matope. Wengine hawana maji ya kutosha au vifaa vya usafi. Haidhuru watu wana mtazamo au hali gani, Jumba letu la Ufalme linapaswa kuwa safi, kwa kuwa ni mahali pa ibada safi panapoitwa kwa jina la Yehova.—Kum. 23:14.

16 Ikiwa tunataka Jumba letu la Ufalme liwe safi, tunahitaji kuwa na utaratibu. Kila baraza la wazee linahitaji kuhakikisha kwamba kuna ratiba ya usafi na vifaa vya kutosha kwa ajili ya kudumisha mwonekano mzuri wa mahali petu pa ibada. Usafi mwingine unahitaji kufanywa kila baada ya mkutano, na mwingine unaweza kufanywa kila baada ya kipindi fulani cha wakati. Hilo linahitaji kuwe na utaratibu na uangalizi mzuri ili kuhakikisha kwamba usafi unafanywa kikamili. Washiriki wote wa kutaniko wana fursa ya pekee ya kushirikiana katika kazi hiyo.

KUDUMISHA MAHALI PETU PA IBADA

17, 18. (a) Tunajifunza nini kutoka kwa watumishi wa Yehova wa zamani kuhusiana na udumishaji wa mahali pa ibada safi? (b) Kwa nini tunapaswa kudumisha Jumba la Ufalme?

17 Watumishi wa Yehova hujitahidi sana kudumisha mahali pao pa ibada kwa kufanya ukarabati unaohitajika. Kwa mfano, Mfalme Yehoashi wa Yuda aliwaagiza makuhani watumie michango iliyotolewa kwenye nyumba ya Yehova ‘kurekebisha mipasuko ya nyumba popote palipopatikana mpasuko wowote.’ (2 Fal. 12:4, 5) Zaidi ya miaka 200 baadaye, Mfalme Yosia alitumia pia michango ya hekalu kugharimia ukarabati muhimu.—Soma 2 Mambo ya Nyakati 34:9-11.

18 Ofisi za tawi zinaripoti kwamba katika nchi fulani, watu hawana mazoea ya kudumisha vifaa au majengo. Huenda ni watu wachache katika nchi hizo wana vifaa au wanajua jinsi ya kufanya hivyo. Lakini tukipuuza udumishaji wa Jumba la Ufalme, matokeo ni kwamba jengo litaanza kuchakaa na halitatoa ushahidi mzuri katika jamii. Kwa upande mwingine, washiriki wote wa kutaniko wanapofanya kila wawezalo ili kudumisha Jumba la Ufalme, hilo linamtukuza Yehova na kuokoa pesa zinazochangwa na waumini wenzetu.

Udumishaji na usafi wa Jumba la Ufalme haupaswi kupuuzwa (Tazama fungu la 16 na 18)

19. Umeazimia kufanya nini kuhusiana na majengo tunayotumia kwa ajili ya ibada safi?

19 Jumba la Ufalme ni jengo lililowekwa wakfu kwa Yehova. Hivyo, si mali ya mtu au kutaniko fulani, haidhuru hati- miliki inatumia jina gani. Kanuni za Kikristo zinaonyesha kwamba tunapaswa kushirikiana kikamili ili kuhakikisha jengo hilo linatimiza kusudi lake. Watu wote kutanikoni wanaweza kuonyesha kwamba wanaheshimu mahali petu pa ibada kwa kuchangia ujenzi wa majumba mapya, na kutumia wakati na nguvu zao kudumisha na kusafisha Jumba la Ufalme. Kwa kuunga mkono jitihada hizo, tunaonyesha kwamba tuna bidii kwa ajili ya mahali pa ibada safi ya Yehova, kama Yesu.—Yoh. 2:17.

^ fu. 2 Ingawa makala hii inazungumzia hasa Majumba ya Ufalme, kanuni zinazotajwa zinahusu pia Majumba ya Kusanyiko na majengo mengine yanayotumika kwa ajili ya ibada safi.