Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SIMULIZI LA MAISHA

‘Visiwa na Vishangilie’

‘Visiwa na Vishangilie’

Ilikuwa siku ambayo sitaisahau. Nilikuwa na ndugu kadhaa kutoka sehemu mbalimbali duniani, na tulisubiri katika chumba cha mikutano cha Baraza Linaloongoza tukiwa na wasiwasi mwingi. Washiriki wa Halmashauri ya Uandikaji walikuwa wanakaribia kuingia, na tulipewa mgawo wa kutoa ripoti kuhusu matatizo yanayowakabili watafsiri. Katika majuma machache yaliyotangulia, tulichunguza matatizo ambayo watafsiri walikabili, na sasa tulipaswa kutoa mapendekezo ya jinsi ya kuyasuluhisha. Ilikuwa Mei 22, 2000. Lakini kwa nini mkutano huo ulikuwa muhimu sana? Kabla sijaeleza, acheni niwasimulie historia ya maisha yangu.

Nilibatizwa huko Queensland, nilifanya upainia katika kisiwa cha Tasmania na umishonari nchini Tuvalu, Samoa, na Fiji

NILIZALIWA Queensland, Australia, mwaka wa 1955. Muda mfupi baadaye, mama yangu, Estelle, alianza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Alibatizwa mwaka uliofuata, na baba yangu, Ron, alikubali kweli baada ya miaka 13. Nilibatizwa mwaka wa 1968 katika mji wa St. George huko Queensland.

Tangu nikiwa mdogo, nilipenda sana kusoma na nilifurahia lugha. Tulipokuwa tukisafiri kwa gari tukiwa familia, huenda wazazi wangu walishangaa waliponiona nimekaa kiti cha nyuma nikisoma kitabu badala ya kutazama mandhari. Lakini kupenda kusoma kulinisaidia shuleni. Katika shule ya sekondari jijini Glenorchy, kisiwani Tasmania, nilipata tuzo kadhaa kwa kufaulu vizuri.

Hata hivyo, ulifika wakati wa kufanya uamuzi mzito. Je, ningekubali fursa ya kulipiwa masomo ya chuo kikuu? Ingawa nilipenda kusoma na kujifunza, ninamshukuru mama yangu kwa kunisaidia nimpende sana Yehova. (1 Kor. 3:18, 19) Kwa ruhusa ya wazazi wangu, nilianza upainia Januari 1971 nikiwa na umri wa miaka 15, mara baada ya kumaliza shule ya sekondari.

Kwa miaka nane iliyofuata, nilipata nafasi ya pekee ya kufanya upainia katika kisiwa cha Tasmania. Katika kipindi hicho, nilimwoa msichana mrembo wa Tasmania, Jenny Alcock, na kwa miaka minne tulitumikia pamoja tukiwa mapainia wa pekee katika maeneo ya mbali huko Smithton na Queenstown.

KUTUMIKIA KWENYE VISIWA VYA PASIFIKI

Mwaka wa 1978, kwa mara ya kwanza tulienda nchi nyingine kuhudhuria kusanyiko la kimataifa huko Port Moresby, Papua New Guinea. Ninakumbuka mmishonari fulani alitoa hotuba kwa lugha ya Hiri Motu. Ingawa sikuelewa alichokuwa akizungumza, hotuba yake ilinichochea niwe mmishonari, nijifunze lugha nyingine, na nitoe hotuba kama hiyo. Hatimaye nilitambua jinsi ninavyoweza kutumia lugha kumtumikia Yehova.

Tuliporudi Australia, tulishangaa sana tulipopewa mgawo wa kuwa wamishonari katika kisiwa cha Funafuti, nchini Tuvalu. Tuliwasili katika kisiwa hicho mnamo Januari 1979. Wakati huo kulikuwa na wahubiri waliobatizwa watatu tu huko Tuvalu.

Nikiwa na Jenny huko Tuvalu

Haikuwa rahisi kujifunza Kituvalu. Kitabu pekee kilichopatikana katika lugha hiyo ni “Agano Jipya.” Hakukuwa na kamusi wala mafunzo ya lugha, hivyo tuliamua kujifunza maneno mapya 10 hadi 20 kila siku. Lakini baada ya muda tulitambua kwamba hatukuelewa maana sahihi ya maneno mengi tuliyokuwa tukijifunza. Badala ya kuwaeleza watu uaguzi ni mbaya, tulikuwa tukiwaambia waepuke kutumia mizani na mikongojo! Hata hivyo, tulihitaji kujifunza lugha hiyo ili tuweze kuongoza mafunzo mengi ya Biblia tuliyoanzisha. Kwa hiyo hatukukata tamaa. Miaka kadhaa baadaye, mtu mmoja ambaye tulimfundisha Biblia alituambia hivi: “Tunafurahi sana kwamba sasa mnaweza kuzungumza lugha yetu. Mwanzoni, hatukuelewa kabisa mlikuwa mnasema nini!”

Kwa upande mwingine, tulikuwa na mazingira mazuri sana ya kujifunza lugha. Kwa kuwa hakukuwa na nyumba za kupanga, tuliishi na familia ya Mashahidi kijijini. Tulilazimika kutumia lugha hiyo kila mahali na kuishi maisha ya kijijini. Hatukuzungumza Kiingereza kwa miaka kadhaa, hivyo Kituvalu kikawa lugha yetu kuu.

Baada ya muda mfupi, watu wengi walianza kupenda kweli. Lakini tungetumia nini kujifunza nao? Hatukuwa na machapisho yoyote katika lugha yao. Wangewezaje kujifunza kibinafsi? Ikiwa wangeanza kuja mikutanoni, wangeimba nyimbo gani, wangetumia machapisho gani, na wangejitayarishaje kwa ajili ya mikutano? Wangewezaje kufanya maendeleo ili wabatizwe? Watu hao wanyenyekevu walihitaji chakula cha kiroho katika lugha yao! (1 Kor. 14:9) Tulijiuliza, ‘Inawezekana siku moja kuwe na machapisho ya Kituvalu, lugha inayozungumzwa na watu wasiozidi 15,000?’ Yehova alijibu maswali hayo na kututhibitishia mambo mawili: (1) Anataka Neno lake litangazwe “kati ya visiwa vilivyo mbali,” na (2) anataka wale ambao wanaonwa na ulimwengu kuwa “watu wanyenyekevu na wa hali ya chini” wapate kimbilio katika jina lake.—Yer. 31:10; Sef. 3:12.

KUTAFSIRI CHAKULA CHA KIROHO

Mwaka wa 1980, ofisi ya tawi ilituomba tufanye kazi ambayo tulihisi hatustahili kabisa kuifanya, yaani, kutafsiri. (1 Kor. 1:28, 29) Mwanzoni, tulinunua mashine ya zamani ya kunakili kutoka serikalini, na tukaitumia kuchapa machapisho tuliyotumia kwenye mikutano yetu. Baadaye tulitafsiri kitabu Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele kwa Kituvalu na tukakichapa katika mashine hiyo. Ninakumbuka harufu kali ya wino na jinsi tulivyojitahidi kuchapa kwa mkono kitabu kizima wakati wa joto kali sana. Wakati huo hatukuwa na umeme!

Haikuwa rahisi kutafsiri katika Kituvalu kwa sababu tulikuwa na vitabu vichache sana. Lakini nyakati nyingine tulipata msaada kwa njia tusiyoitarajia. Asubuhi moja niligonga kimakosa nyumba ya mtu ambaye alikuwa akipinga kweli. Mwenye nyumba, mwanaume mzee aliyekuwa mwalimu, alinikumbusha mara moja kuwa hatupaswi kumtembelea nyumbani kwake. Halafu akasema hivi: “Ningependa kukuambia jambo fulani. Katika machapisho yenu mnatafsiri maneno fulani kwa njia ambayo haitumiwi kwa ukawaida na Watuvalu.” Nilifanya utafiti na kugundua kwamba alikuwa sahihi. Hivyo tulifanya marekebisho yaliyohitajika. Nilishangaa sana kuona jinsi Yehova alivyotupa msaada huo kupitia mpinzani ambaye ni wazi alikuwa akisoma machapisho yetu!

Trakti Habari Njema za Ufalme Na. 30 ya Kituvalu

Chapisho la kwanza la Kituvalu ambalo liligawanywa kwa umma lilikuwa mwaliko wa Ukumbusho. Baada ya hapo, trakti Habari za Ufalme Na. 30 ikatolewa sambamba na Kiingereza. Tulifurahia sana kuwapa watu chapisho la lugha yao! Hatua kwa hatua, broshua na baadhi ya vitabu vikatolewa katika lugha ya Kituvalu. Mwaka wa 1983, ofisi ya tawi ya Australia ilianza kuchapisha gazeti la Mnara wa Mlinzi lenye kurasa 24. Gazeti hilo lilichapishwa mara nne kwa mwaka na kutupatia wastani wa mafungu saba ya kujifunza kila juma. Watu walilipokeaje? Kwa kuwa Watuvalu wanapenda kusoma, machapisho yetu yalipendwa sana. Kila mara gazeti jipya lilipowasili tangazo lilitolewa kwenye taarifa ya habari ya redio ya taifa, nyakati nyingine ilikuwa habari kuu katika vyombo vya habari! *

Tulianza kutafsiri kwa kutumia karatasi na kalamu. Baadaye, maandishi yalichapwa mara kadhaa kabla ya kutumwa katika ofisi ya tawi nchini Australia ili kuchapishwa. Wakati fulani, ofisi ya tawi iliwapa dada wawili kazi ya kuingiza maandishi kwenye kompyuta, hata ingawa hawakuelewa Kituvalu. Njia hiyo ya kuwatumia dada wawili kuingiza maandishi kwenye kompyuta mbili na kisha kuyalinganisha, ilisaidia kuepuka makosa mengi. Kisha tulitumiwa nakala za maandishi hayo ili tuzikague, halafu tulizirudisha ofisi ya tawi ili zichapishwe.

Mambo yamebadilika sana! Siku hizi watafsiri wanaingiza maandishi moja kwa moja kwenye kompyuta. Kwa kawaida, maandishi yaliyofanyiwa marekebisho hupangwa hapohapo kwenye ofisi ya utafsiri ili kutokeza faili za elektroniki ambazo zinatumwa kupitia Intaneti kwenda ofisi za tawi zinazoshughulikia uchapishaji. Hakuna tena haja ya kwenda posta ili kutuma nakala za maandishi yaliyotafsiriwa.

MIGAWO MINGINE

Miaka ilipozidi kusonga, mimi na Jenny tulipata migawo mbalimbali katika eneo la Pasifiki. Mwaka wa 1985, tulipata mgawo wa kutumikia katika ofisi ya tawi ya Samoa. Tukiwa huko tulisaidia kutafsiri katika Kisamoa, Kitonga, na Kitokelau huku tukiendelea kutafsiri Kituvalu. * Kisha mwaka wa 1996 tulipewa mgawo kama huo katika ofisi ya tawi ya Fiji, ambapo tulisaidia kutafsiri katika Kifiji, Kikiribati, Kinauru, Kirotuma, na Kituvalu.

Nikitumia machapisho ya Kituvalu kuwafundisha wengine

Ninashangazwa sana na bidii ya wale wanaotafsiri machapisho yetu. Kazi hiyo inaweza kuchosha sana. Hata hivyo, ndugu na dada hao waaminifu wanaiga tamaa ya Yehova kwa kuhakikisha kwamba habari njema inahubiriwa katika “kila taifa na kabila na lugha na watu.” (Ufu. 14:6) Kwa mfano, mipango ya kutafsiri gazeti la Mnara wa Mlinzi katika lugha ya Kitonga ilipoanza kufanywa, nilikutana na wazee wote wa makutaniko huko Tonga na kuwauliza ni nani angeweza kuzoezwa ili awe mtafsiri. Mzee mmoja, aliyekuwa fundi mzuri wa magari na mashine, alikubali kuacha kazi yake siku iliyofuata naye akaanza mara moja kazi ya kutafsiri. Jambo hilo lilikuwa lenye kugusa moyo sana, kwa sababu alikuwa na familia na hakujua angepata wapi pesa za kutunza familia yake. Lakini Yehova alimtunza yeye na familia yake, na aliendelea kutafsiri kwa miaka mingi.

Watafsiri hao wenye bidii wana mtazamo kama wa Baraza Linaloongoza, ambalo huhangaikia sana mahitaji ya kiroho ya watu wa lugha zote, hata zile zinazozungumzwa na watu wachache. Kwa mfano, wakati fulani swali lilizuka ikiwa kuna faida yoyote ya kuchapisha machapisho ya Kituvalu. Nilitiwa moyo sana na jibu la Baraza Linaloongoza: “Hatuoni sababu yoyote ya ninyi kuacha kutafsiri katika lugha ya Kituvalu. Ingawa ni watu wachache wanaozungumza Kituvalu ikilinganishwa na lugha nyingine, bado watu hao wanahitaji kusikia habari njema katika lugha yao.”

Nikibatiza watu

Mwaka 2003, mimi na Jenny tulihamishwa kutoka Idara ya Utafsiri iliyokuwa kwenye ofisi ya tawi ya Fiji na kupelekwa kwenye Idara ya Utumishi wa Tafsiri huko Patterson, New York. Ilikuwa kama ndoto! Tukajiunga na kikundi kinachosaidia kuanzisha vikundi vipya vya kutafsiri machapisho yetu. Kwa miaka miwili hivi, tulitembelea nchi mbalimbali ili kuwazoeza watafsiri.

MAAMUZI YA KIHISTORIA

Acheni sasa nizungumzie ile ripoti niliyoitaja mwanzoni. Kufikia mwaka 2000, Baraza Linaloongoza liliona kwamba kuna uhitaji wa kuboresha vikundi vya watafsiri ulimwenguni pote. Kufikia wakati huo, watafsiri wengi hawakuwa wamezoezwa vya kutosha. Baada ya kuwasilisha ripoti hiyo kwa Halmashauri ya Uandikaji, Baraza Linaloongoza liliidhinisha programu ya kuwazoeza watafsiri ulimwenguni pote. Programu hiyo ilihusisha mafunzo ya Kiingereza, mbinu za kutafsiri, na jinsi ya kufanya kazi kwa ushirikiano.

Jitihada hizo zimekuwa na matokeo gani? Kwanza, tafsiri imekuwa bora zaidi. Pili, tunatafsiri machapisho katika lugha nyingi zaidi. Tulipoanza umishonari mwaka wa 1979, gazeti la Mnara wa Mlinzi lilichapishwa katika lugha 82 tu. Katika lugha nyingi, gazeti hilo lilichapishwa miezi kadhaa baada ya gazeti la Kiingereza kutolewa. Hata hivyo, sasa gazeti la Mnara wa Mlinzi linagawanywa katika lugha zaidi ya 240, na magazeti ya lugha nyingi kati ya hizo hutolewa sambamba na Kiingereza. Leo chakula cha kiroho kinapatikana katika lugha zaidi ya 700. Ilikuwa kama ndoto kuwazia jambo hilo miaka kadhaa iliyopita.

Mwaka 2004, Baraza Linaloongoza lilifanya uamuzi mwingine wa kihistoria, yaani, kuharakisha kazi ya kutafsiri Biblia. Miezi michache baada ya uamuzi huo, kazi ya kutafsiri Biblia ikawa sehemu ya kawaida ya utafsiri, hivyo lugha nyingi zaidi zikapata fursa ya kutafsiri Biblia Tafsiri ya Ulimwengu Mpya. Kufikia mwaka 2014, Biblia hiyo ilipatikana ikiwa nzima au kwa sehemu katika lugha 128—zikiwemo lugha zinazozungumzwa Kusini mwa Pasifiki.

Nikitoa Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo katika Kituvalu

Jambo moja ambalo sitasahau maishani mwangu ni kusanyiko nililohudhuria nchini Tuvalu mwaka 2011. Kwa miezi mingi, nchi nzima ilikumbwa na ukame mkali sana, na ndugu walifikiri kwamba kusanyiko lisingefanyika. Hata hivyo, siku tuliyofika, mvua kubwa sana ilinyesha na kusanyiko likafanywa hatimaye! Ilikuwa heshima kubwa sana kwangu kutoa Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo katika Kituvalu, ambayo ni kati ya lugha zinazozungumzwa na watu wachache sana. Mwishoni mwa kusanyiko hilo, mvua kubwa ilinyesha tena. Baada ya programu kumalizika, kila mtu alikuwa na maji mengi ya kiroho na maji halisi!

Nikiwahoji wazazi wangu, Ron na Estelle, kusanyikoni huko Townsville, Australia, mwaka 2014

Inasikitisha kwamba Jenny, mwenzi wangu mwaminifu kwa zaidi ya miaka 35, hakushuhudia tukio hilo la kihistoria. Alikufa mwaka 2009 baada ya kuugua kansa kwa miaka kumi. Atakapofufuliwa, bila shaka atafurahi sana kusikia kuhusu kutolewa kwa Biblia ya Kituvalu.

Tangu wakati huo, nimepata baraka ya kuwa na mwandamani mwingine mrembo, Loraini Sikivou. Loraini na Jenny walifanya kazi pamoja Betheli huko Fiji, na Loraini alikuwa mtafsiri. Hivyo, kwa mara nyingine nimepata mke mwaminifu anayependa lugha kama mimi, na tunamtumikia Yehova pamoja!

Nikihubiri na Loraini huko Fiji

Ninapokumbuka miaka iliyopita, ninatiwa moyo sana kuona jinsi Baba yetu mpendwa wa mbinguni, Yehova, anavyoendelea kutimiza mahitaji ya vikundi mbalimbali vya lugha, vidogo kwa vikubwa. (Zab. 49:1-3) Nimeona jinsi watu wanavyofurahi wanapopata kwa mara ya kwanza machapisho yetu katika lugha zao au wanapomsifu Yehova kwa kuimba katika lugha zao. Nyakati kama hizo ninatafakari jinsi Yehova anavyotupenda sana. (Mdo. 2:8, 11) Bado ninakumbuka maneno ya Saulo Teasi, ndugu mwenye umri mkubwa kutoka Tuvalu. Baada ya kuimba wimbo wa Ufalme katika lugha yake kwa mara kwanza, alisema hivi: “Liambie Baraza Linaloongoza kuwa nyimbo hizi zinapendeza zaidi zikiimbwa kwa Kituvalu kuliko Kiingereza.”

Tangu Septemba 2005, nimepata fursa ya kuwa mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova. Ingawa kwa sasa mimi si mtafsiri, ninamshukuru Yehova kwa kuniruhusu nishiriki kuendeleza kazi ya utafsiri ulimwenguni pote. Inafurahisha sana kujua kwamba Yehova anashughulikia mahitaji ya kiroho ya watu wake wote, hata wale wanaoishi kwenye visiwa vya mbali katikati ya Bahari ya Pasifiki! Naam, kama mtunga-zaburi alivyosema, “Yehova amekuwa mfalme! Dunia na ishangilie. Na vile visiwa vingi vishangilie.”—Zab. 97:1.

^ fu. 18 Kwa habari zaidi kuhusu jinsi watu walivyopokea machapisho yetu, tazama gazeti la Mnara wa Mlinzi, la Desemba 15, 2000, ukurasa wa 32; Agosti 1, 1988, ukurasa wa 22; na Amkeni! Desemba 22, 2000, ukurasa wa 9.

^ fu. 22 Kwa habari zaidi kuhusu kazi ya kutafsiri nchini Samoa, tazama Kitabu cha Mwaka cha 2009, ukurasa wa 120-121, 123-124.