Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unajitahidi Kukomaa Kiroho?

Je, Unajitahidi Kukomaa Kiroho?

‘Mpaka sisi sote tufikie kipimo cha kimo ambacho ni cha ujazo wa Kristo.EFE. 4:13.

NYIMBO: 69, 70

1, 2. Kila Mkristo anapaswa kuwa na lengo gani? Toa mfano.

MWANAMKE anapotaka kununua matunda sokoni, si mara zote huchagua matunda makubwa au ya bei nafuu. Badala yake, anachagua matunda ambayo yameiva. Anataka matunda yanayonukia, matamu, na yenye lishe. Naam, anachagua matunda yaliyoiva kabisa, yaani yale yaliyokomaa.

2 Vivyo hivyo, Yehova anataka watumishi wake wakomae kiroho. Kwa hiyo baada ya kujiweka wakfu na kubatizwa, Mkristo anapaswa kuwa na lengo la kukomaa kiroho. Mtume Paulo aliwaandikia Wakristo wa Efeso kuhusu uhitaji wa kukua kiroho. Aliwatia moyo wajitahidi kufikia ‘umoja katika imani na ujuzi sahihi wa Mwana wa Mungu, na kuwa watu waliokomaa, kufikia kipimo cha kimo ambacho ni cha ujazo wa Kristo.’—Efe. 4:13.

3. Hali iliyokuwa katika kutaniko la Efeso inafananaje na hali ya watu wa Yehova leo?

3 Kutaniko la Efeso lilikuwa limedumu kwa miaka kadhaa tangu lianzishwe wakati Paulo alipoliandikia barua. Wanafunzi wengi kutanikoni walikuwa wamekomaa kiroho. Hata hivyo, baadhi yao walihitaji kujitahidi ili wawe wakomavu. Hali iko hivyo leo miongoni mwa Mashahidi wa Yehova. Ndugu na dada wengi wamemtumikia Mungu kwa miaka mingi, nao wamekomaa kiroho. Lakini ni wazi kwamba si wote wamefikia hatua hiyo. Kwa mfano, maelfu ya watu hubatizwa kila mwaka, hivyo wengine bado wanahitaji kujitahidi kukomaa. Namna gani wewe?—Kol. 2:6, 7.

UKUZI WA KIKRISTO

4, 5. Wakristo wakomavu wanatofautianaje? Lakini wote wanajitahidi kufanya nini? (Tazama picha kwenye ukurasa wa 3.)

4 Unapochunguza matunda yaliyoiva sokoni, utagundua kwamba hayafanani. Hata hivyo, yote yana sifa fulani ambazo zinakusaidia kutambua kwamba yameiva. Vivyo hivyo, Wakristo wakomavu hawafanani katika mambo kama vile nchi waliyozaliwa, malezi, afya, umri, na uzoefu. Isitoshe wana utu na utamaduni tofauti. Licha ya tofauti hizo, wale wote wanaokua kiroho wanajitahidi kusitawisha sifa zinazoonyesha wazi kuwa wamekomaa. Jinsi gani?

5 Mkristo mkomavu anamwiga Yesu, ambaye alituwekea mfano mzuri ili tufuate “hatua zake kwa ukaribu.” (1 Pet. 2:21) Yesu alikazia jambo gani muhimu zaidi? Alisema kwamba tunapaswa kumpenda Yehova kwa moyo, nafsi, na akili yetu yote na pia kumpenda jirani yetu kama tunavyojipenda wenyewe. (Mt. 22:37-39) Mkristo mkomavu anajitahidi kutii amri hiyo. Maisha yake yanaonyesha kwamba anathamini sana uhusiano wake na Yehova na anawapenda wengine kutoka moyoni.

Wakristo waliozeeka wanaweza kuonyesha unyenyekevu kama wa Yesu kwa kuwasaidia vijana walio madarakani (Tazama fungu la 6)

6, 7. (a) Ni baadhi ya sifa gani zinazowatambulisha Wakristo wakomavu? (b) Tunapaswa kujiuliza swali gani?

6 Inaeleweka kwamba upendo ni mojawapo ya sifa za tunda la roho ambazo huonyeshwa na Mkristo mkomavu. (Gal. 5:22, 23) Sifa nyingine, kama vile upole, kujizuia, na ustahimilivu, ni muhimu pia. Sifa hizo zinaweza kumsaidia Mkristo mkomavu ashughulikie hali ngumu bila kukasirika, na kuvumilia mambo yenye kuvunja moyo bila kupoteza tumaini. Anapojifunza kibinafsi, anajitahidi kutafuta kanuni za Biblia zitakazomsaidia atofautishe mambo yanayofaa na yasiyofaa. Hatimaye, uamuzi anaofanya unadhihirisha ukomavu wake. Kwa mfano, Mkristo mkomavu anaisikiliza dhamiri yake iliyozoezwa na Biblia. Naye anaonyesha unyenyekevu kwa kutambua kwamba sikuzote njia na viwango vya Yehova ni bora kuliko vyake. * Anahubiri habari njema kwa bidii na anaendeleza umoja kutanikoni.

7 Haidhuru tumemtumikia Yehova kwa muda gani, inafaa kila mmoja wetu ajiulize, ‘Je, kuna marekebisho ninayohitaji kufanya ili nifuate hatua za Yesu kwa ukaribu zaidi, na hivyo niendelee kukua kiroho?’

“CHAKULA KIGUMU NI CHA WATU WAKOMAVU”

8. Ni nini kinachoonyesha kwamba Yesu aliyaelewa vizuri Maandiko?

8 Yesu Kristo aliyaelewa vizuri sana Maandiko. Alipokuwa na umri wa miaka 12, alitumia Maandiko kujadiliana na walimu hekaluni. “Wale wote waliokuwa wakimsikiliza walikuwa wakishangazwa daima na uelewaji wake na majibu yake.” (Luka 2:46, 47) Baadaye, wakati wa huduma yake, Yesu aliwanyamazisha adui zake kwa kutumia Neno la Mungu.—Mt. 22:41-46.

9. (a) Mkristo anayetamani kukua kiroho anapaswa kufanya nini kwa ukawaida? (b) Kwa nini tunajifunza Neno la Mungu?

9 Mkristo anayetamani kukua kiroho anajitahidi kuiga mfano wa Yesu na haridhiki tu kujua mambo ya msingi. Badala yake anachunguza kwa kina Maandiko, akitambua kwamba “chakula kigumu ni cha watu wakomavu.” (Ebr. 5:14) Bila shaka Mkristo mkomavu ana lengo la kupata “ujuzi sahihi wa Mwana wa Mungu.” (Efe. 4:13) Je, unasoma Biblia kila siku? Je, unajifunza kibinafsi kwa ukawaida, ukijitahidi kutenga wakati kila juma kwa ajili ya ibada ya familia? Unaposoma Neno la Mungu, uwe chonjo kutambua kanuni za Biblia zitakazokusaidia kujua maoni na hisia za Yehova. Kisha, jitahidi kuzitumia maishani kwa kuwa kufanya hivyo kutakusaidia umkaribie zaidi Yehova.

10. Mkristo mkomavu ana maoni gani kuhusu njia na kanuni za Mungu? Na hilo lina matokeo gani maishani mwake?

10 Mkristo mkomavu anatambua kwamba kuwa na ujuzi tu hakutoshi. Anapaswa pia kupenda njia na kanuni za Mungu. Njia moja ya kuonyesha upendo huo ni kutanguliza mapenzi ya Yehova maishani. Isitoshe, Mkristo mkomavu ‘ameondolea mbali’ mtazamo na matendo yake ya zamani. Mkristo anapofanya mabadiliko hayo anamwiga Kristo na kuvaa utu mpya “ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu katika uadilifu wa kweli na ushikamanifu.” (Soma Waefeso 4:22-24.) Biblia iliandikwa kwa mwongozo wa roho takatifu. Hivyo, Mkristo anapojifunza kwa kina na kuvipenda viwango vya Biblia, anairuhusu roho takatifu ifanye kazi ndani yake. Jambo hilo linachangia ukuzi wa kiroho.

CHANGIA UMOJA KUTANIKONI

11. Yesu alikabili hali gani alipokuwa duniani?

11 Yesu alikuwa mkamilifu. Hata hivyo, alipokuwa duniani aliishi na wanadamu wasio wakamilifu. Alilelewa na wazazi wasio wakamilifu, na aliishi na watu wa ukoo wasio wakamilifu. Hata wafuasi wake wa karibu walionyesha sifa mbaya kama vile kiburi na ubinafsi. Kwa mfano, siku moja kabla hajauawa, kulitokea “bishano kali kati yao juu ya ni nani kati yao aliyeonekana kuwa mkuu zaidi ya wote.” (Luka 22:24) Lakini Yesu alikuwa na uhakika kwamba wafuasi wake wasio wakamilifu wangekua kiroho na kutokeza kutaniko lenye umoja. Siku hiyohiyo Yesu aliwaombea mitume wake wawe na umoja; alimwambia hivi Baba yake wa mbinguni: “Wote wapate kuwa kitu kimoja, kama vile ambavyo wewe, Baba, umo katika muungano pamoja na mimi na mimi nimo katika muungano pamoja na wewe, ili wao pia wapate kuwa katika muungano pamoja na sisi, . . . ili wapate kuwa kitu kimoja kama vile sisi tulivyo kitu kimoja.”—Yoh. 17:21, 22.

12, 13. (a) Andiko la Waefeso 4:15, 16 linakaziaje uhitaji wa kuchangia umoja kutanikoni? (b) Ndugu Uwe alijifunzaje kuendeleza umoja kutanikoni?

12 Mkristo mkomavu huchangia umoja kutanikoni. (Soma Waefeso 4:1-6, 15, 16.) Lengo letu ni kwamba watu wa Mungu ‘waunganishwe pamoja kwa upatano’ na wote kutanikoni wawe na ushirikiano. Kulingana na Neno la Yehova, tunahitaji kusitawisha unyenyekevu ili tufikie lengo hilo. Ndugu au dada mkomavu huwa tayari kujinyenyekeza ili kuendeleza umoja anaposhirikiana na wanadamu wenzake wasio wakamilifu. Wewe unatendaje unapogundua udhaifu wa ndugu au dada fulani kutanikoni? Au unafanya nini mtu fulani anapokukosea? Je, una mwelekeo wa kujenga ukuta unaokutenganisha na yule aliyekukosea au unajitahidi kujenga daraja linalowaunganisha? Badala ya kujenga ukuta, Mkristo mkomavu hujitahidi kujenga daraja, yaani, kurudisha mahusiano mazuri.

13 Fikiria mfano wa ndugu anayeitwa Uwe. Zamani alikasirishwa sana na makosa ya waumini wenzake. Kisha, aliamua kutumia Biblia na kitabu cha Insight on the Scriptures kujifunza kuhusu maisha ya Daudi. Kwa nini alimchagua Daudi? Uwe anaeleza hivi: “Daudi aliona baadhi ya makosa ya waabudu wenzake. Kwa mfano, Mfalme Sauli alijaribu kumuua, watu fulani walitaka kumpiga kwa mawe, naye mke wake alimdhihaki. (1 Sam. 19:9-11; 30:1-6; 2 Sam. 6:14-22) Daudi hakuruhusu kamwe matendo ya wengine yapunguze upendo wake kwa Yehova. Isitoshe, Daudi alikuwa na rehema, sifa ambayo nilihitaji kusitawisha. Mambo niliyojifunza yalibadili maoni yangu kuhusiana na udhaifu wa waumini wenzangu. Siweki tena akilini makosa ya wengine. Badala yake, ninajitahidi kuendeleza umoja kutanikoni.” Namna gani wewe? Je, una lengo la kuendeleza umoja kutanikoni?

SHIRIKIANA NA WALE WANAOFANYA MAPENZI YA MUNGU

14. Yesu alichagua marafiki wa aina gani?

14 Kwa ujumla, Yesu alikuwa na mahusiano mazuri na watu. Watu wa kila rika—wanaume kwa wanawake, vijana kwa wazee, na hata watoto, walijihisi huru kumkaribia. Hata hivyo, Yesu alichagua kwa uangalifu marafiki wa karibu. Aliwaambia hivi mitume wake waaminifu: “Ninyi ni rafiki zangu ikiwa mnafanya ninalowaamuru ninyi.” (Yoh. 15:14) Yesu alichagua marafiki miongoni mwa watu walioshikamana naye na wale waliomtumikia Yehova kwa moyo wote. Je, unachagua marafiki miongoni mwa watu wanaomtumikia Yehova kwa moyo wote? Kwa nini jambo hilo ni muhimu?

15. Vijana wanaweza kunufaikaje kwa kushirikiana na Wakristo wakomavu?

15 Joto la jua husaidia aina mbalimbali za matunda kuiva vizuri. Vivyo hivyo, upendo wa ndugu na dada zetu unaweza kukusaidia kukomaa kiroho. Labda wewe ni kijana, na unafikiria utafanya nini maishani. Basi ingefaa sana ushirikiane na waumini wenzako ambao wamemtumikia Yehova kwa miaka mingi na kuchangia umoja kutanikoni. Huenda wamevuka milima na mabonde maishani, na kukabili changamoto mbalimbali katika utumishi wao. Marafiki wa aina hiyo wanaweza kukusaidia uchague njia bora ya maisha. Upendo na ushirika wao unaweza kukusaidia ufanye uamuzi wa hekima maishani na ukomae kiroho.—Soma Waebrania 5:14.

16. Watu wenye umri mkubwa kutanikoni walimsaidiaje Helga alipokuwa kijana?

16 Kwa mfano, Helga, anakumbuka kwamba alipokaribia kumaliza shule, wanafunzi wenzake walikuwa wakizungumza sana kuhusu malengo yao ya wakati ujao. Wengi wao walitaka kwenda chuo kikuu ili baadaye wapate kazi nzuri. Helga aliongea na rafiki zake kutanikoni kuhusu jambo hilo. Anasema hivi: “Wengi wao walikuwa wamenizidi umri, nao walinisaidia sana. Walinitia moyo nianze utumishi wa wakati wote. Baadaye, nilitumikia nikiwa painia wa kawaida kwa miaka mitano. Tangu wakati huo ninafurahi kwamba nilitumia miaka mingi ya ujana katika utumishi wa Yehova. Sina sababu yoyote ya kujutia uamuzi huo.”

17, 18. Ni nini kinachoweza kutusaidia tumtumikie Yehova kwa ukamili?

17 Kuiga mfano wa Yesu kutatusaidia tukomae kiroho. Tutamkaribia zaidi Yehova na pia tamaa yetu ya kumtumikia itaongezeka. Mtumishi wa Mungu anaweza kumtumikia Yehova kwa ukamili anapokuwa amekomaa kiroho. Yesu aliwatia moyo wafuasi wake kwa kuwaambia hivi: “Acheni nuru yenu iangaze mbele ya watu, ili wapate kuona matendo yenu mazuri na kumpa utukufu Baba yenu aliye mbinguni.”—Mt. 5:16.

18 Kama tulivyoona, Mkristo mkomavu anaweza kuwa msaada mkubwa sana kutanikoni. Isitoshe, Mkristo anaonyesha ukomavu wa kiroho kwa jinsi anavyotumia dhamiri aliyopewa na Mungu. Dhamiri yetu inaweza kutusaidiaje tufanye uamuzi wa hekima? Na tunawezaje kuheshimu dhamiri za waumini wenzetu? Tutajibu maswali hayo katika makala inayofuata.

^ fu. 6 Kwa mfano, huenda ndugu wenye uzoefu mwingi ambao wamezeeka wakaombwa waachie madaraka fulani na kuwasaidia vijana wanaposhughulikia madaraka hayo.