Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Simameni Imara Katika Imani”

“Simameni Imara Katika Imani”

“Simameni imara katika imani, . . . iweni na nguvu.”—1 KOR. 16:13.

NYIMBO: 60, 64

1. (a) Petro alikabili hali gani kwenye Bahari ya Galilaya? (Tazama picha kwenye ukurasa huu.) (b) Kwa nini Petro alianza kuzama?

MTUME Petro na wanafunzi wengine wanajitahidi sana kupiga makasia ya mashua yao katika Bahari ya Galilaya wakati wa dhoruba kali. Ghafla, wanamwona Yesu akitembea juu ya bahari. Petro anamwomba Yesu ruhusa ya kutembea juu ya maji. Yesu anapomruhusu, Petro anashuka kutoka kwenye mashua na kutembea kimuujiza juu ya bahari kwenda kwa Yesu. Hata hivyo, baada ya muda Petro anaanza kuzama. Kwa nini? Kwa sababu anaitazama ile dhoruba naye anaogopa sana. Petro anapaza sauti ili asaidiwe, na mara moja Yesu anamshika mkono na kumwambia: “Wewe mwenye imani kidogo, kwa nini umekuwa na shaka?”—Mt. 14:24-32.

2. Tutachunguza mambo gani?

2 Acheni tuchunguze mambo matatu kuhusu imani ambayo tunaweza kujifunza kutoka kwa Petro: (1) jinsi ambavyo mwanzoni Petro aliamini kwamba Mungu angemsaidia, (2) sababu zilizofanya imani yake ianze kudhoofika, na (3) mambo yaliyomsaidia kuimarisha imani yake. Kuchunguza mambo hayo kutatusaidia kuona jinsi tunavyoweza ‘kusimama imara katika imani.’—1 Kor. 16:13.

TEGEMEA MSAADA WA MUNGU

3. Kwa nini Petro alishuka kutoka kwenye mashua, nasi tumefanya jambo gani linalofanana na hilo?

3 Petro alikuwa na imani yenye nguvu aliposhuka kutoka kwenye mashua na kutembea juu ya maji. Alipoitwa na Yesu, hakuwa na shaka hata kidogo kwamba nguvu za Mungu zingemsaidia kama zilivyomsaidia Yesu. Vivyo hivyo, imani yetu kwa Yehova ndiyo iliyotuchochea tujiweke wakfu kwake na kubatizwa. Yesu ametualika tuwe wafuasi wake, yaani tufuate hatua zake. Tunapaswa kumwamini Mungu na Yesu, tukitumaini kwamba watatusaidia kwa njia mbalimbali.—Yoh. 14:1; soma 1 Petro 2:21.

4, 5. Kwa nini ni muhimu kuwa na imani?

4 Ni muhimu sana kuwa na imani. Kama vile imani ilivyomwezesha Petro kutembea juu ya maji, imani yetu inatuwezesha kufanya mambo ambayo wengine wanaona hayawezekani. (Mt. 21:21, 22) Kwa mfano, wengi wetu tumebadili mitazamo na kuacha tabia mbaya tulizokuwa nazo hivi kwamba watu wanaotufahamu wanashangaa sana. Yehova alitusaidia kubadilika kwa sababu tulimwamini. (Soma Wakolosai 3:5-10.) Imani yetu ilituchochea tujiweke wakfu kwa Yehova, hivyo tukawa rafiki zake, jambo ambalo hatungeweza kufanya kwa uwezo wetu.—Efe. 2:8.

5 Imani inaendelea kutuimarisha. Kwa mfano, inatusaidia kupambana na mashambulizi ya mpinzani wetu mwenye nguvu, Shetani Ibilisi. (Efe. 6:16) Pia, kumtumaini Yehova kunatusaidia tusihangaike sana tunapokabili hali ngumu. Yehova ameahidi kutupatia mambo tunayohitaji ikiwa tutatanguliza masilahi ya Ufalme. (Mt. 6:30-34) Zaidi ya hayo, imani itatuwezesha kupata zawadi ambayo hakuna mwanadamu anayeweza kuipata kwa uwezo wake, yaani uzima wa milele.—Yoh. 3:16.

TUKIKENGEUKA TUTAPOTEZA IMANI

6, 7. (a) Upepo na mawimbi yaliyomzunguka Petro yanaweza kufananishwa na nini? (b) Tunapaswa kuelewa nini, na kwa nini?

6 Majaribu na vishawishi tunavyokabili tunapoendelea kumtumikia Mungu ni kama upepo na mawimbi yaliyomzunguka Petro alipokuwa akitembea juu ya maji. Yehova anaweza kutusaidia tusimame imara hata kama tunakabili majaribu makali sana. Kumbuka kwamba Petro hakuzama kwa sababu ya dhoruba au mawimbi makubwa. Badala yake, Biblia inasema kwamba ‘alipoitazama ile dhoruba ya upepo, akaogopa.’ (Mt. 14:30) Petro alikengeuka na kuanza kukazia fikira dhoruba badala ya kumkazia fikira Yesu. Hatimaye imani yake ikadhoofika. Vivyo hivyo, ikiwa tunakazia fikira majaribu tunayokabili, tunaweza kuanza kufikiri kwamba Yehova hawezi kutusaidia.

7 Tunapaswa kuelewa kwamba tusipokuwa makini tunaweza kupoteza imani yetu. Biblia inasema kwamba kutokuwa na imani au kuwa na imani dhaifu ni “dhambi ambayo hututatanisha kwa urahisi.” (Ebr. 12:1) Hali aliyokabili Petro inaonyesha kwamba imani yetu inaweza kudhoofika haraka ikiwa tunakazia fikira mambo yasiyofaa. Hivyo tunawezaje kutambua kwamba imani yetu ipo hatarini? Maswali yanayofuata yatatusaidia kujichunguza.

8. Ni mambo gani yanaweza kudhoofisha imani yetu?

8 Je, bado ninaamini kwamba ahadi za Mungu zitatimia? Kwa mfano, Mungu ameahidi kuuharibu mfumo huu. Hata hivyo, je, tumeruhusu burudani za ulimwengu huu zitukengeushe na kudhoofisha imani yetu kuelekea ahadi za Mungu? Ikiwa ndivyo, tunaweza kuanza kufikiri kwamba mwisho uko mbali sana. (Hab. 2:3) Pia, Mungu ameahidi kutusamehe kwa msingi wa fidia. Hata hivyo, tukiendelea kuhisi hatia kwa sababu ya makosa yetu ya zamani, tunaweza kuwa na mashaka ikiwa Yehova “amefuta” dhambi zetu. (Mdo. 3:19) Kwa sababu hiyo, tunaweza kupoteza shangwe yetu katika utumishi wa Mungu na mwishowe tutaacha kufanya mambo ya kiroho.

9. Matokeo yatakuwaje tukitumia nguvu zetu zote kufanya mambo ya kibinafsi?

9 Je, bado ninamtumikia Mungu kwa bidii? Mtume Paulo alionyesha kwamba kumtumikia Yehova kwa bidii kutatusaidia kuwa na “uhakikisho kamili wa tumaini mpaka mwisho.” Hata hivyo, matokeo yatakuwaje tukianza kutumia nguvu zetu zote kufanya mambo ya kibinafsi, kama vile kazi yenye mshahara mnono inayoingiliana na ibada yetu? Imani yetu itadhoofika, nasi “tutakuwa goigoi,” yaani, hatutamtumikia Yehova kwa nguvu zetu zote.—Ebr. 6:10-12.

10. Kuwasamehe wengine kunaonyeshaje kwamba tunamwamini Yehova?

10 Je, ninawasamehe wengine kwa hiari wanaponikosea? Tukikazia fikira jinsi wengine walivyotuumiza au kutuudhi, tunaweza kushawishika kuwakasirikia au kuacha kuongea nao. Hata hivyo, tukiwasamehe wengine tunaonyesha kwamba tunamwamini Yehova. Jinsi gani? Wale wanaotukosea wanakuwa na deni kwetu, kama vile dhambi zetu zinavyotufanya tuwe na deni kwa Mungu. (Luka 11:4) Tunapowasamehe wengine tunaonyesha kwamba tunamtumaini Mungu, huku tukiamini kwamba kupata kibali chake ni bora zaidi kuliko kuwalazimisha waliotukosea walipe deni lao. Wanafunzi wa Yesu walitambua kwamba walihitaji imani ili wawasamehe wengine. Yesu alipowaambia wawasamehe hata wale waliowakosea mara nyingi, wanafunzi hao walimwambia hivi: “Tupe imani zaidi.”—Luka 17:1-5.

11. Ni nini kinachoweza kufanya tusifaidike na ushauri tunaopewa?

11 Je, ninaudhika ninapopewa ushauri wa Kimaandiko? Tunaposhauriwa, huenda tukakazia fikira kasoro za ushauri au udhaifu wa yule anayetushauri, badala ya kufikiria jinsi tunavyoweza kufaidika kwa kutumia ushauri huo. (Met. 19:20) Tukifanya hivyo, tutapoteza nafasi ya kubadili mtazamo wetu ili tuwe na maoni kama ya Yehova.

12. Mtu aliyezoea kuwanung’unikia wale wanaoongoza kutanikoni anaonyesha nini?

12 Je, ninawanung’unikia ndugu wanaoongoza kutanikoni? Waisraeli walipokazia fikira habari mbaya kutoka kwa wale wapelelezi kumi wasio na imani, walianza kuwanung’unikia Musa na Haruni. Yehova alimuuliza Musa: “Watakosa kuniamini mpaka wakati gani?” (Hes. 14:2-4, 11) Naam, manung’uniko ya Waisraeli yalionyesha kwamba hawakumwamini Mungu aliyewachagua Musa na Haruni. Vivyo hivyo, ikiwa tumezoea kuwanung’unikia wale ambao Mungu anawatumia kuongoza watu wake, basi hilo linaonyesha kwamba imani yetu imedhoofika.

13. Kwa nini hatupaswi kuvunjika moyo tunapogundua kwamba imani yetu imedhoofika?

13 Baada ya kuchunguza maswali hayo, usivunjike moyo ukigundua kwamba imani yako imedhoofika. Hata Petro, mtume wa Yesu, aliruhusu woga na shaka zidhoofishe imani yake. Wakati fulani Yesu aliwakaripia mitume wake wote kwa sababu ya kuwa na “imani kidogo.” (Mt. 16:8) Kumbuka kwamba tunajifunza mambo muhimu katika kisa cha Petro kutokana na hatua aliyochukua baada ya imani yake kudhoofika na kuanza kuzama baharini.

IMARISHA IMANI YAKO KWA KUMWIGA YESU

14, 15. (a) Petro alifanya nini alipoanza kuzama? (b) Ingawa hatuwezi kumwona Yesu moja kwa moja, tunawezaje kumtazama kwa makini?

14 Petro alipotazama dhoruba na kuanza kuzama, angeweza kujaribu kuogelea ili arudi kwenye mashua. Huenda ingekuwa rahisi kwake kuamua kufanya hivyo, kwa kuwa alikuwa mwogeleaji stadi. (Yoh. 21:7) Hata hivyo, badala ya kujitegemea, Petro alianza tena kumkazia fikira Yesu na kukubali msaada wake. Ikiwa tunagundua kwamba imani yetu inadhoofika, tunapaswa kuiga mfano wa Petro. Tunawezaje kufanya hivyo?

15 Kama Petro alivyoanza tena kumkazia fikira Yesu ili kupata msaada, tunapaswa ‘kumtazama kwa makini Wakili Mkuu na Mkamilishaji wa imani yetu, Yesu.’ (Soma Waebrania 12:2, 3.) Ni kweli kwamba leo hatuwezi kumwona Yesu moja kwa moja. Hata hivyo, ‘tunamtazama Yesu kwa makini’ tunapochunguza mafundisho na matendo yake na kisha kuyafuata kikamili. Fikiria baadhi ya mambo tunayoweza kufanya ili kumwiga Yesu. Tukitumia mambo hayo maishani, tutaimarisha imani yetu.

Tunaweza kuwa imara katika imani kwa kuiga mfano wa Yesu na kufuata hatua zake kwa ukaribu (Tazama fungu la 15)

16. Tunawezaje kujifunza Biblia kwa njia itakayoimarisha imani yetu?

16 Imarisha imani yako katika Neno la Mungu, Biblia. Yesu alikuwa na uhakika kwamba Biblia ni Neno la Mungu, ambalo lina mwongozo bora wa maisha. (Yoh. 17:17) Ili kumwiga Yesu, tunapaswa kusoma Biblia kila siku, kujifunza, na kutafakari yale tunayosoma. Pia, tunaweza kufanya utafiti kuhusu mambo ambayo hatuyaelewi vizuri. Kwa mfano, je, unaamini kabisa kwamba mwisho uko karibu? Unaweza kuimarisha imani yako kwa kujifunza kwa makini Maandiko yanayothibitisha kuwa tunaishi katika siku za mwisho. Kuchunguza unabii wa Biblia ambao tayari umetimizwa kutakufanya uwe na uhakika zaidi kwamba ahadi za Mungu zitatimia. Kutafakari jinsi ambavyo Biblia imebadili maisha ya ndugu na dada wengine, kutakusaidia uamini zaidi kwamba Biblia ina faida maishani. *1 The. 2:13.

17. Kwa nini Yesu aliendelea kuwa mwaminifu licha ya kukabili majaribu makali, nawe unawezaje kumwiga?

17 Kazia fikira ahadi za Yehova. Yesu aliendelea kuwa mwaminifu licha ya kukabili majaribu makali kwa sababu alikazia fikira “shangwe iliyowekwa mbele yake.” (Ebr. 12:2) Hakukengeushwa na mambo ya ulimwengu. (Mt. 4:8-10) Unaweza kumwiga Yesu kwa kutafakari mambo mazuri ambayo Yehova amekuahidi. Unaweza kujiwazia ukiwa katika Paradiso kwa kuchora au kuandika mambo unayotazamia kufanya baada ya Mungu kuuondoa mfumo huu mwovu. Andika majina ya watu unaotamani kukutana nao watakapofufuliwa na mambo ambayo ungependa kuongea nao. Zione ahadi hizo kuwa zinakuhusu wewe binafsi, badala ya kuziona tu kuwa zinawahusu wanadamu wote kwa ujumla.

18. Sala inawezaje kuimarisha imani yako?

18 Mwombe Mungu akupe imani zaidi. Yesu aliwafundisha wanafunzi wake wamwombe Yehova awape roho takatifu. (Luka 11:9, 13) Unapofanya hivyo, mwombe Yehova akupe imani zaidi; kwa kuwa imani ni sifa ya tunda la roho takatifu. Unaposali, mweleze Yehova mambo hususa. Kwa mfano, unaweza kumwomba Yehova akusaidie ushinde tabia fulani inayoonyesha kwamba una imani dhaifu, kama vile sifa ya kutosamehe.

19. Tunapaswa kuchagua marafiki wenye sifa gani?

19 Shirikiana na watu wenye imani thabiti. Yesu alichagua marafiki kwa uangalifu sana, hasa wale alioshirikiana nao kwa ukaribu. Rafiki zake wa karibu sana, yaani, mitume wake, walikuwa waaminifu, washikamanifu, na walitii amri zake. (Soma Yohana 15:14, 15.) Kwa hiyo, unapochagua marafiki, tafuta wale ambao wanaonyesha imani kwa kumtii Yesu. Kumbuka kwamba marafiki wazuri ni wale wanaowasiliana kwa uhuru, na wapo tayari kushauriwa au kuwashauri wengine.—Met. 27:9.

20. Tunafaidikaje tunapowasaidia wengine waimarishe imani yao?

20 Wasaidie wengine waimarishe imani yao. Maneno na matendo ya Yesu yaliwasaidia wanafunzi wake waimarishe imani yao. (Marko 11:20-24) Tunapaswa kumwiga Yesu kwa kuwa tunapowasaidia wengine wajenge imani yao, imani yetu pia inaimarika. (Met. 11:25) Tunapohubiri na kuwafundisha wengine, acheni tuwathibitishie kuwa Mungu yupo, anatujali, na kwamba Biblia ni Neno lake lililoongozwa na roho. Wasaidie pia ndugu na dada zako waimarishe imani yao. Ukiona ndugu au dada yako ameanza kuwa na shaka kuhusu jambo fulani, labda kwa kuwanung’unikia ndugu wanaoongoza, usifanye haraka kumwepuka. Badala yake, msaidie kwa busara ili aimarishe imani yake. (Yuda 22, 23) Ikiwa wewe ni mwanafunzi, na unafundishwa nadharia ya mageuzi shuleni, tetea kwa ujasiri imani yako kuhusu uumbaji—unaweza kupata matokeo mazuri sana!

21. Yehova amemwahidi nini kila mmoja wetu?

21 Yehova na Yesu walimsaidia Petro kushinda hofu na mashaka. Hatimaye, akawa na imani yenye nguvu na kuwa nguzo katika kutaniko la Kikristo. Vivyo hivyo, Yehova hutusaidia ili tusimame imara katika imani. (Soma 1 Petro 5:9, 10.) Jitihada tunazofanya ili kuimarisha imani yetu si za bure, kwa kuwa tutapata baraka nyingi sana.

^ fu. 16 Kwa mfano, tazama mfululizo wenye kichwa “Biblia Inabadili Maisha” katika toleo la watu wote la Mnara wa Mlinzi.