Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HABARI KUU | MUNGU ANA MAONI GANI KUHUSU VITA?

Maoni ya Mungu Kuhusu Vita Katika Nyakati za Kale

Maoni ya Mungu Kuhusu Vita Katika Nyakati za Kale

Watu walikuwa wakiteswa. Walisali mara nyingi kwa Mungu ili awasaidie, lakini hawakupata msaada. Watu hao walikuwa Waisraeli, watu wa Mungu katika nyakati za kale. Walikandamizwa na taifa lenye nguvu la Misri. (Kutoka 1:13, 14) Kwa miaka mingi, Waisraeli walisubiri Mungu awaondolee utawala wa mabavu wa Misri. Hatimaye, wakati wa Mungu kuchukua hatua uliwadia. (Kutoka 3:7-10) Biblia inaeleza kwamba Mungu alipigana vita na Wamisri. Aliwapiga Wamisri kwa mapigo kumi yenye kuangamiza, na kisha akamuua mfalme wa Misri na jeshi lake kwenye Bahari Nyekundu. (Zaburi 136:15) Yehova Mungu akathibitika kuwa “mtu wa vita” kwa ajili ya watu wake.—Kutoka 15:3, 4.

Kitendo cha Mungu kupigana vita na Wamisri kinaonyesha kwamba hapingi kila vita. Nyakati nyingine, aliwaruhusu Waisraeli wapigane vita. Mathalani, aliwaamuru wapigane vita na Wakanaani waliokuwa waovu sana. (Kumbukumbu la Torati 9:5; 20:17, 18) Alimwagiza Mfalme Daudi apigane vita na Wafilisti waliokuwa wakandamizaji. Hata alimpa Daudi mbinu za kupigana ambazo zingemsaidia ashinde.—2 Samweli 5:17-25.

Masimulizi hayo ya Biblia yanaonyesha kuwa Waisraeli walipokuwa katika hatari ya kuonewa au kutendewa uovu, Mungu aliruhusu vita ili kulinda watu wake na ibada ya kweli. Lakini ona mambo matatu yafuatayo yanayohusu vita hivyo vilivyokubaliwa na Mungu.

  1. MUNGU NDIYE ALIYEAMUA NANI ANGEPIGANA VITA. Pindi moja, Mungu aliwaambia Waisraeli: “Hamtahitaji kupigana katika kisa hiki.” Kwa nini? Kwa sababu Mungu angepigana vita kwa niaba yao. (2 Mambo ya Nyakati 20:17; 32:7, 8) Alifanya hivyo mara nyingi, kama katika kisa kilichotajwa mwanzoni mwa makala hii. Nyakati nyingine, Mungu aliwaamuru watu wake katika Israeli la kale wapigane vita ambavyo aliruhusu, yaani, vile ambavyo vilihusisha kuchukua na kulinda Nchi yao ya Ahadi.—Kumbukumbu la Torati 7:1, 2; Yoshua 10:40.

  2. MUNGU NDIYE ALIYEAMUA LINI VITA HIVYO VINGEPIGANWA. Watumishi wa Mungu walihitaji kusubiri hadi wakati ambapo Mungu aliwaruhusu wakapigane vita ili kuondoa ukandamizaji na uovu uliowazunguka. Hawakupaswa kupigana kabla ya wakati huo kufika. Walipoamua kupigana bila ruhusa, walikosa kibali cha Mungu. Isitoshe, Biblia inaonyesha kwamba Waisraeli walipoamua kupigana vita bila kuruhusiwa na Mungu, matokeo yalikuwa mabaya. *

  3. Ingawa Mungu alipigana na Wakanaani, hakuwaangamiza baadhi yao kama vile Rahabu na familia yake

    MUNGU HAPENDI WANADAMU WAFE HATA KAMA NI WAOVU. Yehova Mungu ni chanzo cha uhai na Muumba wa wanadamu. (Zaburi 36:9) Kwa hiyo, hapendi kuona watu wakifa. Hata hivyo, kwa kusikitisha kuna watu hupanga kuwatesa na hata kuwaua wenzao. (Zaburi 37:12, 14) Ili kukomesha uovu huo, nyakati fulani Mungu huruhusu vita vipiganwe dhidi ya waovu. Pamoja na hayo, miaka yote ambayo aliwaruhusu Waisraeli wapigane, aliendelea kuwa mwenye “rehema” na hakuwa “mwepesi wa hasira” kuelekea wale waliowakandamiza Waisraeli. (Zaburi 86:15) Kwa mfano, aliagiza kwamba kabla Waisraeli hawajavamia jiji, walipaswa ‘kulitangazia masharti ya amani,’ ili kuwapa wakazi wa jiji hilo fursa ya kubadili njia zao na kuepuka vita. (Kumbukumbu la Torati 20:10-13) Kwa kufanya hivyo, Mungu alionyesha ‘anapendezwa, si na kifo cha mwovu, bali kwamba mtu mwovu ageuke na kuiacha njia yake na kwa kweli aendelee kuishi.’—Ezekieli 33:11, 14-16. *

Kutokana na mambo tuliyochunguza tumeona kwamba katika nyakati za kale, Mungu aliona vita kuwa njia halali ya kukomesha uonevu na uovu. Lakini, Mungu—wala si wanadamu—ndiye aliyeamua wakati na wale ambao wangepigana vita. Je, Mungu alifurahia kupigana vita ili aone umwagaji wa damu? Hapana. Kwa kweli, anachukia jeuri. (Zaburi 11:5) Je, maoni ya Mungu kuhusu vita yalibadilika Mwana wake, Yesu Kristo, alipoanza huduma yake katika karne ya kwanza?

^ fu. 7 Kwa mfano, nyakati fulani, Waisraeli walishindwa vita walipoamua kupigana na Waamaleki na Wakanaani baada ya Mungu kuwakataza kufanya hivyo. (Hesabu 14:41-45) Miaka mingi baadaye, Mfalme Yosia mwaminifu alipigana vita bila ruhusa ya Mungu na uamuzi huo ulimfanya apoteze uhai wake.—2 Mambo ya Nyakati 35:20-24.

^ fu. 8 Waisraeli hawakuwatangazia Wakanaani masharti ya amani kabla ya kupigana nao. Kwa nini? Kwa sababu Wakanaani walipewa miaka 400 ya kurekebisha matendo yao maovu. Kufikia wakati ambapo Waisraeli walipigana nao, Wakanaani walikuwa waovu sana. (Mwanzo 15:13-16) Hivyo, walipaswa kuangamizwa kabisa. Hata hivyo, Wakanaani waliobadilika waliokolewa.—Yoshua 6:25; 9:3-27.