Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HABARI KUU | MUNGU ANA MAONI GANI KUHUSU VITA?

Maoni ya Mungu Kuhusu Vita Katika Karne ya Kwanza

Maoni ya Mungu Kuhusu Vita Katika Karne ya Kwanza

Watu walinyanyaswa. Kama mababu zao, Wayahudi wa karne ya kwanza walimwomba Mungu mara nyingi awakomboe kutoka katika Milki ya Roma iliyokuwa ikiwakandamiza. Kisha wakasikia kumhusu Yesu. Je, ndiye Masihi aliyeahidiwa? Si ajabu, watu wengi ‘walitumaini kwamba mtu huyo ndiye angekomboa Israeli’ kutoka kwa Waroma wakandamizaji. (Luka 24:21) Lakini hawakupata msaada. Badala yake, katika mwaka wa 70 W.K., majeshi ya Roma yalikuja na kuharibu Yerusalemu na hekalu lake.

Ni nini kilichotokea? Kwa nini Mungu hakuwapigania Wayahudi kama alivyofanya wakati uliopita? Au kwa nini hakuwaruhusu wapigane vita ili kujikomboa kutoka kwa wale wanaowakandamiza? Je, maoni ya Mungu kuhusu vita yalibadilika? Hapana. Lakini mtazamo wa Wayahudi ulibadilika. Walimkataa Mwana wa Mungu, Yesu, kuwa Masihi. (Matendo 2:36) Kwa hiyo, wakiwa taifa walipoteza uhusiano wao wa pekee na Mungu.—Mathayo 23:37, 38.

Mungu aliacha kuwalinda Wayahudi na Nchi yao ya Ahadi hivyo wasingeweza tena kudai kwamba wanapigana vita kwa msaada wa Mungu. Kama Yesu alivyotabiri, baraka zilizotokana na kupata kibali cha Mungu ziliondolewa kutoka katika taifa la asili la Israeli na kupewa taifa jipya, taifa la kiroho, ambalo baadaye Biblia ililiita kuwa “Israeli wa Mungu.” (Wagalatia 6:16; Mathayo 21:43) Kutaniko la Wakristo watiwa-mafuta lilithibitika kuwa Israeli wa kiroho wa Mungu. Waliambiwa hivi katika karne ya kwanza: “Sasa ninyi ni watu wa Mungu.”—1 Petro 2:9, 10.

Kwa kuwa Wakristo wa karne ya kwanza walikuwa “watu wa Mungu,” je, Mungu alipigana kwa niaba yao, ili kuwakomboa kutoka kwa Waroma wakandamizaji? Au je, Mungu aliwaruhusu wapigane na wale waliokuwa wakiwakandamiza? Hapana, hakufanya hivyo. Kwa nini? Katika vita ambavyo Mungu ameruhusu, Mungu pekee ndiye anayeamua lini vita hivyo vipiganwe, kama makala iliyopita ilivyoonyesha. Mungu hakupigana vita kwa ajili ya Wakristo wa karne ya kwanza wala hakuwaruhusu wapigane vita. Ni wazi kwamba, karne ya kwanza haukuwa wakati wa Mungu kupigana ili kukomesha uovu na uonevu.

Hivyo, kama watumishi wa Mungu wa nyakati za kale, Wakristo hao wa karne ya kwanza walihitaji kusubiri mpaka wakati wa Mungu wa kukomesha uovu na ukandamizaji ufike. Kabla kufika kwa wakati huo, hawakuruhusiwa na Mungu kupigana na maadui zao. Yesu Kristo alionyesha wazi jambo hilo katika mafundisho yake. Kwa mfano, hakuwaagiza wafuasi wake kupigana vita badala yake aliwaambia: “Endeleeni kuwapenda adui zenu na kusali kwa ajili ya wale wanaowatesa.” (Mathayo 5:44) Akitabiri kuhusu wakati ambapo jiji la Yerusalemu la karne ya kwanza lingevamiwa na majeshi ya Roma, Yesu hakuwaagiza wafuasi wake wabaki na kupigana bali aliwaambia wakimbie, nao walifanya hivyo.—Luka 21:20, 21.

Pia, mtume Paulo akiongozwa na roho ya Mungu aliandika hivi: “Msijilipizie kisasi, . . . kwa maana imeandikwa: ‘Kisasi ni changu; mimi nitalipa,’ asema Yehova.” (Waroma 12:19) Paulo alikuwa akinukuu jambo alilosema Mungu karne nyingi mapema kama ilivyoandikwa katika Mambo ya Walawi 19:18 na Kumbukumbu la Torati 32:35. Kama ilivyoonyeshwa katika makala iliyotangulia, njia moja ambayo Mungu aliwalipizia kisasi watu wake katika nyakati za kale ilikuwa ni kwa kuwasaidia walipopigana vita na maadui zao. Hivyo maneno ya Paulo yanaonyesha kwamba maoni ya Mungu kuhusu vita hayajabadilika. Hata katika karne ya kwanza, bado Mungu aliona vita kama njia halali ya kuwalipizia kisasi watumishi wake na kukomesha uovu na ukandamizaji. Hata hivyo, kama ilivyokuwa wakati uliopita, Mungu pekee ndiye anayeamua lini vita vingepiganwa na nani ambaye angepigana vita hivyo.

Hivyo, ni wazi kwamba Mungu hakuwaruhusu Wakristo katika karne ya kwanza wapigane vita. Vipi wakati huu? Je, Mungu ameruhusu kikundi fulani cha watu kipigane vita? Au, je, huu ni wakati wa Mungu kuingilia kati na kupigana vita kwa niaba ya watumishi wake? Mungu ana maoni kuhusu vita vinavyopiganwa leo? Majibu ya maswali hayo yanapatikana katika makala ya mwisho ya mfululizo huu.