Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unachochewa na ‘Zawadi ya Bure’ ya Mungu?

Je, Unachochewa na ‘Zawadi ya Bure’ ya Mungu?

“Mungu apewe shukrani kwa ajili ya zawadi yake ya bure isiyoelezeka.”—2 KOR. 9:15.

NYIMBO: 121, 63

1, 2. (a) ‘Zawadi ya bure isiyoelezeka’ ya Mungu inahusisha nini? (b) Tutazungumzia maswali gani katika makala hii?

YEHOVA alitupatia zawadi bora zaidi ya upendo alipomtuma Mwana wake mzaliwa pekee aje duniani! (Yoh. 3:16; 1 Yoh. 4:9, 10) Mtume Paulo aliita “zawadi . . . ya bure isiyoelezeka” ya Mungu. (2 Kor. 9:15) Kwa nini aliita hivyo?

2 Paulo alijua kwamba dhabihu kamilifu ya Kristo ndiyo msingi wa utimizo wa ahadi zote nzuri za Mungu. (Soma 2 Wakorintho 1:20.) Hivyo, ‘zawadi hiyo ya bure isiyoelezeka’ inahusisha wema na upendo mshikamanifu ambao Yehova anatuonyesha kupitia Yesu. Kwa kweli, zawadi hiyo ni yenye kustaajabisha sana hivi kwamba haiwezi kufafanuliwa kwa njia ambayo tunaweza kuielewa kikamili. Basi, kupokea zawadi hiyo isiyo na kifani kunapaswa kutuathiri jinsi gani? Na zawadi hiyo inapaswa kutuchocheaje tunapojiandaa kwa ajili ya Ukumbusho wa kifo cha Kristo utakaofanywa Jumatano, Machi 23, 2016?

ZAWADI YA PEKEE KUTOKA KWA MUNGU

3, 4. (a) Unahisije mtu fulani anapokupa zawadi? (b) Zawadi ya pekee inawezaje kubadili maisha yako?

3 Unapopewa zawadi, bila shaka unafurahi sana. Hata hivyo, zawadi nyingine ni za pekee sana au zina umuhimu mkubwa hivi kwamba zinabadili maisha yetu. Kwa mfano, wazia kwamba umehukumiwa kifo kwa sababu ya kuhusishwa katika uhalifu fulani. Ghafla, mtu usiyemjua anajitokeza hadharani na kukubali hukumu hiyo kwa niaba yako. Yaani yuko tayari kufa kwa ajili yako! Ungehisije baada ya kupokea zawadi hiyo isiyo na kifani?

4 Ni wazi kwamba upendo huo usio na ubinafsi ungekusukuma ufikirie upya matendo yako na kubadili mtindo wako wa maisha. Huenda ungekuchochea uwe mkarimu, uwapende sana wengine, na kumsamehe yeyote aliyekukosea. Katika maisha yako yote, ungemthamini sana mtu huyo aliyekubali kuadhibiwa kwa niaba yako.

5. Ni katika njia gani zawadi ya Mungu ya fidia ni bora kuliko zawadi nyingine yoyote?

5 Hata hivyo, zawadi ambayo Yehova ametupa kupitia Kristo ni bora zaidi ya ile iliyoelezwa katika mfano huo. (1 Pet. 3:18) Fikiria hili: Kwa sababu ya kurithi dhambi, sote tunakabili adhabu ya kifo. (Rom. 5:12) Lakini upendo ulimchochea Yehova amtume Yesu duniani ili “aonje kifo kwa ajili ya kila mwanadamu.” (Ebr. 2:9) Si tu kwamba Yehova alimtuma Yesu afe kwa niaba yetu, bali pia aliweka msingi wa kuondoa kifo milele. (Isa. 25:7, 8; 1 Kor. 15:22, 26) Wale wote wanaomwamini Yesu watapata uzima wa milele, nao wataishi kwa amani na furaha duniani wakiwa raia wa Ufalme wa Mungu unaotawaliwa na Kristo, na watiwa mafuta, watatawala pamoja na Yesu katika Ufalme huo. (Rom. 6:23; Ufu. 5:9, 10) Zawadi hiyo kutoka kwa Yehova inahusisha baraka gani nyingine?

6. (a) Unatazamia kwa hamu baraka gani zinazotokana na zawadi ya Yehova? (b) Zawadi ya Mungu inatuchochea kufanya mambo gani matatu?

6 Zawadi hiyo kutoka kwa Yehova inahusisha pia kuponywa magonjwa yote, kubadili dunia yetu kuwa paradiso, na kufufuliwa kwa wafu. (Isa. 33:24; 35:5, 6; Yoh. 5:28, 29) Bila shaka, tunampenda Yehova na Mwana wake kwa kutupatia ‘zawadi hiyo ya bure isiyoelezeka.’ Hata hivyo tunapaswa kujiuliza, upendo wa Mungu unatuchochea kufanya nini? Acheni tuchunguze jinsi upendo wa Mungu unavyotuchochea (1) kufuata hatua za Yesu kwa ukaribu, (2) kuwapenda ndugu zetu, na (3) kuwasamehe wengine kutoka moyoni.

“UPENDO ALIO NAO KRISTO HUTULAZIMISHA”

7, 8. Tunapaswa kuhisije kuhusu upendo wa Kristo? Nao unapaswa kutuchochea tufanye nini?

7 Kwanza, ni lazima tuchochewe kuishi kwa ajili ya Kristo Yesu. Mtume Paulo alisema hivi: “Upendo alio nao Kristo hutulazimisha.” (Soma 2 Wakorintho 5:14, 15.) Paulo alitambua kwamba tukikubali upendo wa Kristo usio na kifani, utatulazimisha au kutuchochea tuishi kwa ajili yake. Tunapoelewa vizuri mambo ambayo Yehova ametufanyia na mioyo yetu inapochochewa na upendo wake, tunaanza kutamani kuishi kikamili kwa ajili ya Kristo Yesu. Tunaonyeshaje kwamba tuna tamaa hiyo?

8 Kumpenda Yehova kunatuchochea tuige mfano wa Kristo, kwa kutembea kama alivyotembea na kufuata hatua zake kwa ukaribu. (1 Pet. 2:21; 1 Yoh. 2:6) Tunapowatii Mungu na Kristo tunaonyesha kwamba tunawapenda. Yesu alisema hivi: “Yule aliye na amri zangu na kuzishika, huyo ndiye ambaye hunipenda. Naye anayenipenda atapendwa na Baba yangu, nami nitampenda na kujionyesha wazi kwake.”—Yoh. 14:21; 1 Yoh. 5:3.

9. Tunashinikizwa kufanya nini?

9 Wakati wa majira haya ya Ukumbusho, inafaa tuchunguze mtindo wetu wa maisha. Jiulize hivi: ‘Nimefanya mambo gani mazuri yanayoonyesha kwamba ninafuata hatua za Kristo Yesu? Ni mambo gani ninayoweza kuboresha?’ Ni muhimu kujichunguza kwa njia hiyo, kwa kuwa sikuzote tunashinikizwa kufuata mtindo wa maisha wa ulimwengu huu. (Rom. 12:2) Tusipojihadhari, tunaweza kuwa wafuasi wa wanafalsafa, wanamichezo au watu maarufu wa ulimwengu huu. (Kol. 2:8; 1 Yoh. 2:15-17) Tunawezaje kupinga jambo hilo?

10. Tunaweza kujiuliza maswali gani wakati wa majira haya ya Ukumbusho? Na majibu ya maswali hayo yatatuchochea kufanya nini? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

10 Tunaweza kutumia majira ya Ukumbusho kuwa fursa ya kuchunguza mavazi yetu, muziki na filamu tunazotazama, labda hata mambo tuliyohifadhi katika kompyuta, simu, na kompyuta zetu ndogo (tablets). Unapochunguza mavazi yako, jiulize hivi: ‘Ikiwa ningeenda mahali ambapo Yesu angekuwapo, je, ningeaibika kuvaa mavazi haya?’ (1 Timotheo 2:9, 10.) ‘Na ikiwa ningevaa, je, ingekuwa wazi kwa watu wote kwamba mimi ni mfuasi wa Kristo Yesu?’ Tunaweza kujiuliza maswali kama hayo tunapochagua muziki na filamu tunazotazama. ‘Je, Yesu angefurahia kutazama filamu hii au kusikiliza muziki huu? Iwapo angeazima simu au kompyuta yangu ndogo, je, ningeaibika kwa sababu ya mambo ambayo angeona humo?’ Unapofikiria kusudi la mchezo fulani wa video, jiulize hivi: ‘Je, ingekuwa vigumu kwangu kumweleza Yesu ni kwa nini ninapenda mchezo huu?’ Kumpenda Yehova kunapaswa kutuchochea tuache kabisa jambo lolote lisilomfaa mfuasi wa Kristo, haidhuru inatugharimu kiasi gani. (Mdo. 19:19, 20) Tulipojiweka wakfu kwa Yehova, tuliahidi kwamba hatutaishi tena kwa ajili yetu bali kwa ajili ya Kristo. Hivyo, hatupaswi kushikamana na jambo lolote linaloweza kutuzuia kufuata hatua za Kristo kwa ukaribu.—Mt. 5:29, 30; Flp. 4:8.

11. (a) Kumpenda Yehova na Yesu kunatuchocheaje katika kazi ya kuhubiri? (b) Upendo wetu unaweza kutuchocheaje tuwasaidie wengine kutanikoni?

11 Kumpenda Yesu pia kunatuchochea tuwe na bidii ya kuhubiri na kuwafundisha wengine. (Mt. 28:19, 20; Luka 4:43) Wakati wa majira ya Ukumbusho, tutapata fursa ya kuwa mapainia wasaidizi na kutumia saa 30 au 50 katika kazi ya kuhubiri. Je, unaweza kupanga vizuri mambo yako ili ufanye hivyo? Ndugu fulani mjane mwenye umri wa miaka 84, alihisi kwamba hangeweza kuwa painia msaidizi kwa sababu ya umri wake na matatizo ya kiafya. Hata hivyo, mapainia katika eneo aliloishi walimsaidia. Waliandaa usafiri na kuchagua vizuri eneo ambalo angeweza kuhubiri, ili aweze kufikia lengo lake la kuhubiri saa 30. Je, unaweza kumsaidia mtu fulani katika kutaniko lenu ili naye apate shangwe inayotokana na kufanya upainia msaidizi wakati wa majira ya Ukumbusho? Bila shaka, si wote tunaoweza kufanya upainia msaidizi wakati huo. Hata hivyo, tunaweza kutumia wakati na nguvu zetu kuongeza dhabihu yetu ya sifa kwa Yehova. Tunapofanya hivyo, tunaonyesha kwamba tunachochewa na upendo wa Kristo, kama ilivyokuwa kwa Paulo. Upendo wa Mungu unatuchochea tufanye jambo gani lingine?

TUNA WAJIBU WA KUPENDANA

12. Upendo wa Mungu unatuchochea kufanya nini?

12 Pili, upendo wa Mungu unatuchochea kuwapenda ndugu zetu. Mtume Yohana alitambua hilo, naye aliandika hivi: “Wapendwa, ikiwa Mungu alitupenda hivi, basi sisi wenyewe tuko chini ya wajibu wa kupendana.” (1 Yoh. 4:7-11) Naam, tukitaka kupendwa na Mungu ni lazima tutambue kwamba tuna wajibu wa kuwapenda ndugu zetu. (1 Yoh. 3:16) Tunawezaje kuonyesha kwamba tunawapenda Wakristo wenzetu?

13. Yesu aliweka mfano gani inapohusu kuwapenda wengine?

13 Fikiria mfano wa Yesu. Katika huduma yake, aliwajali sana watu wa hali ya chini. Aliwaponya watu wenye udhaifu mbalimbali, kama vile vipofu, vilema, viziwi, na mabubu. (Mt. 11:4, 5) Yesu alifurahia kuwafundisha watu wenye njaa ya kiroho, wale ambao viongozi wa dini ya Kiyahudi waliwaona kuwa “watu waliolaaniwa.” (Yoh. 7:49) Aliwapenda watu hao, naye alijitahidi kuwahudumia.—Mt. 20:28.

Je, unaweza kumsaidia ndugu au dada fulani aliyezeeka katika huduma? (Tazama fungu la 14)

14. Unaweza kufanya nini ili kuonyesha kwamba unawapenda ndugu zako?

14 Majira ya Ukumbusho yanakupa fursa ya kumwiga Yesu kwa kutenga wakati wa kuwafikiria ndugu na dada unaoweza kuwasaidia katika kutaniko lenu. Unapofanya hivyo, bila shaka utaona baadhi ya watu wanaoweza kunufaishwa na upendo wako. Labda kuna ndugu na dada waliozeeka ambao wanahitaji msaada. Je, unaweza kuwatembelea ndugu na dada hao wapendwa? Je, unaweza kuwapelekea chakula, kuwasaidia kazi za nyumbani, kuwapeleka kwenye mikutano, au kuhubiri nao? (Soma Luka 14:12-14.) Ni lazima turuhusu upendo wa Mungu utuchochee kuwasaidia na kuwaonyesha ndugu zetu kwamba tunawapenda.

KUWAONYESHA REHEMA NDUGU NA DADA ZETU

15. Tunapaswa kutambua nini?

15 Tatu, upendo wa Yehova unapaswa kutuchochea tuwasamehe ndugu na dada zetu. Kwa kuwa sote ni watoto wa mwanadamu wa kwanza, Adamu, tumerithi dhambi na adhabu yake, yaani kifo. Hakuna yeyote kati yetu anaweza kusema, “Sihitaji fidia.” Hata mtumishi mwaminifu zaidi wa Mungu anahitaji sana fadhili zisizostahiliwa za Yehova kupitia Kristo. Kila mmoja wetu anapaswa kutambua kwamba tumesamehewa deni kubwa sana. Kwa nini jambo hilo ni muhimu? Tunapata jibu katika mfano wa Yesu.

16, 17. (a) Tunajifunza nini katika mfano wa Yesu kuhusu mfalme na watumwa? (b) Baada ya kutafakari mfano wa Yesu, umeazimia kufanya nini?

16 Yesu alisimulia mfano wa mfalme ambaye alimsamehe mtumwa wake deni kubwa la talanta 10,000, au dinari 60,000,000. Hata hivyo, mtumwa aliyesamehewa deni kubwa zaidi hakuwa tayari kumsamehe mtumwa mwenzake aliyekuwa na deni dogo, yaani dinari 100. Mfalme alikasirika sana alipojua kwamba mtumwa aliyeonyeshwa rehema alikataa kumsamehe mtumwa mwenzake. Mfalme alisema hivi: “Mtumwa mwovu, nilifuta lile deni lote kwa ajili yako, uliponisihi. Haikukupasa wewe, nawe, kuwa na rehema juu ya mtumwa mwenzako, kama mimi pia nilivyokuwa na rehema juu yako?” (Mt. 18:23-35) Naam, rehema ambayo mfalme aliionyesha kwa njia ya pekee ilipaswa kumchochea mtumwa huyo amsamehe mtumwa mwenzake. Hivyo basi, upendo na rehema ya Mungu inapaswa kutuchochea tufanye nini?

17 Majira ya Ukumbusho yanatupatia fursa ya kujichunguza ikiwa tuna kinyongo dhidi ya ndugu au dada fulani. Ikiwa ndivyo, basi huo ungekuwa wakati mzuri wa kumwiga Yehova, ambaye yuko “tayari kusamehe.” (Zab. 86:5; Neh. 9:17) Tukithamini rehema ya Yehova ya kufuta kabisa deni letu kubwa, tutakuwa tayari kuwasamehe wengine kutoka moyoni. Ni wazi kwamba hatuwezi kutarajia Yehova atupende au atusamehe ikiwa hatuwapendi na kuwasamehe wengine. (Mt. 6:14, 15) Ni kweli kwamba kuwasamehe wengine hakutabadili yaliyopita, hata hivyo kutatusaidia tufurahie zaidi wakati ujao.

18. Upendo wa Mungu ulimsaidiaje Lily avumilie udhaifu wa Carol?

18 Huenda isiwe rahisi ‘kuvumilia’ kila siku udhaifu wa ndugu na dada zetu. (Soma Wakolosai 3:13, 14; Waefeso 4:32.) Kwa mfano, Lily ni dada mseja kutanikoni ambaye alijitolea kumsaidia mjane fulani aitwaye Carol. [1] Lily alimsafirisha Carol popote alipotaka, alimsaidia kununua bidhaa, na alimtendea kwa fadhili katika njia nyingine nyingi. Licha ya mambo yote ambayo Lily alifanya, nyakati zote Carol alilalamika na haikuwa rahisi kumsaidia. Hata hivyo, Lily alikazia fikira sifa nzuri za Carol. Aliendelea kumsaidia kwa miaka kadhaa hadi Carol alipougua na kufa. Ingawa haikuwa rahisi kumsaidia, Lily anasema hivi: “Ninatazamia kwa hamu kumwona Carol atakapofufuliwa. Ninataka kumjua atakapokuwa mkamilifu.” Naam, upendo wa Mungu unaweza kutuchochea tuwavumilie ndugu na dada zetu huku tukitazamia wakati ambapo udhaifu wa kibinadamu hautakuwapo milele.

19. ‘Zawadi ya bure isiyoelezeka ya Mungu’ inakuchocheaje?

19 Kwa kweli Yehova ametupatia “zawadi yake ya bure isiyoelezeka.” Sikuzote na tumshukuru kwa zawadi hiyo yenye thamani! Wakati wa majira haya ya Ukumbusho, tuna fursa za kutafakari na kuthamini mambo yote ambayo Yehova na Yesu wametufanyia. Acheni upendo wao utuchochee kufuata hatua za Yesu kwa ukaribu, kuwasaidia na kuwaonyesha ndugu zetu kwamba tunawapenda, na kuwasamehe ndugu zetu kutoka moyoni.

^ [1] (fungu la 18) Baadhi ya majina katika makala hii yamebadilishwa.