Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HABARI KUU | MTU UNAYEMPENDA ANAPOKUFA

Wafu Wataishi Tena!

Wafu Wataishi Tena!

Huenda unakumbuka kwamba Gail, aliyetajwa mwanzoni mwa mfululizo huu, alikuwa na mashaka kama angeweza kukabiliana na huzuni ya kifo cha mume wake, Rob. Hata hivyo, anatarajia kumuona tena Rob katika ulimwengu mpya ambao Mungu ameahidi. Anasema,“andiko ninalopenda sana ni Ufunuo 21:3, 4.” Linasema hivi: “Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao. Naye atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.”

Gail anasema hivi: “Ahadi hiyo inafariji sana. Ninawasikitikia sana watu waliofiwa ambao hawajui lolote kuhusu tumaini hili la kuwaona tena wapendwa wao.” Gail anatenda kulingana na imani yake kwa kujitolea kueneza injili wakati wote, akiwahubiria jirani zake kuhusu ahadi za Mungu za wakati ujao ambapo “kifo hakitakuwapo tena.”

Ayubu alikuwa na uhakika kwamba ataishi tena

Huenda ukasema ‘Haiwezekani!’ Lakini fikiria mfano wa mwanaume aliyeitwa Ayubu. Alikuwa na ugonjwa mbaya sana. (Ayubu 2:7) Ingawa Ayubu alitamani kufa, bado aliamini kwamba Mungu ana uwezo wa kumfufua ili aishi tena duniani. Alisema hivi kwa uhakika: “Laiti ungenificha katika Kaburi . . . Wewe utaita, na mimi mwenyewe nitakujibu. Kwa kuwa utaitamani sana kazi ya mikono yako.” (Ayubu 14:13, 15) Ayubu alikuwa na uhakika kwamba Mungu wake hangemsahau na angetamani kumfufua.

Hivi karibuni, Mungu atamfufua Ayubu pamoja na watu wengine wengi wakati dunia hii itakapogeuzwa kuwa paradiso. (Luka 23:42, 43) Biblia inatuhakikishia hivi katika andiko la Matendo 24:15, “Kutakuwa na ufufuo.” Pia, Yesu alisema hivi: “Msistaajabie jambo hili, kwa sababu saa inakuja ambayo wale wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti yake na kutoka.” (Yohana 5:28, 29) Ayubu ataona ahadi hiyo ikitimizwa. Atarudia “nguvu za ujana wake” na mwili wake utakuwa “laini kuliko wakati wa ujana.” (Ayubu 33:24, 25) Wale wote watakaopata kibali cha Mungu watafurahia jambo hilo watakapofufuliwa ili waishi duniani.

Ikiwa umefiwa na mtu unayempenda, huenda mambo tuliyozungumzia yasiondoe moja kwa moja huzuni yako. Hata hivyo, ukitafakari ahadi za Mungu zinazopatikana katika Biblia, utapata tumaini la kweli na nguvu za kuvumilia.—1 Wathesalonike 4:13.

Je, ungependa kujifunza mengi zaidi kuhusu jinsi ya kukabiliana na huzuni? Au je, una maswali mengine, kama vile “Kwa nini Mungu ameruhusu uovu na mateso?” Tafadhali tembelea tovuti yetu ya jw.org/sw ili uone jinsi Biblia inavyotoa majibu yanayofariji.