Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Baba ya Yosefu alikuwa nani?

Yosefu, seremala wa Nazareti, alikuwa baba mlezi wa Yesu. Lakini baba ya Yosefu alikuwa nani? Historia ya ukoo wa Yesu katika Injili ya Mathayo inamtaja baba ya Yosefu kuwa ni Yakobo huku Luka akisema kwamba Yosefu alikuwa “mwana wa Heli.” Kwa nini majina hayo yanatofautiana?—Luka 3:23; Mathayo 1:16.

Simulizi la Mathayo linasema hivi: “Yakobo akamzaa Yosefu.” Mathayo anatumia neno la Kigiriki linaloonyesha wazi kwamba Yakobo alikuwa baba mzazi wa Yosefu. Hivyo Mathayo alikuwa akionyesha ukoo wa asili wa Yosefu, yaani, ukoo wa kifalme wa Daudi. Kupitia ukoo huo, Yesu aliyelelewa na Yosefu alirithi haki ya kuwa mtawala.

Kwa upande mwingine, simulizi la Luka linasema: “Yosefu, mwana wa Heli.” Maneno hayo, “mwana wa,” yanaweza kumaanisha “mwana mkwe wa.” Kisa kama hicho kinapatikana katika Luka 3:27 ambapo Shealtieli ambaye baba yake mzazi alikuwa Yekonia, anatajwa kuwa “mwana wa Neri.” (1 Mambo ya Nyakati 3:17; Mathayo 1:12) Inaonekana kuwa Shealtieli alimwoa binti wa Neri, hivyo akawa mwana mkwe wake. Vivyo hivyo, Yosefu alikuwa mwana wa Heli katika njia hiyo, kwa kuwa alimwoa binti ya Heli aitwaye Maria. Kwa hiyo, Luka anautaja ukoo wa Yesu “kulingana na mwili,” kupitia mama yake mzazi, Maria. (Waroma 1:3) Hivyo, Biblia inatueleza kuhusu pande mbili tofauti na muhimu za ukoo wa Yesu.

Ni aina gani za vitambaa na rangi zilizopatikana katika nyakati za Biblia?

Sufu iliyopakwa rangi iliyopatikana karibu na bahari ya chumvi ikiwa na tarehe ya kabla ya mwaka 135 W.K.

Manyoya ya kondoo, mbuzi na ngamia yalitumika sana kutengenezea vitambaa katika eneo la kale la Mashariki ya Kati. Vitambaa vilivyopatikana sana vilikuwa vya sufu, na mara nyingi Biblia inataja kuhusu kondoo, kukata manyoya, na mavazi ya sufu. (1 Samweli 25:2; 2 Wafalme 3:⁠4; Ayubu 31:20) Mimea ya kitani iliyolimwa huko Misri na Israeli ilitumiwa kutengeneza mavazi. (Mwanzo 41:42; Yoshua 2:6) Inawezekana kwamba Waisraeli katika nyakati za Biblia hawakulima zao la pamba, hata hivyo, Maandiko yanataja kuhusu matumizi ya vitambaa vya pamba huko Uajemi. (Esta 1:6) Vitambaa vya hariri viliuzwa kwa bei ghali zaidi na inawezekana kwamba vililetwa na wafanyabiashara kutoka Mashariki ya Mbali.​—Ufunuo 18:​11, 12.

Kitabu Jesus and His World kinasema hivi: “Sufu ilikuwa na rangi mbalimbali za asili, kuanzia rangi nyeupe hadi rangi ya kahawia iliyo na madoa-madoa.” Isitoshe, sufu ilipakwa rangi. Rangi ya zambarau iliyokuwa na gharama kubwa ilitokana na aina fulani ya konokono na mimea mbalimbali, mizizi, majani na wadudu walitumika kutengeneza rangi kama vile nyekundu, njano, bluu na nyeusi.