Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HABARI KUU | KWA NINI YESU ALITESEKA NA KUFA?

Je, Kweli Yalitukia?

Je, Kweli Yalitukia?

Mwaka wa 33 W.K., Yesu Mnazareti aliuawa. Alishtakiwa kwa uwongo kuwa mchochezi, akapigwa kikatili, na kutundikwa mtini. Alikufa kwa maumivu makali sana. Lakini Mungu alimfufua, na siku 40 baadaye, Yesu akapaa kwenda mbinguni.

Simulizi hilo la pekee linatoka katika Injili nne za Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, ambazo hujulikana kama Agano Jipya. Je, kweli mambo hayo yalitukia? Hilo ni swali muhimu sana. Ikiwa mambo hayo hayakutukia, imani ya Kikristo ni bure na tumaini la uzima wa milele katika Paradiso ni ndoto tu. (1 Wakorintho 15:14) Kwa upande mwingine, ikiwa mambo hayo yalitukia, basi kuna tumaini zuri ambalo unaweza kupata. Kwa hiyo, masimulizi ya Injili ni ya kweli au hadithi tu?

HABARI ZA UHAKIKA

Tofauti na hekaya zilizobuniwa, masimulizi ya Injili ni sahihi na yanaeleza mambo hususa. Kwa mfano, masimulizi hayo yamejaa majina ya maeneo halisi ambayo yanaweza kutembelewa leo. Yanataja kuhusu watu halisi, ambao wanahistoria wamethibitisha kwamba waliishi.—Luka 3:1, 2, 23.

Yesu anatajwa na waandishi wa karne ya kwanza na ya pili. * Kifo chake kinachofafanuliwa katika Injili kinapatana na jinsi Waroma walivyokuwa wakiwaua wahalifu. Pia, matukio yanaelezwa kwa unyoofu kutia ndani hata makosa ya baadhi ya wanafunzi wa Yesu. (Mathayo 26:56; Luka 22:24-26; Yohana 18:10, 11) Mambo yote hayo yanaonyesha wazi kwamba waandishi wa Injili walikuwa wanyoofu na walisema mambo kwa usahihi kumhusu Yesu.

UFUFUO WA YESU

Ingawa watu wengi hukubali kwamba Yesu aliishi na kufa, baadhi wana mashaka na ufufuo wake. Hata mitume wake hawakuamini waliposikia kwa mara ya kwanza kwamba amefufuliwa. (Luka 24:11) Hata hivyo, waliamini kwamba Yesu amefufuliwa walipomwona katika pindi tofauti-tofauti. Hata katika kisa kimoja, watu 500 walimwona Yesu.—1 Wakorintho 15:6.

Bila kuogopa kukamatwa na kuuawa, wanafunzi wa Yesu waliwatangazia watu wote ufufuo wa Yesu kwa ujasiri—hata wale waliomuua. (Matendo 4:1-3, 10, 19, 20; 5:27-32) Je, wanafunzi hao wote wangekuwa na ujasiri kama wasingekuwa na uhakika kwamba Yesu amefufuliwa? Kwa kweli, ufufuo wa Yesu umewachochea watu wengi ulimwenguni wavutiwe na Ukristo sasa na wakati uliopita.

Masimulizi ya Injili ya kifo na ufufuo wa Yesu ni sahihi. Ukiyasoma kwa makini utapata uhakika kwamba matukio hayo ni ya kweli. Usadikisho wako utaimarishwa zaidi ukielewa kwa nini mambo hayo yalitukia. Makala inayofuata inaeleza jambo hilo.

^ fu. 7 Tasito, aliyezaliwa mwaka wa 55 W.K., aliandika kuwa, “Kristo, ambaye ndiye chanzo cha jina [Wakristo], alihukumiwa kifo na gavana wetu Pontio Pilato wakati wa utawala wa Tiberio.” Yesu anatajwa pia na Suetonius (karne ya kwanza); mwanahistoria wa Kiyahudi Yosefo (karne ya kwanza); na Plini Mdogo, gavana wa Bithinia (mwanzoni mwa karne ya pili).