Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HABARI KUU

Kwa Nini Yesu Aliteseka na Kufa?

Kwa Nini Yesu Aliteseka na Kufa?

“Kupitia mtu mmoja [Adamu] dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi.”—Waroma 5:12

Utajibuje ukiulizwa, “Je, unataka kuishi milele?” Huenda watu wengi wakasema kwamba wanataka lakini wanahisi haiwezekani. Wanasema kifo ni sehemu ya maisha na hakiepukiki.

Hata hivyo, tuseme swali hilo ligeuzwe na uulizwe, “Uko tayari kufa?” Katika hali ya kawaida, watu wengi watajibu hapana. Hilo linaonyesha nini? Ni asili yetu kutamani kuishi, ijapokuwa tunakabili matatizo. Biblia inaonyesha Mungu aliwaumba wanadamu wakiwa na tamaa ya kuishi. Ndiyo maana inasema kuwa, “wakati usio na kipimo ameuweka ndani ya moyo wao.”—Mhubiri 3:11.

Hata hivyo, ukweli ni kwamba wanadamu hawaishi milele. Hivyo basi, ni nini kilitukia? Na Je, Mungu amefanya jambo lolote ili kurekebisha hali hiyo? Majibu ya Biblia yanatia moyo, na yanahusiana na mateso na kifo cha Yesu.

NI NINI KILICHOTUKIA?

Sura tatu za kwanza za kitabu cha Biblia cha Mwanzo zinatueleza kwamba Mungu aliwapa mume na mke wa kwanza, Adamu na Hawa, tarajio la kuishi milele na aliwaambia jambo la kufanya ili tarajio hilo litimie. Kisha simulizi hilo linaeleza jinsi walivyoshindwa kumtii Mungu na wakapoteza tarajio hilo. Simulizi hilo linaelezwa kwa njia rahisi hivi kwamba baadhi ya watu wanaona kuwa ni hadithi. Kitabu cha Mwanzo kinaeleza mambo ya kweli kama vitabu vya Injili. *

Uasi wa Adamu ulitokeza nini? Biblia inasema hivi: “Kupitia mtu mmoja [Adamu] dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, na hivyo kifo kikaenea kwa watu wote kwa sababu wote walikuwa wamefanya dhambi.” (Waroma 5:12) Kwa kumwasi Mungu, Adamu alitenda dhambi. Hivyo akapoteza tarajio la kuishi milele na hatimaye akafa. Tukiwa wazao wake, tumerithi dhambi. Hivyo, tunaugua, tunazeeka, na kufa. Ufafanuzi huo unapatana na jambo ambalo wanasayansi wamegundua kuhusu jinsi watoto wanavyorithi tabia fulani kutoka kwa wazazi wao. Lakini je, Mungu amefanya lolote ili kurekebisha jambo hilo?

JAMBO AMBALO MUNGU AMEFANYA

Mungu amefanya mpango ili kurudisha, au kununua tena, kitu ambacho Adamu aliwapotezea wazao wake, yaani, tumaini la kuishi milele. Mungu alifanyaje?

“Mshahara ambao dhambi hulipa ni kifo,” inasema Biblia katika Waroma 6:23. Hilo linamaanisha kwamba kifo ni matokeo ya dhambi. Adamu alitenda dhambi, hivyo akafa. Vivyo hivyo, tunatenda dhambi na hivyo lazima tupate mshahara wa dhambi, yaani, kifo. Ingawa hatuna hatia, tumerithi dhambi hiyo. Hivyo, Mungu alimtuma Mwana wake, Yesu, abebe ‘mshahara wa dhambi’ kwa ajili yetu. Jambo hilo linawezekanaje?

Kifo cha Yesu kinatufungulia njia ya kupata maisha yenye furaha milele

Kwa kuwa mtu mmoja, mwanadamu mkamilifu Adamu, alituletea dhambi na kifo kwa sababu ya kutotii, mwanadamu mkamilifu aliyetii hadi kifo alihitajika ili kutuondolea mzigo huo. Biblia inaeleza jambo hilo kwa njia hii: “Kama vile kupitia kutotii kwa mtu mmoja wengi walifanywa watenda-dhambi, vivyo hivyo pia kupitia kutii kwa mtu mmoja wengi watafanywa kuwa waadilifu.” (Waroma 5:19) Yesu alikuwa huyo “mtu mmoja.” Alitoka mbinguni, akawa mwanadamu mkamilifu *, na akafa kwa niaba yetu. Matokeo ni kwamba tunaweza kuwa na msimamo mzuri mbele za Mungu na kupata tarajio la kuishi milele.

KWA NINI YESU ALITESEKA NA KUFA?

Hata hivyo, kwa nini ilikuwa lazima Yesu afe ili kutimiza hilo? Je, Mungu Mweza-Yote asingeweza kutoa agizo kwamba wazao wa Adamu waruhusiwe kuishi milele? Ni kweli alikuwa na mamlaka ya kufanya hivyo. Lakini kufanya hivyo kungepuuza amri yake kwamba mshahara wa dhambi ni kifo. Amri hiyo si kanuni ndogo inayoweza kupuuzwa au kubadilishwa kulingana na hali. Ni msingi wa haki ya kweli.—Zaburi 37:28.

Ikiwa Mungu angepuuza haki katika kisa hiki, watu wangejiuliza ikiwa atafanya hivyo tena katika mambo mengine pia. Kwa mfano, je, angetumia haki kuamua ni nani kati ya wazao wa Adamu anayestahili kupata uzima wa milele? Je, anaweza kutumainiwa katika kutimiza ahadi zake? Kutumia haki katika kutuletea ukombozi kunatuhakikishia kwamba sikuzote Mungu atafanya lililo sawa.

Kupitia kifo cha Yesu cha kidhabihu, Mungu alituletea tarajio la kuishi milele katika Paradiso hapa duniani. Ona maneno ya Yesu katika Yohana 3:16: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.” Hivyo, kifo cha Yesu kinaonyesha Mungu anavyotenda haki, lakini pia kinaonyesha jinsi anavyowapenda sana wanadamu.

Hata hivyo, kwa nini Yesu alihitaji kuteseka na kufa kwa maumivu makali kama inavyoonyeshwa katika Injili? Kwa kupata majaribu makali na kuwa mwaminifu, Yesu alipinga dai la Shetani kwamba wanadamu hawawezi kuendelea kuwa washikamanifu kwa Mungu wanapojaribiwa. (Ayubu 2:4, 5) Dai hilo lilionekana halali Shetani alipomshawishi Adamu mkamilifu atende dhambi. Lakini Yesu—ambaye alikuwa sawa kabisa na Adamu—aliendelea kuwa mwaminifu ingawa alipata mateso makali. (1 Wakorintho 15:45) Hivyo akathibitisha kwamba Adamu angeweza pia kumtii Mungu ikiwa angetaka. Kwa kuvumilia majaribu, Yesu alituwekea mfano wa kuiga. (1 Petro 2:21) Kutokana na utii wake, Mungu alimthawabisha Mwana wake, Yesu kwa kumpa uhai usioweza kufa mbinguni.

JINSI UNAVYOWEZA KUNUFAIKA

Kifo cha Yesu ni halisi. Njia ya kupata uzima wa milele iko wazi. Je, unataka kuishi milele? Yesu alituonyesha jambo la kufanya aliposema hivi: “Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.”—Yohana 17:3.

Wachapishaji wa gazeti hili wanakualika ujifunze mengi zaidi kumhusu Mungu wa kweli Yehova, na kumhusu Mwana wake, Yesu Kristo. Mashahidi wa Yehova katika eneo unaloishi watafurahi kukusaidia. Pia unaweza kupata habari zaidi kwa kutembelea tovuti yetu ya www.pr418.com/sw.

^ fu. 8 Soma makala yenye kichwa “The Historical Character of Genesis,” ya kitabu cha Insight on the Scriptures, buku la 1, ukurasa wa 922, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 13 Yehova alihamisha uhai wa Mwana wake kutoka mbinguni na kuutia katika tumbo la Maria, na roho ya Mungu ikamlinda Yesu ili asirithi kutokamilika kutoka kwa Maria.—Luka 1:31, 35.