Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Kutii Angalisho Lenye Kutolewa Mbele ya Wakati Kunaweza Kuokoa Uzima Wako!

Kutii Angalisho Lenye Kutolewa Mbele ya Wakati Kunaweza Kuokoa Uzima Wako!

Mwezi wa 12, 2004, tetemeko la inchi la kipimo cha 9.1 lilitikisa Simeulue, kisiwa kimoja cha kaskazini-mangaribi mwa Sumatra, inchi ya Indonesia. Watu wote wenye walikuwa pembeni ya bahari waliangalia katika bahari. Maji yalianza kupunguka kwa njia yenye haiko ya kawaida. Mara moja, watu wakaanza kukimbilia kwenye vilima, na kulalamika, “Smong! Smong!” neno la eneo hilo lenye kutumiwa ili kumaanisha tsunami (mafuriko makubwa). Katika dakika 30, maji yenye kuletwa na upepo mukali yalijitupa kwenye eneo la pembeni ya bahari, na kuharibisha nyumba na vijiji vingi.

Kisiwa cha Simeulue kilikuwa mahali pa kwanza penye palipigwa na tsunami hiyo yenye ilitokeza uharibifu mukubwa. Lakini, juu ya wakaaji 78 000 wa kisiwa hicho, ni watu 7 tu ndio walikufa. Sababu gani ni watu kidogo tu ndio walikufa? * Wakaaji wa kisiwa hicho wanazoea kusema hivi: ‘Kama tetemeko la nguvu linatokea na bahari inajikokota, kimbilia kwenye vilima, kwa sababu bahari itarudia haraka.’ Watu wa kisiwa hicho wamejifunza kutambua kama tsunami iko karibu kwa kuangalia mabadiliko katika bahari. Kutii angalisho lenye lilitolewa mbele ya wakati kuliokoa uzima wao.

Biblia inazungumuzia tukio la kuhuzunisha lenye kuwa karibu, ni kusema, ‘ziki kubwa [mateso makubwa] ya namna ambayo haijapata kutukia tangu mwanzo wa ulimwengu mupaka sasa, hapana, wala haitatukia tena.’ (Mathayo 24:21) Lakini huo hautakuwa mwisho wa dunia yetu kupitia matendo ya wanadamu ao kupitia musiba fulani wa asili, kwa sababu Mungu anakusudia dunia ibakie milele. (Mhubiri 1:4) Lakini, ziki hiyo yenye kuwa karibu ni njia Mungu atatumia ili ‘kuwaharibisha wale wanaoharibisha dunia.’ Itakuwa mwisho wa ubaya wote na mateso yote. (Ufunuo 11:18; Methali 2:22) Hiyo itakuwa baraka kweli!

Tena, tofauti na tsunamis mbalimbali, matetemeko ya inchi, ao milipuko ya volkano, uharibifu wenye utatokea wakati unaokuja hautaua watu wenye hawako na kosa. Biblia inasema kama “Mungu ni upendo.” Mungu huyo ambaye jina lake ni Yehova, anaahidi kama “waadilifu [wenye haki] wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake.” (1 Yohana 4:8; Zaburi 37:29) Sasa, namna gani unaweza kuokoka ziki kubwa na kufurahia baraka zenye Mungu anaahidi? Siri ni kutii angalisho lenye kutolewa mbele ya wakati!

TAMBUA MABADILIKO MAKUBWA YENYE KUTOKEA KATIKA DUNIA

Hatuwezi kujua tarehe ubaya wote na mateso yote yataisha, kwa sababu Yesu alisema hivi: ‘Kuhusu siku ile na saa ile hakuna mutu anayejua, wala malaika wa mbinguni wala Mwana, ila Baba tu.’ Lakini, Yesu alitutia moyo ‘tuendelee kukesha.’ (Mathayo 24:36; 25:13) Sababu gani? Biblia inatufasiria mambo yenye yatatokea katika dunia mbele Mungu alete mwisho. Mabadiliko ya mara moja yenye yalitokea katika bahari yalisaidia wakaaji wa kisiwa cha Simeulue wajue kama tsunami ilikuwa karibu kutokea. Kisanduku chenye kuwa katika habari hii kinaonyesha mabadiliko fulani kati ya yale yenye kuzungumuziwa katika Biblia.

Kwa kweli, mabadiliko ao hali fulani kati ya hizo zenye kuonyeshwa katika kisanduku zilitokea zamani kwa kiasi fulani, lakini haiko kwa wakati uleule. Hata hivyo, Yesu alisema kama wakati tungeona “mambo yote hayo,” tungejua kama mwisho uko karibu. (Mathayo 24:33) Ujiulize, ‘Ni wakati gani katika historia mambo hayo yenye kuelezwa (1) yametokea kwa kiasi kikubwa sana katika dunia yote, (2) yametokea kwa wakati uleule, na (3) yamekuwa mengi zaidi sana kuliko zamani?’ Ni wazi kama tunaishi wakati huo.

MUNGU ANAONYESHA KAMA ANATUPENDA

Presidenti mumoja wa zamani wa inchi ya Amerika alisema hivi: “Angalisho zenye kutolewa mbele ya wakati . . . zinaokoa uzima.” Kisha tsunami hiyo ya 2004, chombo fulani cha kutoa angalisho kiliwekwa katika eneo lenye lilipigwa nayo ili watu wasikufe wakati tsunami hiyo itatokea tena. Mungu pia amefanya vile. Amekamata mipango juu ya kutolea watu angalisho mbele mwisho ufike. Biblia ilitabiri hivi: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.”—Mathayo 24:14.

Mwaka jana tu, Mashahidi wa Yehova walifanya saa karibu miliare mbili katika kazi ya kuhubiri habari njema katika inchi 240 na katika luga zaidi ya 700. Kazi hiyo ya kuhubiri ndilo jambo lenye kuhakikisha sana kama mwisho uko karibu. Kwa sababu wanapenda majirani wao, Mashahidi wa Yehova wanafanya yao yote ili kuambia wengine juu ya siku ya hukumu ya Mungu yenye iko karibu sana. (Mathayo 22:39) Kwa sababu habari hii inaweza kukuletea faida, hilo linaonyesha kama Mungu anakupenda. Kumbuka kama, ‘[Mungu] hataki yeyote aangamizwe bali [lakini] anataka wote wafikie toba.’ (2 Petro 3:9) Utaitika upendo wa Mungu na kutii angalisho lenye anakutolea mbele ya wakati?

KIMBILIA MAHALI KWENYE KUKO USALAMA!

Kumbuka kama wakaaji wa vijiji vya Simeulue vya pembeni ya bahari walikimbilia kwenye vilima wakati waliona maji ya bahari yanapunguka; hawakungoja maji yarudie tena. Walipona kwa sababu walifanya haraka. Ili kuokoka ziki yenye kuwa karibu, wewe pia unapaswa kukimbilia kwenye vilima kwa njia ya mufano, mbele ikuwe kuchelewa. Namna gani? Nabii Isaya aliongozwa na roho ya Mungu ili kuandika mualiko wenye kuchochea ambao unatolewa katika “siku za mwisho,” ni kusema, wakati wenye tunaishi leo. Mualiko huo unasema hivi: ‘Njooni [mukuje], tuende juu kwenye mulima wa Yehova, . . . atatufundisha njia zake, nasi tutatembea katika mapito yake.’—Isaya 2:2, 3.

Kuenda juu ya mulima kunakusaidia kuona mambo muzuri na ni mahali kwenye kuko usalama. Katika njia hiyohiyo, kujua njia za Mungu kupitia Biblia kuko kunasaidia mamilioni ya watu leo katika dunia yote wafanye mabadiliko yenye kuleta faida katika maisha yao. (2 Timotheo 3:16, 17) Kwa kufanya vile, wanaanza ‘kutembea katika mapito [ya Mungu]’ na wanakubaliwa na kulindwa naye.

Utaitika mualiko huo na kupata ulinzi wenye Mungu anatoa kwa upendo katika siku hizi ngumu? Tunakutia moyo uchunguze kwa uangalifu ushuhuda wa Maandiko wenye kuonyesha kama tunaishi katika “siku za mwisho,” ambao unaonyeshwa katika kisanduku chenye kuwa katika habari hii. Mashahidi wa Yehova wa eneo lenu watafurahi kukutolea musaada wowote wenye unaweza kuwa nao lazima ili kuelewa maandiko muzuri na pia namna ya kuyatumikisha katika maisha yako. Ao unaweza kupata majibu ya maulizo yako kwenye adresi yetu ya Internete www.pr418.com. Fungua kichwa MAFUNDISHO YA BIBLIA > MAJIBU YA MASWALI YA BIBLIA.

^ fu. 3 Tsunami hiyo ya mwaka wa 2004 iliua watu zaidi ya 220 000. Ilikuwa moja kati ya tsunamis zenye ziliharibu zaidi katika historia.