Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Ni wakati gani watu wa Mungu walichukuliwa mateka na Babiloni Mkubwa?

Utekwa huo wa kiroho ulianza karne ya pili W.K. hadi mwaka wa 1919. Kwa nini uelewaji wetu wa zamani ulihitaji kurekebishwa?

Kuna uthibitisho mwingi unaoonyesha kwamba utekwa huo uliisha mwaka wa 1919 Wakristo watiwa mafuta walipokusanywa katika kutaniko lililopangwa upya. Fikiria hili: Watu wa Mungu walijaribiwa na kusafishwa baada ya Ufalme wa Mungu kusimamishwa mbinguni mwaka wa 1914. * (Mal. 3:1-4) Kisha, mwaka wa 1919, Yesu alimweka rasmi “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” awaongoze watu wa Mungu waliosafishwa na awape chakula “kwa wakati unaofaa.” (Mt. 24:45-47) Huo ndio mwaka ambao watu wa Mungu walianza kurudi katika milki yao ya kiroho waliyopewa na Mungu. Ulikuwa pia wakati ambapo walikombolewa kutoka katika utekwa wa mfano wa Babiloni Mkubwa. (Ufu. 18:4) Hata hivyo, utekwa huo ulianza lini?

Kwa miaka mingi, tulieleza kwamba utekwa huo ulianza mwaka wa 1918 na ulidumu kwa muda mfupi watu wa Mungu walipokuwa chini ya mamlaka ya Babiloni Mkubwa. Kwa mfano, gazeti la Mnara wa Mlinzi la Machi 15, 1992, lilieleza hivi: “Hata hivyo, kama vile watu wa Mungu wa kale walivyoingizwa katika utumwa wa Kibabuloni kwa muda fulani, katika 1918 watumishi wa Yehova walipata kuingia katika kadiri fulani ya utumwa wa Babuloni Mkubwa.” Lakini utafiti zaidi umeonyesha kwamba utekwa huo ulianza miaka mingi kabla ya mwaka wa 1918.

Kwa mfano, acheni tufikirie unabii fulani uliotabiri utekwa huo na kuachiliwa huru kwa watu wa Mungu. Unapatikana katika Ezekieli 37:1-14. Katika maono, Ezekieli aliona bonde lililojaa mifupa. Yehova alimweleza kwamba mifupa hiyo inawakilisha “nyumba nzima ya Israeli.” Katika utimizo mkubwa zaidi, unabii huo wa kurudishwa kwa watu wa Mungu unawahusu “Israeli wa Mungu.” (Gal. 6:16; Mdo. 3:21) Kisha, Ezekieli aliona mifupa hiyo ikianza kuwa hai nayo ikawa jeshi kubwa. Maono hayo yalionyesha kwa njia bora sana ufufuo wa kiroho wa watu wa Mungu ambao ulifikia upeo wakati wa matukio ya mwaka wa 1919. Lakini maono hayo yanafunua utekwa huo ungedumu kwa muda gani?

Kwanza, tunasoma kwamba mifupa hiyo ilikuwa ama “imekauka” au “mikavu sana.” (Eze. 37:2, 11) Hilo linaonyesha kwamba mifupa hiyo ilikuwa ya watu ambao walikuwa wamekufa kwa muda mrefu sana. Pili, mifupa hiyo ilirudishiwa uhai hatua kwa hatua, si ghafla. Mwanzoni, kulikuwa na kelele, sauti ya kugongana, nayo “ikaanza kukaribiana, mfupa kwa mfupa.” Kisha, “kano na nyama” zikaongezwa. Halafu, mifupa, kano, na nyama zikafunikwa na ngozi. Mwishowe, “pumzi ikaanza kuingia ndani yao, nao wakaanza kuishi.” Kisha, Yehova akawaweka watu hao waliorudishiwa uhai katika nchi yao. Mambo hayo yote yangechukua wakati.—Eze. 37:7-10, 14.

Utekwa wa Israeli la kale ulidumu kwa muda mrefu. Ulianza mwaka wa 740 K.W.K. ufalme wa kaskazini wa makabila kumi ulipoanguka na watu wengi wakapelekwa uhamishoni. Kisha, katika mwaka wa 607 K.W.K. Yerusalemu lilipoharibiwa, watu wa ufalme wa kusini wa Yuda walipelekwa uhamishoni pia. Kipindi hicho cha utekwa kiliisha mwaka wa 537 K.W.K. Wayahudi waliobaki waliporudi Yerusalemu kujenga upya hekalu na kurudisha ibada safi.

Tukiwa na habari hizo za Kimaandiko akilini, tunaona wazi kwamba utekwa wa watu wa Mungu chini ya Babiloni Mkubwa lazima uwe ulichukua muda mrefu zaidi, si tu kuanzia mwaka wa 1918 hadi 1919. Utekwa huo unalingana na wakati ambapo magugu ya mfano yangekua pamoja na ngano inayofananisha “wana wa ufalme.” (Mt. 13:36-43) Kipindi hicho cha ukuzi kinawakilisha wakati ambapo waasi imani walikuwa wengi sana kuliko Wakristo wa kweli. Katika maana hiyo, kutaniko la Kikristo lilikuwa limechukuliwa mateka na Babiloni Mkubwa. Utekwa huo ulianza wakati fulani katika karne ya pili W.K., nao uliendelea hadi wakati wa kusafishwa kwa hekalu la kiroho katika siku za mwisho.—Mdo. 20:29, 30; 2 The. 2:3, 6; 1 Yoh. 2:18, 19.

Katika kipindi hicho kirefu cha utekwa wa kiroho, makasisi na washirika wao wa kisiasa, ambao walitamani kuendelea kuwa na mamlaka, waliwaficha Neno la Mungu watu waliokuwa chini yao. Wakati mwingine, ilikuwa kinyume cha sheria kwa watu kusoma Biblia katika lugha ambayo walielewa. Baadhi ya watu waliofanya hivyo walichomwa moto wakiwa wamefungwa juu ya nguzo ya mti. Yeyote ambaye alikuwa na maoni tofauti na mafundisho ya makasisi alitendewa kwa ukatili, na hilo lilifanya iwe vigumu kueneza nuru ya kweli.

Namna gani jambo la pili, yaani kurudishwa kwa watu wa Mungu? Jambo hilo lilitukia lini na jinsi gani? Kurudishwa kiroho kwa watu wa Mungu kulitokea hatua kwa hatua. Kuliambatana na “sauti ya kugongana” iliyotokea karne kadhaa kabla ya siku za mwisho kuanza. Ingawa mafundisho ya dini za uwongo yalikuwa na nguvu kwa muda mrefu, watu fulani waaminifu waliitetea ibada ya kweli kwa kadiri walivyoweza. Baadhi yao walijitahidi kutafsiri na kuchapisha Biblia katika lugha ambayo watu wengi walielewa. Wengine walitangaza kweli ambazo walikuwa wamegundua katika Neno la Mungu.

Kisha, mwishoni mwa miaka ya 1800, Charles Taze Russell na wenzake walijitahidi sana kurudisha kweli za Biblia. Ni kana kwamba nyama na ngozi ya mfano ilianza kufunika mifupa ya kiroho. Gazeti la Zion’s Watch Tower na machapisho mengine yaliwasaidia watu wenye mioyo minyofu kutambua kweli za kiroho. Baadaye watu wa Mungu waliimarishwa pia na sinema ya “Photo-Drama of Creation” iliyotolewa mwaka wa 1914 na kitabu The Finished Mystery kilichotolewa mwaka wa 1917. Mwishowe, mwaka wa 1919, watu wa Mungu walipewa uhai katika maana ya kiroho, na wakawekwa katika nchi yao mpya ya kiroho. Kadiri ambavyo wakati umepita, watiwa mafuta walio duniani wameungwa mkono na wale walio na tumaini la kuishi duniani, nao wamekuwa “jeshi kubwa, naam, kubwa sana.”—Eze. 37:10; Zek. 8:20-23. *

Kwa sababu hizo, inaonekana wazi kwamba watu wa Mungu walichukuliwa mateka na Babiloni Mkubwa uasi imani ulipoongezeka katika karne ya pili W.K. Hicho kilikuwa kipindi cha giza, kilichofanana na wakati ambapo Waisraeli walikuwa uhamishoni. Hata hivyo, tunafurahi kwamba baada ya watu wa Mungu kunyanyaswa kiroho kwa karne nyingi, tunaishi katika kipindi ambacho “wale walio na ufahamu watang’aa kama mwangaza” na “wengi watajitakasa” na “kusafishwa”!—Dan. 12:3, 10.

Je, Shetani alimchukua Yesu kihalisi na kumpeleka hekaluni alipokuwa akimshawishi?

Kwa ufupi, hatuna uhakika ikiwa Yesu alisimama hekaluni au alifanya hivyo tu kupitia maono. Nyakati fulani, machapisho yetu yameeleza kwamba mambo yote mawili yanawezekana.

Fikiria kwanza kile ambacho Biblia inasema. Mtume Mathayo alichochewa na roho takatifu kuandika hivi katika Injili yake kuhusu tukio hilo: “Ndipo Ibilisi akamchukua [Yesu], akaenda pamoja naye, na kuingia katika lile jiji takatifu, naye akamsimamisha juu ya mnara wa hekalu.” (Mt. 4:5) Luka anasimulia hivi tukio hilohilo: “Sasa akamwongoza kuingia Yerusalemu, akamsimamisha juu ya mnara wa hekalu.”—Luka 4:9.

Zamani, machapisho yetu yalieleza kwamba tukio hilo huenda halikutukia kihalisi. Kwa mfano, gazeti la Mnara wa Mlinzi, toleo la Machi 1, 1961, lilieleza hivi: “Haielekei kwamba mambo yote yanayopatikana katika simulizi linalohusu kushawishiwa kwa Yesu nyikani yalitukia kihalisi. Kwa kweli, hakuna mlima wowote ambapo mtu angeweza kusimama juu yake na kuonyeshwa ‘falme zote za ulimwengu na utukufu wazo.’ Kwa hiyo pia, tunaweza kukata shauri kwamba Shetani hakumchukua Yesu kihalisi au kimwili na ‘kwenda pamoja naye’ na kumsimamisha ‘juu ya mnara wa hekalu.’ Haikuwa lazima kufanya hivyo ili kishawishi kiwe na nguvu.” Hata hivyo, matoleo yaliyofuata ya gazeti la Mnara wa Mlinzi yalieleza kwamba ikiwa Kristo angekubali kujitupa chini, basi huenda angekufa.

Wengine wamesema kwamba Yesu hakuruhusiwa kusimama juu ya patakatifu pa hekalu kwa sababu hakuwa Mlawi. Hivyo, ilidhaniwa kwamba huenda Shetani ‘alimchukua’ Yesu na kwenda pamoja naye kwenye hekalu kwa njia ya maono. Jambo hilo linafanana na kile kilichotokea kwa nabii Ezekieli karne kadhaa mapema.—Eze. 8:3, 7-10; 11:1, 24; 37:1, 2.

Hata hivyo, ikiwa kishawishi hicho kilitokea tu kwa njia ya maono, maswali yafuatayo yanazuka:

  • Je, kishawishi hicho kilikuwa halisi au cha kuwaziwa?

  • Ikiwa kusudi la vishawishi vingine lilikuwa kumshawishi Yesu afanye vitendo halisi kama vile kuyabadili mawe yawe mkate au kumfanyia Shetani tendo halisi la ibada, je, kishawishi hiki hakingekuwa sawa na hivyo, yaani kumtaka Yesu aruke kihalisi kutoka juu ya hekalu?

Kwa upande mwingine, ikiwa Yesu alisimama kihalisi juu ya mnara wa hekalu, maswali mengine yanazuka:

  • Je, Yesu alivunja Sheria kwa kusimama juu ya patakatifu?

  • Yesu alifikaje Yerusalemu kutoka nyikani?

Utafiti zaidi unatusaidia kuelewa mambo fulani ambayo huenda yakajibu maswali hayo mawili ya mwisho.

Kwanza, Profesa D. A. Carson anaeleza kwamba neno la Kigiriki hi·e·ron’, ambalo limetafsiriwa “hekalu” katika masimulizi ya Mathayo na Luka, “yaelekea linamaanisha jengo lenyewe na maeneo yote yaliyolizunguka, si patakatifu penyewe.” Kwa hiyo si lazima iwe kwamba Yesu angesimama juu ya patakatifu penyewe. Kwa mfano, angeweza kusimama upande wa kusini mashariki mwa eneo la hekalu. Kutoka mahali hapo hadi chini kwenye Bonde la Kidroni palikuwa na urefu wa meta 137. Sehemu hiyo ya jengo ilikuwa na paa tambarare yenye ukingo na ilikuwa ndefu zaidi kuliko zote hekaluni. Mwanahistoria wa kale Josephus alisema kwamba ikiwa mtu angesimama hapo juu na kutazama chini, “angepatwa na kizunguzungu” kwa sababu ya urefu wa sehemu hiyo. Kwa kuwa Yesu hakuwa Mlawi, angeruhusiwa kusimama katika sehemu hiyo, na kwa kufanya hivyo hangesababisha vurugu.

Lakini Yesu alichukuliwaje kutoka nyikani mpaka hekaluni? Jibu la msingi ni kwamba hatuwezi kuwa na uhakika. Maelezo mafupi ya vishawishi hivyo hayaelezi urefu wa kipindi kilichohusika au mahali ambapo Yesu alikuwa huko nyikani. Hatuwezi kupuuza uwezekano wa kwamba huenda Yesu alitembea hadi Yerusalemu, ingawa kufanya hivyo huenda kungechukua wakati. Simulizi hilo halitaji kihususa ikiwa Yesu alibaki nyikani katika kipindi chote alipokuwa akishawishiwa. Badala yake, linasema tu kwamba alichukuliwa hadi Yerusalemu.

Lakini vipi kuhusu kishawishi ambacho Yesu alionyeshwa “falme zote za ulimwengu”? Ni wazi kwamba hakuona kihalisi falme zote: hakuna mlima halisi ambapo falme zote zinaweza kuonekana. Kwa hiyo, huenda Shetani alitumia aina fulani ya maono kumwonyesha Yesu falme hizo, kama vile tu projekta na skrini zinavyoweza kutumiwa kumwonyesha mtu picha za sehemu mbalimbali duniani. Hata ingawa huenda maono yalitumiwa, “tendo la ibada” lingekuwa halisi, si la kuwaziwa. (Mt. 4:8, 9) Hivyo inaweza kusemwa kwamba kishawishi cha kuruka kutoka juu ya mnara wa hekalu kilihusisha kitendo halisi chenye matokeo halisi, na hivyo kufanya kishawishi hicho kiwe na nguvu kuliko tu ikiwa kingetokea kupitia maono.

Kama ilivyotajwa mwanzoni, hatuwezi kushikilia maoni fulani kuhusu jambo hilo. Hivyo, hatuwezi kupuuza uwezekano wa kwamba Yesu alienda Yerusalemu na kusimama juu ya mnara wa hekalu. Lakini jambo moja ambalo tunaweza kuwa na uhakika nalo ni kwamba vishawishi hivyo vilikuwa halisi na kwamba katika visa vyote, Yesu alimjibu Ibilisi kwa njia ya kukata maneno.

^ fu. 2 Tazama gazeti la Mnara wa Mlinzi la Julai 15, 2013, uku. 10-12, fu. 5-8, 12.

^ fu. 1 Andiko la Ezekieli 37:1-14 na Ufunuo 11:7-12 yanazungumzia kurudishwa katika maana ya kiroho kulikotokea mwaka wa 1919. Hata hivyo, unabii wa Ezekieli ulitabiri kurudishwa kikamili kwa watu wote wa Mungu baada ya kipindi kirefu sana cha utekwa. Kwa upande mwingine, unabii wa Ufunuo unazungumzia kuhusu kikundi kidogo cha ndugu watiwa mafuta ambao walikuwa wakiongoza waliporudishiwa nguvu ili wawe hai kiroho baada ya kipindi kifupi cha kulazimishwa kuwa katika hali ya kutotenda.