Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Inawezekana Kusikuwe Jeuri Katika Dunia?

Inawezekana Kusikuwe Jeuri Katika Dunia?

Wewe ao mutu wa familia yako amekwisha kutendewa kwa jeuri? Uko na sababu yenye kufanya uogope kwamba siku fulani utatendewa hivyo? Jeuri, ni kusema, tendo la kutesa ao kuua watu wengine, imeitwa “tatizo la afya lenye kuongozeka na lenye kupata watu wengi katika dunia.” Tuone mifano fulani.

JEURI NYUMBANI NA KULALWA KINGUVU: Shirika la Umoja wa Mataifa linatoa ripoti hii: “Siku fulani katika maisha yake, mwanamuke mumoja kati ya wanawake tatu anatendewa kwa jeuri ao kulalwa kinguvu na mutu wa karibu.” Jambo la huzuni ni hili: “Inakadiriwa kwamba katika dunia yote, mwanamuke mumoja kati ya wanawake tano atalalwa kinguvu ao ataponyoka kulalwa kinguvu.”

JEURI KATIKA BARABARA: Inasemekana kwamba, vikundi zaidi ya 30000 vya watu wenye jeuri vinatendea wengine mubaya katika inchi ya États-Unis. Katika Amerika ya Kusini, karibu mutu 1 kati ya watu 3 ametendewa kwa jeuri.

MAUAJI: Inakadiriwa kwamba karibu watu 500000 waliuawa katika mwaka moja wa hivi karibuni. Hiyo ni hesabu kubwa kuliko hesabu ya watu wenye waliuawa katika vita mbalimbali. Hesabu ya mauaji yenye kutokea katika sehemu ya kusini ya Afrika na Amerika ya Kati iko juu zaidi, ni kusema, watu zaidi ya mara ine tukilinganisha na hesabu yenye kukadiriwa ya watu wenye waliuawa katika dunia yote. Katika mwaka moja, watu zaidi ya 100000 waliuawa katika Amerika ya Latini, na watu karibu 50000 katika inchi ya Brazili tu. Inawezekana kusikuwe jeuri katika dunia milele?

INAWEZEKANA KUMALIZA JEURI?

Sababu gani jeuri inaenea sana katika dunia? Kuna mambo mengi yenye kufanya kukuwe jeuri, kama vile mambo yenye kufuata: magumu yenye kutokea kwa sababu ya tofauti za hali ya maisha na za kifeza, kuzarau maisha ya wengine, kunywa pombe kupita kipimo na kutumia dawa za kulewesha, watoto kuona matendo ya jeuri ya watu wakubwa, na kwa sababu inaonekana kuwa watu wenye wanatenda kwa jeuri hawapewe malipizi.

Kwa kweli, maendeleo yamefanywa katika sehemu fulani za dunia ili kuzuia jeuri. Inasemekana kwamba katika miaka kumi yenye imepita, mauaji yamepunguka kwa kiasi cha 80 juu ya 100 katika muji wenye kujaa watu wengi wa São Paulo, inchi ya Brazili. Lakini, matendo ya jeuri ya kila namna yangali katika muji huo, na hesabu ya mauaji ingali ya wakaaji 10 hivi juu ya 100000. Sasa, ni wakati gani jeuri itaishaka milele katika dunia?

Ili jeuri iishe kabisa, watu wanapaswa kubadilisha tabia na mawazo yao. Ili watu wenye jeuri wabadilike, wanapaswa kuacha tabia kama vile kiburi, kutamani vitu vya wengine, na uchoyo, na wanapaswa kuonyesha sifa kama vile upendo, heshima, na kuhangaikia wengine.

Ni nini inaweza kumusaidia mutu afanye mabadiliko hayo makubwa? Fikiria mambo yenye Biblia inafundisha:

  • ‘Kumupenda Mungu kunamaanisha hivi, kwamba tuzishike amri zake.’—1 Yohana 5:3.

  • ‘Kumuogopa Yehova kunamaanisha kuchukia yaliyo mabaya.’ *Methali 8:13.

Kumupenda Mungu na kuogopa kumuchukiza ni mambo yenye yanaweza kuwapatia watu nguvu ili wabadilishe maisha yao, hata watu wenye jeuri. Hawabadilike kijuu-juu tu, lakini wanabadilika kabisa-kabisa. Hilo linawezekana kabisa?

Tufikirie mufano wa Alex, * mwenye alifanya miaka 19 katika gereza moja la inchi ya Brazili kwa sababu ya matendo ya jeuri. Alikuwa Shahidi katika mwaka wa 2000, kisha kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Alibadilisha kabisa tabia yake yenye jeuri? Ndiyo, na Alex anahuzunika kabisa kwa sababu ya matendo ya mubaya yenye alifanya. Anasema hivi: “Nimefikia kumupenda Mungu kwa sababu amenifanya nijisikie kuwa nimesamehewa kabisa. Nimebadilisha tabia zangu ili kumuonyesha Yehova shukrani na ili kumuonyesha kwamba ninamupenda.”

César, mwenye kuwa pia katika inchi ya Brazili, alikuwa kati ya watu wenye silaha wenye walizoea kubomoa nyumba za watu na kuiba. Alifanya hivyo kwa miaka 15 hivi. Ni nini ilimusaidia abadilike? Wakati alikuwa katika gereza, Mashahidi wa Yehova walimutembelea, na yeye pia alijifunza Biblia. César anasema hivi: “Kwa mara ya kwanza nilielewa kwamba maisha yangu yalikuwa na kusudi. Nilijifunza kumupenda Mungu. Nilijifunza pia kumuogopa, ni kusema, kuwa na woga wenye kufaa wa kuepuka kurudilia mambo ya mubaya yenye kumuletea Yehova huzuni. Nilitaka kabisa kumuonyesha shukrani juu ya wema wake. Upendo na woga huo vilinichochea kufanya mabadiliko.”

Ona namna unaweza kuishi katika dunia yenye haina jeuri

Mifano hiyo mbili inatufundisha nini? Mifano hiyo inatufundisha kwamba Biblia iko na uwezo wa kugeuza kabisa maisha ya watu kwa kubadilisha namna yao ya kufikiri. (Waefeso 4:23) Alex, mwenye tumekwisha kutaja anasema hivi: “Mambo yenye nilijifunza katika Biblia yalikuwa kama maji safi yenye kumwangika juu yangu. Yalianza kunisafisha na kuondoa hatua kwa hatua mawazo mabaya yenye yalikuwa ndani yangu. Sikuwazia kama ningeweza kuachana na mawazo hayo.” Kwa kweli, wakati tunajaza akili yetu ujumbe safi wa Biblia, ujumbe huo unaondoa ao kumaliza ubaya. Neno la Mungu liko na uwezo wa kusafisha. (Waefeso 5:26) Matokeo ni kwamba, watu wakali na wenye kujipenda wenyewe wanaweza kubadilisha matendo yao, na kuwa watu wema na wenye kufanya amani. (Waroma 12:18) Wanapata amani katika maisha yao kwa kutumikisha kanuni za Biblia.—Isaya 48:18.

Mashahidi wa Yehova zaidi ya milioni munane wenye kuwa katika inchi 240 wamevumbua siri ya kumaliza jeuri. Watu wa kila rangi ya ngozi na kila hali ya maisha na desturi wamejifunza kumupenda na kumuogopa Mungu na pia kupendana kati yao. Kwa hiyo, wanaishi kwa amani kama familia ya duniani pote. (1 Petro 4:8) Wanaonyesha waziwazi kwamba inawezekana dunia isikuwe na jeuri.

JEURI INAKARIBIA KUISHA KATIKA DUNIA!

Biblia inaahidi kwamba karibuni Mungu ataondoa jeuri katika dunia. Ulimwengu wa leo wenye jeuri unangojea ‘ile siku ya hukumu na ya kuangamizwa kwa watu wasiomuogopa Mungu.’ (2 Petro 3:5-7) Hakutakuwa tena watu wenye jeuri ambao watatesa wengine. Ni nini inatuhakikishia kwamba Mungu iko tayari kutusaidia na kuondoa jeuri katika dunia?

Biblia inasema kwamba ‘mutu yeyote anayependa jeuri nafsi Yake [Mungu] hakika inamuchukia.’ (Zaburi 11:5) Muumbaji anapenda amani na haki. (Zaburi 33:5; 37:28) Ndiyo sababu hatakubali watu wenye jeuri waendelee kuwa katika dunia milele.

Kwa kweli, ulimwengu mupya wenye amani unakaribia. (Zaburi 37:11; 72:14) Sababu gani usijifunze mengi zaidi ili kujua yale unapaswa kufanya ili kuishi katika dunia yenye haitakuwa tena na jeuri?

^ fu. 12 Yehova ni jina la Mungu kama vile inaonyeshwa katika Biblia.

^ fu. 14 Majina fulani yamebadilishwa.