Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HABARI KUU | UNAWEZA KUPATA WAPI FARAJA?

Faraja Wakati wa Matatizo

Faraja Wakati wa Matatizo

Kuna aina mbalimbali za matatizo. Ni kweli kwamba hatuwezi kuzungumzia matatizo yote ambayo wanadamu hukabili, hata hivyo, tutazungumzia mifano minne iliyotajwa mwanzoni mwa makala hii. Chunguza jinsi watu waliokabili matatizo ya aina mbalimbali walivyopata faraja ya kweli kutoka kwa Mungu.

UNAPOKOSA AJIRA

“Nilijifunza kukubali kazi za aina mbalimbali, na tuliepuka matumizi yasiyo ya lazima.”​—Jonathan

Seth * anakumbuka hivi: “Mimi na mke wangu tuliachishwa kazi wakati mmoja. Kwa miaka miwili tulitegemea msaada kutoka kwa familia na kufanya vibarua. Kwa sababu hiyo mke wangu, Priscilla, alishuka moyo nami nilijihisi sifai.

“Tulikabilianaje na hali hiyo? Priscilla alikumbuka kwa kawaida maneno ya Yesu yaliyo katika Mathayo 6:34. Yesu alisema tusihangaike juu ya kesho, kwa maana kesho itakuwa na mahangaiko yake yenyewe. Pia, sala za kutoka moyoni zilimsaidia asonge mbele. Kwa upande wangu, andiko la Zaburi 55:22 lilinifariji. Kama mtunga zaburi, nilimtupia Yehova mahangaiko yangu, naye alinitegemeza. Ingawa nimepata kazi, tunajitahidi kuishi maisha rahisi kulingana na shauri la Yesu katika Mathayo 6:20-22. Zaidi ya yote, tumemkaribia Mungu zaidi na tumekuwa na uhusiano wa karibu.”

Jonathan anaeleza hivi: “Biashara ya familia yetu ilipofilisika, nilihofia sana wakati ujao. Kuporomoka kwa uchumi kulisababisha biashara yetu iliyodumu kwa miaka 20 kufilisika. Tulianza kugombana na mke wangu kwa sababu ya pesa. Tuliogopa kununua vitu kwa kutumia kadi ya benki kwa kuhofia kwamba wauzaji wangeikataa.

“Hata hivyo, Neno la Mungu na roho yake vilitusaidia kufanya maamuzi yanayofaa. Nilijifunza kukubali kazi za aina mbalimbali, na tuliepuka matumizi yasiyo ya lazima. Pia, Mashahidi wa Yehova wenzetu walitupatia msaada. Walitusaidia kuendelea kujiheshimu na hali zilipokuwa ngumu walitupatia msaada.”

NDOA INAPOVUNJIKA

Raquel anakumbuka: “Mume wangu aliponiacha ghafla, nilikasirika na kuumia. Nililemewa na huzuni nyingi. Hata hivyo, nilimkaribia Mungu, naye akanifariji. Kusali kila siku kulinisaidia kuwa na amani ya Mungu ambayo ililinda moyo wangu. Kwa kweli, Mungu aliuponya moyo wangu uliovunjika.

“Pia, ninashukuru kwa sababu Neno lake Biblia, limenisaidia kudhibiti hasira na kuondoa kinyongo. Nilitafakari maneno ya mtume Paulo yaliyo katika Waroma 12:21: ‘Usiache ushindwe na uovu, bali endelea kuushinda uovu kwa wema.’

“Kuna wakati wa ‘kuacha kutafuta kilichopotea.’ . . . Sasa, nina malengo mapya maishani.”​—Raquel

“Rafiki yangu mmoja alinieleza kuhusu umuhimu wa kuendelea na maisha. Alinisomea Mhubiri 3:6 na kwa fadhili akaniambia kwamba kuna wakati wa ‘kuacha kutafuta kilichopotea.’ Huo ulikuwa ushauri wenye kuumiza, lakini ulinifaa. Sasa nina malengo mapya maishani.”

Elizabeth anasema: “Ndoa inapovunjika, unahitaji msaada wa kihisia. Nilikuwa na rafiki wa karibu ambaye kila siku alinisaidia kihisia. Alilia pamoja nami, alinifariji, na kunisaidia nijihisi kwamba ninapendwa na sijapuuzwa. Nina uhakika kwamba Yehova alimtumia ili kunisaidia kupona maumivu yangu ya kihisia.”

UGONJWA NA UZEE

“Baada ya kusali kwa Mungu, mimi huhisi kwamba roho yake imenitia nguvu.”​—Luis

Luis aliyetajwa katika makala ya kwanza ya gazeti hili, ana tatizo kubwa la moyo, na amenusurika kufa mara mbili. Kwa sasa, anahitaji kutumia kifaa cha kumsaidia kupumua kwa saa 16 kila siku. Luis anasema hivi: “Mimi husali kwa Yehova kwa ukawaida. Baada ya kusali kwa Mungu, mimi huhisi kwamba roho yake imenitia nguvu. Sala hunipa ujasiri wa kuendelea kuishi kwa sababu ninamwamini Mungu na ninajua kwamba ananijali.”

Petra mwenye umri wa miaka 80 hivi anasema: “Ningependa kufanya mambo mengi, lakini hali yangu hainiruhusu. Kadiri nguvu zinavyoendelea kupungua mimi hujihisi vibaya. Ninajiona kuwa dhaifu na ninalazimika kutumia dawa kwa ukawaida. Mara nyingi mimi hukumbuka jinsi Yesu alivyomwomba Baba yake amwondolee tatizo fulani ikiwa ingewezekana. Hata hivyo, Yehova alimwimarisha Yesu, na huniimarisha mimi pia. Kusali kila siku huniimarisha sana. Baada ya kuzungumza na Yehova, mimi hujihisi vizuri sana.”—Mathayo 26:39.

Julian ambaye ameugua ugonjwa wa mfumo wa neva kwa karibu miaka 30 anahisi hivyo pia. Anasema hivi: “Nimeacha cheo changu na sasa ninatumia kiti chenye magurudumu. Hata hivyo, maisha yangu yana kusudi kwa sababu ninawasaidia wengine. Kutoa kunaweza kupunguza mkazo, na Yehova hututia nguvu wakati wa shida kama anavyoahidi. Kama mtume Paulo, ninaweza kusema hivi kwa hakika: “Kwa mambo yote nina nguvu kupitia yeye anayenipa nguvu.’”—Wafilipi 4:13.

TUNAPOFIWA

Antonio anakumbuka hivi: “Mwanzoni sikuamini nilipopata taarifa kwamba baba yangu amekufa katika aksidenti ya barabarani. Hakupaswa kufa, kwa kuwa alikuwa mpita njia tu. Hata hivyo, singeweza kufanya jambo lolote. Kabla ya kufa alilazwa katika chumba cha wagonjwa mahututi kwa siku tano. Nilijidhibiti ili nisilie mbele ya mama yangu, lakini nilipokuwa peke yangu nililia kwa uchungu. Mara kwa mara nilijiuliza ‘Kwa nini?’

“Katika kipindi hicho kigumu, niliendelea kumwomba Yehova anisaidie kudhibiti hisia zangu na kuwa na amani ya akili. Pole kwa pole nilihisi utulivu. Nilikumbuka kwamba Biblia husema ‘tukio lisilotazamiwa’ linaweza kumpata yeyote. Kwa kuwa Mungu hasemi uwongo, nina uhakika kwamba nitamwona baba yangu atakapofufuliwa.”—Mhubiri 9:11; Yohana 11:25; Tito 1:2.

“Ingawa aksidenti hiyo ya ndege ilisababisha kifo cha mtoto wetu, tuna kumbukumbu za mambo mengi mazuri tuliyofurahia pamoja.”​—Robert

Robert, aliyetajwa katika makala ya kwanza ana maoni kama hayo. Anasema: “Kwa sababu ya kusali kwa Yehova, mimi na mke wangu tumepata amani ya akili inayotajwa katika Wafilipi 4:6, 7. Amani hiyo ya akili ilitusaidia kuzungumza na waandishi wa habari kuhusu tumaini letu la ufufuo. Ingawa aksidenti hiyo ya ndege ilisababisha kifo cha mtoto wetu, tuna kumbukumbu za mambo mengi mazuri tuliyofurahia pamoja. Sisi huzithamini kumbukumbu hizo.

“Mashahidi wenzetu walipotueleza kwamba walituona katika televisheni tukieleza kuhusu imani yetu kwa utulivu, tuliwaambia kwamba hilo lilitokana na sala nyingi zilizotolewa kwa niaba yetu. Ninaamini kwamba Yehova alituimarisha kupitia jumbe nyingi za faraja walizotutumia.”

Mifano hiyo inaonyesha kwamba Mungu anaweza kuandaa faraja kwa watu wanaokabili matatizo na changamoto mbalimbali. Namna gani wewe? Hata iwe unakabili tatizo gani maishani, unaweza kupata faraja. * Mwombe Yehova akusaidie. Yeye ni “Mungu wa faraja yote.”—2 Wakorintho 1:3.

^ fu. 5 Baadhi ya majina katika makala hii yamebadilishwa.

^ fu. 23 Ikiwa ungependa kumkaribia Mungu na kupata faraja, tafadhali wasiliana na Mashahidi wa Yehova walio katika eneo lenu au utume barua katika ofisi ya tawi iliyo karibu nawe.