Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

HABARI KUBWA | TUNAWEZA KUPATA KITULIZO WAPI?

Kupata Kitulizo Wakati wa Magumu

Kupata Kitulizo Wakati wa Magumu

Magumu yanatokea katika njia nyingi. Hatuwezi kuzungumuzia kila namna ya magumu katika habari hii, lakini acha tuzungumuzie mifano ine yenye tumekwisha kutaja. Tuone namna watu wenye walipambana na magumu tofauti walipata kitulizo cha kweli kutoka kwa Mungu.

WAKATI MUTU HANA KAZI

“Nilijifunza kukubali kazi yoyote, na tuliepuka kununua vitu vyenye hatukuwa navyo lazima.”—Jonathan

Seth * anakumbuka mambo yenye yalimufikia. Anasema hivi: “Mimi na bibi yangu tulipoteza kazi kwa wakati mumoja. Kwa miaka mbili tulilazimika kuishi kupitia musaada wenye familia ilitutolea na kupitia kazi ndogo za kutafutisha. Kwa hiyo, bibi yangu Priscilla, alishuka moyo, na nikajiona kuwa mutu wa bure.

“Ni nini ilitusaidia kuvumilia? Priscilla aliendelea kukumbuka maneno ya Yesu yenye kuwa katika andiko la Mathayo 6:34. Yesu alisema kwamba hatupaswe kuhangaika juu ya kesho, kwa sababu kila siku iko na mahangaiko yake. Na sala za bibi yangu zenye kutoka moyoni zilimupatia nguvu ya kuendelea kuvumilia. Kwa upande wangu, Zaburi 55:22 ilinituliza. Kama muandikaji wa zaburi hiyo, nilitupa muzigo wangu kwa Yehova, na nikajisikia kwamba amenitegemeza kabisa. Hata kama leo niko na kazi, tunaendelea kufanya maisha yetu yakuwe mepesi kulingana na shauri la Yesu lenye kuwa katika Mathayo 6:20-22. Zaidi ya yote, tumemukaribia Mungu zaidi, na mimi na bibi yangu tumekaribiana zaidi.”

Jonathan anasema hivi: “Niliogopa juu ya wakati unaokuja kwa sababu biashara yetu ndogo ya familia ilianguka. Miaka 20 ya kazi ngumu iligeuka kuwa bure kwa sababu ya matatizo ya feza (crise économique). Mimi na bibi yangu tulianza kubishana kwa sababu ya feza. Hatungeweza kununua vitu kupitia kadi yetu ya kujikopesha kwa sababu tuliogopa kwamba wataikataa.

“Lakini Neno la Mungu na roho yake takatifu vilinisaidia kukamata maamuzi ya muzuri. Nilijifunza kukubali kazi yoyote, na tuliepuka kununua vitu vyenye hatukuwa navyo lazima. Kwa sababu tuko Mashahidi wa Yehova, tulisaidiwa pia na waamini wenzetu. Walifanya tujisikie kuwa wa maana na walitusaidia wakati maisha yetu yalikuwa magumu sana.”

WAKATI NDOA INAVUNJIKA

Raquel anakumbuka mambo yenye yalimufikia. Anasema hivi: “Wakati bwana yangu aliniacha bila kutazamia, niliumia moyoni na kukasirika. Na nilijisikia mubaya sana. Lakini, nilimukaribia Mungu, na akanituliza. Amani ya Mungu ililinda moyo wangu wakati nilisali kwake kila siku. Nilijisikia kama ametengeneza moyo wangu wenye kuvunjika.

“Na kupitia Neno lake, Biblia, nilifikia kushinda hali ya kukasirika na kuweka kinyongo. Niliamini kabisa maneno ya mutume Paulo yenye kupatikana katika andiko la Waroma 12:21. Andiko hilo linasema hivi: ‘Usiache ushindwe na uovu, bali endelea kushinda uovu kwa wema.’

“Kuna wakati wenye tunapaswa ‘kuacha kutafuta kilichopotea.’ . . . Niko sasa na mipango mipya ya kutimiza katika maisha.”—Raquel

“Rafiki mumoja muzuri alinisaidia nielewe kwamba ni jambo la lazima kuendelea na maisha. Alinionyesha andiko la Mhubiri 3:6 na akaniambia kwa upole kwamba kuna wakati wenye tunapaswa ‘kuacha kutafuta kilichopotea.’ Sikufurahia shauri hilo, lakini lilikuwa shauri lenye nilikuwa nalo lazima. Niko sasa na mipango mipya ya kutimiza katika maisha.”

Elizabeth anasema hivi: “Wakati ndoa yako inavunjika, uko na lazima ya watu wa kukutegemeza. Nilipata rafiki wa sana mwenye alinitegemeza kila mara. Alilia pamoja na mimi, alinituliza, na alifanya nijisikie kuwa mwenye kupendwa kuliko kujisikia kuwa mwenye kutupiliwa. Niko hakika kwamba Yehova alitumia dada huyo ili kuponyesha vidonda vyangu vya moyo.”

WAKATI WA MAGONJWA AO UZEE

“Kisha kusali, ninasikia kwamba roho yake inanipatia nguvu.”—Luis

Luis, mwenye tulitaja katika habari ya kwanza alipata ugonjwa hatari wa moyo, na mara mbili alikaribia kufa. Kwa sasa iko na lazima ya kutumia kifaa cha kumupatia oksijeni kwa saa 16 kila siku. Anasema hivi: “Ninasali kwa Yehova kila mara. Na kisha kusali, ninasikia kwamba roho yake inanipatia nguvu. Sala inanipatia nguvu ya kusonga mbele kwa sababu niko na imani katika Mungu na kwa sababu ninajua kwamba ananihangaikia.”

Mwanamuke mumoja mwenye kuitwa Petra iko na miaka zaidi ya 80. Anasema hivi: “Ninapenda kufanya mambo mengi, lakini sina uwezo. Ninajisikia mubaya sana kuona namna nguvu zangu zinaendelea kupunguka. Ninajisikia mwenye kuchoka sana na kila siku ninapaswa kutumia dawa. Mara nyingi ninafikiria namna Yesu alimuomba Baba yake ili jambo fulani ngumu lipitilie mbali kama inawezekana. Lakini Yehova alimupatia Yesu nguvu, na ananipatia pia nguvu. Sala ni dawa yangu ya kila siku. Ninajisikia muzuri zaidi kisha kusali kwa Mungu.”—Mathayo 26:39.

Julian, mwenye amekuwa anapambana na ugonjwa wa mishipa ya ufahamu kwa miaka karibu 30, anajisikia hivyo pia. Mwanaume huyo anasema hivi: “Nimeacha kutumia kiti cha cheo katika kazi na kuanza kutumia kiti cha vilema. Lakini maisha yangu yako na maana kwa sababu nimejitolea ili kutumikia wengine. Kutoa kunaweza kupunguza mateso, na Yehova anaendelea kutimiza ahadi yake ya kutupatia nguvu wakati wa magumu. Kama vile mutume Paulo, ninaweza kusema kabisa kwamba: ‘Kwa mambo yote nina nguvu kupitia yeye anayenipatia nguvu.’”—Wafilipi 4:13.

WAKATI UNAFIWA

Antonio anakumbuka mambo yenye yalimupata. Anasema hivi: “Wakati baba yangu alikufa katika aksidenti ya barabara, sikuamini palepale. Jambo hilo lilionekana kuwa la bila haki, kwa sababu baba yangu alikuwa anajitembeza kwa miguu bila kosa lolote. Lakini sikuwa na jambo lenye ningeweza kufanya. Alipoteza ufahamu kwa siku tano mbele akufe. Nilijizuia kulia mbele ya mama yangu, lakini wakati nilikuwa peke yangu nilianza kulia sana. Niliendelea kujiuliza, ‘Sababu gani? Sababu gani jambo hilo lilitokea?’

“Katika siku hizo zenye huzuni kubwa, niliendelea kuomba Yehova anisaidie kujizuia na anipatie amani. Na hatua kwa hatua nilijisikia muzuri zaidi. Nilikumbuka kwamba Biblia inasema kuwa ‘tukio lenye halitazimiwe’ linaweza kumupata mutu yeyote. Kwa sababu Mungu hawezi kusema uongo, niko hakika kwamba nitaona tena baba yangu wakati wa ufufuo.”—Mhubiri 9:11; Yohana 11:25; Tito 1:2.

“Hata kama aksidenti ya avion iliua mutoto wetu, tunaendelea kukumbuka mambo mengi ya kufurahisha yenye tulipitisha pamoja naye.”—Robert

Robert, mwenye tulitaja katika habari ya kwanza iko na mawazo kama hayo. Anasema hivi: “Mimi pamoja na bibi yangu, tulipata amani ya akili yenye kutajwa katika andiko la Wafilipi 4:6, 7. Tulipata amani hiyo kupitia sala zetu kwa Yehova. Amani hiyo ya ndani ilitusaidia kuzungumuza na watangazaji wa habari juu ya tumaini letu la ufufuo. Hata kama aksidenti ya avion iliua mutoto wetu, tunaendelea kukumbuka mambo mengi ya kufurahisha yenye tulipitisha pamoja naye. Tunajikaza kukaza akili yetu juu ya mambo hayo.

“Wakati Mashahidi wenzetu walituambia kwamba walituona kwenye televizyo namna tulikuwa tunafasiria kwa utulivu mambo yenye tunaamini, tuliwaambia hilo liliwezekana kupitia tu sala nyingi zenye walitoa kwa ajili yetu. Ninaamini kabisa kwamba Yehova alitutegemeza kupitia ujumbe wao mbalimbali wenye kutuliza.”

Kama vile mifano yenye tunatoka kuona inaonyesha, Mungu anatolea watu kitulizo wakati wanapata magumu. Sasa wewe? Hata kama uko na magumu gani katika maisha, unaweza kupata kitulizo ili kupambana na magumu hayo. * Kwa hiyo, umutegemee Yehova ili akusaidie. Yeye ni “Mungu wa faraja yote.”—2 Wakorintho 1:3.

^ fu. 5 Majina fulani yamebadilishwa katika habari hii.

^ fu. 23 Kama unapenda kupata musaada ili kumukaribia Mungu na kupata kitulizo kutoka kwake, tafazali uonane na Mashahidi wa Yehova wa eneo lenu ao uandikie biro yao ya karibu na kwenye unaishi.