Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Nendeni Mkafanye Wanafunzi Kutoka kwa Watu wa Mataifa Yote

“Nendeni Mkafanye Wanafunzi Kutoka kwa Watu wa Mataifa Yote

“Nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, mkiwabatiza . . . , na kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi.”—MT. 28:19, 20.

NYIMBO: 141, 97

1, 2. Maneno ya Yesu kwenye Mathayo 24:14 yanazusha maswali gani?

IWE watu wanasikiliza ujumbe wetu au wanaupinga vikali, wengi wao wanakubali kwamba Mashahidi wa Yehova wanajulikana sana kwa sababu ya kazi yao ya kuhubiri. Huenda umekutana na watu katika huduma ambao wamesema kwamba ingawa hawakubaliani na imani yetu, wanatuheshimu kwa sababu ya kazi tunayofanya. Kama tujuavyo, Yesu alitabiri kwamba habari njema ya Ufalme ingehubiriwa katika dunia yote inayokaliwa. (Mt. 24:14) Hata hivyo, tunajuaje kwamba kazi tunayofanya inatimiza unabii wa Yesu? Je, ni kimbelembele kufikiri kwamba sisi ndio tunaofanya kazi hiyo?

2 Dini nyingi zinafikiri kwamba zinahubiri Injili, au habari njema. Hata hivyo, wafuasi wake hawajitahidi kufanya mengi zaidi ya kutoa ushuhuda, ibada za kanisa, au programu zinazotolewa kupitia vyombo vya habari, kama vile televisheni na Intaneti. Wengine wanasema kwamba wanaeneza Injili wanaposhiriki kutoa misaada au katika miradi ya maendeleo katika nyanja za matibabu na elimu. Je, hivyo ndivyo Yesu alivyowaamuru wanafunzi wake wafanye?

3. Kulingana na Mathayo 28:19, 20, wafuasi wa Yesu wanapaswa kufanya mambo gani manne?

3 Je, wanafunzi wa Yesu walipaswa kukaa tu na kusubiri watu waje kwao? La hasha! Baada ya kufufuliwa, Yesu alizungumza na mamia ya wanafunzi wake na kuwaambia hivi: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, mkiwabatiza . . . , na kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi.” (Mt. 28:19, 20) Hivyo, tunahitaji kufanya mambo manne. Lazima tufanye wanafunzi, tuwabatize, na tuwafundishe. Lakini tunahitaji kufanya nini kwanza? Yesu alisema: “Nendeni”! Msomi mmoja wa Biblia alisema hivi kuhusu amri hiyo: “Ni jukumu la kila anayeamini ‘kwenda,’ iwe ni kwenda mtaa wa pili au kuvuka ng’ambo ya bahari.”—Mt. 10:7; Luka 10:3.

4. Kuwa “wavuvi wa watu” kunahusisha nini?

4 Je, Yesu alikuwa akizungumzia jitihada za mfuasi mmojammoja, au kikundi kilichopangwa kufanya kampeni ya kuhubiri habari njema? Kwa kuwa mtu mmoja hangeweza kwenda kwa “mataifa yote,” kazi hii ingehitaji jitihada za pamoja za kikundi cha watu. Yesu alionyesha hilo alipowaalika wanafunzi wake wawe “wavuvi wa watu.” (Soma Mathayo 4:18-22.) Uvuvi unaozungumziwa hapa si ule wa kutumia ndoano na chambo, ambapo mvuvi anakaa tu na kusubiri samaki anaswe. Badala yake, ni uvuvi wa kutumia nyavu, kazi kubwa ambayo wakati mwingine ingehusisha jitihada za watu wengi.—Luka 5:1-11.

5. Ni maswali gani manne ambayo yanahitaji kujibiwa, na kwa nini?

5 Ili tujue ni nani leo wanaotimiza unabii wa Yesu wa kuhubiri habari njema, tunahitaji kujibu maswali haya manne:

  • Ni ujumbe gani unaopaswa kuhubiriwa?

  • Kazi hiyo inapaswa kufanywa kwa lengo gani?

  • Ni mbinu gani zinazopaswa kutumiwa?

  • Kazi hiyo inapaswa kuenea kadiri gani, nayo ingeendelea hadi lini?

Majibu ya maswali hayo yatatusaidia kutambua ni nani wanaofanya kazi hiyo inayookoa uhai, nayo yataimarisha azimio letu la kuendelea kuifanya kwa uaminifu.—1 Tim. 4:16.

NI UJUMBE GANI UNAOPASWA KUHUBIRIWA?

6. Kwa nini unaweza kuwa na uhakika kwamba Mashahidi wa Yehova wanahubiri ujumbe ambao Yesu alisema tuhubiri?

6 Soma Luka 4:43. Yesu alihubiri “habari njema ya ufalme,” na anatarajia wanafunzi wake wafanye vivyo hivyo. Ni kikundi gani cha watu kinachohubiri ujumbe huo kwa “mataifa yote”? Jibu ni wazi! Ni Mashahidi wa Yehova pekee. Hata baadhi ya wapinzani wetu wanakubali ukweli huo. Kwa mfano, kasisi fulani mmishonari alimwambia Shahidi mmoja kwamba ameishi katika nchi mbalimbali, na katika kila nchi aliwauliza Mashahidi wanahubiri ujumbe gani. Walimjibu nini? Kasisi huyo alisema hivi: “Wote walikuwa wapumbavu sana hivi kwamba walitoa jibu lilelile: ‘Habari njema ya Ufalme.’” Hata hivyo, hawakuwa “wapumbavu,” badala yake, Mashahidi hao walisema kwa upatano, kama Wakristo wa kweli wanavyopaswa kufanya. (1 Kor. 1:10) Maneno yao yanalingana na ujumbe ulio katika gazeti la Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova. Gazeti hilo linapatikana katika lugha zaidi ya 254 na kwa wastani nakala milioni 59 hivi za kila toleo huchapishwa. Hilo ndilo gazeti linalosambazwa zaidi duniani.

7. Tunajuaje kwamba makasisi wa dini zinazodai kuwa za Kikristo hawahubiri ujumbe ambao Yesu alisema tuhubiri?

7 Makasisi wa dini zinazodai kuwa za Kikristo hawahubiri kuhusu Ufalme wa Mungu. Wanapozungumza kuhusu Ufalme, wengi wao husema kwamba Ufalme huo ni hisia au hali fulani iliyo moyoni mwa Mkristo. (Luka 17:21) Hawawasaidii watu waelewe kwamba Ufalme wa Mungu ni serikali ya mbinguni inayotawaliwa na Yesu Kristo ambayo itasuluhisha matatizo yote ya wanadamu, na hivi karibuni itaondoa uovu wote duniani. (Ufu. 19:11-21) Badala yake, wanamkumbuka Yesu wakati wa Krismasi na Ista pekee. Inaonekana hawajui kabisa kile ambacho Yesu atatimiza akiwa Mtawala mpya wa dunia. Kwa kuwa hawajui ni ujumbe gani wanaopaswa kuhubiri, haishangazi kwamba hawajui pia lengo la kufanya kazi hiyo.

KAZI HIYO INAPASWA KUFANYWA KWA LENGO GANI?

8. Hatupaswi kuwa na lengo gani tunapofanya kazi ya kuhubiri?

8 Kazi ya kuhubiri inapaswa kufanywa kwa lengo gani? Lengo halipaswi kuwa kukusanya pesa na kujenga majengo ya kifahari. Yesu aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Mlipokea bure, toeni bure.” (Mt. 10:8) Hatupaswi kutumia Neno la Mungu kufanya biashara. (2 Kor. 2:17) Wale wanaohubiri ujumbe huo hawapaswi kutafuta faida za kibinafsi kwa sababu ya kazi wanayofanya. (Soma Matendo 20:33-35.) Licha ya mwongozo huo ulio wazi, makanisa mengi yanakazia fikira kukusanya pesa au kuimarisha hali yake ya kiuchumi. Yanafanya hivyo kwa kuwa yanahitaji kuwategemeza makasisi wanaolipwa na wafanyakazi wengine wengi. Katika visa vingi, viongozi wa dini zinazodai kuwa za Kikristo wamejikusanyia utajiri mkubwa.—Ufu. 17:4, 5.

9. Mashahidi wa Yehova wameonyeshaje kwamba wanafanya kazi ya kuhubiri wakiwa na lengo linalofaa?

9 Mashahidi wa Yehova wana historia gani kuhusu kukusanya pesa? Kazi yao inategemezwa kwa michango ya hiari. (2 Kor. 9:7) Hawakusanyi sadaka katika Majumba yao ya Ufalme au makusanyikoni. Hata hivyo, mwaka jana pekee, Mashahidi wa Yehova walitumia saa bilioni 1.93 katika kazi ya kuhubiri habari njema na kuongoza mafunzo ya Biblia zaidi ya milioni tisa kila mwezi bila malipo. Jambo la kushangaza ni kwamba hawalipwi kwa kazi yao na wanafurahia kujilipia gharama zote zinazohusika. Akizungumzia kazi ya Mashahidi wa Yehova, mtafiti mmoja alisema hivi: “Kusudi kuu ni kuhubiri na kufundisha. . . . Hawana makasisi, jambo ambalo hupunguza gharama kwa kiasi kikubwa.” Hivyo basi, kwa nini tunafanya kazi hiyo? Kwa ufupi, tunafanya kazi hiyo kwa hiari kwa sababu tunampenda Yehova na jirani zetu. Roho hiyo ya kujitolea inapatana na unabii ulio katika Zaburi 110:3. (Soma.)

NI MBINU GANI ZINAZOPASWA KUTUMIWA?

Tunahubiri mahali popote ambapo watu wanapatikana (Tazama fungu la 10)

10. Yesu na wanafunzi wake walitumia mbinu gani kuhubiri?

10 Yesu na wanafunzi wake walitumia mbinu gani kuhubiri habari njema? Walienda popote ambapo watu walipatikana, yaani maeneo ya umma na katika nyumba zao. Kazi ya kuhubiri ilihusisha kuwatafuta wanaostahili nyumba kwa nyumba. (Mt. 10:11; Luka 8:1; Mdo. 5:42; 20:20) Utaratibu huo unaonyesha kwamba kazi hiyo ingefanywa bila ubaguzi.

11, 12. Inapohusu kuhubiri habari njema, kuna tofauti gani kati ya watu wa Yehova na dini zinazodai kuwa za Kikristo?

11 Namna gani dini zinazodai kuwa za Kikristo? Kwa ujumla, washiriki wa makanisa wamewaachia makasisi wanaolipwa kazi hiyo ya kuhubiri. Makasisi hao hawajitahidi kuwa “wavuvi wa watu,” badala yake wanahangaikia zaidi kudumisha idadi ya waumini ambao tayari wanao. Ni kweli kwamba nyakati nyingine huenda baadhi ya makasisi wakawatia moyo waumini wao wahubiri. Kwa mfano, mwanzoni mwa mwaka 2001, Papa John Paul II alisema hivi katika barua yake: “Kwa miaka mingi, nimesema tena na tena kuhusu kueneza upya injili. Ninasema tena sasa . . . Lazima tuwe na usadikisho kama wa Paulo, aliyesema hivi: ‘Ole wangu nisipoihubiri Injili.’” Aliendelea kusema kwamba utume huo “hauwezi kuachiwa kikundi fulani tu cha ‘watalaamu’ lakini unawahusu watu wote wa Mungu.” Hata hivyo, ni wangapi wameitikia mwito huo?

12 Namna gani Mashahidi wa Yehova? Wao pekee ndio wanaohubiri kwamba Yesu anatawala akiwa Mfalme tangu 1914. Wanatanguliza kazi ya kuhubiri kama Yesu alivyoagiza. (Marko 13:10) Kitabu kimoja (Pillars of Faith—American Congregations and Their Partners) kinasema hivi: “Kwa Mashahidi wa Yehova, umishonari ndiyo kazi wanayotanguliza kuliko kitu kingine chochote.” Akirejelea mambo ambayo Shahidi mmoja alisema, mwandishi wa kitabu hicho alisema hivi: “Wanadamu wenzao wanapokabili njaa, upweke, na afya mbaya, wanajitahidi kuwasaidia, . . . lakini hawasahau kamwe kwamba kazi yao ya msingi ni kuwapa wengine ujumbe wa kiroho kuhusu mwisho wa ulimwengu na umuhimu wa wokovu.” Mashahidi wa Yehova wanaendelea kuhubiri ujumbe huo, wakitumia mbinu ambazo Yesu na wanafunzi wake walitumia.

KAZI HIYO INGEENEA KADIRI GANI, NAYO INGEENDELEA HADI LINI?

13. Kazi ya kuhubiri inapaswa kuenea kadiri gani?

13 Yesu alieleza jinsi ambavyo kazi ya kuhubiri ingeenea kwa kusema kwamba habari njema ingehubiriwa “katika dunia yote inayokaliwa.” (Mt. 24:14) Wanafunzi wangefanywa kutoka “kwa watu wa mataifa yote.” (Mt. 28:19, 20) Hilo linamaanisha kwamba kazi hiyo ingefanywa duniani pote.

14, 15. Ni nini kinachothibitisha kwamba Mashahidi wa Yehova wametimiza unabii wa Yesu kuhusu kuenea kwa kazi ya kuhubiri? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

14 Ili tuelewe jinsi ambavyo Mashahidi wa Yehova wametimiza unabii wa Yesu kuhusu kuenea kwa kazi ya kuhubiri, acheni tuchunguze takwimu fulani. Nchini Marekani, kuna makasisi 600,000 hivi kutoka katika vikundi tofauti-tofauti vya kidini ilhali kuna Mashahidi wa Yehova 1,200,000 hivi. Ulimwenguni pote, kuna mapadri 400,000 hivi wa Kanisa Katoliki. Sasa fikiria idadi ya Mashahidi wanaofanya kazi ya kuhubiri ujumbe wa Ufalme unaopatikana katika Biblia. Ulimwenguni pote, wahudumu milioni nane hivi wanajitolea kuwahubiria watu katika nchi 240. Wanatimiza kazi yenye kustaajabisha sana inayomletea Yehova sifa na utukufu!—Zab. 34:1; 51:15.

15 Tukiwa Mashahidi wa Yehova, tunatamani kuwahubiria habari njema watu wengi iwezekanavyo kabla ya mwisho kuja. Kwa sababu hiyo, tunafanya kazi ya pekee ya kutafsiri na kuchapisha machapisho ya Biblia. Mamilioni ya vitabu, magazeti, trakti, na mialiko ya makusanyiko na ya Ukumbusho imesambazwa bila malipo. Tumetafsiri machapisho mbalimbali katika lugha zaidi ya 700. Nakala zaidi ya milioni 200 za Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko Matakatifu zimechapishwa katika lugha zaidi ya 130. Mwaka jana pekee, tulichapisha machapisho ya Biblia bilioni 4.5 hivi. Tovuti yetu rasmi ina habari katika lugha zaidi ya 750. Ni kikundi gani kingine cha kidini kinachofanya kazi kama hiyo?

16. Tunajuaje kwamba Mashahidi wa Yehova wana roho ya Mungu?

16 Kazi hiyo iliyotabiriwa ingeendelea kwa muda gani? Yesu alisema kwamba kazi hiyo ambayo ingefanywa duniani pote ingeendelea hadi katika siku za mwisho, “na ndipo ule mwisho utakapokuja.” Ni kikundi gani kingine cha kidini kinachohubiri habari njema bila kuacha katika siku hizi za mwisho zenye misukosuko? Baadhi ya watu tunaokutana nao katika huduma wanaweza kusema hivi: “Sisi tuna roho takatifu, lakini nyinyi mnafanya kazi.” Kwa kuwa tunaendelea kufanya kazi hiyo, je, hilo halithibitishi kwamba tuna roho ya Mungu? (Mdo. 1:8; 1 Pet. 4:14) Mara kwa mara, vikundi fulani vya kidini vinajaribu kufanya kazi ambayo Mashahidi wa Yehova hufanya, lakini mara nyingi vinashindwa. Wengine wamefanya kazi ya umishonari kwa kipindi fulani na baadaye wanarudia maisha yao ya kawaida. Na wengine wanajaribu kuhubiri nyumba kwa nyumba. Hata hivyo, wanahubiri ujumbe gani? Jibu la swali hilo linaonyesha wazi kwamba hawafanyi kazi ambayo Kristo alianzisha.

NI NANI HASA WANAOHUBIRI HABARI NJEMA LEO?

17, 18. (a) Kwa nini tuna uhakika kwamba Mashahidi wa Yehova ndio wanaohubiri habari njema ya Ufalme leo? (b) Ni nini kinachotusaidia tuendelee kufanya kazi hiyo?

17 Ni nani hasa wanaohubiri habari njema ya Ufalme leo? Tunaweza kusema hivi kwa uhakika: “Ni Mashahidi wa Yehova!” Kwa nini tuna uhakika huo? Kwa sababu tunahubiri ujumbe ambao Yesu alisema tuhubiri, yaani, habari njema ya Ufalme. Tunatumia mbinu zinazofaa kwa kwenda mahali ambapo watu wanapatikana. Tunafanya kazi ya kuhubiri tukiwa na lengo linalofaa kwa kuwa hatutafuti faida za kifedha, bali tunachochewa na upendo. Kazi yetu imeenea sana, na inawafikia watu wa lugha na mataifa yote. Nasi tutaendelea kufanya kazi hiyo bila kuacha, mwaka baada ya mwaka, mpaka mwisho utakapokuja.

18 Kwa kweli, tunashangazwa sana na mambo ambayo watu wa Mungu wanatimiza katika siku hizi zenye kusisimua. Lakini mambo hayo yote yamewezekanaje? Mtume Paulo anajibu katika barua yake kwa Wafilipi: “Mungu ndiye ambaye, kwa ajili ya mapenzi yake mema, anatenda ndani yenu ili ninyi muwe na nia na kutenda pia.” (Flp. 2:13) Acheni tuendelee kuimarishwa na Baba yetu mwenye upendo tunapofanya yote tuwezayo na kutimiza kwa ukamili huduma yetu.—2 Tim. 4:5.