Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wakristo wanapaswa kutumia dhamiri yao iliyozoezwa na Biblia wanaposhughulika na wafanyakazi wa serikali

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Ni nini kinachoweza kuwasaidia Wakristo waamue ikiwa inafaa kuwapa zawadi au bakshishi wafanyakazi wa serikali?

Tunahitaji kuzingatia mambo kadhaa. Lazima Wakristo wawe wanyofu. Wana wajibu wa kutii sheria za nchi ikiwa hazipingani na sheria ya Yehova. (Mt. 22:21; Rom. 13:1, 2; Ebr. 13:18) Isitoshe, wanajitahidi kuheshimu tamaduni na hisia za watu katika eneo wanaloishi na ‘kuwapenda jirani zao kama wao wenyewe.’ (Mt. 22:39; Rom. 12:17, 18; 1 The. 4:11, 12) Kutumia kanuni hizo kutawasaidia Wakristo katika sehemu mbalimbali za dunia wajue maoni wanayopaswa kuwa nayo kuhusu desturi ya kutoa zawadi na bakshishi.

Katika maeneo mengi, si lazima mtu awape chochote watumishi wa umma ili apate kitu anachohitaji. Watumishi hao wa umma wanafanya kazi walizopangiwa na serikali, na hawaombi wala hawatarajii kupewa chochote zaidi ya mshahara wao. Katika nchi nyingi, ni kinyume cha sheria kwa mfanyakazi wa serikali kuomba au kupokea kitu chochote chenye thamani kwa ajili ya kazi yake, hata iwe ametimiza majukumu yake kwa kufuata sheria kikamili. Zawadi kama hiyo ingeonwa kuwa rushwa, hata ikiwa haikubadili utendaji wake wa kazi. Chini ya hali kama hizo, hakuna haja kwa Mkristo kujiuliza kama ni sawa au si sawa kuwapa zawadi au bakshishi wafanyakazi wa serikali. Ni kosa kutoa zawadi kama hizo.

Hata hivyo, wafanyakazi wa umma katika maeneo ambayo hayana sheria kama hizo au sheria hizo hazitekelezwi, wana maoni tofauti kuhusu zawadi au bakshishi. Katika nchi fulani, maofisa wa serikali wanatumia vibaya mamlaka yao ili kupokea pesa au zawadi nyingine kutoka kwa watu wanaopaswa kuwahudumia, na hawako tayari kufanya chochote bila kupewa kitu fulani. Kwa hiyo, mara nyingi wale wanaohalalisha ndoa, wanaokusanya kodi, wanaotoa vibali vya ujenzi, na wengine wanadai wapewe kitu fulani. Wasipopewa, wafanyakazi hao wanaweka vizuizi ili iwe vigumu, au isiwezekane, kwa raia kupata haki yao ya kisheria. Inaripotiwa kwamba katika nchi fulani kikosi cha zimamoto hakiwezi kuanza kuzima moto kabla ya kupewa pesa.

Nyakati fulani, huenda ikafaa kutoa zawadi ili kuonyesha kwamba tunathamini huduma ambayo tumepata kihalali

Katika maeneo ambayo watu wamezoea kufanya hivyo, wengine wanahisi kwamba hawawezi kuepuka jambo hilo. Chini ya hali hiyo, huenda Mkristo akaona kwamba kutoa kitu fulani ni kama malipo ya ziada ya huduma anayohitaji. Hata hivyo, katika mazingira ambayo ufisadi ni jambo la kawaida, Mkristo anahitaji kuwa mwangalifu ili atofautishe mambo yanayokubalika na yasiyokubalika machoni pa Mungu. Kuna tofauti kubwa kati ya kutoa kitu fulani ili ufanyiwe jambo ambalo ni haki yako na kutoa zawadi ili ufanyiwe kile ambacho huna haki ya kupata. Katika maeneo ambayo ufisadi umekita mizizi, watu fulani hutoa zawadi ili wapewe huduma ambayo hawapaswi kupata au wanampa polisi au mkaguzi wa serikali “kitu fulani” ili waepuke kutozwa faini iliyo halali kisheria. Bila shaka, ni kosa kumrubuni mtu yeyote kwa kumpa “zawadi,” kama tu ilivyo kosa kukubali “zawadi” kama hiyo. Matendo yote mawili yanapotosha haki.—Kut. 23:8; Kum. 16:19; Met. 17:23.

Kwa sababu ya dhamiri yao iliyozoezwa na Biblia, Wakristo wengi wakomavu hawatoi zawadi ambazo wafanyakazi wa serikali wanaomba. Wanahisi kwamba kufanya hivyo ni kuendeleza au kuchochea ufisadi. Hivyo, wanakataa kutoa zawadi yoyote wanayoombwa.

Ingawa Wakristo wakomavu wanatambua kwamba kutoa zawadi ili kupokea huduma fulani kinyume cha sheria ni kama kutoa hongo, hali katika eneo zinaweza kumruhusu mtu atoe zawadi ili kuonyesha shukrani au ili huduma fulani isicheleweshwe isivyo lazima. Katika visa fulani, baada ya kupata matibabu ya bure kwenye hospitali ya umma, Wakristo fulani huwapa madaktari na wauguzi zawadi ili kuonyesha kwamba wanashukuru kwa kupata matibabu. Wanafanya hivyo baada ya kupokea matibabu, wala si kabla, ili isionekane kwamba zawadi hiyo ni hongo au ombi la kutendewa kwa upendeleo.

Haiwezekani kuzungumzia hali zote zinazoweza kutokea katika kila nchi. Hivyo, haidhuru kuna hali gani katika eneo lenu, Wakristo wanapaswa kufanya uamuzi ambao hautachafua dhamiri yao. (Rom. 14:1-6) Wanapaswa kuepuka kuvunja sheria. (Rom. 13:1-7) Wanapaswa kuepuka matendo yoyote yanayoweza kuliletea suto jina la Yehova au kuwakwaza wengine. (Mt. 6:9; 1 Kor. 10:32) Na maamuzi yao yanapaswa kuonyesha kwamba wanawapenda jirani zao.—Marko 12:31.

Kutaniko linaweza kuonyeshaje shangwe tangazo la kurudishwa kwa mtu aliyetengwa na ushirika linapotolewa?

Andiko la Luka sura ya 15 linaeleza mfano mzuri wa Yesu kuhusu mtu aliyekuwa na kondoo 100. Kondoo mmoja alipopotea, mtu huyo aliacha kondoo 99 nyikani na kwenda kumtafuta ‘mpaka alipompata.’ Yesu aliendelea kusema hivi: “Akiisha kumpata humweka juu ya mabega yake na kushangilia. Naye anapofika nyumbani huwaita rafiki zake na jirani zake pamoja, akiwaambia, ‘Shangilieni pamoja nami, kwa sababu nimempata kondoo wangu aliyekuwa amepotea.’” Yesu alimalizia kwa kusema hivi: “Mimi ninawaambia ninyi kwamba ndivyo kutakavyokuwa na shangwe zaidi mbinguni juu ya mtenda-dhambi mmoja anayetubu kuliko juu ya waadilifu 99 ambao hawahitaji kutubu.”—Luka 15:4-7.

Muktadha unaonyesha kwamba Yesu alisema maneno hayo ili kurekebisha mtazamo wa waandishi na Mafarisayo, ambao walimkosoa kwa kushirikiana na wakusanya kodi na watenda dhambi. (Luka 15:1-3) Yesu alisema kwamba shangwe hutokea mbinguni mtenda dhambi anapotubu. Swali ni ‘Kwa kuwa shangwe hutokea mbinguni, je, hakupaswi pia kuwa na shangwe duniani mtenda dhambi anapotubu, kugeuka, na kunyoosha mapito ya miguu yake?’—Ebr. 12:13.

Mtu anaporudishwa kutanikoni, tuna sababu nzuri ya kufurahi. Mtu huyo atahitaji kuendelea kudumisha uaminifu wake kwa Mungu, lakini ilikuwa lazima atubu ili arudishwe kutanikoni, na tunafurahi kwamba alitubu. Hivyo, si vibaya ikiwa wasikilizaji wataamua kupiga makofi kwa heshima wazee wanapotangaza kwamba mtu fulani amerudishwa kutanikoni.

Ni nini kingeweza ‘kutibua’ maji ya dimbwi la Bethzatha huko Yerusalemu?

Katika siku za Yesu, wakazi fulani wa Yerusalemu waliamini kwamba dimbwi la Bethzatha lilikuwa na nguvu za kuponya maji yake “yanapotibuliwa.” (Yoh. 5:​1-7) Hivyo, watu waliokuwa wakitafuta tiba walikusanyika hapo.

Imeelezwa kwamba Wayahudi walikuwa na desturi ya kutumia dimbwi hilo kujitakasa. Dimbwi hilo lilipata maji kutoka katika dimbwi lingine lililotumika kuhifadhi maji katika eneo hilohilo. Utafiti unaonyesha kwamba madimbwi hayo mawili yalitenganishwa na bwawa. Kulikuwa na mwingilio katika bwawa hilo ambao ungeweza kufunguliwa ili kuruhusu maji kutoka kwenye dimbwi la kuhifadhi maji kwenda kwenye dimbwi la Bethzatha. Maji yalipokuwa yakiingia, bila shaka hilo lilitibua maji kwenye dimbwi la Bethzatha.

Ni vizuri tukumbuke kwamba andiko la Yohana 5:​4, lililosema kwamba malaika alikuwa akitibua maji, halipatikani katika hati za Kigiriki zinazokubalika zaidi, kama vile Kodeksi ya Sinai ya karne ya nne. Hata hivyo, katika dimbwi la Bethzatha, Yesu alimponya mtu aliyekuwa mgonjwa kwa miaka 38. Mtu huyo aliponywa mara moja bila hata kuingia kwenye dimbwi.