Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Faidika Kikamili na Chakula cha Kiroho Kutoka kwa Yehova

Faidika Kikamili na Chakula cha Kiroho Kutoka kwa Yehova

“Mimi, Yehova, ni Mungu wako, Yeye anayekufundisha ili ujifaidi mwenyewe.”—ISA. 48:17.

NYIMBO: 117, 114

1, 2. (a) Mashahidi wa Yehova wana maoni gani kuhusu Biblia? (b) Unapenda sehemu gani ya Biblia?

MASHAHIDI WA YEHOVA wanaipenda Biblia kwa kuwa inatoa mafundisho yanayotegemeka, yanayotufariji na kutupatia tumaini. (Rom. 15:4) Hatuioni Biblia kuwa mkusanyo wa mawazo ya wanadamu, bali kama ‘vile ilivyo kwa kweli,’ yaani, “neno la Mungu.”—1 The. 2:13.

2 Bila shaka sote tunapenda sehemu fulani za Biblia. Watu fulani hufurahia sana Injili, ambazo zinatuonyesha utu bora wa Yehova kupitia Mwana wake. (Yoh. 14:9) Wengine wanafurahia kusoma unabii wa Biblia, kama vile Ufunuo, unaoonyesha “mambo ambayo lazima yatendeke upesi.” (Ufu. 1:1) Na ni nani kati yetu ambaye hajafarijika kwa kusoma kitabu cha Zaburi au kupata masomo muhimu maishani katika kitabu cha Methali? Kwa kweli, Biblia ni kitabu kwa ajili ya watu wote.

3, 4. (a) Tuna maoni gani kuhusu machapisho yetu? (b) Ni machapisho gani ambayo yametayarishwa kwa ajili ya vikundi fulani hususa vya watu?

3 Kuipenda Biblia kunatufanya tupende pia machapisho yetu. Kwa mfano, tunathamini chakula cha kiroho tunachopokea kupitia vitabu, broshua, magazeti, na machapisho mengine. Tunajua kwamba chakula hicho kinachotoka kwa Yehova kinatusaidia tuendelee kuwa macho kiroho, kinatujenga, na kutuwezesha kuwa na “afya katika imani.”—Tito 2:2.

4 Zaidi ya kupokea machapisho yaliyotayarishwa kwa ajili ya Mashahidi wa Yehova kwa ujumla, tunapata machapisho ya Biblia kwa ajili ya vikundi hususa vya watu. Baadhi ya habari zimekusudiwa kuwasaidia vijana, na nyingine zinawasaidia wazazi wao. Habari nyingi zinazochapishwa na zinazopatikana kwenye tovuti yetu zimetayarishwa kwa ajili ya watu ambao si Mashahidi. Chakula hicho kingi cha kiroho kinatukumbusha kwamba Yehova anatimiza ahadi yake ya kuvifanyia “vikundi vyote vya watu . . . karamu ya vyakula vinono vilivyotiwa mafuta.”—Isa. 25:6.

5. Tuna uhakika kwamba Yehova anathamini nini?

5 Inaelekea kwamba wengi wetu tunatamani tungekuwa na muda zaidi wa kusoma Biblia na machapisho yetu. Tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova anathamini jitihada zetu za ‘kujinunulia wakati unaofaa’ ili tusome Biblia na kujifunza kibinafsi. (Efe. 5:15, 16) Ni kweli kwamba nyakati nyingine huenda tusiweze kutumia kikamili chakula chote cha kiroho tunachopata. Hata hivyo, tunahitaji kujihadhari na hatari fulani. Hatari gani?

6. Ni nini kinachoweza kufanya tusifaidike kikamili na chakula fulani cha kiroho kutoka kwa Yehova?

6 Ni hatari kufikiri kwamba chakula fulani cha kiroho hakituhusu kwa kuwa kufanya hivyo kutafanya tusifaidike kikamili. Kwa mfano, namna gani ikiwa unaona kwamba sehemu fulani ya Biblia haikuhusu? Au vipi ikiwa habari fulani imetayarishwa kwa ajili ya kikundi hususa cha watu? Je, tunasoma habari hiyo kijuu-juu tu au hatuisomi kabisa? Tukifanya hivyo, huenda tukakosa habari zenye faida kubwa sana kwetu. Tunaweza kuepukaje kuingia kwenye mtego huo? Kila mmoja wetu anapaswa kukumbuka kwamba Mungu ndiye Chanzo cha chakula cha kiroho tunachopokea. Alisema hivi kupitia nabii Isaya: “Mimi, Yehova, ni Mungu wako, Yeye anayekufundisha ili ujifaidi mwenyewe.” (Isa. 48:17) Acheni tufikirie mapendekezo matatu yatakayotusaidia tufaidike na sehemu zote za Biblia na vyakula tofauti-tofauti vya kiroho tunavyopokea.

JINSI YA KUFAIDIKA UNAPOSOMA BIBLIA

7. Kwa nini tunahitaji kusoma Biblia tukiwa na mtazamo unaofaa?

7 Soma ukiwa na mtazamo unaofaa. Biblia inasema wazi kwamba “andiko lote limeongozwa na roho ya Mungu nalo ni lenye faida.” (2 Tim. 3:16) Ni kweli kwamba mwanzoni sehemu fulani za Biblia ziliandikwa kwa ajili ya mtu au kikundi fulani. Hiyo ndiyo sababu tunahitaji kusoma Maandiko tukiwa na mtazamo unaofaa. Ndugu mmoja anasema hivi: “Ninaposoma Biblia, ninajitahidi kukumbuka kwamba kuna mambo kadhaa tunayoweza kujifunza katika andiko lilelile.” Anaongeza hivi: “Kukumbuka hilo hunichochea kufikiria njia mbalimbali za kutumia andiko fulani.” Kabla ya kusoma Neno la Mungu, ni vizuri tusali ili tuwe na mtazamo unaofaa na hekima ya kutambua mambo ambayo Yehova anataka tujifunze.—Ezra 7:10; soma Yakobo 1:5.

Je, unafaidika kikamili na usomaji wako wa Biblia? (Tazama fungu la 7)

8, 9. (a) Tunaposoma Biblia, huenda tukajiuliza maswali gani? (b) Matakwa ambayo wazee Wakristo wanapaswa kutimiza yanatufundisha nini kumhusu Yehova?

8 Jiulize maswali. Unaposoma andiko fulani, tua na ujiulize maswali kama haya: ‘Andiko hili linanifundisha nini kumhusu Yehova? Ninaweza kutumiaje habari hii maishani mwangu? Ninaweza kuitumiaje kuwasaidia wengine?’ Tukitafakari maswali kama hayo, tutafaidika sana na usomaji wetu wa Biblia. Kwa mfano, fikiria sifa ambazo Mkristo anapaswa kuwa nazo ili astahili kuwa mzee. (Soma 1 Timotheo 3:2-7.) Kwa kuwa wengi wetu si wazee kutanikoni, huenda mwanzoni tukafikiri kwamba habari hiyo haituhusu. Lakini, tunapotafakari baadhi ya majibu ya maswali yafuatayo, tutagundua kwamba sote tunaweza kufaidika sana na sifa hizo.

9 Andiko hili linanifundisha nini kumhusu Yehova? Orodha ya sifa hizo inafunua kwamba Yehova anataka wale wanaowekwa rasmi kulitunza kutaniko watimize viwango vya juu. Anatarajia waweke mfano mzuri, na atawatoza hesabu kutokana na jinsi wanavyolitendea kutaniko, “ambalo alilinunua kwa damu ya Mwana wake mwenyewe.” (Mdo. 20:28) Yehova anataka tuhisi tukiwa salama tunapotunzwa na wachungaji waliowekwa rasmi. (Isa. 32:1, 2) Kwa hiyo, matakwa ya Kimaandiko ambayo wazee Wakristo wanapaswa kutimiza yanatukumbusha kwamba Yehova anatujali sana.

10, 11. (a) Tunaposoma matakwa ambayo wazee wanapaswa kutimiza, tunaweza kutumiaje habari hiyo maishani mwetu? (b) Tunaweza kutumiaje habari hiyo kuwasaidia wengine?

10 Ninaweza kutumiaje habari hii maishani mwangu? Mara kwa mara, mwanaume aliyewekwa rasmi anapaswa kujichunguza kama anatimiza matakwa hayo ya kiroho, na kutafuta sifa anazohitaji kuboresha. Ndugu ambaye “anajitahidi kufikia cheo cha mwangalizi” anahitaji kuchunguza kwa makini sifa hizo, kwa kuwa anapaswa kujitahidi kadiri awezavyo kuzisitawisha. (1 Tim. 3:1) Kwa kweli, kila Mkristo anaweza kujifunza kutokana na matakwa yaliyoorodheshwa kwenye mistari hiyo, kwa kuwa mambo mengi yanayotajwa ni yale ambayo Yehova anataka Wakristo wote watimize. Kwa mfano, sisi sote tunapaswa kuwa na usawaziko na utimamu wa akili. (Flp. 4:5; 1 Pet. 4:7) Wazee wanapokuwa “vielelezo kwa kundi,” tunaweza kujifunza kutoka kwao na ‘kuiga imani yao.’—1 Pet. 5:3; Ebr. 13:7.

11 Ninaweza kutumiaje habari hii kuwasaidia wengine? Tunaweza kutumia orodha ya matakwa ya waangalizi Wakristo kuwasaidia watu wanaopendezwa, au wanafunzi wa Biblia, waone jinsi ambavyo wazee wa kutaniko wanatofautiana na makasisi wa dini zinazodai kuwa za Kikristo. Pia, tunaposoma orodha hiyo, huenda tukakumbuka jinsi wazee kutanikoni wanavyojitahidi kufanya kazi kwa ajili yetu. Kutafakari jinsi wanavyojitoa kunatufanya ‘tuwatilie maanani wale wanaofanya kazi kwa bidii’ kati yetu. (1 The. 5:12) Kadiri tunavyowaonyesha heshima waangalizi wetu wanaofanya kazi kwa bidii, ndivyo tunavyowaongezea shangwe.—Ebr. 13:17.

12, 13. (a) Tunaweza kufanya utafiti gani kwa kutumia vifaa tulivyo navyo? (b) Toa mfano unaoonyesha jinsi habari za ziada zinavyoweza kutusaidia tujifunze mambo ambayo hayaonekani wazi.

12 Fanya utafiti. Tunaweza kutumia vifaa tulivyo navyo kuchunguza habari zifuatazo:

  • Ni nani aliyeandika sehemu hii ya Biblia?

  • Iliandikwa lini na wapi?

  • Kulikuwa na matukio gani muhimu kitabu hicho cha Biblia kilipoandikwa?

Habari kama hizo zinaweza kutusaidia tujifunze mambo ambayo hayaonekani wazi.

13 Kwa mfano, fikiria andiko la Ezekieli 14:13, 14, linalosema hivi: “Kwa habari ya nchi, ikiwa itanitendea dhambi kwa kutenda kwa kukosa uaminifu, pia nitaunyoosha mkono wangu juu yake na kuivunjia fimbo ambazo mikate ya mviringo huning’inizwa, nami nitaleta njaa juu yake na kumkatilia mbali mtu wa udongo na mnyama wa kufugwa kutoka ndani yake. ‘Na kama watu hawa watatu wangekuwa katikati yake, Noa, Danieli na Ayubu, wao wenyewe kwa sababu ya uadilifu wao wangeikomboa nafsi yao,’ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova.” Tunapofanya utafiti tunagundua kwamba sehemu hii ya Ezekieli iliandikwa mwaka wa 612 K.W.K. Kufikia wakati huo, Noa na Ayubu walikuwa wamekufa karne kadhaa zilizopita, na rekodi yao ya uaminifu ilikuwa kwenye kumbukumbu ya Mungu. Lakini bado Danieli alikuwa hai. Huenda alikuwa na umri wa miaka 20 hivi Yehova aliposema kwamba alikuwa mwadilifu kama Noa na Ayubu. Jambo hilo linatufundisha nini? Yehova anatambua na kuthamini utimilifu wa waabudu wake wote waaminifu, wakiwemo vijana.—Zab. 148:12-14.

FAIDIKA NA MACHAPISHO MBALIMBALI

14. Habari zilizochapishwa kwa ajili ya vijana zinawasaidiaje, na wengine wanaweza kufaidikaje na habari hizo? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

14 Kama vile tunavyofaidika kwa kujifunza sehemu zote za Neno la Mungu, ndivyo tunavyoweza kufaidika na chakula chote cha kiroho tulicho nacho. Fikiria mifano michache. Habari kwa ajili ya vijana. Katika miaka ya karibuni, machapisho yetu mengi yamechapishwa kwa ajili ya vijana. [1] Baadhi ya habari hizo zimekusudiwa kuwasaidia wakabiliane na vishawishi shuleni au changamoto za kubalehe. Sote tunaweza kufaidikaje na habari hizo? Tunapozisoma, tunakumbushwa mambo ambayo vijana wanakabili. Na hilo linafanya iwe rahisi zaidi kwetu kuwasaidia na kuwatia moyo.

15. Kwa nini Wakristo ambao ni watu wazima wanapaswa kusoma habari zilizotayarishwa kwa ajili ya vijana?

15 Si vijana pekee wanaokabili matatizo yanayozungumziwa kwenye makala hizo. Sisi sote tunahitaji kutetea imani yetu, kudhibiti hisia, kupinga vishawishi, na kuepuka marafiki wabaya na burudani zisizofaa. Habari hizo na nyingine nyingi zimezungumziwa kwenye makala zilizotayarishwa kwa ajili ya vijana. Je, Wakristo ambao ni watu wazima wanapaswa kuaibika kusoma makala hizo? La hasha! Ingawa zimeandikwa kwa njia inayowavutia vijana, habari hizo zinategemea kanuni za Maandiko zisizopitwa na wakati, hivyo sote tunaweza kufaidika na chakula hicho cha kiroho.

16. Machapisho yetu yanawasaidia vijana kwa njia gani nyingine?

16 Zaidi ya kuwasaidia vijana wakabiliane na matatizo, machapisho yetu yanawasaidia pia wakue kiroho na wamkaribie Yehova. (Soma Mhubiri 12:1, 13.) Jambo hilo linaweza kuwanufaisha pia Wakristo ambao ni watu wazima. Kwa mfano, gazeti la Amkeni! la Aprili 2009 lilikuwa na makala yenye kichwa: “Vijana Huuliza . . . Ninaweza Kufanya Nini ili Nifurahie Kusoma Biblia?” Makala hiyo ilikuwa na mapendekezo mbalimbali na pia sanduku ambalo mtu angeweza kukata na kuweka ndani ya Biblia. Je, watu wazima pia wamefaidika na makala hiyo? Mke mwenye umri wa miaka 24 ambaye ana watoto aliandika hivi: “Sikuzote imekuwa vigumu kwangu kusoma Biblia. Nilifuata madokezo katika makala hiyo, na ninatumia vizuri sanduku linaloweza kukatwa kwenye gazeti hilo. Sasa, mimi hutazamia kwa hamu usomaji wangu wa Biblia. Ninaona uhusiano ulioko kati ya vitabu mbalimbali vya Biblia. Sijawahi kamwe kufurahia kusoma Biblia kama ninavyofurahia sasa.”

17, 18. Tunaweza kufaidikaje tunaposoma habari zilizotayarishwa kwa ajili ya watu wote? Toa mfano.

17 Habari zilizotayarishwa kwa ajili ya watu wote. Tangu mwaka 2008 tumefurahia toleo la funzo la Mnara wa Mlinzi, ambalo limetayarishwa kwa ajili ya Mashahidi wa Yehova. Lakini namna gani magazeti ambayo yametayarishwa kwa ajili ya watu wote? Je, tunaweza kufaidika kwa kuyasoma? Fikiria mfano huu. Wazia kwamba uko kwenye Jumba la Ufalme na kabla ya hotuba ya watu wote, unagundua kwamba mtu uliyemwalika amehudhuria mkutano. Bila shaka unafurahi sana. Msemaji anapoendelea kutoa hotuba, inaelekea unamfikiria mgeni huyo na kuwazia jinsi anavyoipokea habari inayozungumziwa. Jambo hilo linafanya uithamini zaidi hotuba hiyo.

18 Inaweza kuwa hivyo pia tunaposoma habari zilizotayarishwa kwa ajili ya watu wote. Kwa mfano, toleo la watu wote la Mnara wa Mlinzi linazungumzia habari za Kimaandiko kwa njia ambayo watu wasio Mashahidi wanaweza kuelewa. Makala nyingi zilizo kwenye tovuti ya jw.org/sw, kama vile sehemu zenye kichwa: “Majibu ya Maswali ya Biblia” na “Maswali Yanayoulizwa Mara Nyingi,” zimetayarishwa kwa njia hiyo pia. Kusoma makala hizo kunafanya tuthamini zaidi kweli ambazo tayari tunazijua vizuri. Isitoshe, makala hizo zinaweza kutufundisha njia mpya za kueleza mambo tunayoamini tunaposhiriki katika huduma. Vivyo hivyo, gazeti la Amkeni! linaimarisha imani yetu juu ya kuwapo kwa Mungu wa kweli, na linatusaidia kujua jinsi ya kutetea imani yetu.—Soma 1 Petro 3:15.

19. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunamshukuru Yehova kwa kutupatia chakula cha kiroho?

19 Kwa kweli, Yehova ametupatia chakula kingi sana ili kutimiza ‘uhitaji wetu wa kiroho.’ (Mt. 5:3) Na tuendelee kutumia chakula chote cha kiroho tulicho nacho. Tukifanya hivyo, tutaonyesha kwamba tunamshukuru sana Yule ambaye anatufundisha ili tujifaidi wenyewe.—Isa. 48:17.

^ [1] (fungu la 14) Habari hizo zinahusisha kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, buku la 1 na 2, na vilevile mfululizo wa makala zenye kichwa: “Vijana Huuliza,” ambazo sasa zinapatikana kwenye mtandao pekee.