Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoka Katika Hifadhi Ya Vitu Vyetu Vya Kale

“Kwa Wale Waliokabidhiwa Kazi”

“Kwa Wale Waliokabidhiwa Kazi”

BAADA ya mvua kunyesha na upepo kuvuma kwa siku nyingi, mwishowe siku ya Jumatatu, Septemba 1, 1919, kulikuwa na jua na joto. Alasiri ya siku hiyo, wajumbe wasiozidi 1,000 walikusanyika kwenye jumba lenye viti 2,500 kusikiliza sehemu ya kwanza ya kusanyiko lililofanyika Cedar Point, Ohio, Marekani. Kufikia jioni, wajumbe wengine 2,000 waliwasili wakitumia mashua, magari, na magari-moshi. Siku ya Jumanne, kulikuwa na watu wengi sana hivi kwamba sehemu iliyobaki ya programu ya kusanyiko ilifanyiwa nje chini ya miti.

Miale ya jua ilipenya katikati ya majani na kivuli kilitokeza maumbo maridadi juu ya makoti ya wanaume. Upepo mwanana wa Ziwa Erie ulipuliza kofia za wanawake zenye manyoya. Ndugu mmoja alikumbuka hivi: “Tukiwa kwenye mazingira hayo maridadi, tofauti na ulimwengu wenye kelele, ni kama tulikuwa katika paradiso.”

Mandhari hiyo ilipendeza sana, lakini shangwe kubwa ya wahudhuriaji ilivutia zaidi. Gazeti la eneo hilo liliandika hivi: “Wote wanaonekana wamejitoa sana, ni wachangamfu na wana shangwe kwelikweli.” Wanafunzi wa Biblia walifurahia sana ushirika wa Kikristo baada ya kupitia majaribu makali miaka michache iliyotangulia. Walikabili upinzani katika kipindi cha vita, migawanyiko makutanikoni, kufungwa kwa Betheli ya Brooklyn, na wengi walifungwa gerezani kwa ajili ya Ufalme, wakiwemo ndugu nane walioongoza ambao baadhi yao walihukumiwa vifungo vya miaka 20. *

Baadhi ya Wanafunzi wa Biblia walivunjika moyo na kuacha kuhubiri katika kipindi hicho kigumu. Lakini wengi walifanya yote wawezayo kuendelea kuhubiri licha ya kukandamizwa na wenye mamlaka. Katika kisa fulani, mchunguzi mmoja alisema kwamba licha ya kuonywa vikali, Wanafunzi wa Biblia aliowahoji walisisitiza kuwa “wangeendelea kuhubiri neno la Mungu hadi mwisho.”

Katika kipindi hicho cha majaribu, Wanafunzi waaminifu wa Biblia walikuwa “wakitafuta mwongozo wa Bwana, . . . na kusali Baba awaongoze nyakati zote.” Sasa walikuwa wameungana kwa shangwe katika kusanyiko la Cedar Point. Dada mmoja alisema maneno yaliyowakilisha hisia za wengi ambao hawakujua jinsi ambavyo “wangeanzisha upya kazi ya kuhubiri.” Ndugu hao walitamani kurudi kazini mara moja.

KIFAA KIPYA KILICHOITWA “GA”!

Kwa juma zima, wajumbe walijiuliza herufi “GA” zilimaanisha nini. Herufi hizo zilikuwa zimeandikwa kwenye programu ya kusanyiko, kadi za kuwakaribisha, na mabango yaliyokuwa kwenye eneo la kusanyiko. Siku ya Ijumaa, iliyoitwa “Siku ya Wafanyakazi Wenzi,” Joseph F. Rutherford alieleza maana ya herufi hizo ambazo zilikuwa fumbo kwa wahudhuriaji 6,000. Herufi “GA” zilimaanisha The Golden Age, gazeti jipya ambalo lingetumiwa katika huduma. *

Ndugu Rutherford alisema hivi kuhusu watiwa mafuta wenzake: “Kwa macho ya imani wanatazama mbele na kuona kwamba baada ya kipindi cha matatizo kutakuwa na enzi mpya yenye utukufu ya utawala wa Masihi. . . . Wanaona kuwa wajibu na heshima kubwa kuutangazia ulimwengu kwamba kutakuwa na enzi mpya. Kufanya hivyo ni sehemu ya kazi waliyopewa na Mungu.”

Gazeti The Golden Age, “Jarida la Uhakika, Tumaini, na Usadikisho,” lingetumiwa kuanzisha mbinu mpya ya kueneza kweli, yaani, kampeni ya nyumba kwa nyumba ya kuwaomba watu wajiandikishe ili walipokee kila mwezi. Walipoulizwa ni wangapi waliotaka kufanya kazi hiyo, wote walisimama kwa shangwe. Kisha, “wakiwa na bidii na shangwe ambayo wale wanaofuata hatua za Yesu wanapata,” waliimba hivi: “Tuma nuru yako na kweli, Ee Bwana.” Ndugu J. M. Norris alikumbuka hivi: “Siwezi kamwe kusahau tulivyoimba kwa hisia, ni kana kwamba miti ilitikisika.”

Baada ya programu, wajumbe walisimama kwenye foleni kwa saa nyingi ili wawe wa kwanza kujiandikisha kupokea gazeti hilo. Wengi wao walihisi kama Mabel Philbrick, aliyesema hivi: “Ilisisimua sana kujua kwamba kwa mara nyingine tulikuwa na kazi ya kufanya!”

“KWA WALE WALIOKABIDHIWA KAZI”

Wanafunzi wa Biblia 7,000 hivi walijitayarisha kufanya kazi. Kulikuwa na maelezo yafuatayo kwenye trakti iliyoitwa Organization Method na kijitabu Kwa Wale Waliokabidhiwa Kazi: Idara mpya ya Utumishi huko makao makuu ingeelekeza kazi. Kila kutaniko lilipaswa kuanzisha Halmashauri ya Utumishi na mkurugenzi angewekwa rasmi ili awasilishe maagizo. Maeneo ya kuhubiri yangegawanywa katika visehemu vyenye nyumba 150 hadi 200. Kungekuwa na Mkutano wa Utumishi kila Alhamisi jioni ili ndugu wasimulie mambo yaliyoonwa na watoe ripoti za utumishi.

Herman Philbrick alisema hivi: “Tuliporudi nyumbani, tulianza kampeni ya kuwaomba watu wajiandikishe kupokea magazeti.” Watu kila mahali waliwasikiliza. Beulah Covey alisema hivi: “Inaonekana kwamba baada ya vita na huzuni nyingi, kila mtu alitaka kusikia kuhusu enzi mpya.” Arthur Claus aliandika hivi: “Wote kutanikoni walishangaa sana kuona jinsi idadi ya watu waliojiandikisha ilivyokuwa kubwa.” Ndani ya miezi miwili baada ya nakala ya kwanza kutolewa, nakala karibu 500,000 za gazeti la Amkeni! zilikuwa zimesambazwa na watu 50,000 walikuwa wamejiandikisha kulipokea.

Gazeti la Mnara wa Mlinzi la Julai 1, 1920 lilikuwa na makala yenye kichwa “Injili ya Ufalme.” Ndugu A. H. Macmillan alisema kwamba makala hiyo iliwatia moyo kwa mara ya kwanza ndugu na dada ulimwenguni pote wahubiri kuhusu Ufalme wa Mungu. Makala hiyo iliwahimiza Wakristo wote watiwa mafuta “wautolee ulimwengu ushuhuda kwamba ufalme wa mbinguni umekaribia.” Leo, ndugu za Kristo “waliokabidhiwa kazi” wameungwa mkono na mamilioni ya waandamani wanaohubiri neno kwa bidii huku wakisubiri enzi mpya ya utawala wa Masihi.

^ fu. 5 Tazama kitabu Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu, sura ya 6, yenye kichwa “Wakati wa Kutahini (1914-1918).”

^ fu. 9 Mwaka wa 1937 gazeti hilo liliitwa Consolation na mwaka wa 1946 likaitwa Amkeni!