Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HABARI KUU | UKWELI KUHUSU MAONO YA MBINGUNI

Ukweli Kuhusu Wale Wanaoishi Mbinguni

Ukweli Kuhusu Wale Wanaoishi Mbinguni

Je, umewahi kujiuliza ni nani wanaoishi mbinguni? Watu wengi hujiuliza swali hilo. Kwa miaka mingi watu wamekuwa na makisio mbalimbali kuhusu hali ya mbinguni. Baadhi ya watu huamini kwamba mababu waliokufa huishi huko na wanapaswa kuheshimiwa. Wengine hufikiri kwamba ni mahali ambako malaika na watu wema waliokufa huishi kwa amani na furaha tele. Ilhali wengine huamini kwamba mbinguni ni makao ya mamilioni ya miungu.

Watu wengi huamini kwamba hatuwezi kuelewa hali ya mbinguni kwa kuwa hakuna mtu aliyeshuka duniani na kueleza ukweli kuhusu mbinguni. Hata hivyo, maoni hayo hayafai. Yesu Kristo aliishi mbinguni kabla ya kuja duniani. Aliwaambia hivi viongozi wa dini katika karne ya kwanza: “Nimeshuka kutoka mbinguni kufanya, si mapenzi yangu, bali mapenzi yake aliyenituma.” Yesu aliwaeleza mitume wake kuhusu hali ya mbinguni aliposema hivi: “Katika nyumba ya Baba yangu mna makao mengi.”—Yohana 6:38; 14:2.

Kwa kweli, Mungu ambaye jina lake ni Yehova, ndiye baba ya Yesu, na “makao” yake ni mbinguni. (Zaburi 83:18) Hivyo, Yehova Mungu na Yesu Kristo ndio wanaoweza kutueleza ukweli. Waliwafunulia watumishi waaminifu wa zamani habari nyingi kuhusu hali ya mbinguni kupitia maono.

Makala inayofuata itazungumzia baadhi ya maono yaliyo katika Biblia ambayo wanadamu walipokea. Unapochunguza maono hayo, kumbuka kwamba makao ya mbinguni ni tofauti na makao ya duniani, hakuna vitu tunavyoweza kugusa au kuona. Kwa sababu hiyo, Mungu alitumia maono rahisi ili kutusaidia kuelewa. Maono hayo yatatusaidia kuwajua wale wanaoishi katika “makao” ya mbinguni.