Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tunathamini Kupokea Fadhili Zisizostahiliwa za Mungu

Tunathamini Kupokea Fadhili Zisizostahiliwa za Mungu

“Sisi sote tulipokea . . . fadhili zisizostahiliwa juu ya fadhili zisizostahiliwa.”YOH. 1:16.

NYIMBO: 95, 13

1, 2. (a) Fafanua mfano wa Yesu kumhusu mkulima wa mizabibu. (b) Mfano huo unaonyeshaje sifa za ukarimu na fadhili zisizostahiliwa?

ILIKUWA asubuhi na mapema mkulima alipoenda sokoni kutafuta wafanyakazi kwa ajili ya shamba lake la mizabibu. Alikubaliana na wanaume aliokutana nao mshahara ambao angewalipa, nao wakaenda kufanya kazi. Hata hivyo, mkulima huyo alihitaji wafanyakazi zaidi, hivyo alirudi sokoni mara kadhaa siku hiyo ili kutafuta wanaume wengine, naye akawaahidi kuwalipa mshahara mzuri hata wale alioajiri wakati wa alasiri. Ilipofika jioni, aliwaita wafanyakazi wake na kuwalipa mshahara uleule kila mmoja, iwe walifanya kazi kwa saa nyingi au kwa saa moja. Wale waliofanya kazi kwa muda mrefu walipogundua jambo hilo, wakaanza kulalamika. Mkulima akawajibu: ‘Je, hamkukubali kiasi cha pesa nilichowalipa? Je, si halali kwangu kuwalipa wafanyakazi wangu mshahara ninaotaka? Au mnaona wivu kwa sababu mimi ni mkarimu?’—Mt. 20:1-15, maelezo ya chini, NWT.

2 Mfano wa Yesu unatukumbusha sifa moja ya Yehova ambayo inaonyeshwa mara nyingi katika Biblia, yaani, “fadhili [zake] zisizostahiliwa.” [1] (Soma 2 Wakorintho 6:1.) Ni kana kwamba wale waliofanya kazi kwa saa moja tu hawakustahili kupata mshahara wa siku nzima, lakini mkulima huyo aliwaonyesha fadhili zisizo za kawaida. Msomi mmoja aliandika hivi kuhusu maneno “fadhili zisizostahiliwa,” ambayo yanatafsiriwa “neema” katika tafsiri nyingi za Biblia: “Wazo kuu la maneno hayo ni zawadi inayotolewa bure na isiyostahiliwa, kitu ambacho mtu anapewa bila kukifanyia kazi.”

ZAWADI KUU KUTOKA KWA YEHOVA

3, 4. Kwa nini Yehova anawaonyesha wanadamu wote fadhili zisizostahiliwa, na anafanya hivyo jinsi gani?

3 Maandiko yanazungumzia “zawadi ya bure ya fadhili zisizostahiliwa za Mungu.” (Efe. 3:7) Kwa nini Yehova anatupatia “zawadi ya bure,” na anafanya hivyo jinsi gani? Ikiwa tungefuata viwango vya Yehova kikamili, tungestahili kupata fadhili zake. Hata hivyo, tunashindwa kuvifuata kikamili. Hiyo ndiyo sababu Mfalme Sulemani mwenye hekima aliandika hivi: “Hakuna mwanadamu aliye mwadilifu duniani ambaye huendelea kufanya mema na asifanye dhambi.” (Mhu. 7:20) Vivyo hivyo, mtume Paulo alisema hivi: “Wote wamefanya dhambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu,” na “mshahara ambao dhambi hulipa ni kifo.” (Rom. 3:23; 6:23a) Hilo ndilo jambo tunalostahili.

4 Hata hivyo, Yehova aliwapenda sana wanadamu wenye dhambi hivi kwamba akamtuma “Mwana wake mzaliwa-pekee” afe kwa ajili yetu. Huo ndio wonyesho mkubwa zaidi wa fadhili zisizostahiliwa. (Yoh. 3:16) Hivyo, Paulo aliandika kumhusu Yesu kwamba “amevikwa taji la utukufu na heshima kwa kupatwa na kifo, ili kwa fadhili zisizostahiliwa za Mungu aonje kifo kwa ajili ya kila mwanadamu.” (Ebr. 2:9) Naam, “zawadi ambayo Mungu hutoa ni uzima wa milele kupitia Kristo Yesu Bwana wetu.”—Rom. 6:23b.

5, 6. Tutapata matokeo gani tukitawaliwa na (a) dhambi? (b) fadhili zisizostahiliwa?

5 Wanadamu walirithije dhambi na kifo? Biblia inaeleza hivi: “Kwa kosa la mtu mmoja [Adamu] kifo kilitawala kama mfalme” juu ya wazao wa Adamu. (Rom. 5:12, 14, 17) Hata hivyo, tunaweza kuchagua kutotawaliwa na dhambi. Hilo linawezekanaje? Tunapoonyesha imani katika dhabihu ya fidia ya Kristo, tunatawaliwa na fadhili zisizostahiliwa za Yehova. Biblia inasema hivi: “Mahali ambapo dhambi ilizidi, fadhili zisizostahiliwa zilizidi hata zaidi. Kwa kusudi gani? Kwamba, kama vile dhambi ilivyotawala kama mfalme pamoja na kifo, vivyo hivyo pia fadhili zisizostahiliwa zitawale kama mfalme kupitia uadilifu kwa tazamio la uzima wa milele kupitia Yesu Kristo.”—Rom. 5:20, 21.

6 Ingawa sisi ni watenda-dhambi, si lazima dhambi itawale maisha yetu. Tunapofanya dhambi, tunamwomba Yehova msamaha. Paulo aliwaonya hivi Wakristo: “Dhambi haipaswi kuwa bwana juu yenu, kwa kuwa ninyi hamko chini ya sheria bali chini ya fadhili zisizostahiliwa.” (Rom. 6:14) Hivyo, tunatawaliwa na fadhili zisizostahiliwa. Hilo lina matokeo gani? Paulo anaeleza hivi: “Fadhili zisizostahiliwa za Mungu . . . [zinatufundisha] kukataa kabisa kutomwogopa Mungu na tamaa za kilimwengu na tuishi kwa utimamu wa akili na uadilifu na ujitoaji-kimungu katikati ya mfumo wa mambo wa sasa.”—Tito 2:11, 12.

FADHILI ZISIZOSTAHILIWA “ZINAZOONYESHWA KWA NJIA MBALIMBALI”

7, 8. Inamaanisha nini kwamba fadhili zisizostahiliwa za Yehova ‘zinaonyeshwa kwa njia mbalimbali’? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

7 Mtume Petro aliandika hivi: “Kwa kadiri ambayo kila mmoja amepokea zawadi, itumieni katika kuhudumiana kama wasimamizi-nyumba wazuri wa fadhili zisizostahiliwa za Mungu zinazoonyeshwa kwa njia mbalimbali.” (1 Pet. 4:10) Hilo linamaanisha nini? Linamaanisha kwamba hata tupate jaribu la namna gani, Yehova atatuwezesha kukabiliana nalo. (1 Pet. 1:6) Sikuzote Mungu atatuonyesha fadhili zisizostahiliwa za kutusaidia kuvumilia jaribu hilo.

8 Kwa kweli, fadhili zisizostahiliwa za Yehova zinaonyeshwa kwa njia mbalimbali. Mtume Yohana aliandika hivi: “Sisi sote tulipokea kutokana na wingi alio nao, hata fadhili zisizostahiliwa juu ya fadhili zisizostahiliwa.” (Yoh. 1:16) Wonyesho mbalimbali wa fadhili za Yehova hutokeza baraka nyingi. Ni nini baadhi ya baraka hizo?

9. Tunapata manufaa gani kutokana na fadhili zisizostahiliwa za Yehova, na tunaweza kuonyeshaje kwamba tunazithamini?

9 Kusamehewa dhambi zetu. Kwa sababu ya fadhili zisizostahiliwa za Yehova, tunapotubu na kuendelea kujitahidi kupambana na mwelekeo wetu wa kufanya dhambi, tunasamehewa. (Soma 1 Yohana 1:8, 9.) Rehema ya Mungu inapaswa kutuchochea kumthamini na kumtukuza. Paulo alipowaandikia Wakristo wenzake waliotiwa mafuta, alisema hivi: “[Yehova] alitukomboa kutoka katika mamlaka ya giza, akatuhamisha na kutuingiza katika ufalme wa Mwana wa upendo wake, ambaye kwa njia yake tunaachiliwa huru kupitia fidia, kusamehewa dhambi zetu.” (Kol. 1:13, 14) Kusamehewa dhambi zetu kunatufanya tupate baraka nyingine nyingi.

10. Tunafurahia nini kwa sababu ya fadhili zisizostahiliwa za Mungu?

10 Kuwa na amani pamoja na Mungu. Tulizaliwa tukiwa adui za Mungu kwa sababu ya hali yetu ya dhambi. Paulo alikubaliana na hilo aliposema hivi: “Tulipokuwa adui tulipatanishwa na Mungu kupitia kifo cha Mwana wake.” (Rom. 5:10) Kupatanishwa huko kumetuwezesha kuwa na amani pamoja na Yehova. Paulo alihusianisha pendeleo hilo na fadhili zisizostahiliwa za Yehova, alipowaambia hivi Wakristo wenzake waliotiwa mafuta: “Kwa kuwa sasa tumetangazwa kuwa waadilifu kutokana na imani, na tufurahie amani pamoja na Mungu kupitia Bwana wetu Yesu Kristo, ambaye kupitia yeye pia tumekaribia kwa njia ya imani kuingia katika fadhili hizi zisizostahiliwa ambamo sasa tunasimama.” (Rom. 5:1, 2) Hiyo ni baraka iliyoje!

Pendeleo la kusikiliza habari njema (Tazama fungu la 11)

11. Watiwa mafuta wanawaletaje “kondoo wengine” kwenye uadilifu?

11 Tunaweza kuwa waadilifu machoni pa Mungu. Sisi sote ni watenda-dhambi. Hata hivyo, nabii Danieli alitabiri kwamba katika siku za mwisho, “wale walio na ufahamu,” yaani, watiwa mafuta, “[wangewaleta] wengi kwenye uadilifu.” (Soma Danieli 12:3.) Kupitia kazi ya kuhubiri na kufundisha, wamewaleta mamilioni ya “kondoo wengine” kwenye msimamo wa uadilifu machoni pa Yehova. (Yoh. 10:16) Hata hivyo, jambo hilo limewezekana kwa sababu ya fadhili zisizostahiliwa za Yehova. Paulo alifafanua hivi: “Ni zawadi ya bure kwamba wanatangazwa kuwa waadilifu kwa fadhili [za Mungu] zisizostahiliwa kupitia kuachiliwa huru kwa njia ya fidia ambayo Kristo Yesu alilipa.”—Rom. 3:23, 24.

Baraka ya sala (Tazama fungu la 12)

12. Sala inahusianaje na fadhili zisizostahiliwa za Mungu?

12 Kukaribia kiti cha Ufalme cha Mungu kupitia sala. Kwa sababu ya fadhili zake zisizostahiliwa, Yehova ametupatia pendeleo la kukaribia kiti chake cha Ufalme mbinguni kupitia sala. Kwa hakika, Paulo alikiita kiti cha Ufalme cha Yehova, “kiti cha ufalme cha fadhili zisizostahiliwa” na anatualika tukikaribie “tukiwa na uhuru wa kusema.” (Ebr. 4:16a) Yehova ametupatia pendeleo hilo kupitia Mwana wake, “ambaye kwa njia yake tuna uhuru huu wa kusema na tuna uwezo wa kukaribia tukiwa na uhakika kupitia imani yetu katika yeye.” (Efe. 3:12) Kumkaribia katika sala wakati wowote na mahali popote ni wonyesho wa pekee wa fadhili zisizostahiliwa za Yehova.

Kupata msaada wakati unaofaa (Tazama fungu la 13)

13. Fadhili zisizostahiliwa zinaweza kutusaidiaje “kwa wakati unaofaa”?

13 Kupata msaada kwa wakati unaofaa. Paulo alitutia moyo tumkaribie Yehova kwa uhuru katika sala “ili tupokee rehema na kupata fadhili zisizostahiliwa kuwa msaada kwa wakati unaofaa.” (Ebr. 4:16b) Wakati wowote tunapokabili majaribu au hali ngumu maishani, tunaweza kumlilia Yehova ili atusaidie kwa kutuonyesha rehema. Ingawa hatustahili, mara nyingi Yehova anajibu sala zetu kupitia Wakristo wenzetu, “hivi kwamba tuwe hodari na kusema: ‘Yehova ni msaidizi wangu; sitaogopa. Mwanadamu anaweza kunitenda nini?’”—Ebr. 13:6.

14. Fadhili zisizostahiliwa za Yehova zinanufaishaje mioyo yetu?

14 Kupata faraja moyoni. Baraka kubwa inayotokana na fadhili zisizostahiliwa za Yehova ni kufarijiwa tunapovunjika moyo. (Zab. 51:17) Paulo aliwaandikia hivi Wakristo walioishi Thesalonike, ambao walikuwa wakikabili mateso: “Bwana wetu Yesu Kristo mwenyewe na Mungu Baba yetu, aliyetupenda na kutupa sisi faraja ya milele na tumaini jema kwa njia ya fadhili zisizostahiliwa, na aifariji mioyo yenu na kuwaimarisha ninyi katika kila tendo na neno jema.” (2 The. 2:16, 17) Tunafarijika sana tunapotambua jinsi Yehova anavyotutunza kwa upendo kwa sababu ya fadhili zake zisizo na kifani!

15. Fadhili zisizostahiliwa za Mungu zinatupatia tumaini gani?

15 Kuwa na tumaini la uzima wa milele. Kwa kuwa sisi ni watenda-dhambi, bila msaada hatungekuwa na tumaini lolote. (Soma Zaburi 49:7, 8.) Hata hivyo, Yehova ametupatia tumaini zuri ajabu! Yesu aliwaahidi hivi wafuasi wake: “Haya ndiyo mapenzi ya Baba yangu, kwamba kila mtu ambaye humtazama Mwana na kumwamini awe na uzima wa milele.” (Yoh. 6:40) Naam, tumaini la uzima wa milele ni zawadi na wonyesho mkuu wa fadhili zisizostahiliwa za Mungu. Paulo alikubaliana na jambo hilo, naye alisema hivi: “Fadhili zisizostahiliwa za Mungu zinazowaletea watu wa namna zote wokovu zimeonyeshwa.”—Tito 2:11.

USITUMIE VIBAYA FADHILI ZISIZOSTAHILIWA ZA MUNGU

16. Baadhi ya Wakristo wa mapema walitumiaje vibaya fadhili zisizostahiliwa za Mungu?

16 Tunapokea baraka nyingi kwa sababu ya fadhili zisizostahiliwa za Yehova. Hata hivyo, hatupaswi kuzitumia vibaya, yaani, kuzigeuza kuwa kisingizio cha kutenda dhambi. Baadhi ya Wakristo wa mapema walijaribu ‘kuzigeuza fadhili zisizostahiliwa za Mungu kuwa kisingizio cha mwenendo mpotovu.’ (Yuda 4) Inaelekea Wakristo hao wasio washikamanifu waliwaza kwamba wangeweza kufanya dhambi na kisha wamwombe Yehova msamaha kila mara. Hata walijaribu kuwashawishi ndugu wengine wajiunge nao katika matendo yao mapotovu. Leo pia, mtu yeyote anayefanya hivyo “[anaitendea] kwa dharau ile roho ya fadhili zisizostahiliwa.”—Ebr. 10:29.

17. Petro alitoa ushauri gani mkali?

17 Leo, Shetani amewapotosha Wakristo fulani wafikiri kwamba wanaweza kutenda dhambi na Yehova atawasamehe bila kutubu. Ingawa Yehova yuko tayari kuwasamehe watenda-dhambi wanaotubu, anatarajia wajitahidi kupambana na mwelekeo wao wa kutenda dhambi. Alimwongoza kwa roho Petro aandike hivi: “Kwa hiyo, ninyi, wapendwa, mkiwa na ujuzi huu wa kimbele, jilindeni ili msichukuliwe mbali pamoja nao kwa kosa la watu wanaokaidi sheria, mwanguke kutoka kwenye uimara wenu wenyewe. Hapana, bali endeleeni kukua katika fadhili zisizostahiliwa na ujuzi juu ya Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo.”—2 Pet. 3:17, 18.

FADHILI ZISIZOSTAHILIWA ZINATUPATIA WAJIBU

18. Kwa sababu ya fadhili zisizostahiliwa za Yehova, tuna majukumu gani?

18 Tunamshukuru sana Yehova kwa kutuonyesha fadhili zisizostahiliwa. Kwa hiyo, tunapaswa tutumie zawadi zetu kumheshimu Yehova na kuwasaidia wengine. Tuna wajibu wa kufanya hivyo. Tunaweza kutumiaje zawadi hizo? Paulo anajibu hivi: “Kwa kuwa tuna zawadi zinazotofautiana kulingana na fadhili zisizostahiliwa tulizopewa, kama . . . ni huduma, na tuwe katika huduma hii; au yeye anayefundisha, na awe katika kufundisha kwake; au yeye anayehimiza, na awe katika kuhimiza kwake; . . . yeye anayeonyesha rehema, na afanye hivyo kwa uchangamfu.” (Rom. 12:6-8) Hivyo, kwa sababu ya fadhili zisizostahiliwa za Yehova, tuna jukumu la kuhubiri kwa bidii, kufundisha wengine, kutia moyo ndugu na dada zetu, na kusamehe wale wanaotukosea.

19. Ni wajibu gani tulio nao ambao tutachunguza katika makala inayofuata?

19 Kwa kuwa tumebarikiwa kupokea fadhili zisizostahiliwa za Yehova, tunapaswa kuchochewa kufanya yote tuwezayo “kutoa ushahidi kamili kuhusu habari njema ya fadhili zisizostahiliwa za Mungu.” (Mdo. 20:24) Tutachunguza kwa undani wajibu huo katika makala inayofuata.

^ [1] (fungu la 2) Tazama kichwa “Undeserved kindness” kwenye “Glossary of Bible Terms” katika Tafsiri ya Ulimwengu Mpya toleo la 2013 ya Kiingereza.