Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Eneza Habari Njema za Fadhili Zisizostahiliwa

Eneza Habari Njema za Fadhili Zisizostahiliwa

‘Toa ushahidi kamili kuhusu habari njema ya fadhili zisizostahiliwa za Mungu.’MDO. 20:24.

NYIMBO: 101, 84

1, 2. Mtume Paulo alionyeshaje kwamba alithamini fadhili zisizostahiliwa za Mungu?

MTUME Paulo angeweza kusema hivi kwa unyoofu: “Fadhili [za Mungu] zisizostahiliwa zilizonielekea mimi hazikuwa za bure.” (Soma 1 Wakorintho 15:9, 10.) Paulo alijua vema kwamba hakufanyia kazi au kustahili kupata rehema nyingi za Mungu kwa kuwa alikuwa akiwatesa Wakristo hapo awali.

2 Alipokuwa akikaribia kufa, Paulo alimwandikia mfanyakazi mwenzake Timotheo hivi: “Mimi namshukuru Kristo Yesu Bwana wetu, aliyenipa nguvu, kwa sababu aliniona kuwa mwaminifu kwa kunigawia huduma.” (1 Tim. 1:12-14) Alipewa huduma gani? Paulo aliwaambia wazee huko Efeso mambo yaliyohusika katika huduma hiyo aliposema hivi: “Siifanyi nafsi yangu kuwa kitu chenye thamani sana kwangu, kama tu ningepata kumaliza mwendo wangu na huduma niliyopokea kutoka kwa Bwana Yesu, kutoa ushahidi kamili kuhusu habari njema ya fadhili zisizostahiliwa za Mungu.”Mdo. 20:24.

3. Paulo alipewa huduma gani ya pekee? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

3 Ni ‘habari gani njema’ ambayo Paulo alihubiri inayokazia fadhili zisizostahiliwa za Yehova? Aliwaambia Wakristo Waefeso hivi: “Mmesikia juu ya usimamizi-nyumba wa fadhili zisizostahiliwa za Mungu ambao nilipewa kwa ajili yenu.” (Efe. 3:1, 2) Paulo alipewa mgawo wa kueneza habari njema kwa watu wasio Wayahudi ili wao pia wawe miongoni mwa wale ambao wangeitwa kushirikiana na Kristo katika Ufalme wa Kimasihi. (Soma Waefeso 3:5-8.) Paulo alihubiri kwa bidii na hivyo akawawekea mfano mzuri Wakristo leo, naye alionyesha kwamba hakuwa amepokea fadhili zisizostahiliwa za Mungu “bure.”

JE, UNACHOCHEWA NA FADHILI ZISIZOSTAHILIWA ZA MUNGU?

4, 5. Kwa nini tunaweza kusema kwamba “habari njema ya Ufalme” ni sawa na “habari njema ya fadhili zisizostahiliwa za Mungu”?

4 Katika siku hizi za mwisho, watu wa Yehova wamepewa mgawo wa kuhubiri “habari njema ya ufalme . . . katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote.” (Mt. 24:14) Ujumbe tunaoeneza pia ni “habari njema ya fadhili zisizostahiliwa za Mungu” kwa kuwa baraka zote tunazotumaini kupokea chini ya utawala wa Ufalme zinatokana na fadhili za Yehova zilizoonyeshwa kupitia Kristo. (Efe. 1:3) Tukiwa mtu mmojammoja, je, tunamwiga Paulo kwa kuonyesha shukrani kwa sababu ya fadhili zisizostahiliwa za Yehova kwa kuhubiri kwa bidii?—Soma Waroma 1:14-16.

5 Katika makala iliyotangulia, tulijifunza jinsi tunavyoweza kufaidika katika njia nyingi na fadhili zisizostahiliwa za Yehova licha ya kuwa wenye dhambi. Kwa hiyo, tuna wajibu wa kufanya yote tuwezayo kuwajulisha watu wote jinsi Yehova anavyoonyesha upendo na jinsi wao wanavyoweza kunufaishwa nao. Tunaweza kuwasaidia watu wathamini fadhili zisizostahiliwa za Mungu katika njia zipi?

ENEZA HABARI NJEMA YA DHABIHU YA FIDIA

6, 7. Tunapowaeleza watu kuhusu fidia, tunaenezaje habari njema za fadhili zisizostahiliwa za Mungu?

6 Leo, watu wengi hawajuti wanapotenda dhambi, kwa hiyo hawaelewi sababu inayofanya wanadamu wahitaji fidia. Wakati huohuo, wengi zaidi wanaona kwamba kuishi bila vizuizi hakuleti furaha. Kwa ujumla, watu wengi hutambua maana ya dhambi, jinsi inavyotuathiri, na mambo wanayopaswa kufanya ili wakombolewe kutoka katika utumwa wa dhambi, baada ya kuzungumza na Mashahidi wa Yehova. Watu wenye mioyo minyoofu wanafurahi kujua kwamba Yehova alimtuma Mwana wake duniani kutufidia kutoka kwa dhambi na matokeo yake kifo, kwa sababu ya upendo wake mwingi na fadhili zisizostahiliwa.—1 Yoh. 4:9, 10.

7 Paulo alipokuwa akizungumza kuhusu Mwana mpendwa wa Yehova, aliandika hivi: “Kwa njia yake [Yesu] tuna kuachiliwa huru kwa njia ya fidia kupitia damu ya huyo, ndiyo, msamaha wa makosa yetu, kulingana na utajiri wa fadhili zake [Yehova] zisizostahiliwa.” (Efe. 1:7) Dhabihu ya fidia ya Kristo ni uthibitisho mkubwa zaidi kwamba Mungu anatupenda na inaonyesha utajiri wa fadhili Zake zisizostahiliwa. Inafariji sana kujifunza kwamba tukionyesha imani katika damu ya Yesu iliyomwagwa, tutasamehewa dhambi zetu na kuwa na dhamiri safi! (Ebr. 9:14) Bila shaka hizo ni habari njema za kuwaeleza wengine!

WASAIDIE WATU WAWE MARAFIKI WA MUNGU

8. Kwa nini wanadamu wenye dhambi wanahitaji kupatanishwa na Mungu?

8 Tuna wajibu wa kuwajulisha wanadamu wenzetu kwamba wanaweza kuwa marafiki wa Muumba wao. Ikiwa watu hawaonyeshi imani katika dhabihu ya Yesu, Mungu anawaona kuwa maadui wake. Mtume Yohana aliandika hivi: “Yule anayemwamini Mwana ana uzima wa milele; yule asiyemtii Mwana hataona uzima, bali ghadhabu ya Mungu hukaa juu yake.” (Yoh. 3:36) Tunafurahi kujua kwamba tunaweza kupatanishwa na Mungu kupitia dhabihu ya Kristo. Paulo alisema hivi: “Hapo zamani mlikuwa mmetengwa, nanyi mlikuwa adui kwa sababu akili zenu zilikuwa zimekazwa juu ya matendo maovu, yeye sasa amewapatanisha tena kwa njia ya mwili wenye nyama wa huyo kupitia kifo chake.”—Kol. 1:21, 22.

9, 10. (a) Kristo aliwapa ndugu zake watiwa mafuta daraka gani? (b) “Kondoo wengine” wanawasaidiaje ndugu zao watiwa mafuta?

9 Kristo amewapa ndugu zake watiwa mafuta duniani kile ambacho Paulo alikiita “huduma ya upatanisho.” Akieleza kuhusu huduma hiyo, Paulo aliwaandikia hivi Wakristo watiwa mafuta wa karne ya kwanza: “Mambo yote yametoka kwa Mungu, aliyetupatanisha sisi kwake mwenyewe kupitia Kristo na kutupa sisi huduma ya upatanisho, yaani, kwamba Mungu kupitia Kristo alikuwa akiupatanisha ulimwengu kwake mwenyewe, bila kuwahesabia makosa yao, naye alitukabidhi sisi lile neno la upatanisho. Kwa hiyo sisi ni mabalozi walio badala ya Kristo, kana kwamba Mungu alikuwa akisihi kupitia sisi. Kama walio badala ya Kristo tunaomba: ‘Mpatanishwe pamoja na Mungu.’”—2 Kor. 5:18-20.

10 “Kondoo wengine” wana pendeleo la kuwasaidia ndugu zao watiwa mafuta katika huduma hii. (Yoh. 10:16) Wanatumikia wakiwa wajumbe wa Kristo, nao wanafanya kazi kubwa zaidi ya kuwafundisha watu kweli za kiroho na kuwasaidia wasitawishe uhusiano pamoja na Yehova. Hiyo ni sehemu muhimu ya kazi ya kutoa ushahidi kamili kuhusu habari njema ya fadhili zisizostahiliwa za Mungu.

WAFUNDISHE WATU KWAMBA MUNGU HUSIKILIZA SALA

11, 12. Watu wanapojifunza kwamba wanaweza kusali kwa Yehova, kwa nini hiyo ni habari njema?

11 Watu wengi wanasali ili wajihisi vizuri, hata hivyo, hawaamini kwamba Mungu husikiliza sala zao. Wanahitaji kujua kwamba Yehova ni “msikiaji wa sala.” Mtunga-zaburi Daudi aliandika hivi: “Ee msikiaji wa sala, kwako wewe watu wote wenye mwili watakuja. Mambo yenye makosa yamekuwa na nguvu kuliko mimi. Nayo makosa yetu, wewe mwenyewe utayafunika.”—Zab. 65:2, 3.

12 Yesu aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Mkiomba jambo lolote katika jina langu, nitalifanya.” (Yoh. 14:14) Bila shaka, “jambo lolote” linamaanisha chochote kinachopatana na mapenzi ya Yehova. Yohana anatuhakikishia hivi: “Na huu ndio uhakika ambao tunao kwake, kwamba, hata tukiomba nini kulingana na mapenzi yake, yeye hutusikia.” (1 Yoh. 5:14) Inapendeza sana kuwafundisha wengine kwamba sala si njia ya kutuliza akili na hisia tu, badala yake inatusaidia kukaribia “kiti cha ufalme cha fadhili zisizostahiliwa” cha Yehova. (Ebr. 4:16) Kwa kuwafundisha wasali kwa njia inayofaa, kwa mtu anayefaa, na kuomba mambo yanayofaa, tunaweza kuwasaidia wamkaribie Yehova na kupata faraja wanapofadhaika.—Zab. 4:1; 145:18.

FADHILI ZISIZOSTAHILIWA KATIKA MFUMO MPYA WA MAMBO

13, 14. (a) Watiwa mafuta watakuwa na mapendeleo gani makubwa wakati ujao? (b) Watiwa mafuta watawafanyia wanadamu kazi gani nzuri?

13 Yehova ataonyesha fadhili zisizostahiliwa hata zaidi “katika mifumo ya mambo inayokuja.” Akirejelea pendeleo kubwa sana ambalo Mungu amewapa wale 144,000 watakaotawala na Kristo katika Ufalme wake wa mbinguni, Paulo aliandika hivi: “Mungu, aliye tajiri katika rehema, kwa upendo wake mkubwa aliotupenda nao, alitufanya hai pamoja na Kristo, tulipokuwa wafu katika makosa—kwa fadhili zisizostahiliwa ninyi mmeokolewa—naye alituinua pamoja na kutuketisha pamoja katika mahali pa kimbingu katika muungano na Kristo Yesu, ili katika mifumo ya mambo inayokuja uonyeshwe utajiri mwingi zaidi wa fadhili zake zisizostahiliwa katika neema yake kutuelekea sisi katika muungano na Kristo Yesu.”—Efe. 2:4-7.

14 Ni vigumu kuwazia mambo mazuri mno ambayo Yehova amewatayarishia Wakristo watiwa mafuta watakapotawala na Kristo mbinguni. (Luka 22:28-30; Flp. 3:20, 21; 1 Yoh. 3:2) Yehova ‘atawaonyesha’ hasa watiwa mafuta “utajiri mwingi zaidi wa fadhili zake zisizostahiliwa.” Watafanyiza “Yerusalemu Jipya,” bibi-arusi wa Kristo. (Ufu. 3:12; 17:14; 21:2, 9, 10) Wakiwa pamoja na Yesu ‘wataponya mataifa.’ Watasaidia wanadamu wawe huru kutokana na madhara ya dhambi na kifo na kuwasaidia wawe wakamilifu.—Soma Ufunuo 22:1, 2, 17.

15, 16. Yehova atawaonyeshaje “kondoo wengine” fadhili zake zisizostahiliwa wakati ujao?

15 Katika andiko la Waefeso 2:7 tunasoma kwamba Mungu ataonyesha fadhili zisizostahiliwa “katika mifumo ya mambo inayokuja.” Bila shaka, katika mfumo mpya wa Yehova hapa duniani tutashuhudia “utajiri mwingi zaidi wa fadhili zake zisizostahiliwa.” (Luka 18:29, 30) Njia moja kuu ambayo Yehova ataonyesha fadhili zisizostahiliwa duniani ni kupitia ufufuo wa wanadamu kutoka katika “Kaburi.” (Ayu. 14:13-15; Yoh. 5:28, 29) Wanaume na wanawake waaminifu wa zamani waliokufa kabla ya Kristo kujidhabihu, pamoja na “kondoo wengine” wanaokufa wakiwa waaminifu katika siku za mwisho, watafufuliwa ili waendelee kumtumikia Yehova.

16 Mamilioni ya wanadamu waliokufa bila kujifunza kumhusu Mungu watafufuliwa pia. Watapewa nafasi ya kujitiisha chini ya enzi kuu ya Yehova. Yohana aliandika hivi: “Nikawaona wafu, wakubwa kwa wadogo, wamesimama mbele ya kile kiti cha ufalme, na vitabu vya kukunjwa vikafunguliwa. Lakini kitabu kingine cha kukunjwa kikafunguliwa; hicho ni kitabu cha uzima. Na wafu wakahukumiwa kutokana na mambo yale yaliyoandikwa katika vile vitabu kulingana na matendo yao. Na bahari ikawatoa wale wafu waliokuwa ndani yake, na kifo na Kaburi vikawatoa wale wafu waliokuwa ndani yake, nao walihukumiwa kila mmoja kulingana na matendo yake.” (Ufu. 20:12, 13) Bila shaka, watakaofufuliwa watahitaji kujifunza kutumia kanuni za Mungu zilizo katika Biblia. Pia, watahitaji kufuata maagizo mapya yanayofaa ambayo yatafunuliwa katika “vitabu vya kukunjwa” vyenye matakwa ya Yehova ya kuishi katika mfumo mpya wa mambo. Kufunuliwa kwa habari zilizo kwenye vitabu vya kukunjwa ni wonyesho mwingine wa fadhili zisizostahiliwa za Yehova.

ENDELEA KUENEZA HABARI NJEMA

17. Tunapaswa kukumbuka nini tunapohubiri?

17 Ni muhimu sana kuhubiri habari njema ya Ufalme sasa kuliko wakati mwingine wowote kwa sababu mwisho umekaribia! (Marko 13:10) Kwa hakika, habari njema inakazia fadhili zisizostahiliwa za Yehova. Tunapaswa kukumbuka jambo hilo tunapohubiri. Lengo letu tunapohubiri ni kumtukuza Yehova. Tunaweza kufanya hivyo kwa kuwaonyesha watu kwamba ahadi zote kuhusu baraka za ulimwengu mpya zinaonyesha fadhili nyingi sana za Yehova.

Tumikieni kwa bidii mkiwa “wasimamizi-nyumba wazuri wa fadhili zisizostahiliwa za Mungu.” —1 Pet. 4:10 (Tazama fungu la 17 hadi 19)

18, 19. Tunatukuza fadhili zisizostahiliwa za Yehova jinsi gani?

18 Tunapowahubiria wengine, tunaweza kuwaeleza kwamba chini ya utawala wa Ufalme wa Kristo, wanadamu watapata faida kamili za dhabihu ya fidia na hatua kwa hatua watafikia ukamilifu. Biblia inasema hivi: “Uumbaji wenyewe pia utawekwa huru kutoka katika utumwa wa uharibifu na kuwa na uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu.” (Rom. 8:21) Hilo litawezekana tu kupitia fadhili za Yehova zisizo na kifani.

19 Tuna pendeleo la kuwaambia wote watakaosikiliza ahadi hii yenye kusisimua katika Ufunuo 21:4, 5: “[Mungu] atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.” Na Yehova, yule aliyeketi juu ya kiti cha Ufalme anasema hivi: “Tazama! Ninafanya vitu vyote kuwa vipya.” Pia, anasema: “Andika, kwa sababu maneno haya ni ya uaminifu na ya kweli.” Kwa kweli, tunatukuza fadhili zisizostahiliwa za Yehova tunapowahubiria wengine habari njema kwa bidii!