Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tafuta Ufalme, Si Vitu

Tafuta Ufalme, Si Vitu

“Tafuteni ufalme wa Mungu, na vitu hivi vyote vitaongezwa kwenu.” —LUKA 12:31, Zaire Swahili Bible.

NYIMBO: 40, 98

1. Kuna tofauti gani kati ya vitu tunavyohitaji na vitu tunavyotaka?

INASEMEKANA kwamba mwanadamu anahitaji vitu vichache lakini vitu anavyotaka ni vingi sana. Inaelekea watu wengi hawawezi kutofautisha kati ya vitu wanavyohitaji na vitu wanavyotaka. Kuna tofauti gani? Mahitaji ni vitu ambavyo lazima uwe navyo kwa sababu uhai wako unavitegemea. Mahitaji ya lazima ni chakula, mavazi, na makazi. Kitu unachotaka ni kitu unachopenda kuwa nacho ingawa si cha lazima ili uishi.

2. Ni baadhi ya vitu gani ambavyo watu wanataka?

2 Vitu ambavyo watu wanataka vinaweza kutofautiana sana ikitegemea mahali wanapoishi. Katika nchi maskini huenda watu wengi wakataka kupata pesa za kununua simu, pikipiki, au eneo la kuishi. Katika nchi tajiri, huenda watu wakatamani kununua nguo za bei ghali, nyumba kubwa zaidi, au gari la kifahari. Kwa vyovyote vile, kuna hatari ya kunaswa na mtego wa kupenda vitu vya kimwili, yaani, tamaa ya kupata vitu vingi zaidi, iwe tunavihitaji au la, ama tunaweza kuvinunua au hatuwezi.

JIHADHARI NA MTEGO WA KUPENDA VITU VYA KIMWILI

3. Kupenda vitu vya kimwili kunamaanisha nini?

3 Kupenda vitu vya kimwili kunamaanisha nini? Kunamaanisha kukazia fikira zaidi vitu vya kimwili kuliko uhusiano wetu na Mungu. Chanzo cha kupenda vitu vya kimwili hutokana na tamaa ya mtu, mambo anayotanguliza na kukazia maishani. Kunatufanya tutamani kumiliki vitu vingi zaidi vya kimwili. Huenda mtu anayependa vitu vya kimwili asiwe na pesa nyingi au asiweze kununua vitu vya bei ghali. Hata maskini wanaweza kupenda vitu vya kimwili na kupuuza kutafuta kwanza Ufalme.—Ebr. 13:5.

4. Shetani anatumiaje “tamaa ya macho”?

4 Shetani anatumia mfumo wa kibiashara wa ulimwengu huu kutushawishi tuamini kwamba ili tufurahie maisha tunapaswa kuwa na vitu vingi vya kimwili kuliko tunavyohitaji. Anatumia kwa ustadi “tamaa ya macho.” (1 Yoh. 2:15-17; Mwa. 3:6; Met. 27:20) Kila siku, tunaona na kusikia matangazo ya biashara ambayo yanatushawishi tununue vitu vipya. Je, umewahi kununua kitu fulani usichohitaji kwa sababu tu ulikiona kwenye tangazo la biashara au dukani? Je, baadaye ulitambua kwamba ungeweza kuishi bila kitu hicho? Vitu hivyo ambavyo si vya lazima vinafanya maisha yetu yawe magumu na yatulemee. Vinaweza kutunasa na kutufanya tupuuze ratiba yetu ya mambo ya kiroho kama vile kujifunza Biblia, kutayarisha na kuhudhuria mikutano, na kuhubiri. Kumbuka, mtume Yohana alitoa onyo hili: “Ulimwengu unapitilia mbali na pia tamaa yake.”

5. Tunaweza kupatwa na nini ikiwa tutatumia nguvu zetu zote kutafuta vitu vingi vya kimwili?

5 Shetani anataka tutumikie Utajiri badala ya kumtumikia Yehova. (Mt. 6:24) Lakini ikiwa tunataka tu kupata vitu vingi vya kimwili, maisha yetu hayatakuwa na kusudi. Tunaweza kukata tamaa au kupata matatizo ya kiuchumi, na jambo baya hata zaidi, huenda tukapoteza imani yetu kwa Yehova na Ufalme wake. (1 Tim. 6:9, 10; Ufu. 3:17) Ni kama Yesu alivyosema katika mfano wake kuhusu mpandaji. Ujumbe wa Ufalme “[unapopandwa] katikati ya miiba . . . , tamaa za mambo yale mengine hupenya na kulisonga neno, nalo hukosa kuzaa matunda.”—Marko 4:14, 18, 19.

6. Tunajifunza nini kutoka kwa Baruku?

6 Mfikirie Baruku, mwandishi wa nabii Yeremia. Jiji la Yerusalemu lilipokuwa karibu kuharibiwa kama ilivyotabiriwa, Baruku alianza “kujitafutia makuu,” vitu ambavyo havingedumu. Hata hivyo, jambo pekee alilopaswa kutumaini ni kutimizwa kwa ahadi hii ya Yehova: “Nitakupa wewe nafsi yako kuwa nyara.” (Yer. 45:1-5) Bila shaka, Mungu hangehifadhi mali ya mtu yeyote katika jiji ambalo lingeharibiwa. (Yer. 20:5) Kwa kuwa tunakaribia mwisho wa mfumo wa mambo, huu si wakati wa kujirundikia vitu vya kimwili. Tusitarajie kwamba tutaokoka dhiki kuu tukiwa na vitu vyetu vya kimwili hata viwe vya thamani kadiri gani.—Met. 11:4; Mt. 24:21, 22; Luka 12:15.

7. Tutazungumzia nini na kwa nini?

7 Yesu alitoa ushauri bora kuhusu jinsi ya kupata mahitaji ya lazima maishani pasipo kukengeushwa, kupenda vitu vya kimwili, au kuhangaika kupita kiasi. Alizungumzia jambo hilo katika Mahubiri ya Mlimani. (Mt. 6:19-21) Acheni tusome na kuchanganua sehemu ya mahubiri hayo katika Mathayo 6:25-34. Tukifanya hivyo, tutasadiki kwamba tunapaswa ‘tuutafute ufalme,’ si vitu.—Luka 12:31, (ZSB).

YEHOVA HUTUANDALIA MAHITAJI YETU

8, 9. (a) Kwa nini hatupaswi kuwa na wasiwasi kupita kiasi kuhusu mahitaji yetu? (b) Yesu alijua nini kuhusu wanadamu na mahitaji yao?

8 Soma Mathayo 6:25. Yesu alipowaambia wasikilizaji wake ‘waache kuhangaika juu ya nafsi zao,’ ni kana kwamba aliwaambia ‘waache kuwa na wasiwasi.’ Walihangaikia mambo ambayo hawakupaswa kuhangaikia. Yesu alikuwa na sababu nzuri ya kuwaambia waache kufanya hivyo. Wasiwasi au mahangaiko yasiyo ya lazima hata kuhusu mambo yanayofaa, yanaweza kumkengeusha mtu na kumfanya asikazie fikira mambo ya kiroho yaliyo muhimu zaidi maishani. Yesu aliwajali sana wanafunzi wake na hivyo akawaonya mara nne kuhusu hatari hiyo katika mahubiri yake.—Mt. 6:27, 28, 31, 34.

9 Kwa nini Yesu alituambia tusiwe na wasiwasi kuhusu tutakachokula, kunywa, au kuvaa? Je, hayo si mahitaji muhimu zaidi maishani? Bila shaka! Ikiwa tutakosa njia ya kupata mahitaji hayo, je, hatutakuwa na mahangaiko? Bila shaka tutakuwa na mahangaiko, na Yesu alitambua hilo. Alielewa mahitaji ya watu ya kila siku. Isitoshe, alijua hali ngumu ambazo wanafunzi wake wangekabili karne nyingi baadaye katika “siku za mwisho,” ambazo zingekuwa “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Tim. 3:1) Hali hizo zinatia ndani ukosefu wa ajira, kuongezeka kwa bei za bidhaa, ukosefu wa chakula, na umaskini wa kupindukia. Hata hivyo, Yesu alitambua pia kwamba ‘nafsi inamaanisha zaidi ya chakula na mwili zaidi ya mavazi.’

10. Yesu alipowafunza wafuasi wake jinsi ya kusali, alisema ni nini kinachopaswa kuwa muhimu zaidi maishani mwao?

10 Mwanzoni mwa mahubiri yake, Yesu aliwafundisha wasikilizaji wake wamwombe Baba yao wa mbinguni awapatie mahitaji yao ya kimwili, alipowaambia wasali hivi: “Utupe leo mkate wetu kwa ajili ya siku hii.” (Mt. 6:11) Au kama alivyosema baadaye: “Utupe mkate wetu kwa ajili ya siku kulingana na mahitaji ya siku hiyo.” (Luka 11:3) Lakini ushauri huo haumaanishi kwamba tunapaswa kufikiria daima mahitaji ya kimwili. Katika sala hiyo ya kielelezo, Yesu alionyesha kwamba kusali Ufalme wa Mungu uje ndilo jambo muhimu zaidi. (Mt. 6:10; Luka 11:2) Ili kuwafanya wasikilizaji wake wasiwe na wasiwasi, Yesu alikazia kwamba sikuzote Yehova hutuandalia mahitaji yetu kwa njia isiyo na kifani.

11, 12. Tunajifunza nini kuhusu jinsi Yehova anavyowatunza ndege wa mbinguni? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

11 Soma Mathayo 6:26. Tunapaswa “[kuwaangalia] kwa makini ndege wa mbinguni.” Ingawa ni viumbe wadogo, wanakula matunda, mbegu, wadudu, au minyoo wengi. Kwa kweli ikiwa ndege angekuwa mkubwa kama mwanadamu, angekula chakula kingi zaidi kuliko mwanadamu. Hata hivyo, hawahitaji kulima wala kupanda mimea ili kupata chakula. Yehova huwaandalia kila kitu wanachohitaji. (Zab. 147:9) Bila shaka, hawalishi chakula katika vinywa vyao! Wanahitaji kwenda kukitafuta, na chakula hicho hupatikana kwa wingi.

12 Yesu hakuwazia kamwe kwamba Baba yake wa mbinguni angeweza kuwaandalia ndege chakula na kutowaandalia wanadamu mahitaji ya msingi. [1] (1 Pet. 5:6, 7) Ingawa Yehova hatatulisha chakula katika vinywa vyetu, anaweza kubariki jitihada zetu za kukuza chakula tunachohitaji, au kupata pesa za kununua vitu tunavyohitaji kila siku. Tunapokuwa na uhitaji, anaweza kuwachochea wengine watugawie walicho nacho. Ingawa Yesu hakutaja kwamba ndege wa mbinguni wanapewa makao, Yehova amewapa uwezo na vifaa vya kujitengenezea viota. Vivyo hivyo, Yehova anaweza kutusaidia kupata makao yanayofaa familia zetu.

13. Ni nini kinachothibitisha kwamba tuna thamani zaidi ya ndege wa mbinguni?

13 Yesu aliwauliza wasikilizaji wake hivi: “Je, ninyi si bora kuliko [ndege wa mbinguni]?” Bila shaka, Yesu alisema hivyo kwa sababu alijua kwamba baada ya muda mfupi angetoa uhai wake kwa ajili ya wanadamu. (Linganisha Luka 12:6, 7.) Dhabihu ya fidia ya Kristo haikutolewa kwa ajili ya viumbe wengine wowote. Yesu hakufa kwa ajili ya ndege wa mbinguni bali kwa ajili yetu ili tuweze kuishi milele.—Mt. 20:28.

14. Mtu mwenye mahangaiko hawezi kufanya nini?

14 Soma Mathayo 6:27. Kwa nini Yesu alisema kwamba mtu anayehangaika hawezi kuongeza hata kipimo cha mkono mmoja kwenye uhai wake? Kwa sababu kuwa na wasiwasi kuhusu mahitaji yetu ya kila siku hakutatusaidia kuwa na maisha marefu zaidi. Badala yake, kuhangaika kupita kiasi kunaweza kufanya tufe haraka.

15, 16. (a) Tunajifunza nini kuhusu jinsi Yehova anavyoyatunza mayungiyungi ya shamba? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.) (b) Huenda tukahitaji kujiuliza maswali gani na kwa nini?

15 Soma Mathayo 6:28-30. Ni nani asiyependa kuvaa mavazi mazuri hasa anapokuwa katika shughuli za kiroho kama vile kuhubiri, kuhudhuria mikutano na makusanyiko? Hata hivyo, je, tunapaswa ‘kuhangaika kuhusu mavazi’? Kwa mara nyingine, Yesu anaelekeza fikira zetu kwa uumbaji wa Yehova. Kuhusiana na hilo, tunaweza kujifunza kwa kutazama “mayungiyungi ya shamba.” Huenda ikawa Yesu alikuwa akifikiria maua mbalimbali yenye kupendeza yanayofanana na mayungiyungi. Maua hayo hayahitaji kusokota au kufuma nguo za kujivika. Hata hivyo, yanapendeza sana yanapochanua! “Hata Sulemani katika utukufu wake wote hakupambwa kama moja la haya”!

16 Kumbuka jambo ambalo Yesu alisema: “Ikiwa Mungu huivika hivyo mimea ya shambani . . . , je, yeye hataona ni afadhali zaidi awavike, ninyi wenye imani kidogo?” Bila shaka atafanya hivyo! Lakini wanafunzi wa Yesu walihitaji imani zaidi. (Mt. 8:26; 14:31; 16:8; 17:20) Walihitaji kuwa na imani yenye nguvu zaidi na kumtumaini Yehova. Namna gani sisi? Tuna imani yenye nguvu kadiri gani kwamba Yehova anatamani na anaweza kutuandalia mahitaji yetu?

17. Ni jambo gani linaloweza kuharibu uhusiano wetu na Yehova?

17 Soma Mathayo 6:31, 32. Hatupaswi kuwaiga watu wa “mataifa” ambao hawana imani katika Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo anayewajali wale wanaotanguliza masilahi ya Ufalme maishani mwao. Kujaribu kujikusanyia “vitu ambavyo mataifa yanafuatilia kwa tamaa,” kutaharibu uhusiano wetu na Yehova. Badala ya kujikusanyia vitu vya kimwili, tunaweza kuwa na uhakika kwamba sikuzote tukifanya kile tunachopaswa kufanya, yaani, kutanguliza mambo ya kiroho maishani, Yehova hatatunyima jambo lolote jema. “Ujitoaji-kimungu” unapaswa kutuchochea turidhike na “chakula na kitu cha kujifunika,” au mahali pa kuishi.—1 Tim. 6:6-8.

JE, UNATANGULIZA UFALME WA MUNGU MAISHANI?

18. Yehova anajua nini kumhusu kila mmoja wetu, na atatufanyia nini?

18 Soma Mathayo 6:33. Wanafunzi wa Yesu wanapaswa kutanguliza Ufalme maishani. Tukifanya hivyo, “[tutaongezewa] hivi vitu vingine vyote” kama Yesu alivyosema. Kwa nini alisema hivyo? Alieleza hivi katika mstari uliotangulia: “Baba yenu wa mbinguni anajua mnahitaji vitu hivi vyote,” yaani, mahitaji ya lazima maishani. Yehova anajua vitu tunavyohitaji hata kabla ya sisi kugundua kwamba tunavihitaji. (Flp. 4:19) Anajua nguo yako ambayo itachakaa hivi karibuni. Anajua chakula tunachohitaji na makao yanayotufaa kulingana na ukubwa wa familia yetu. Yehova atahakikisha tunapata kile tunachohitaji hasa.

19. Kwa nini hatupaswi kuwa na wasiwasi kuhusu mambo yanayoweza kutokea wakati ujao?

19 Soma Mathayo 6:34. Yesu alisema hivi kwa mara ya pili: “Msihangaike kamwe.” Alitaka tushughulikie mahangaiko tuliyo nayo kwa siku hiyo tu, huku tukiwa na uhakika kabisa kwamba Yehova atatusaidia. Mtu anapokuwa na wasiwasi kuhusu mambo yanayoweza kutukia wakati ujao, huenda akajaribu kujitegemea badala ya kumtegemea Mungu, na jambo hilo linaweza kuathiri uhusiano wake na Yehova.—Met. 3:5, 6; Flp. 4:6, 7.

TAFUTA UFALME KWANZA NA YEHOVA ATAONGEZA VITU VINGINE

Je, unaweza kurahisisha maisha yako ili ukazie fikira zaidi Ufalme? (Tazama fungu la 20)

20. (a) Unaweza kujiwekea miradi gani katika utumishi wa Yehova? (b) Unaweza kufanya nini ili kurahisisha maisha yako?

20 Ni ubatili kudhabihu masilahi ya Ufalme ili kufuatilia vitu vya kimwili. Badala yake, tunapaswa kufuatilia mambo ya kiroho. Kwa mfano, je, unaweza kuhamia kutaniko lenye uhitaji mkubwa wa wahubiri wa Ufalme? Je, unaweza kuwa painia? Ikiwa wewe ni painia, je, umefikiria kujaza ombi la kuhudhuria Shule ya Waeneza-Injili wa Ufalme? Je, unaweza kujitolea kwa muda kufanya kazi Betheli au katika ofisi ya kutafsiri? Je, unaweza kuwa mjitoleaji katika kazi ya Usanifu/Ujenzi na kufanya kazi kwa muda ya kujenga Majumba ya Ufalme? Fikiria jinsi unavyoweza kurahisisha maisha yako ili ufanye mengi zaidi katika kazi ya Ufalme. Sali na utafakari maelezo yaliyopo katika sanduku lenye kichwa “ Jinsi ya Kurahisisha Maisha Yako,” na uanze kuchukua hatua zitakazokuwezesha kufikia mradi wako.

21. Ni nini kitakachokusaidia umkaribie Yehova zaidi?

21 Yesu alikuwa na sababu nzuri ya kutufundisha tutafute Ufalme na si vitu. Tukifanya hivyo, hatutahangaika kamwe kuhusu mahitaji yetu ya kimwili. Tunamkaribia Yehova kwa sababu tunatumaini kwamba atatutunza. Tunajifunza kujidhibiti kwa kutonunua kila kitu tunachotamani au kila kitu kinachopatikana ulimwenguni hata kama tuna pesa za kukinunua. Tukirahisisha maisha yetu sasa tutafaulu “[kushika] imara uzima ulio wa kweli” wakati ujao.—1 Tim. 6:19.

^ [1] (fungu la 12) Ili kuelewa kwa nini wakati mwingine Yehova anaweza kuruhusu Mkristo akose chakula cha kutosha, ona makala “Maswali Kutoka kwa Wasomaji” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Septemba 15, 2014, ukurasa wa 22.