Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Usiogope. Mimi Mwenyewe Nitakusaidia”

“Usiogope. Mimi Mwenyewe Nitakusaidia”

WAZIA kwamba unatembea barabarani usiku. Ghafla unatambua kwamba mtu fulani anakufuata. Unaposimama naye anasimama. Unapotembea haraka naye pia anaongeza mwendo. Unaanza kukimbia kuelekea nyumba ya rafiki yako iliyo karibu. Rafiki yako anapofungua mlango na kukukaribisha ndani, unahisi ukiwa salama.

Labda hujawahi kukabili hali kama hiyo, lakini mahangaiko mengine ya maisha yanaweza kukufanya uwe na wasiwasi. Kwa mfano, je, unapambana na udhaifu fulani lakini unakushinda? Je, umekosa ajira kwa muda mrefu na umeshindwa kupata kazi yoyote licha ya jitihada nyingi unazofanya? Je, una wasiwasi kwamba utazeeka na kukabili matatizo ya afya? Au kuna jambo lingine lolote linalokufadhaisha?

Hata iwe unakabili tatizo gani, ni vizuri kuwa na rafiki unayeweza kumweleza mahangaiko yako na ambaye yuko tayari kukusaidia. Je, una rafiki kama huyo? Bila shaka! Yehova ndiye rafiki huyo. Andiko la Isaya 41:8-13 linasema kwamba mzee wa ukoo Abrahamu alikuwa na urafiki kama huo na Yehova. Katika mstari wa 10 na 13, Yehova anawaahidi hivi watumishi wake: “Usiogope, kwa maana mimi nipo pamoja nawe. Usitazame huku na huku, kwa maana mimi ni Mungu wako. Nitakutia nguvu. Nitakusaidia kwelikweli. Nitakushika kwelikweli kwa mkono wangu wa kuume wa uadilifu. Kwa maana mimi, Yehova Mungu wako, ninaushika mkono wako wa kuume, Mwenye kukuambia, ‘Usiogope. Mimi mwenyewe nitakusaidia.’”

“NITAKUSHIKA KWELIKWELI”

Maneno ya Yehova yanatufariji sana. Jaribu kuwazia kile ambacho Yehova anatuahidi. Mstari huo hausemi kwamba unatembea pamoja na Yehova ukiwa umemshika mkono, ingawa hilo ni wazo lenye kuvutia. Ikiwa ungetembea pamoja naye, basi mkono wa kulia wa Yehova ungeushika mkono wako wa kushoto. Hata hivyo, Yehova ananyoosha ‘mkono wake wa kuume wa uadilifu’ na kuushika “mkono wako wa kuume,” kana kwamba anakuvuta kutoka katika hali fulani ngumu maishani. Yehova anapokushika mkono wako wa kuume anakuimarisha kwa kukuambia hivi: “Usiogope. Mimi mwenyewe nitakusaidia.”

Je, unamwona Yehova kuwa Baba mwenye upendo na Rafiki atakayekusaidia unapofadhaika? Yehova anakujali, anahangaikia hali yako, na anataka kukusaidia. Unapokabili hali ngumu, Yehova anataka uhisi ukiwa salama kwa sababu anakupenda sana. Kwa kweli, yeye ni “msaada unaopatikana kwa utayari wakati wa taabu.”—Zab. 46:1.

KUHISI HATIA KWA MAKOSA YALIYOPITA

Watu fulani hujilaumu kwa sababu ya mwenendo wao wa zamani na wanajiuliza ikiwa Mungu amewasamehe. Ikiwa unakabili hali kama hiyo, mfikirie mwanamume mwaminifu, Ayubu, ambaye alijilaumu kwa “makosa ya ujana” wake. (Ayu. 13:26) Mtunga zaburi Daudi alikuwa na hisia kama hizo naye alimwomba Yehova hivi: “Usizikumbuke dhambi za ujana wangu na maasi yangu.” (Zab. 25:7) Kwa kuwa sisi si wakamilifu, sote ‘tumefanya dhambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu.’—Rom. 3:23.

Ujumbe ulio katika andiko la Isaya sura ya 41 uliwahusu watu wa kale wa Mungu. Walikuwa wamefanya dhambi sana hivi kwamba Yehova aliamua kutekeleza hukumu juu yao kwa kuwapeleka uhamishoni Babiloni. (Isa. 39:6, 7) Hata hivyo, Mungu alifikiria wakati ujao ambapo angewakomboa wale wote ambao wangetubu na kumrudia! (Isa. 41:8, 9; 49:8) Yehova anaonyesha upendo na rehema kama hiyo kuelekea wale wanaotubu kwa unyoofu na wanaotaka kibali chake.—Zab. 51:1.

Fikiria mfano wa Takuya * aliyekuwa akijitahidi kushinda mazoea machafu ya kutazama ponografia na kupiga punyeto. Alirudia jambo hilo mara kwa mara. Alihisije? “Nilihisi kwamba sifai kabisa, lakini kila mara niliposali kwa Yehova na kumwomba msamaha, alinisaidia.” Yehova alimsaidiaje? Wazee wa kutaniko lake walimwambia awapigie simu wakati wowote aliporudia zoea hilo. Anakiri hivi: “Haikuwa rahisi kuwapigia simu, lakini kila nilipowapigia, niliimarishwa.” Kisha wazee walifanya mipango ili mwangalizi wa mzunguko amfanyie ziara ya uchungaji. Mwangalizi huyo alimwambia hivi: “Sikuja hapa bila sababu. Nimekuja kwa sababu wazee walitaka nije. Walikuchagua ili upate ziara hii ya uchungaji.” Takuya anakumbuka hivi: “Ingawa mimi ndiye niliyekuwa nikifanya dhambi, Yehova aliwatumia wazee kuandaa msaada kwa ajili yangu.” Mwishowe, Takuya aliacha mazoea hayo mabaya, akawa painia wa kawaida, na sasa anatumikia katika ofisi ya tawi. Mungu anaweza kukusaidia jinsi alivyomsaidia ndugu huyo.

UNAPOKUWA NA WASIWASI KUHUSU KUPATA RIZIKI

Watu wengi wanahangaika kwa sababu hawana kazi. Baadhi ya watu wamepoteza kazi na ni vigumu kwao kupata kazi nyingine. Ungehisije ikiwa kila mahali unapokwenda kutafuta kazi unakosa kuajiriwa? Katika hali kama hizo, watu fulani wanahisi kwamba hawafai. Yehova anaweza kukusaidiaje? Huenda asikupe kazi nzuri mara moja, lakini anaweza kukusaidia ukumbuke maneno haya ya Mfalme Daudi: “Nilikuwa kijana, pia nimezeeka, na bado sijamwona mtu yeyote mwadilifu akiwa ameachwa kabisa, wala uzao wake ukitafuta mkate.” (Zab. 37:25) Naam, Yehova anakuona kuwa mwenye thamani, na kwa ‘mkono wake wa kuume wa uadilifu’ anaweza kukusaidia kupata kile unachohitaji ili uendelee kumtumikia.

Yehova anaweza kukusaidiaje ukipoteza kazi?

Sara, anayeishi Kolombia, alitambua jinsi Yehova alivyomsaidia. Alipata pesa nyingi kwa sababu alifanya kazi ya wakati wote kwenye kampuni iliyojulikana sana. Lakini alitaka kuongeza utumishi wake kwa Yehova, hivyo akaacha kazi hiyo na kuwa painia. Hata hivyo, haikuwa rahisi kwake kupata kazi ya muda. Alifungua duka la kuuza aiskrimu lakini alifilisika na akalazimika kulifunga. Sara anasema hivi: “Ingawa miaka mitatu ilipita bila kupata kazi, Yehova alinisaidia kuvumilia.” Alijifunza jinsi ya kutofautisha vitu anavyotaka na anavyohitaji na kutohangaika juu ya kesho. (Mt. 6:33, 34) Mwishowe, mwajiri wake wa zamani alimwita na kumwahidi kwamba atampa kazi aliyokuwa akifanya. Alimwambia kwamba angekubali tu kufanya kazi ya muda na angefanya hivyo ikiwa angepewa nafasi ya kuhubiri na kuhudhuria mikutano. Ingawa Sara hapati pesa nyingi kama mwanzoni, anaweza kujitegemeza akiwa painia. Anasema kwamba katika kipindi hicho kigumu, aliuona mkono wenye upendo wa Yehova.

UNAPOKUWA NA WASIWASI KUHUSU KUZEEKA

Watu wengi wana wasiwasi kwamba watazeeka na hivi karibuni watastaafu. Wana shaka ikiwa watakuwa na pesa za kutosha ili waishi bila matatizo. Pia, wana wasiwasi kuhusu matatizo ya afya ambayo wanaweza kupata watakapozeeka. Inaelekea Daudi ndiye aliyemwomba Yehova hivi: “Usinitupe wakati wa uzee; wakati tu nguvu zangu zinapungua, usiniache.”—Zab. 71:9, 18.

Hivyo basi, watumishi wa Yehova wanaweza kuhisije salama watakapozeeka? Wanahitaji kuendelea kusitawisha imani kwa Mungu, wakitumaini kwamba atawapatia mahitaji yao. Kwa kweli, ikiwa wamezoea maisha ya starehe, huenda wakahitaji kurahisisha maisha yao na kuridhika na vitu vichache vya kimwili. Wanaweza kutambua kwamba kula “chakula cha mboga za majani” badala ya “ng’ombe-dume aliyenoneshwa,” kunaweza kufurahisha na hata kuboresha afya yao! (Met. 15:17) Ukikazia fikira kumfurahisha Yehova, atakuandalia mahitaji yako hata utakapozeeka.

José na Rose wakiwa pamoja na Tony na Wendy

Wafikirie José na Rose, ambao wamekuwa watumishi wa wakati wote kwa zaidi ya miaka 65. Kwa miaka mingi, waliishi na baba ya Rose ambaye alihitaji kutunzwa mchana na usiku. Pia, José alihitaji kuvumilia maumivu ya matibabu ya kemikali na upasuaji alipokuwa akitibiwa kansa. Je, Yehova amenyoosha mkono wake wa kuume na kuwashika wenzi hao waaminifu? Ndiyo. Jinsi gani? Amefanya hivyo kupitia Tony na Wendy, wenzi wa ndoa katika kutaniko lao ambao wamewapa nyumba. Tony na Wendy walitaka mapainia waishi kwenye nyumba yao bila kulipia kodi. Miaka mingi mapema, Tony alipokuwa anasoma sekondari, aliwaona José na Rose kupitia dirishani wakienda kuhubiri kila siku. Aliwapenda kwa sababu ya bidii waliyokuwa nayo, na hilo lilimchochea sana. Walipotafakari jinsi wenzi hao waliozeeka walivyojitoa kwa Yehova katika maisha yao yote, Tony na Wendy waliamua kuwapa mahali pa kuishi. Kwa miaka 15 iliyopita, wamewasaidia José na Rose, ambao sasa wana umri wa miaka 85 hivi. Wenzi hao waliozeeka wanaona msaada wanaopata kutoka kwa wenzi hao vijana kuwa zawadi kutoka kwa Yehova.

Yehova anakuahidi hivi: “Usiogope. Mimi mwenyewe nitakusaidia.” Anaunyoosha ‘mkono wake wa kuume wa uadilifu’ kwako pia. Je, utamnyooshea mkono wako?

^ fu. 11 Baadhi ya majina yamebadilishwa.