Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Mtindo Wako wa Mavazi Unamtukuza Mungu?

Je, Mtindo Wako wa Mavazi Unamtukuza Mungu?

“Fanyeni mambo yote kwa utukufu wa Mungu.”—1 KOR. 10:31.

NYIMBO: 34, 61

1, 2. Kwa nini Mashahidi wa Yehova wanadumisha viwango vya juu inapohusu mavazi? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

GAZETI moja la Uholanzi lilisema hivi kuhusu jinsi viongozi wa kidini walivyovalia walipohudhuria mkutano fulani wa kidini: “Watu wengi walivalia kwa njia isiyo rasmi, hasa kwa sababu kulikuwa na joto.” Hata hivyo, gazeti hilohilo lilisema hivi kuhusu kusanyiko la Mashahidi wa Yehova: “Wavulana na wanaume wamevaa koti na tai, nao wasichana na wanawake wamevaa sketi zenye urefu . . . unaofaa lakini za kisasa.” Kwa kweli, mara nyingi Mashahidi wa Yehova wamepongezwa kwa kuvalia “mavazi yenye mpangilio mzuri, pamoja na kiasi na utimamu wa akili . . . kwa njia inayowafaa [wale] wanaodai kumheshimu Mungu.” (1 Tim. 2:9, 10) Mtume Paulo alikuwa akizungumza kuhusu wanawake, lakini viwango hivyo vinawahusu wanaume Wakristo pia.

2 Viwango vinavyofaa vya mavazi ni jambo zito kwetu tukiwa watu wa Yehova na kwa Mungu tunayemwabudu. (Mwa. 3:21) Yale ambayo Maandiko yanasema kuhusu mavazi na mapambo yanathibitisha kwamba Mwenye Enzi Kuu wa ulimwengu anataka waabudu wake wa kweli wadumishe viwango vya juu vya mavazi. Kwa hiyo, mavazi na mapambo tunayochagua hayapaswi kutegemea mapendezi yetu tu. Tunapaswa kuzingatia pia mambo yanayompendeza Bwana Mwenye Enzi Kuu, Yehova.

3. Tunaweza kujifunza nini kuhusu mavazi katika Sheria ambayo Mungu aliwapa Waisraeli?

3 Kwa mfano, Sheria ambayo Mungu aliwapa Waisraeli ilikuwa na maagizo ambayo yaliwalinda dhidi ya maisha yenye upotovu wa maadili uliofanywa waziwazi na mataifa yaliyowazunguka. Sheria hiyo ilionyesha kwamba Yehova anachukizwa na mavazi ambayo hayaonyeshi tofauti kati ya mwanamume na mwanamke. (Soma Kumbukumbu la Torati 22:5.) Maagizo ambayo Mungu alitoa kuhusu mavazi yanaonyesha wazi kwamba hapendezwi na mitindo inayowafanya wanaume waonekane kama wanawake, wanawake waonekane kama wanaume, au inayofanya iwe vigumu kutofautisha wanaume na wanawake.

4. Ni nini kinachoweza kuwasaidia Wakristo wafanye maamuzi mazuri kuhusu mavazi?

4 Neno la Mungu lina kanuni zinazowasaidia Wakristo wafanye maamuzi mazuri kuhusu jinsi wanavyopaswa kuvalia. Kanuni hizo zinafaa haidhuru mahali wanapoishi, tamaduni zao, au hali ya hewa. Hatuhitaji orodha zenye habari nyingi kuhusu mitindo ya mavazi inayofaa na isiyofaa. Badala yake, tunaongozwa na kanuni za Biblia zinazotupatia uhuru wa kuchagua kulingana na mapendezi ya kibinafsi. Acheni tuchunguze baadhi ya kanuni za Biblia zinazoweza kutusaidia kufahamu “mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu” tunapoamua jinsi tutakavyovaa.—Rom. 12:1, 2.

“TUNAJIPENDEKEZA KUWA WAHUDUMU WA MUNGU”

5, 6. Mavazi yetu yanapaswa kuwafanya watu wawe na maoni gani kutuhusu?

5 Mtume Paulo aliongozwa na roho kukazia kanuni muhimu inayopatikana katika andiko la 2 Wakorintho 6:4. (Soma.) Mwonekano wetu hueleza mengi kutuhusu. Watu wanaweza kuamua sisi ni watu wa aina gani ikitegemea “kile kinachoonekana kwa macho.” (1 Sam. 16:7) Hivyo, tukiwa wahudumu wa Mungu tunaelewa kwamba kuvaa kunahusisha mengi zaidi ya kuvalia mavazi tunayopenda. Kanuni tunazopata katika Neno la Mungu zinapaswa kutuchochea tuepuke mavazi yanayobana, yanayoonyesha sehemu za mwili, au yanayochochea hamu ya ngono. Hilo linamaanisha kwamba hatupaswi kuvaa nguo zinazoonyesha au zinazoelekezea fikira sehemu zetu za siri. Mavazi yetu hayapaswi kumfanya mtu yeyote aaibike au atazame upande mwingine anapotuangalia.

6 Tunapokuwa nadhifu, safi, wenye kiasi, na tunapojipamba kwa njia inayofaa, watu watatuheshimu kama wahudumu wa Bwana Mwenye Enzi Kuu, Yehova. Na wanaweza kuvutwa kwa Mungu tunayemwabudu. Isitoshe, tunapovalia kwa njia inayofaa tunaliletea sifa tengenezo tunalowakilisha. Kwa sababu hiyo, inaelekea wengine watasikiliza ujumbe wetu unaookoa uhai.

7, 8. Ni pindi gani hasa ambazo tunahitaji kuvalia kwa njia inayofaa?

7 Tunapaswa kuvalia kwa njia inayofaa kwa kuwa tunamwabudu Mungu mtakatifu, na tunawafikiria ndugu na dada zetu wa kiroho na vilevile watu katika eneo letu. Mavazi yetu yanapaswa kumtukuza Yehova na ujumbe tunaohubiri. (Rom. 13:8-10) Ni muhimu hata zaidi kuvalia vizuri hasa tunaposhiriki katika utendaji wa Kikristo, kama vile kuhudhuria mikutano au kuhubiri. Tunapaswa kuvalia “kwa njia inayowafaa [watu] wanaodai kumheshimu Mungu.” (1 Tim. 2:10) Ni kweli kwamba mavazi yanayofaa eneo moja huenda yasifae eneo lingine. Kwa hiyo, watu wa Yehova ulimwenguni pote huzingatia tamaduni za eneo lao ili wasiwakwaze watu.

Je, mtindo wako wa mavazi utawachochea wengine wamheshimu Mungu unayemwakilisha? (Tazama fungu la 7 na 8)

8 Soma 1 Wakorintho 10:31. Tunapohudhuria makusanyiko, mavazi yetu yanapaswa kuwa yenye kiasi na yanayofaa, wala hatupaswi kuiga mitindo inayopita kiasi ambayo ni ya kawaida ulimwenguni. Hata tunapokuwa mahali petu pa kulala au tunapofurahia pindi za kabla na baada ya kusanyiko, tunataka kuepuka kuvalia kwa njia ya kizembe au isiyo nadhifu. Hivyo, tutajivunia kujitambulisha kuwa Mashahidi wa Yehova. Naam, tutajihisi huru kutoa ushahidi wakati wowote.

9, 10. Kwa nini tunapaswa kutumia andiko la Wafilipi 2:4 inapohusu jinsi tunavyovalia?

9 Soma Wafilipi 2:4. Kwa nini Wakristo wanapaswa kufikiria jinsi mavazi yao yanavyowaathiri waabudu wenzao? Sababu moja ni kwamba watu wa Mungu wanajitahidi sana kutumia shauri hili la Biblia: “Viueni viungo vya mwili wenu vilivyo duniani kwa habari ya uasherati, uchafu, hamu ya ngono.” (Kol. 3:2, 5) Hatungependa kufanya iwe vigumu kwa waabudu wenzetu kutii shauri hilo. Ndugu na dada ambao wameacha maisha ya upotovu wa maadili kingono huenda bado wanapambana na mwelekeo wenye dhambi. (1 Kor. 6:9, 10) Bila shaka hatungependa kufanya pambano lao liwe gumu zaidi!

10 Tunapokuwa pamoja na ndugu na dada zetu, namna yetu ya kuvalia inapaswa kufanya kutaniko liwe mahali safi kiadili. Inapaswa kuwa hivyo iwe tupo mikutanoni au mahali pengine. Tuna uhuru wa kuchagua mavazi tunayotaka kuvaa. Hata hivyo, sote tuna wajibu wa kuvaa mavazi yatakayofanya iwe rahisi kwa wengine kubaki safi kiadili na kudumisha viwango vya Mungu vya utakatifu katika mawazo, maneno, na mwenendo. (1 Pet. 1:15, 16) Upendo wa kweli “haujiendeshi bila adabu, hautafuti faida zake wenyewe.”—1 Kor. 13:4, 5.

MAVAZI YANAYOFAA WAKATI NA MAHALI PANAPOFAA

11, 12. Tunapaswa kufikiria mambo gani tunapochagua mavazi?

11 Watumishi wa Mungu wanapofanya maamuzi kuhusu mavazi, wanazingatia kwamba “kuna wakati wa kila jambo na [wakati wa] kila kazi.” (Mhu. 3:1, 17) Ni kweli kwamba sisi huamua mavazi tutakayovaa ikitegemea hali ya hewa, misimu na hali mbalimbali. Hata hivyo, viwango vya Yehova havibadiliki kulingana na hali ya hewa.—Mal. 3:6.

12 Katika maeneo yenye joto, inaweza kuwa vigumu kuhakikisha kwamba mtindo wetu wa kuvalia unaheshimika, unafaa, na unaonyesha utimamu wa akili. Kwa hiyo, ndugu na dada zetu wanathamini tunapojitahidi kuvaa nguo ambazo hazibani au zilizolegea sana hivi kwamba zinaonyesha viungo vya mwili. (Ayu. 31:1) Pia, tunapostarehe ufuoni au kwenye kidimbwi cha kuogelea, nguo zetu za kuogelea zinapaswa kuonyesha kwamba tuna sifa ya kiasi. (Met. 11:2, 20) Hata ikiwa watu wengi ulimwenguni wanavaa nguo za kuogelea zinazoonyesha sehemu za mwili, sisi tunaomtumikia Yehova tunataka kumletea sifa Mungu wetu mtakatifu tunayempenda.

13. Kwa nini tunapaswa kufikiria kwa uzito shauri la 1 Wakorintho 10:32, 33 tunapochagua mavazi yetu?

13 Kuna kanuni nyingine muhimu inayotusaidia kuchagua mavazi yanayofaa. Kanuni hiyo inahusu kuhangaikia dhamiri za wengine iwe ni waabudu wenzetu au la. (Soma 1 Wakorintho 10:32, 33.) Tunapaswa kuchukua kwa uzito jukumu letu la kuepuka kuvaa nguo zinazoweza kuwaudhi wengine. Paulo aliandika hivi: “Kila mmoja wetu na ampendeze jirani yake katika yaliyo mema kwa ajili ya kujengwa kwake.” Kisha akatueleza sababu ya kufanya hivyo: “Kwa maana hata Kristo hakujipendeza mwenyewe.” (Rom. 15:2, 3) Naam, Yesu aliona kuwatanguliza wengine kuwa jambo muhimu kuliko mapendezi yake ya kibinafsi. Kufanya hivyo kulimsaidia hasa kutimiza mapenzi ya Mungu. Hivyo, tutaepuka vitu au mitindo ya mavazi tunayopenda ambayo inaweza kufanya watu tunaotaka kuwahubiria wasitusikilize.

14. Wazazi wanaweza kuwazoezaje watoto wao kumtukuza Mungu kupitia jinsi wanavyovalia?

14 Wazazi Wakristo wana jukumu la kufundisha familia zao zifuate kanuni za Biblia. Hilo linahusisha kuhakikisha kwamba wao wenyewe na watoto wao pia wanajitahidi kufanya moyo wa Mungu ushangilie kwa kuwa na kiasi katika mavazi na mapambo yao. (Met. 22:6; 27:11) Wazazi wanaweza kuwasaidia watoto wao wamheshimu Mungu mtakatifu wanayemwabudu kwa kuwawekea mfano unaofaa, na kwa kuwapa mwongozo mzuri na wenye upendo. Inapendeza sana wazazi wanapowafundisha watoto wao jinsi ya kupata nguo zinazofaa na mahali pa kuzipata! Hilo linamaanisha kuwafundisha kutonunua nguo wanazopenda tu, bali pia zitakazowawezesha kutimiza jukumu lao la kumwakilisha Yehova Mungu.

TUMIA UHURU WAKO WA KUCHAGUA KWA HEKIMA

15. Ni nini kinachopaswa kutuongoza tunapochagua mavazi yetu?

15 Neno la Mungu lina mwongozo mzuri unaoweza kutusaidia kufanya maamuzi ya hekima yatakayomtukuza Mungu. Hata hivyo, bado tuna uhuru wa kuchagua mavazi tunayopenda. Tuna mapendezi tofauti-tofauti na uwezo wetu wa kifedha unatofautiana. Ingawa hivyo, sikuzote mavazi yetu yanapaswa kuwa nadhifu, safi, yenye kiasi, yanayofaa hali, na yanayokubalika katika eneo letu.

16. Kwa nini ni vizuri tujitahidi kuvaa kwa njia inayofaa?

16 Ni kweli kwamba si rahisi kufanya uamuzi unaoonyesha utimamu wa akili na unaozingatia mambo yote. Maduka mengi yanauza nguo zinazopendwa na wengi, kwa hiyo huenda ukatumia muda na jitihada nyingi ili upate sketi, gauni, na blauzi zinazofaa au suti na suruali ambazo hazibani sana. Hata hivyo, waabudu wenzetu wataona na kuthamini jinsi tunavyojitahidi kutoka moyoni kutafuta nguo zinazovutia na zinazofaa. Na uradhi tunaopata kwa kumletea Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo utukufu unazidi changamoto zozote tunazokabili tunapotafuta nguo zinazofaa.

17. Ni mambo gani yanayoweza kumsaidia ndugu aamue ikiwa atafuga ndevu au la?

17 Vipi kuhusu suala la akina ndugu kufuga ndevu? Kulingana na Sheria ya Musa, ilikuwa lazima kwa wanaume kufuga ndevu. Hata hivyo, Wakristo hawako chini ya Sheria ya Musa, wala hawahitaji kuifuata. (Law. 19:27; 21:5; Gal. 3:24, 25) Katika tamaduni fulani, ndevu zilizonyolewa vizuri zinakubalika na haziwakengeushi watu wasisikilize ujumbe wa Ufalme. Hata baadhi ya ndugu waliowekwa rasmi wanafuga ndevu. Hata hivyo, ndugu fulani huenda wakaamua kutofuga ndevu. (1 Kor. 8:9, 13; 10:32) Katika maeneo mengine, si kawaida kwa watu kufuga ndevu na hazikubaliki kwa wahudumu Wakristo. Kwa kweli, katika maeneo kama hayo kufuga ndevu kunaweza kufanya ndugu asimletee Mungu utukufu na kunaweza kufanya alaumiwe.—Rom. 15:1-3; 1 Tim. 3:2, 7

18, 19. Andiko la Mika 6:8 linatusaidiaje tunapojitahidi kumpendeza Mungu kwa mtindo wetu wa mavazi?

18 Tunafurahi kwamba Yehova hajatupatia orodha yenye kulemea ya sheria nyingi kuhusu mavazi na mapambo. Badala yake, ameturuhusu tuwe na uhuru wa kuchagua na tufanye maamuzi yanayoonyesha utimamu wa akili na yanayoongozwa na kanuni bora za Kimaandiko. Hivyo, hata katika mavazi na mapambo yetu tunaweza kuonyesha kwamba tunataka “kuwa na kiasi katika kutembea na Mungu” wetu.—Mika 6:8.

19 Kuwa na sifa ya kiasi kunahusisha kujichunguza kwa unyenyekevu kwa kujilinganisha na utakatifu wa Yehova. Tunatambua kwamba viwango vyake ndivyo vinavyotoa mwongozo bora maishani. Pia, kuwa na kiasi kunahusisha kuheshimu hisia na maoni ya wengine. Kwa hiyo, tukiishi kulingana na viwango vyake vya juu na kuheshimu maoni ya wengine tutakuwa na “kiasi katika kutembea na Mungu.”

20. Mavazi na mapambo yetu yanapaswa kuwafanya watu wawe na maoni gani kutuhusu?

20 Mavazi yetu yanapaswa kututambulisha kuwa waabudu wa Yehova na si vinginevyo. Ndugu na dada zetu na watu kwa ujumla wanapaswa kuona kwamba tunamwakilisha inavyofaa Mungu wetu mwadilifu. Ni Mungu mwenye viwango vya juu, nasi kwa shangwe tunajitahidi kuishi kulingana na viwango hivyo. Ndugu na dada walio na mwenendo mzuri na wanaojipamba kwa njia inayofaa, wanastahili pongezi kwa kuwa wanawavuta watu wenye moyo mnyoofu kwenye ujumbe wa Biblia unaookoa uhai, na wanamletea Yehova utukufu na shangwe. Tunapofanya maamuzi ya hekima kuhusu mavazi tutaendelea kumletea sifa Yule anayejivika “utukufu na fahari.”—Zab. 104:1, 2.