Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Dumisha Hali Nzuri ya Kiroho Unapotumikia Kwenye Eneo la Kigeni

Dumisha Hali Nzuri ya Kiroho Unapotumikia Kwenye Eneo la Kigeni

“Moyoni mwangu nimeweka hazina ya maneno yako.”—ZAB. 119:11.

NYIMBO: 142, 92

1-3. (a) Tunapaswa kutanguliza nini licha ya hali zetu? (b) Watu wanaojifunza lugha mpya wanakabili changamoto gani za pekee, na hilo linatokeza maswali gani? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

MAELFU ya Mashahidi wa Yehova leo wanashiriki kwa bidii katika kutimiza unabii wa kutangaza habari njema “kwa kila taifa na kabila na lugha na watu.” (Ufu. 14:6) Je, wewe ni mmoja wa wale wanaojifunza lugha ya kigeni? Je, wewe ni mmishonari au umejitolea kwenye eneo lenye uhitaji katika nchi nyingine? Au je, umeanza kuhudhuria mikutano ya lugha ya kigeni kwenye nchi yenu?

2 Tukiwa watumishi wa Mungu, sote tunahitaji kutanguliza hali yetu ya kiroho na pia ya familia yetu. (Mt. 5:3) Hata hivyo, huenda nyakati fulani ikawa vigumu kuwa na funzo la kibinafsi lenye kina kwa sababu ya shughuli nyingi. Lakini wale wanaotumikia kwenye eneo la kigeni wanakabili changamoto nyingi zaidi.

3 Zaidi ya kujifunza lugha mpya, wale wanaotumikia kwenye eneo la kigeni wanahitaji pia kuhakikisha kwamba wanajilisha chakula kigumu cha kiroho. (1 Kor. 2:10) Wanaweza kufanya hivyo jinsi gani ikiwa hawawezi kuelewa kikamili lugha inayozungumzwa kutanikoni? Na kwa nini wazazi Wakristo wanahitaji kuhakikisha kwamba Neno la Mungu linafikia mioyo ya watoto wao?

JAMBO LINALOWEZA KUHATARISHA HALI YA KIROHO

4. Ni nini kinachoweza kuhatarisha hali yetu ya kiroho? Toa mfano.

4 Kutoelewa kikamili Neno la Mungu katika lugha ya kigeni ni jambo linaloweza kuhatarisha hali yetu ya kiroho. Katika karne ya tano K.W.K., Nehemia alisikitika alipogundua kwamba baadhi ya watoto wa Wayahudi waliotoka Babiloni hawangeweza kuzungumza Kiebrania. (Soma Nehemia 13:23, 24.) Kwa kweli, watoto hao walikuwa karibu kupoteza utambulisho wao wakiwa watumishi wa Mungu kwa sababu hawakuelewa kikamili Neno la Mungu.—Neh. 8:2, 8.

5, 6. Baadhi ya wazazi wanaotumikia kwenye eneo la lugha ya kigeni wametambua nini, na kwa nini?

5 Baadhi ya wazazi Wakristo wanaotumikia kwenye eneo la lugha ya kigeni wametambua kwamba hali ya kiroho ya watoto wao imedhoofika. Kwa kuwa watoto hao hawaelewi kikamili kile kinachosemwa mikutanoni, mioyo yao haiguswi na mambo ya kiroho yanayozungumzwa kwenye Jumba la Ufalme. Pedro [1] ambaye alihama pamoja na familia yake kutoka Amerika Kusini kwenda Australia, anasema hivi: “Tunapaswa kuhusisha moyo na hisia tunapozungumzia mambo ya kiroho.”—Luka 24:32.

6 Tunaposoma habari katika lugha ya kigeni, huenda moyo wetu usiguswe kama tunaposoma habari hiyo katika lugha yetu wenyewe. Isitoshe, kushindwa kuwasiliana vizuri katika lugha nyingine, kunaweza kutulemea kiakili na kiroho. Kwa hiyo, ingawa tunahitaji kudumisha tamaa yetu ya kumtumikia Yehova katika eneo la lugha ya kigeni, ni muhimu pia tulinde hali yetu ya kiroho.—Mt. 4:4.

WALILINDA HALI YAO YA KIROHO

7. Wababiloni walijaribu jinsi gani kumfanya Danieli afuate utamaduni na dini yao?

7 Danieli na waandamani wake walipopelekwa uhamishoni, Wababiloni walijaribu kuwafanya wafuate utamaduni wao kwa kuwafundisha “lugha ya Wakaldayo.” Isitoshe, ofisa mkuu aliyekuwa akiwazoeza aliwapa majina ya Kibabiloni. (Dan. 1:3-7) Jina alilopewa Danieli liliwakilisha jina la mungu mkuu wa Wababiloni, Beli. Inaelekea Mfalme Nebukadneza alitaka kuonyesha kwamba Yehova, Mungu wa Danieli, alikuwa ametiishwa kwa mungu wa Babiloni.—Dan. 4:8.

8. Ni nini kilichomsaidia Danieli kudumisha hali nzuri ya kiroho katika nchi ya kigeni?

8 Ingawa Danieli alipewa chakula kitamu cha mfalme, “aliazimia moyoni mwake kwamba hatajitia unajisi.” (Dan. 1:8) Kwa kuwa aliendelea kujifunza “vitabu” vitakatifu katika lugha yake, alidumisha hali nzuri ya kiroho alipokuwa kwenye nchi ya kigeni. (Dan. 9:2) Hivyo, hata baada ya kuishi Babiloni kwa miaka 70 hivi, bado alifahamika kwa jina lake la Kiebrania.—Dan. 5:13.

9. Kama inavyoelezwa katika Zaburi ya 119, Neno la Mungu lilikuwa na matokeo gani kwa mwandikaji wa zaburi hiyo?

9 Neno la Mungu lilimsaidia mwandikaji wa Zaburi ya 119 kubaki tofauti na wengine. Alilazimika kuvumilia dhihaka za washiriki fulani wa makao ya Mfalme. (Zab. 119:23, 61) Hata hivyo, aliruhusu maneno ya Mungu yapenye kabisa moyoni mwake.—Soma Zaburi 119:11, 46.

DUMISHA HALI NZURI YA KIROHO

10, 11. (a) Tunapaswa kuwa na lengo gani tunapojifunza Neno la Mungu? (b) Tunaweza kufikiaje lengo hilo? Toa mfano.

10 Ingawa huenda tukawa na shughuli nyingi za kitheokrasi na za kikazi, sote tunahitaji kutenga wakati kwa ajili ya funzo la kibinafsi na ibada ya familia. (Efe. 5:15, 16) Hata hivyo, lengo letu halipaswi kuwa tu kumaliza kusoma kurasa kadhaa au kuandaa majibu kwa ajili ya mikutano. Tungependa kuhakikisha kwamba tunaruhusu Neno la Mungu lipenye moyoni mwetu na kuimarisha imani yetu.

11 Ili tufikie lengo hilo, ni muhimu tunapojifunza tuzingatie mahitaji ya wengine, bila kusahau kutafakari kuhusu mahitaji yetu ya kiroho. (Flp. 1:9, 10) Ni lazima tutambue kwamba tunapojitayarisha kwa ajili ya huduma, mikutano, au hotuba huenda sisi wenyewe tusitumie habari zote tunazosoma. Kuhusiana na hilo, fikiria mfano huu: Ingawa mpishi anahitaji kuonja chakula anapokitayarisha, afya yake haiwezi kutegemezwa na chakula anachoonja pekee. Ikiwa anataka kuendelea kuwa mwenye afya nzuri, lazima ale chakula chenye lishe. Vivyo hivyo, tunapaswa kujitahidi kulisha moyo wetu chakula cha kiroho kinachotimiza mahitaji yetu binafsi.

12, 13. Kwa nini wahubiri wengi wanaotumikia katika eneo la lugha ya kigeni wamenufaika kujifunza kwa ukawaida katika lugha zao?

12 Wahubiri wengi wanaotumikia katika eneo la lugha ya kigeni wamenufaika kwa kujifunza Biblia kwa ukawaida katika ‘lugha walizozaliwa nazo.’ (Mdo. 2:8) Hata wamishonari wanatambua kwamba ili wabaki imara katika migawo yao, hawawezi kutegemea tu uelewaji wa msingi wa chakula cha kiroho wanachopata kwenye mikutano.

13 Alain, ambaye amekuwa akijifunza Kiajemi kwa angalau miaka minane, anakiri hivi: “Ninapotayarisha mikutano katika Kiajemi, kwa kawaida mimi huzingatia zaidi lugha yenyewe. Kwa kuwa ninakazia fikira kujifunza lugha, moyo wangu hauguswi kikamili na mawazo ya kiroho ninayosoma. Hiyo ndiyo sababu mimi hutenga wakati kujifunza Biblia na machapisho mengine katika lugha yangu.”

FIKIA MIOYO YA WATOTO WAKO

14. Wazazi wanapaswa kuhakikisha nini, na kwa nini?

14 Wazazi Wakristo wanapaswa kuhakikisha kwamba hatua kwa hatua Neno la Mungu linafikia mioyo na akili za watoto wao. Baada ya kutumikia katika eneo la lugha ya kigeni kwa zaidi ya miaka mitatu, Serge na mke wake, Muriel, walitambua kwamba mwana wao mwenye umri wa miaka 17 hakuwa akifurahia utendaji wa kiroho. Muriel anasema hivi: “Alikasirika kila mara alipoenda kuhubiri katika lugha nyingine, lakini zamani alipenda kuhubiri katika lugha yake ya Kifaransa.” Serge anaeleza hivi: “Tulipotambua kwamba hali hiyo ilikuwa ikimzuia mwana wetu kufanya maendeleo ya kiroho, tuliamua kurudi kwenye kutaniko letu la awali.”

Hakikisha kwamba kweli inagusa mioyo ya watoto wako (Tazama fungu la 14 na 15)

15. (a) Ni mambo gani yanayoweza kuwafanya wazazi warudi kwenye kutaniko linalotumia lugha ambayo watoto wao wanaelewa vizuri? (b) Andiko la Kumbukumbu la Torati 6:5-7 linawahimiza wazazi wafanye nini?

15 Ni mambo gani yanayoweza kufanya wazazi warudi kwenye kutaniko linalotumia lugha ambayo watoto wao wanaelewa vizuri? Kwanza, wanapaswa kuchunguza ikiwa wana muda na vifaa vya kutosha kuwasaidia watoto wao wampende Yehova na wakati huohuo wawafundishe lugha ya kigeni. Pili, wanaweza kugundua kwamba watoto wao wameacha kupendezwa na mambo ya kiroho au na eneo la lugha ya kigeni wanalotumikia. Katika hali kama hizo, wazazi Wakristo wanaweza kufikiria kurudi kwenye kutaniko linalotumia lugha ambayo watoto wao wanaelewa vizuri mpaka watakapochukua msimamo imara katika kweli.—Soma Kumbukumbu la Torati 6:5-7.

16, 17. Baadhi ya wazazi wamefaulu jinsi gani kuwasaidia watoto wao kiroho wanapotumikia katika eneo la kigeni?

16 Kwa upande mwingine, baadhi ya wazazi wamepata njia za kuwafundisha watoto wao katika lugha yao, na wakati huohuo wakihudhuria mikutano katika kutaniko au kikundi cha lugha ya kigeni. Charles, ambaye ana mabinti watatu wenye umri wa miaka kati ya 9 na 13, anashirikiana na kikundi cha lugha ya Lingala. Anaeleza hivi: “Tuliamua kujifunza na watoto wetu na kufanya ibada ya familia katika lugha yetu. Lakini pia, tulitenga wakati wa kufanya mazoezi na michezo katika lugha ya Lingala ili wafurahie kujifunza lugha hiyo.”

Jitahidi kujifunza lugha ya kigeni na utoe maelezo katika mikutano (Tazama fungu la 16 na 17)

17 Kevin, ambaye ana mabinti wawili wenye umri wa miaka mitano na mwingine minane, anajitahidi kuwafundisha binti zake kwa sababu hawaelewi vizuri mikutano katika lugha ya kigeni. Anaeleza hivi: “Mimi na mke wangu tunajifunza pamoja na wasichana wote wawili katika lugha yetu, Kifaransa. Pia, tuna lengo la kuhudhuria mikutano ya Kifaransa angalau mara moja kwa mwezi, na tunatumia siku zetu za likizo kuhudhuria makusanyiko katika lugha yetu.”

18. (a) Ni kanuni gani inayopatikana katika andiko la Waroma 15:1, 2 inayoweza kukusaidia kutambua kile kitakachowafaa zaidi watoto wako? (b) Wazazi wengine wametoa mapendekezo gani? (Tazama maelezo ya ziada.)

18 Bila shaka, kila familia inahitaji kuamua ni nini kinachoweza kuboresha hali ya kiroho ya watoto wao. [2] (Gal. 6:5) Muriel, aliyetajwa awali, anakiri kwamba yeye na mume wake walihitaji kudhabihu mapendezi yao ili mwana wao anufaike kiroho. (Soma Waroma 15:1, 2.) Serge anaamini kwamba walifanya uamuzi unaofaa. Anasema hivi: “Tangu tuliporudi kwenye kutaniko la Kifaransa, mwana wetu alinawiri kiroho na kubatizwa. Sasa yeye ni painia wa kawaida. Hata anafikiria kurudi kwenye kikundi cha lugha ya kigeni!”

RUHUSU NENO LA MUNGU LIGUSE MOYO WAKO

19, 20. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunalipenda Neno la Mungu?

19 Kwa upendo, Yehova ameandaa Neno lake, Biblia, katika lugha nyingi ili “watu wa namna zote wapate ujuzi sahihi wa kweli.” (1 Tim. 2:4) Anajua kwamba wanadamu wanaweza kutosheleza uhitaji wao wa kiroho wanaposoma mawazo yake katika lugha inayogusa moyo wao.

20 Tunapaswa kuazimia kujilisha chakula kigumu cha kiroho licha ya hali zetu za kibinafsi. Tukijifunza Biblia kwa ukawaida katika lugha inayogusa moyo wetu, tutadumisha hali nzuri ya kiroho na pia ya familia yetu, na tutaonyesha kwamba tumeweka hazina ya maneno ya Mungu moyoni mwetu.—Zab. 119:11.

^ [1] (fungu la 5) Majina yamebadilishwa.

^ [2] (fungu la 18) Ili upate maelezo zaidi kuhusu kanuni za Biblia zinazoweza kusaidia familia yako, soma makala yenye kichwa “Kuwalea Watoto Katika Nchi ya Kigeni—Magumu na Thawabu” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Oktoba 15, 2002.