Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, ‘Unalinda Hekima Inayotumika’?

Je, ‘Unalinda Hekima Inayotumika’?

KUNA hadithi kuhusu mvulana mdogo maskini aliyeishi katika kijiji kimoja cha mbali. Watu wa eneo hilo walimcheka wakifikiri kwamba alikuwa mpumbavu. Wageni walipotembelea kijiji hicho, baadhi ya wanakijiji walimfanyia mzaha mbele ya rafiki zao. Wangemwonyesha sarafu mbili, moja kubwa ya fedha na nyingine ndogo ya dhahabu iliyokuwa na thamani sawa na sarafu mbili za fedha. Wangemwambia hivi: “Chagua sarafu unayotaka kati ya hizi.” Mvulana huyo angechagua sarafu ya fedha na kukimbia.

Siku moja, mgeni fulani alimwuliza hivi mvulana huyo: “Hujui kwamba sarafu ya dhahabu ina thamani kubwa kuliko sarafu ya fedha?” Mvulana huyo alitabasamu na kusema, “Najua.” Kisha, mgeni huyo akamwuliza, “Kwa nini basi huwa unachukua sarafu ya fedha? Ukichukua sarafu ya dhahabu utapata pesa nyingi zaidi!” Kijana huyo akasema, “Nikichukua sarafu ya dhahabu, watu wataacha kucheza mchezo huo nami. Unajua nimekusanya sarafu ngapi za fedha kufikia sasa?” Mvulana huyo mdogo kwenye hadithi hiyo alionyesha sifa ambayo watu wazima wanahitaji kuwa nayo, yaani, hekima inayotumika.

Biblia inasema hivi: “Linda hekima inayotumika na uwezo wa kufikiri. Ndipo utakapotembea kwa usalama njiani mwako, na hata mguu wako hautagonga chochote.” (Met. 3:21, 23) Kwa hiyo, kujua maana ya “hekima inayotumika” na jinsi ya kuitumia kunahusisha usalama wetu. Hilo litatusaidia tusijikwae kiroho, na hivyo tuwe wenye usawaziko.

“HEKIMA INAYOTUMIKA” NI NINI?

Hekima inayotumika inatofautiana na ujuzi na uelewaji. Mtu mwenye ujuzi huwa na habari nyingi. Mtu mwenye uelewaji anaweza kuona jinsi habari fulani zinavyohusiana. Mtu mwenye hekima huishi kupatana na ujuzi na uelewaji alio nao.

Kwa mfano, mtu anaweza kusoma na kuelewa kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kwa muda mfupi. Huenda majibu yake wakati wa funzo la Biblia yakawa sahihi. Anaweza kuanza kuhudhuria mikutano ya kutaniko na hata kutoa maelezo mazuri. Mambo yote hayo yanaweza kuonyesha kwamba anafanya maendeleo ya kiroho, lakini je, inamaanisha kwamba tayari amepata hekima? Huenda isiwe hivyo. Inawezekana kwamba ana uwezo mzuri tu wa kuelewa mambo. Hata hivyo, anapoanza kuishi kupatana na kweli anazojifunza, akitumia ujuzi na uelewaji kwa njia inayofaa, tunaweza kusema kwamba ameanza kuwa mwenye hekima. Akifanya maamuzi mazuri na kuonyesha kwamba alifikiri kwa makini kuhusu matokeo ya maamuzi yake, inakuwa wazi zaidi kwamba ana hekima inayotumika.

Andiko la Mathayo 7:24-27 linasimulia mfano wa Yesu kuhusu watu wawili waliojenga nyumba. Mmoja wao anatajwa kuwa mwenye “busara.” Kwa kuwa mwanamume huyo alifikiria mapema kuhusu mambo yanayoweza kutokea, alijenga nyumba yake juu ya mwamba. Alifikiria matokeo ya maamuzi yake. Hakuwazia tu kwamba afadhali atumie pesa kidogo na muda mfupi kwa kujenga nyumba yake juu ya mchanga. Kwa hekima, alifikiria jinsi ambavyo maamuzi yake yangeathiri wakati wake ujao. Kwa hiyo, dhoruba ilipokuja, nyumba yake ilibaki imara. Sasa, swali ni, Tunaweza kuipataje na kuilinda sifa hiyo yenye thamani ya hekima inayotumika?

NINAWEZA KUIPATAJE?

Kwanza, ona kwamba Mika 6:9 inasema hivi: “Naye mtu mwenye hekima inayotumika ataliogopa jina [la Mungu].” Kuliogopa jina la Yehova kunamaanisha kumheshimu. Kunamaanisha kuwa na hofu inayofaa kuelekea yule anayewakilishwa na jina hilo, kutia ndani viwango vyake. Ili umheshimu mtu, unahitaji kujua njia yake ya kufikiri. Ndipo utaweza kumtumaini na kujifunza kutoka kwake, na hivyo kuiga njia yake ya kufanya maamuzi. Ikiwa tunafikiria kwa makini jinsi maamuzi yetu yanavyoweza kuathiri uhusiano wetu na Yehova, na ikiwa tunafanya maamuzi kulingana na viwango vyake, basi tumeanza kupata hekima inayotumika.

Pili, Methali 18:1 inasema hivi: “Mtu anayejitenga na wengine atatafuta mapendezi yake mwenyewe; atashindana na hekima yote inayotumika.” Tusipokuwa waangalifu, tunaweza kujitenga na Yehova na watu wake. Ili tusijitenge, tunahitaji kushirikiana na watu wanaoogopa jina la Mungu na wanaoheshimu viwango vyake. Tunahitaji kuwa katika Jumba la Ufalme na kushirikiana kwa ukawaida na kutaniko la Kikristo ikiwa hali zetu zinaruhusu. Tukiwa mikutanoni, tunahitaji kufungua akili na mioyo yetu ili turuhusu yanayosemwa yatuguse.

Kwa kuongezea, tukimmiminia Yehova mioyo yetu katika sala, tutamkaribia zaidi. (Met. 3:5, 6) Ikiwa tutafungua akili na mioyo yetu tunaposoma Biblia na machapisho yanayoandaliwa na tengenezo la Yehova, tutatambua matokeo ya muda mrefu ya matendo yetu, na hivyo kutenda kupatana na ujuzi huo. Tunahitaji pia kufungua mioyo yetu ili tupokee mashauri tunayopata kutoka kwa ndugu wakomavu. (Met. 19:20) Kwa kufanya hivyo, tutaimarisha sifa hiyo muhimu badala ya ‘kushindana na hekima yote inayotumika.’

ITASAIDIAJE FAMILIA YANGU?

Hekima inayotumika inaweza kulinda familia. Kwa mfano, Biblia inamhimiza mke ‘amheshimu sana’ mume wake. (Efe. 5:33) Mume anaweza kufanya nini ili mke wake amheshimu sana? Akimlazimisha mke wake kumheshimu, heshima atakayopata haitadumu kwa muda mrefu. Huenda mke huyo akaonyesha kiasi fulani cha heshima mume wake akiwepo ili kuepuka mabishano. Lakini je, ataendelea kumheshimu ikiwa hayupo karibu? Inaelekea kwamba hatafanya hivyo. Mume anahitaji kufikiria mambo ambayo yatamfanya mke wake aendelee kumheshimu. Akionyesha sifa za tunda la roho, kwa kumpenda na kuwa mwenye fadhili, atamchochea mke wake amheshimu sana. Ingawa hivyo, mke Mkristo anapaswa kumheshimu mume wake iwe mume huyo anamfanyia mambo yanayomchochea amheshimu au la.—Gal. 5:22, 23.

Biblia inasema pia kwamba mume anapaswa kumpenda mke wake. (Efe. 5:28, 33) Kwa kuwa mke angetaka mume wake aendelee kumpenda, huenda akafikiri kwamba ni afadhali amfiche mambo fulani mabaya kujihusu ingawa ana haki ya kuyajua. Hata hivyo, je, kufanya hivyo kunaonyesha kwamba anaongozwa na hekima inayotumika? Na je, matokeo yatakuwaje mume atakapogundua mambo aliyofichwa? Je, atampenda zaidi? Huenda isiwe rahisi kwake kuendelea kumpenda. Badala ya kumficha, mke akitafuta wakati unaofaa kumweleza mambo hayo kwa njia ya utulivu, inaelekea mume wake atathamini unyoofu huo. Na sasa atampenda zaidi.

Njia yako ya kuwatia nidhamu watoto wako itaathiri uhusiano wenu baadaye

Watoto wanapaswa kuwatii wazazi wao na kutiwa nidhamu katika njia ya Yehova. (Efe. 6:1, 4) Je, hilo linamaanisha kwamba wazazi wanapaswa kuandika orodha ndefu ya mambo ambayo watoto wanapaswa kufanya na ambayo hawapaswi kufanya? Mambo mengi zaidi yanahusika kuliko kujua tu sheria za nyumbani au adhabu za kufanya makosa. Mzazi mwenye hekima inayotumika humsaidia mtoto wake aelewe kwa nini anapaswa kutii.

Kwa mfano, vipi ikiwa mtoto anazungumza na mzazi wake bila heshima? Kuzungumza kwa ukali au kumwadhibu kwa sababu ya hasira kunaweza kumwaibisha mtoto na kumnyamazisha. Lakini kufanya hivyo kunaweza kumfanya afunge kinyongo, jambo linaloweza kusababisha ajitenge na wazazi wake.

Wazazi wanaositawisha hekima inayotumika watafikiria kuhusu njia wanayotumia kuwatia nidhamu watoto wao na jinsi itakavyowaathiri wakati ujao. Wazazi hawapaswi kuchukua hatua haraka wanapokasirishwa na watoto wao. Ingekuwa bora wazungumze na mtoto kwa utulivu na upendo wakiwa faraghani, na kumweleza kwamba Yehova anatarajia awaheshimu wazazi wake ili apate manufaa ya muda mrefu. Hivyo, mtoto anapowatii wazazi wake, atatambua kwamba anamheshimu Yehova. (Efe. 6:2, 3) Kuzungumza naye kwa njia hiyo yenye fadhili kunaweza kufikia moyo wa mtoto. Atatambua kwamba wazazi wake wanamjali kikweli, na atawaheshimu zaidi. Kufanya hivyo kutafanya iwe rahisi kwa mtoto kuomba msaada wa wazazi wake atakapopata matatizo makubwa zaidi wakati ujao.

Baadhi ya wazazi huepuka kuwarekebisha watoto wao kwa sababu wanaogopa huenda wakawaumiza hisia. Lakini hali itakuwaje mtoto huyo atakapokuwa mkubwa? Je, atamwogopa Yehova na kutambua hekima ya kukubali viwango vyake? Je, atakuwa tayari kufungua moyo na akili yake ili aongozwe na Yehova, au atajitenga kiroho?—Met. 13:1; 29:21.

Mchongaji sanamu mzuri hufikiria mapema kuhusu kile anachotaka kuchonga. Hachongi ovyoovyo tu akitazamia kutokeza sanamu nzuri. Wazazi wenye hekima inayotumika hutumia muda mwingi kujifunza na kutumia viwango vya Yehova, na wanapofanya hivyo wanaonyesha kwamba wanahofu jina lake. Kwa kutojitenga na Yehova na tengenezo lake, wanapata hekima inayotumika na kuitumia kujenga familia zao.

Kila siku tunahitaji kufanya maamuzi ambayo huenda yakaathiri maisha yetu kwa miaka mingi. Badala ya kufanya maamuzi haraka-haraka kwa kuongozwa na hisia, kwa nini usitue na kufikiri? Fikiria kwa makini matokeo ya muda mrefu ya maamuzi yako. Tafuta mwongozo wa Yehova na utumie hekima yake. Ukifanya hivyo, utakuwa umelinda hekima inayotumika, nayo itakupatia uzima.—Met. 3:21, 22.