Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Onyesha Imani Yako Katika Ahadi za Yehova

Onyesha Imani Yako Katika Ahadi za Yehova

“Imani ni . . . uthibitisho ulio wazi wa mambo halisi ingawa hayaonekani.”—EBR. 11:1.

NYIMBO: 54, 125

1. Tunapaswa kuionaje imani ya Kikristo?

IMANI ya Kikristo ni sifa yenye thamani. Si wanadamu wote walio nayo. (2 The. 3:2) Hata hivyo, Yehova amemgawia kila mwabudu wake “kipimo cha imani.” (Rom. 12:3; Gal. 5:22) Wale wote walio nayo wanapaswa kumshukuru sana Yehova.

2, 3. (a) Mtu aliye na imani anaweza kupata baraka gani? (b) Tutachunguza maswali gani?

2 Yesu Kristo alisema kwamba Baba yake wa mbinguni huwavuta watu kwake kupitia Mwana Wake. (Yoh. 6:44, 65) Kwa hiyo, kwa kumwamini Yesu mtu anaweza kupata msamaha wa dhambi. Hilo humpa tumaini la kufurahia uhusiano wa milele pamoja na Yehova. (Rom. 6:23) Je, tunastahili baraka hiyo nzuri ajabu? Kwa kuwa sisi ni wenye dhambi, tunastahili tu kufa. (Zab. 103:10) Lakini Yehova aliona jambo zuri ndani yetu. Kwa sababu ya fadhili zake zisizostahiliwa, alifungua mioyo yetu ili tupokee habari njema. Hivyo, tukaanza kuonyesha imani katika Yesu tukiwa na tumaini la kupata uzima wa milele.—Soma 1 Yohana 4:9, 10.

3 Lakini imani ni nini hasa? Je, ni kuelewa tu kusudi la Mungu la wakati ujao kutuelekea? Na swali muhimu hata zaidi ni; tunapaswa kufanya mambo gani ili tuonyeshe kwamba tuna imani?

‘ONYESHA IMANI MOYONI MWAKO’

4. Eleza kwa nini kuwa na imani kunahusisha mengi zaidi ya kuelewa kusudi la Mungu.

4 Imani inahusisha mengi zaidi ya kuelewa kusudi la Mungu. Mtu aliye na imani huchochewa sana kutoka moyoni kutenda kulingana na mapenzi ya Mungu. Imani katika njia ya Mungu ya kuwakomboa wanadamu humchochea mtu aliye na imani awaambie wengine habari hizo njema. Mtume Paulo alieleza hivi: “Kwa maana ukitangaza waziwazi lile ‘neno lililo katika kinywa chako mwenyewe,’ kwamba Yesu ni Bwana, na kuonyesha imani moyoni mwako kwamba Mungu alimfufua kutoka kwa wafu, utaokolewa. Kwa maana kwa moyo mtu huonyesha imani kwa ajili ya uadilifu, lakini kwa kinywa mtu hufanya tangazo la hadharani kwa ajili ya wokovu.”—Rom. 10:9, 10; 2 Kor. 4:13.

5. Kwa nini kuwa na imani ni jambo muhimu sana, na tunaweza kuidumishaje ikiwa imara? Toa mfano.

5 Ni wazi kwamba tumaini letu la kupata uzima wa milele katika ulimwengu mpya wa Mungu linategemea kuwa na imani na kuendelea kuidumisha ikiwa imara. Uhitaji wa kuendelea kudumisha imani yetu ikiwa imara unaweza kulinganishwa na jinsi ambavyo mmea unahitaji maji. Mmea huendelea kubadilika kadiri unavyokua. Unaweza kufa kwa sababu ya kukosa maji au kuendelea kusitawi ikiwa utapata maji kwa ukawaida. Mmea ambao wakati fulani ulikuwa umesitawi, unaweza kufa ikiwa utakosa maji ya kutosha. Ndivyo ilivyo na imani yetu pia. Tusipoitunza, itanyauka na kufa. (Luka 22:32; Ebr. 3:12) Lakini tukiitunza vizuri, imani yetu itaendelea kuwa hai na ‘kukua,’ nasi tutakuwa “wenye afya katika imani.”—2 The. 1:3; Tito 2:2.

JINSI BIBLIA INAVYOFAFANUA IMANI

6. Andiko la Waebrania 11:1 linafafanua imani katika njia gani mbili?

6 Biblia inaeleza maana ya neno imani katika andiko la Waebrania 11:1. (Soma.) Imani inahusisha mambo mawili ambayo hatuwezi kuyaona: (1) “Mambo yanayotumainiwa.” Mambo hayo yanatia ndani matukio ya wakati ujao ambayo yameahidiwa lakini bado hayajatukia, kama vile mwisho wa uovu, na kuja kwa ulimwengu mpya. (2) “Mambo halisi ingawa hayaonekani.” Katika muktadha huo, neno la Kigiriki linalotafsiriwa “uthibitisho ulio wazi” linarejelea usadikisho hakika wa mambo yasiyoonekana, kama vile kuwepo kwa Yehova Mungu, Yesu Kristo, malaika, na utendaji wa Ufalme wa Mungu. (Ebr. 11:3) Tunaweza kuthibitishaje kwamba tumaini letu ni hakika na kwamba tunaamini mambo yasiyoonekana yanayotajwa katika Neno la Mungu? Ni kupitia maneno na matendo yetu, mambo yanayokamilisha imani yetu.

7. Mfano wa Noa unatusaidiaje kuelewa kile kinachomaanishwa na kuwa na imani? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

7 Andiko la Waebrania 11:7 linazungumzia imani ya Noa ambaye, “baada ya kupewa onyo la kimungu la mambo ambayo yalikuwa bado hayajaonekana, alionyesha woga wa kimungu na kujenga safina kwa ajili ya kuiokoa nyumba yake.” Noa alionyesha imani yake kwa kujenga safina. Bila shaka, jirani zake walimwuliza kwa nini alikuwa akijenga jengo kubwa hivyo. Je, Noa alinyamaza tu au kuwaambia kwamba mambo hayo hayawahusu? La, hasha! Imani yake ilimchochea kuwahubiria kwa ujasiri na kuwaonya kuhusu hukumu ya Mungu iliyokuwa ikikaribia. Inaelekea kwamba Noa alirudia maneno yaleyale ambayo Yehova alikuwa amemwambia: “Mwisho wa wote wenye mwili umekuja mbele zangu, kwa maana dunia imejaa jeuri kwa sababu yao . . . mimi ninaleta gharika ya maji duniani ili kuharibu kutoka chini ya mbingu wote wenye mwili walio na nguvu za uhai ndani yao. Kila kitu kilicho duniani kitakata pumzi.” Hakuna shaka pia kwamba Noa aliwaeleza watu jambo pekee la kufanya ili waokoke gharika. Alirudia amri hii ya Mungu: “Nawe uingie ndani ya safina.” Na kwa njia hiyo, Noa alionyesha kwamba ana imani kwa kuwa “mhubiri wa uadilifu.”—Mwa. 6:13, 17, 18; 2 Pet. 2:5.

8. Mwanafunzi Yakobo aliongozwa na roho ya Mungu kueleza nini kuhusu maana ya imani ya kweli ya Kikristo?

8 Inaelekea barua ya Yakobo iliandikwa muda mfupi baada ya mtume Paulo kuongozwa na roho kuandika maana ya imani. Kama Paulo, Yakobo alieleza kwamba imani ya kweli ya Kikristo haihusishi kuamini tu, bali inahusisha pia matendo. Yakobo aliandika hivi: “Nionyeshe imani yako bila matendo, nami nitakuonyesha imani yangu kwa matendo yangu.” (Yak. 2:18) Kisha, Yakobo anaonyesha tofauti iliyo wazi kati ya mtu anayeamini tu na mtu anayeonyesha imani. Roho waovu wanaamini kwamba kuna Mungu lakini hawana imani ya kweli. Badala yake, wanapinga kutimizwa kwa kusudi la Mungu kupitia matendo yao yanayoonyesha kwamba hawana imani. (Yak. 2:19, 20) Tofauti na hilo, akizungumzia mwanamume mwingine mwenye imani aliyeishi zamani, Yakobo anauliza hivi: “Je, Abrahamu baba yetu hakutangazwa kuwa mwadilifu kwa matendo baada ya kumtoa Isaka mwana wake juu ya madhabahu? Mnaona kwamba imani yake ilitenda pamoja na matendo yake na kwa matendo yake imani yake ilikamilishwa.” Kisha, ili kukazia kwamba imani inapaswa kuonyeshwa kwa matendo, Yakobo anaongeza hivi: “Kama vile ambavyo mwili bila roho umekufa, vivyo hivyo pia imani bila matendo imekufa.”—Yak. 2:21-23, 26.

9, 10. Mtume Yohana anatusaidiaje kuelewa umuhimu wa kuonyesha imani?

9 Zaidi ya miaka 30 baadaye, mtume Yohana aliandika Injili pamoja na barua tatu. Je, alitambua kile ambacho imani ya kweli ya Kikristo ilimaanisha hasa kama ilivyoelezwa na waandikaji wengine wa Biblia walioongozwa na roho? Yohana alitumia kitenzi cha Kigiriki kinachotafsiriwa “kuonyesha imani,” mara nyingi zaidi kuliko waandikaji wengine wote wa Biblia.

10 Kwa mfano, Yohana alieleza hivi: “Yule anayemwamini Mwana ana uzima wa milele; yule asiyemtii Mwana hataona uzima, bali ghadhabu ya Mungu hukaa juu yake.” (Yoh. 3:36) Imani ya Kikristo inahusisha kutii amri za Yesu. Yohana alinukuu mara nyingi maneno ya Yesu yanayoonyesha kwamba tunapaswa kuendelea kuonyesha imani sikuzote.—Yoh. 3:16; 6:29, 40; 11:25, 26; 14:1, 12.

11. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunathamini kuijua kweli?

11 Tunafurahi sana kwamba Yehova alitumia roho yake takatifu kutufunulia kweli na kutusaidia kuonyesha imani katika habari njema! (Soma Luka 10:21.) Hatupaswi kamwe kuacha kumshukuru Yehova kwa kutuvuta kwake kupitia Mwana wake ambaye ni “Wakili Mkuu na Mkamilishaji wa imani yetu.” (Ebr. 12:2) Ili tuonyeshe kwamba tunathamini fadhili hizo zisizostahiliwa, tunapaswa kuendelea kuimarisha imani yetu kupitia sala na kujifunza Neno la Mungu.—Efe. 6:18; 1 Pet. 2:2.

Onyesha imani yako kwa kuhubiri habari njema kila unapopata fursa (Tazama fungu la 12)

12. Tunapaswa kuonyesha imani kwa kufanya mambo gani?

12 Tunapaswa kuendelea kuonyesha kwamba tuna imani katika ahadi za Yehova. Mambo tunayofanya kuonyesha imani yetu yanapaswa kuonwa waziwazi na watu wengine. Kwa mfano, tunaendelea kuhubiri kuhusu Ufalme wa Mungu na kushiriki katika kazi ya kufanya wanafunzi. Pia, tunaendelea kuwatendea “wote mema, na hasa wale ambao katika imani ni jamaa zetu.” (Gal. 6:10) Na tunajitahidi sana “[kuuvua] utu wa zamani pamoja na mazoea yake,” na kujilinda kutokana na kitu chochote kinachoweza kutudhoofisha kiroho.—Kol. 3:5, 8-10.

IMANI KWA MUNGU NI SEHEMU YA MSINGI WETU WA KIKRISTO

13. “Imani kwa Mungu” ni muhimu kadiri gani? Inafananishwa na nini, na kwa nini?

13 Biblia inasema hivi: “Bila imani haiwezekani kamwe kumpendeza vema, kwa maana yule anayemkaribia Mungu lazima aamini kwamba yeye yuko na kwamba yeye huwa mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.” (Ebr. 11:6) Neno la Mungu linaeleza kwamba “imani kwa Mungu” ni sehemu ya “msingi” unaohitajiwa ili mtu awe Mkristo wa kweli na aendelee kuwa hivyo. (Ebr. 6:1) Na katika msingi huo, Wakristo wanapaswa ‘kuongeza kwenye imani yao’ sifa nyingine muhimu ili waendelee “[kujitunza] katika upendo wa Mungu.”—Soma 2 Petro 1:5-7; Yuda 20, 21.

14, 15. Ni sifa gani iliyo muhimu zaidi kati ya imani na upendo?

14 Waandikaji wa Maandiko ya Kigiriki walikazia umuhimu wa imani kwa kuizungumzia mara nyingi sana. Hakuna sifa nyingine ya Kikristo ambayo imetajwa mara nyingi hivyo. Je, hilo linamaanisha kwamba imani ndiyo sifa muhimu zaidi ya Kikristo?

15 Akilinganisha sifa ya imani na sifa ya upendo, Paulo aliandika hivi: “Ikiwa nina imani yote kuweza kuhamisha milima, lakini sina upendo, mimi si kitu.” (1 Kor. 13:2) Yesu alikazia sifa iliyo muhimu zaidi tunayopaswa kuwa nayo, yaani, kumpenda Mungu, alipojibu swali hili: “Amri iliyo kuu katika ile Sheria ni gani?” (Mt. 22:35-40) Upendo ni msingi wa sifa nyingi muhimu za Kikristo, kutia ndani imani. Biblia inasema kwamba “upendo . . . huamini mambo yote.” Mtu akiwa na upendo ataamini mambo ambayo Mungu amesema katika Neno lake la kweli.—1 Kor. 13:4, 7.

16, 17. Katika Maandiko, sifa ya imani na upendo zimekaziwaje zikiwa pamoja? Ni sifa gani iliyo muhimu zaidi, na kwa nini?

16 Kwa kuwa imani na upendo ni sifa muhimu, waandikaji wa Maandiko ya Kigiriki walikazia sifa hizo mara nyingi zikiwa pamoja, mara kwa mara wakizitaja katika sentensi ileile. Paulo aliwahimiza Wakristo wenzake “[wavae] bamba la kifuani la imani na upendo.” (1 The. 5:8) Petro aliandika hivi: “Ninyi mnampenda [Yesu], ingawa hamkumwona yeye kamwe. Ingawa hammwoni wakati wa sasa, bado mnaonyesha imani katika yeye.” (1 Pet. 1:8) Yakobo aliwauliza hivi ndugu zake watiwa mafuta: “Mungu alichagua walio maskini kwa habari ya ulimwengu ili wawe matajiri katika imani na warithi wa ufalme, aliowaahidi wale wanaompenda, sivyo?” (Yak. 2:5) Yohana aliandika: “Hii ndiyo amri [ya Mungu], kwamba tuwe na imani katika jina la Mwana wake Yesu Kristo na tuwe tukipendana.”—1 Yoh. 3:23.

17 Ingawa imani ni muhimu, mambo fulani tunayoamini yatapitilia mbali tutakapoona ahadi za Mungu zikitimizwa na tumaini letu la Kikristo litakapotimia. Lakini uhitaji wa kuendelea kukuza upendo wetu kwa Mungu na kwa jirani utaendelea mpaka milele. Hiyo ndiyo sababu Paulo aliandika hivi: “Sasa, hata hivyo, inabaki imani, tumaini, upendo, hayo matatu; lakini lililo kubwa zaidi kati ya hayo ni upendo.”—1 Kor. 13:13.

WONYESHO MKUBWA SANA WA IMANI

18, 19. Tunaona wonyesho gani mkubwa wa imani leo, na ni nani anayestahili kusifiwa kuhusiana na jambo hilo?

18 Katika siku zetu, watu wa Yehova wamekuwa wakionyesha imani yao katika Ufalme wa Mungu unaotawala. Hilo limetokeza ukuzi wa paradiso ya kiroho ya ulimwenguni pote yenye raia zaidi ya milioni nane. Ni mahali ambapo roho ya Mungu ipo kwa wingi. (Gal. 5:22, 23) Huo ni wonyesho mkubwa sana wa imani ya kweli ya Kikristo na upendo!

19 Umoja huo hautokani na jitihada za wanadamu. Mungu ndiye ametuwezesha tuwe na umoja huo. Kazi hii nzuri inaleta “sifa kwa Yehova, ishara mpaka wakati usio na kipimo ambayo haitakatiliwa mbali.” (Isa. 55:13) Kwa kweli, “[kuokolewa] kupitia imani” ni “zawadi ya Mungu.” (Efe. 2:8) Paradiso yetu ya kiroho itaendelea kukua na kusitawi mpaka dunia yote ijawe na wanadamu wakamilifu, waadilifu, na wenye furaha kwa utukufu wa jina la Yehova milele. Na tuendelee kuonyesha imani yetu katika ahadi za Yehova!