Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Kazi Ni Kubwa”

“Kazi Ni Kubwa”

ULIKUWA wakati wa mkutano muhimu sana katika jiji la Yerusalemu. Mfalme Daudi alikuwa amewaita wakuu, maofisa wa makao ya mfalme, na wanaume wenye nguvu. Nao walifurahi sana kusikia tangazo la pekee. Yehova alikuwa amemwagiza Sulemani mwana wa Daudi ajenge jumba kubwa kwa ajili ya ibada ya Mungu wa kweli. Daudi, mfalme wa Israeli ambaye tayari alikuwa amezeeka, alipokea ramani ya ujenzi kupitia maono, na akampa Sulemani michoro hiyo. Daudi alisema hivi: “Kazi ni kubwa; kwa kuwa jumba hilo la kifalme si la mwanadamu, bali ni la Yehova Mungu.”—1 Nya. 28:1, 2, 6, 11, 12; 29:1.

Kisha Daudi akauliza hivi: “Ni nani anayejitolea kuujaza mkono wake leo kwa zawadi kwa ajili ya Yehova?” (1 Nya. 29:5) Ikiwa ungekuwepo wakati huo, ungetendaje baada ya kusikia maneno hayo? Je, ungechochewa kutoa mchango kwa ajili ya kazi hiyo kubwa? Waisraeli walichukua hatua mara moja. Kwa kweli, “[walishangilia] kutokana na matoleo yao ya hiari waliyotoa, kwa maana walimtolea Yehova matoleo ya hiari kwa moyo kamili.”—1 Nya. 29:9.

Karne nyingi baadaye, Yehova alianzisha mpango mkubwa zaidi wa ibada kuliko ule uliokuwa katika hekalu. Alianzisha hekalu kubwa la kiroho, yaani, mpango ambao ungewawezesha wanadamu kumwabudu Mungu kwa msingi wa dhabihu ya Yesu. (Ebr. 9:11, 12) Yehova anawasaidiaje watu wapatanishwe naye leo? Ni kupitia kazi yetu ya kuhubiri na kuwafundisha watu Biblia. (Mt. 28:19, 20) Kwa sababu ya kazi hiyo, kila mwaka wahubiri huongoza mamilioni ya mafunzo ya Biblia, maelfu ya wanafunzi hubatizwa, na mamia ya makutaniko huanzishwa.

Ukuzi huo umetokeza uhitaji mkubwa zaidi wa machapisho ya Biblia, kujenga na kudumisha Majumba ya Ufalme, na kununua viwanja kwa ajili ya majumba ya makusanyiko. Je, si kweli kwamba kazi yetu ya kutangaza habari njema ni kubwa na yenye kuridhisha sana?—Mt. 24:14.

Kumpenda Mungu na jirani na kuwa na hisi ya uharaka kuelekea kazi ya kuhubiri Ufalme huwachochea watu wa Mungu ‘wajitolee kuujaza mkono wao zawadi kwa ajili ya Yehova’ kwa kutoa michango ya hiari. Tunafurahi sana ‘kumheshimu Yehova kwa vitu vyetu vyenye thamani,’ na kuona jinsi mali zetu zinavyotumiwa kwa uaminifu na kwa busara kutimiza kazi kubwa zaidi katika historia ya wanadamu!—Met. 3:9.