Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Waliwekwa Huru Kutoka Katika Dini za Uwongo

Waliwekwa Huru Kutoka Katika Dini za Uwongo

“Tokeni kwake, watu wangu.”—UFU. 18:4.

NYIMBO: 101, 93

1. Tunajuaje kwamba watu wa Mungu wangeweza kuwekwa huru kutoka kwenye utekwa wa Babiloni Mkubwa, na tutachunguza maswali gani?

KATIKA makala iliyotangulia, tulijifunza jinsi ambavyo Wakristo waaminifu walikuwa katika aina fulani ya utekwa wa Babiloni. Hata hivyo, jambo la kupendeza ni kwamba hawangebaki katika hali hiyo milele. Mungu alikuwa ametoa amri hii: “Tokeni kwake, watu wangu.” Amri hiyo ingekosa maana ikiwa hakuna mtu ambaye angeweza kutoka kwenye utumwa wa milki ya ulimwenguni pote ya dini ya uwongo. (Soma Ufunuo 18:4.) Bila shaka, tuna hamu ya kujua watu wa Mungu waliwekwa huru lini kutokana na utumwa wa Babiloni. Lakini kwanza tunapaswa kujibu maswali yafuatayo: Wanafunzi wa Biblia walichukua msimamo gani kuhusu Babiloni Mkubwa kabla ya mwaka 1914? Ndugu zetu walihubiri kwa bidii kadiri gani wakati wa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu? Je, kuna uhusiano wowote kati ya uhitaji wao wa kurekebishwa na kutiwa nidhamu katika kipindi hicho cha vita na utekwa wao katika Babiloni?

KUANGUKA KWA BABILONI

2. Kulingana na ujuzi waliokuwa wamepata, Wanafunzi wa Biblia wa mapema walichukua msimamo gani kuelekea dini za uwongo?

2 Katika miaka iliyotangulia Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, Charles Taze Russell na waandamani wake walitambua kwamba dini zinazodai kuwa za Kikristo hazikuwa zikifundisha kweli ya Biblia. Kwa hiyo, kulingana na ujuzi waliokuwa wamepata, waliazimia kwamba hawatashirikiana na dini hizo. Kwa mfano, Novemba mwaka 1879, gazeti la Zion’s Watch Tower lilisema hivi waziwazi kuhusu msimamo wao wa Kimaandiko: “Kila kanisa linalodai kuwa bikira safi aliyeposwa kwa Kristo, lakini kwa kweli limeungana na kutegemezwa na (hayawani) wa ulimwengu lazima sisi tulishutumu kwa lugha ya maandiko kuwa ni kanisa kahaba.” Walikuwa wakirejelea Babiloni Mkubwa.—Soma Ufunuo 17:1, 2.

3. Wanafunzi wa Biblia walichukua msimamo gani thabiti ulioonyesha kwamba walielewa kilichomaanishwa na kujitenga na dini za uwongo? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

3 Wanaume na wanawake waliomwogopa Mungu walijua mambo waliyopaswa kufanya. Hawangetazamia kupokea baraka za Mungu ikiwa wangeendelea kuunga mkono dini za uwongo. Hivyo basi, Wanafunzi wengi wa Biblia waliandika barua za kujiondoa katika makanisa waliyokuwa wakishirikiana nayo. Katika visa fulani, walisoma barua hizo mbele ya kanisa zima. Mahali ambapo hilo halikuruhusiwa, baadhi ya Wanafunzi wa Biblia walituma barua kwa kila mshiriki wa kanisa. Hawakutaka kujihusisha hata kidogo na dini za uwongo! Katika miaka iliyotangulia, ingekuwa hatari sana kufanya hivyo, hata wangeweza kuuawa. Lakini kufikia mwaka 1870, serikali za nchi nyingi zilikuwa zimeacha kuunga mkono makanisa. Kwa kuwa hawakuogopa kuadhibiwa, raia wa nchi hizo walikuwa huru kuzungumzia mambo ya kidini na kupinga mafundisho ya makanisa waziwazi.

4. Wakati wa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, kulikuwa na uhusiano gani kati ya watu wa Mungu na Babiloni Mkubwa?

4 Wanafunzi wa Biblia walielewa kwamba haikutosha tu kuwajulisha watu wa familia, marafiki, na washiriki wa kanisa lao kuhusu msimamo wao wa kujitenga na dini za uwongo. Ulimwengu wote ulihitaji kujua ukweli kuhusu Babiloni Mkubwa, kwamba ni kahaba wa kidini! Ili kufanya hivyo, kuanzia Desemba 1917 hadi mwanzoni mwa mwaka 1918, idadi ndogo ya Wanafunzi wa Biblia walisambaza nakala 10,000,000 za trakti iliyozungumzia kuanguka kwa Babiloni (The Fall of Babylon), iliyoshutumu vikali dini zinazodai kuwa za Kikristo. Kama unavyoweza kuwazia, makasisi walikasirika sana; lakini bila woga Wanafunzi wa Biblia waliendelea kufanya kazi hiyo muhimu kwa bidii. Walikuwa wameazimia kumtii “Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.” (Mdo. 5:29) Tunaweza kufikia mkataa gani? Kwamba, badala ya kuendelea kuwa watumwa wa Babiloni Mkubwa katika kipindi hicho cha vita, wanaume na wanawake hao Wakristo walikuwa wakijiondoa kwenye uvutano wa Babiloni na kuwasaidia wengine wafanye hivyo.

WALIFANYA KAZI KWA BIDII WAKATI WA VITA VYA KWANZA VYA ULIMWENGU

5. Kuna ushahidi gani kwamba ndugu zetu walihubiri kwa bidii wakati wa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu?

5 Kwa miaka mingi, tuliamini kwamba watu wa Yehova walikosa kibali chake kwa sababu hawakuhubiri kwa bidii wakati wa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu. Kwa sababu hiyo tuliamini kwamba Yehova aliwaruhusu wachukuliwe mateka na Babiloni Mkubwa kwa kipindi kifupi cha wakati. Hata hivyo, ndugu na dada waaminifu waliomtumikia Mungu katika kipindi cha mwaka 1914 hadi 1918, walionyesha wazi kwamba watu wa Bwana wakiwa kikundi walifanya yote waliyoweza ili kuendelea kuhubiri. Kuna ushahidi wa kutosha unaothibitisha maelezo yao. Uelewaji sahihi zaidi wa historia ya tengenezo letu umetusaidia kuelewa vizuri baadhi ya matukio yaliyorekodiwa katika Biblia.

6, 7. (a) Wanafunzi wa Biblia walihitaji kushinda changamoto gani wakati wa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu? (b) Toa mifano inayoonyesha kwamba Wanafunzi wa Biblia walikuwa na bidii.

6 Ukweli wa mambo ni kwamba Wanafunzi wa Biblia waliokuwepo wakati wa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu (1914-1918), walitoa ushahidi mkubwa katika kipindi hicho. Hata hivyo, kuna sababu kadhaa zilizofanya isiwe rahisi kwao kufanya hivyo. Tutachunguza sababu mbili. Kwanza kabisa, katika siku hizo kazi kubwa iliyofanywa ilihusisha kusambaza machapisho yaliyotegemea Biblia. Kitabu The Finished Mystery kilipopigwa marufuku na mamlaka za serikali mwaka 1918, ilikuwa vigumu kwa ndugu wengi kuhubiri. Hawakuwa wamejifunza kuhubiri kwa kutumia Biblia pekee, na walikuwa wakitegemea kitabu The Finished Mystery “kizungumze” kwa niaba yao. Sababu ya pili ni Homa ya Kihispania iliyotokea mwaka 1918 na kusababisha madhara makubwa. Kuenea kwa homa hiyo hatari kuliwazuia Wanafunzi wa Biblia kuhubiri katika maeneo mbalimbali. Hata hivyo, licha ya sababu hizo na changamoto nyingine, Wanafunzi wa Biblia wakiwa kikundi walifanya yote waliyoweza ili kuendelea kuhubiri.

Wanafunzi wa Biblia walikuwa na bidii sana! (Tazama fungu la 6 na la 7)

7 Katika mwaka 1914 pekee, idadi ndogo ya Wanafunzi wa Biblia walionyesha sinema ya “Photo-Drama of Creation” kwa watu zaidi ya 9,000,000. Sinema hiyo iliunganisha picha na slaidi zenye sauti na ilionyesha historia ya mwanadamu tangu alipoumbwa hadi mwisho wa utawala wa miaka 1,000 wa Kristo. Hilo lilikuwa jambo la pekee sana! Idadi ya watu walioona sinema hiyo katika mwaka 1914 pekee, ni kubwa zaidi ya idadi ya wahubiri wote wa Ufalme ulimwenguni pote leo! Ripoti zinaonyesha pia kwamba katika mwaka 1916, jumla ya watu 809,393 walihudhuria mikutano ya watu wote nchini Marekani, na katika mwaka 1918, idadi hiyo iliongezeka hadi kufikia 949,444. Ni wazi kwamba Wanafunzi hao wa Biblia walikuwa na bidii sana!

8. Mahitaji ya kiroho ya akina ndugu yalitimizwa jinsi gani wakati wa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu?

8 Wakati wa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, jitihada nyingi zilifanywa ili kuandaa chakula cha kiroho na kuwatia moyo Wanafunzi wa Biblia waliokuwa wakiishi katika maeneo mbalimbali. Maandalizi hayo yaliwasaidia ndugu na dada waendelee kuhubiri kwa bidii. Richard H. Barber, ambaye alikuwa mhubiri mwenye bidii wakati huo, anakumbuka hivi: “Tulihakikisha kwamba waangalizi wachache wanaosafiri wanaendelea kufanya kazi na kwamba gazeti la Mnara wa Mlinzi linaendelea kuchapishwa na kutumwa nchini Kanada ambako lilikuwa limepigwa marufuku. Nilikuwa na pendeleo la kutuma chapa ndogo za nakala ya kitabu The Finished Mystery, kwa ndugu ambao nakala zao zilikuwa zimechukuliwa na wenye mamlaka. Ndugu Rutherford aliomba tupange makusanyiko katika majiji kadhaa yaliyo magharibi mwa Marekani na tuombe wasemaji wafanye yote wawezayo kuwatia moyo akina ndugu.”

WALIHITAJI KUSAFISHWA

9. (a) Ni nini kinaonyesha kwamba watu wa Mungu walihitaji kurekebishwa na kutiwa nidhamu katika miaka ya 1914 hadi 1919? (b) Ingawa watu wa Mungu walihitaji kutiwa nidhamu, hilo halimaanishi nini?

9 Wanafunzi wa Biblia walioishi katika miaka ya 1914 hadi 1919, walifanya mambo fulani ambayo hayakupatana na kanuni za Kimaandiko. Ingawa walikuwa wanyoofu, ndugu hao hawakuelewa kikamili maana ya kujitiisha kwa mamlaka za serikali. (Rom. 13:1) Kwa hiyo, wakiwa kikundi, hawakujitenga kikamili na mambo ya kivita. Kwa mfano, rais wa Marekani alipoagiza kwamba Mei 30, mwaka 1918, itengwe kuwa siku ya kuombea amani, gazeti la Mnara wa Mlinzi liliwahimiza Wanafunzi wa Biblia wajiunge katika maombi hayo. Baadhi ya akina ndugu waliweka dhamana ya pesa ili kutegemeza shughuli za kivita, na wengine walienda vitani wakiwa na silaha za vita. Hata hivyo, isingekuwa sahihi kukata shauri kwamba Wanafunzi wa Biblia walipelekwa kwenye utekwa wa Babiloni Mkubwa kwa sababu walihitaji kurekebishwa na kutiwa nidhamu. Kinyume cha hilo, walielewa wajibu wao wa kujitenga na dini za uwongo, na wakati wa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, utumwa wao ulikuwa karibu kufikia mwisho.—Soma Luka 12:47, 48.

10. Wanafunzi wa Biblia walionyeshaje kwamba wanaheshimu uhai?

10 Ingawa hawakuelewa kikamili maana ya kutojihusisha na mambo ya kisiasa kama tunavyoelewa leo, Wanafunzi wa Biblia walijua vizuri kwamba Biblia inasema tusiue. Hivyo, hata ndugu wachache waliobeba silaha na kwenda vitani wakati wa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, walikataa kwa uthabiti kutumia silaha hizo kuua wanadamu wenzao. Baadhi ya wale waliokataa kufanya hivyo walipelekwa kwenye mstari wa mbele vitani ili wauawe.

11. Msimamo wa Kimaandiko wa Wanafunzi wa Biblia kuhusu vita uliwafanya wenye mamlaka watendeje?

11 Ingawa msimamo wa ndugu hao kuhusu vita haukuwa kamili, ni wazi kwamba Ibilisi alikasirishwa na uamuzi wao. Kwa hiyo, akatunga “matatizo kwa njia ya amri.” (Zab. 94:20) Alipokuwa akizungumza na Ndugu J. F. Rutherford na W. E. Van Amburgh, Meja-Jenerali wa jeshi la Marekani James Franklin Bell alifunua siri na kusema kwamba Idara ya Sheria ya Marekani ilikuwa imepeleka mswada bungeni ambao ungeidhinisha hukumu ya kifo kwa watu waliokataa kubeba silaha walipoenda vitani. Alikuwa akizungumzia Wanafunzi wa Biblia. Akiwa amekasirika sana, Jenerali Bell alimwambia hivi Ndugu Rutherford: “Mswada huo haukupitishwa kwa sababu [Rais wa Marekani] Wilson aliupinga; lakini tunajua tutakavyowapata, na tutawakamata!”

12, 13. (a) Kwa nini wanaume wanane waliosimamia kazi ya kuhubiri walihukumiwa vifungo virefu gerezani? (b) Je, kifungo hicho kilivunja azimio lao la kumtii Yehova? Eleza.

12 Wenye mamlaka walitekeleza vitisho hivyo. Wawakilishi wa shirika la Watch Tower Society, Ndugu Rutherford, Van Amburgh, na wengine sita walikamatwa. Alipokuwa akisoma hukumu yao, hakimu aliyeshughulikia kesi hiyo alisema hivi: “Propaganda ya kidini ya wanaume hawa ni hatari kuliko kikosi kimoja cha Jeshi la Ujerumani . . . Wameshutumu maofisa wa sheria wa Serikali, kitengo cha kijeshi cha ujasusi, na wamewapinga moja kwa moja viongozi wa makanisa yote. Wanapaswa kuadhibiwa vikali.” (Kitabu Faith on the March, cha A. H. Macmillan, uku. 99) Na kwa kweli waliadhibiwa vikali. Wanafunzi hao wanane wa Biblia walihukumiwa vifungo vya muda mrefu na kufungwa katika gereza kuu huko Atlanta, Georgia, Marekani. Lakini vita vilipoisha, waliachiliwa na mashtaka dhidi yao yakaondolewa.

13 Hata walipokuwa gerezani, ndugu hao wanane walishikilia kwa uthabiti kanuni za Kimaandiko kulingana na jinsi walivyozielewa. Katika ombi lao la msamaha kwa rais wa Marekani, waliandika hivi: “Maandiko yametangaza mapenzi ya Bwana kwamba ‘Usiue,’ kwa hiyo mshiriki yeyote wa shirika la International Bible Students Association aliyejitoa kwa Bwana ambaye atavunja agano lake atapoteza kibali cha Mungu na ataangamizwa kabisa. Kwa hiyo, washiriki hao hawangeshiriki kuwaua wanadamu wenzao kwa hiari au kimakusudi.” Maneno hayo yalionyesha ujasiri mkubwa! Ni wazi kwamba ndugu hao hawakuwa na nia yoyote ya kulegeza msimamo wao!

HATIMAYE WANAWEKWA HURU!

14. Tumia Maandiko kueleza kilichotukia tangu mwaka 1914 hadi 1919.

14 Andiko la Malaki 3:1-3 linazungumzia mambo ambayo yangetukia kuanzia mwaka 1914 hadi mwanzoni mwa mwaka 1919, wakati ambapo “wana wa Lawi,” yaani, watiwa mafuta wangesafishwa. (Soma.) Katika kipindi hicho, Yehova Mungu, “Bwana wa kweli,” pamoja na Yesu Kristo, “mjumbe wa agano,” walikuja katika hekalu la kiroho ili kukagua waliokuwa wakitumikia huko. Baada ya kutiwa nidhamu iliyohitajiwa, watu wa Yehova waliosafishwa walikuwa tayari kupokea migawo zaidi ya utumishi. Katika mwaka 1919, “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” aliwekwa rasmi ili aandae chakula cha kiroho kwa ajili ya watumishi wa nyumbani. (Mt. 24:45) Sasa watu wa Mungu walikuwa huru kutokana na uvutano wa Babiloni Mkubwa. Tangu wakati huo ujuzi wao kuhusu mapenzi ya Yehova umeendelea kuongezeka kwa sababu ya fadhili zake zisizostahiliwa na wamempenda zaidi Baba yao wa mbinguni. Bila shaka, wanathamini sana baraka hizo! [1]

15. Kwa kuwa tumewekwa huru kutoka kwenye utekwa wa Babiloni Mkubwa, tunapaswa kufanya nini?

15 Inasisimua sana kujua kwamba hatimaye tumewekwa huru kutoka kwenye utekwa wa Babiloni Mkubwa! Jitihada za Shetani za kuwaangamiza Wakristo wa kweli zimeshindwa kabisa. Hata hivyo, hatupaswi kusahau kusudi la Yehova la kutupatia uhuru huo. (2 Kor. 6:1) Bado watu wengi wanyoofu wako katika utekwa wa dini za uwongo. Wanahitaji msaada ili watoke katika utekwa huo, nasi tunaweza kuwasaidia. Hivyo basi, acheni tuwaige ndugu na dada zetu walioishi katika karne zilizotangulia kwa kufanya yote tuwezayo kuwasaidia watu wanyoofu watoke kwenye utekwa huo!

^ [1] (fungu la 14) Utekwa wa Wayahudi wa miaka 70 huko Babiloni una ulinganifu mkubwa na kilichowapata Wakristo baada ya uasi imani kutokea. Hata hivyo, haielekei kwamba utekwa wa Kiyahudi ni mfano wa kinabii wa mambo yaliyowapata Wakristo. Jambo moja linalofanya tufikie mkataa huo ni kwamba kipindi cha utekwa kinatofautiana. Kwa hiyo, hatupaswi kulinganisha mambo hususa yaliyowapata Wayahudi walipokuwa utekwani na hali iliyowapata Wakristo watiwa mafuta katika miaka iliyotangulia mwaka 1919.