Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

KUTOKA KATIKA HIFADHI YA VITU VYETU VYA KALE

“Amkeni, Enyi Wahubiri wa Ufalme Nchini Uingereza!”

“Amkeni, Enyi Wahubiri wa Ufalme Nchini Uingereza!”

“AMKENI, enyi wahubiri wa Ufalme nchini Uingereza!” (Informant, * ya Desemba 1937, toleo la London) Huo ulikuwa mwito ulio wazi na wa uharaka. Na kichwa kidogo chenye kuvuta fikira kiliongeza hivi: “Hakujawa na Ongezeko Kubwa kwa Miaka Kumi.” Ripoti ya utumishi ya miaka kumi, kuanzia mwaka 1928 hadi 1937, iliyokuwa kwenye ukurasa wa kwanza, ilithibitisha jambo hilo.

JE, KWELI MAPAINIA WALIKUWA WENGI KUPITA KIASI?

Ni nini kilichokuwa kimefanya bidii ya wahubiri nchini Uingereza ipungue? Inaonekana makutaniko yalikuwa yamezoea kufanya mambo kidesturi kwa miaka mingi, licha ya kwamba hali zilikuwa zimebadilika. Isitoshe, ofisi ya tawi ilikuwa imeamua kwamba mapainia 200 hivi wangetosha kutumikia katika eneo lililokuwa chini ya ofisi hiyo, nao wangehubiri katika maeneo ya mbali badala ya kushirikiana na makutaniko. Kwa hiyo, ofisi ya tawi iliwaambia wahubiri waliotaka kutumikia wakiwa mapainia kwamba hakukuwa na uhitaji nchini Uingereza, na ikawahimiza watumikie katika nchi nyingine za Ulaya. Mapainia wengi walitii himizo hilo na kuhama Uingereza ili wakatumikie kwenye nchi kama vile Ufaransa, ingawa hawakujua vizuri lugha zilizozungumzwa huko.

“MWITO WA KUANZA KUTENDA TENA”

Makala hiyo ya mwaka 1937, iliweka lengo kwa ajili ya mwaka 1938: Kuhubiri saa milioni moja! Lengo hilo lingefikiwa tu ikiwa mapainia wangehubiri saa 110 kwa mwezi nao wahubiri saa 15. Makala hiyo ilipendekeza pia kwamba vikundi vya utumishi vipangwe na kuhubiri saa tano kwa siku, na wahubiri wakazie fikira kufanya ziara za kurudia, hasa jioni za katikati ya juma.

Wakiwa wenye bidii, mapainia wenye shangwe walikazia fikira kazi ya kuhubiri

Kukaziwa upya kwa kazi ya kuhubiri kuliwasisimua wahubiri wengi. Hilda Padgett * anakumbuka hivi: “Ulikuwa mwito wa kuanza kutenda tena kutoka makao makuu ambao wengi wetu walikuwa wameusubiri kwa hamu, na matokeo yalikuwa mazuri sana.” Dada E. F. Wallis alisema hivi: “Pendekezo la kuhubiri saa tano kwa siku lilikuwa zuri sana! Hakukuwa na kitu kingine chenye kufurahisha kama kufanya kazi siku nzima katika utumishi wa Bwana. . . . Tulirudi nyumbani tukiwa tumechoka lakini wenye shangwe sana!” Kijana mmoja aliyeitwa Stephen Miller, aliitikia mwito huo bila kukawia. Alitaka kutumikia kwa kuwa hali zilimruhusu. Anakumbuka vikundi vya wahubiri waliosafiri kwa baiskeli na kuhubiri siku nzima, na jioni wakati wa majira ya joto wangewachezea watu hotuba zilizorekodiwa. Pia, walitembea barabarani wakiwa wamevaa mabango, wakitangaza kwa bidii habari njema na kuwapatia wapita njia magazeti.

Makala hiyo pia ilitoa ombi hili lenye kutia moyo: “Tunahitaji mapainia 1,000.” Mwelekezo mpya kuhusu maeneo ulionyesha kwamba mapainia walipaswa kushirikiana na makutaniko ili kuyategemeza na kuyaimarisha badala ya kuhubiri maeneo ya mbali. Joyce Ellis (ambaye mwanzoni aliitwa Barber) anakumbuka hivi: “Ndugu wengi walitambua kwamba walipaswa kuwa mapainia.” Anaongeza hivi: “Ingawa wakati huo nilikuwa na umri wa miaka 13 tu, nilijua kwamba nilitaka kuwa painia.” Alifikia lengo lake Julai 1940, akiwa na umri wa miaka 15. Peter, ambaye alikuja kuwa mume wa Joyce, aliitikia ‘mwito wa kuamka,’ na ‘akaanza kufikiria kuwa painia.’ Katika Juni 1940, alipokuwa na umri wa miaka 17, alisafiri kwa baiskeli mwendo wa kilometa 105 mpaka Scarborough kwenye mgawo wake wa kwanza.

Cyril na Kitty Johnson walikuwa baadhi ya mapainia wapya wenye kujidhabihu. Waliamua kuuza nyumba na vitu vyao ili kujitegemeza katika utumishi wa wakati wote. Cyril aliacha kazi, na baada ya mwezi mmoja walikuwa tayari kuanza upainia. Anakumbuka hivi: “Tulikuwa na uhakika kuhusu uamuzi wetu. Tuliufanya kwa hiari na tuliufurahia.”

NYUMBA ZA MAPAINIA

Idadi ya mapainia ilipozidi kuongezeka, ndugu waliosimamia kazi ya kuhubiri walifikiria njia za kuwategemeza. Jim Carr, aliyetumikia akiwa mtumishi wa kanda (sasa anaitwa mwangalizi wa mzunguko) mwaka 1938, alifuata pendekezo la kuanzisha nyumba za mapainia kwenye majiji makubwa. Mapainia walitiwa moyo waishi pamoja wakiwa kikundi ili kupunguza gharama. Jijini Sheffield, mapainia walikodi nyumba kubwa na ndugu mmoja mwenye kutegemeka aliwekwa ili asimamie nyumba hiyo. Makutaniko ya eneo hilo yalichangia pesa na samani. Jim anakumbuka hivi: “Kila mtu alijitahidi kufanikisha mpango huo.” Mapainia kumi wenye bidii waliishi hapo, na walikuwa na ratiba nzuri ya mambo ya kiroho. “Walizungumzia andiko [la siku] kila asubuhi wakati wa kiamsha kinywa,” na “kila siku mapainia walienda kuhubiri katika maeneo mbalimbali ya jiji.”

Nchini Uingereza wahubiri wengi sana walianza kufanya upainia

Wahubiri pamoja na mapainia waliitikia mwito na kufikia lengo la kuhubiri saa milioni moja katika mwaka 1938. Kwa kweli, ripoti zinaonyesha kwamba kulikuwa na ongezeko katika nyanja zote za huduma. Katika kipindi cha miaka mitano, idadi ya wahubiri nchini Uingereza iliongezeka kwa karibu mara tatu. Kufanya kazi ya Ufalme kwa bidii kuliwaimarisha watu wa Yehova na kuwasaidia kukabiliana na kipindi kigumu cha vita kilichokuwa kikikaribia.

Leo, idadi ya mapainia nchini Uingereza imeanza kuongezeka tena kadiri vita vya Mungu vya Har–Magedoni vinapozidi kukaribia. Kumekuwa na vilele vipya vya mapainia katika miaka kumi iliyopita, na katika Oktoba 2015 walifikia kilele cha mapainia 13,224. Mapainia hawa wanatambua kabisa kwamba njia bora zaidi ya kutumia maisha yao ni kuwa wahudumu wa wakati wote.

^ fu. 3 Baadaye iliitwa Huduma Yetu ya Ufalme.

^ fu. 8 Simulizi la maisha la Dada Padgett linapatikana katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Oktoba 1, 1995, uku. 19-24.