Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Muendelee Kutiana Moyo Kila Siku

Muendelee Kutiana Moyo Kila Siku

‘Ikiwa kuna neno lolote la kitia moyo mulilo nalo kwa ajili ya watu, muliseme.’—MATENDO 13:15.

NYIMBO: 121, 45

1, 2. Sababu gani ni jambo la maana kutia wengine moyo?

CRISTINA, mwenye kuwa na miaka 18 anasema hivi: “Wazazi wangu hawanitie moyo hata kidogo, lakini wananichambua-chambua sana. Na maneno yao yananiumiza sana. Wananiambia kama ningali mutoto, sitajuaka kitu hata siku moja, na kama niko munene. Kwa hiyo, mara nyingi ninalia na sipendi kuzungumuza nao. Ninajisikia kuwa mutu wa bure.” [1] (Soma maelezo kwenye mwisho wa habari hii.) Maisha yanaweza kuwa magumu wakati wengine hawatutie moyo!

2 Kwa upande mwingine, fikiria namna tunaweza kusaidia sana wengine wakati tunawatia moyo. Rubén anasema hivi: “Nimepiganisha kwa miaka mingi mawazo ya kujisikia kuwa mutu wa bure. Lakini, siku moja nilikuwa ninahubiri na muzee fulani na alitambua kama sikukuwa na furaha. Alinisikiliza kwa huruma wakati nilikuwa ninamuelezea namna nilikuwa ninajisikia. Kisha alinikumbusha mambo ya muzuri yenye nilikuwa ninafanya. Na pia alinikumbusha maneno ya Yesu yenye kuonyesha kama kila mumoja wetu ni wa maana kuliko shomoro (aina fulani ya ndege) wengi. Kila mara ninakumbuka andiko hilo, na linaendelea kugusa moyo wangu. Maneno ya muzee huyo yalinisaidia sana.”—Mathayo 10:31.

3. (a) Mutume Paulo alisema nini juu ya kutia wengine moyo? (b) Tutazungumuzia nini katika habari hii?

3 Biblia inasema kama tunapaswa kutiana moyo sikuzote. Mutume Paulo aliandikia Wakristo Waebrania hivi: ‘Mujihazari, akina ndugu, ili moyo muovu unaokosa imani usije ukasitawi [ukakomaa] ndani ya yeyote kati yenu kwa kujiondoa kwa Mungu aliye hai; lakini muendelee kuhimizana [kutiana moyo] kila siku.’ Paulo alifasiria sababu gani. Alisema hivi: ‘Ili yeyote kati yenu asije akafanywa kuwa mugumu kwa nguvu za udanganyifu za zambi.’ (Waebrania 3:12, 13) Fikiria namna ulifurahi sana wakati mutu fulani alikutia moyo. Kwa hiyo, sababu gani tunapaswa kutia moyo ndugu na dada zetu? Namna Yehova, Yesu, na mutume Paulo walitia wengine moyo inaweza kutufundisha nini? Na ni katika njia gani tunaweza kutiana moyo? Tuzungumuzie basi maulizo hayo.

SISI WOTE TUKO NA LAZIMA YA KUTIWA MOYO

4. Ni nani wako na lazima ya kutiwa moyo? Sababu gani watu wengi leo hawatie wengine moyo?

4 Sisi wote tuko na lazima ya kutiwa moyo. Sababu gani ni jambo la maana sana wazazi watie moyo watoto wao? Mwalimu mumoja mwenye kuitwa Timothy Evans anasema kama watoto “wako na lazima ya kutiwa moyo kama vile mimea iko na lazima ya maji.” Anaongeza hivi: “Wakati mutoto anatiwa moyo, anajisikia kuwa mutu wa maana na anaona kama anapendwa.” Lakini, kwa sababu tunaishi katika “siku za mwisho,” watu wengi wanajipenda wenyewe na “upendo [wao] wa asili” kwa ajili ya wengine uko kidogo. (2 Timotheo 3:1-5) Wazazi fulani hawatie moyo watoto wao kwa sababu wazazi wao pia hawakuwatia moyo hata kidogo. Watu wenye kukomaa pia wako na lazima ya kutiwa moyo, lakini mara nyingi hilo halifanyike. Kwa mufano, watu wengi wananungunika kuwa hakuna hata mutu mumoja mwenye anawapongeza juu ya mambo yenye wanafanya kwenye kazi.

5. Namna gani tunaweza kutia wengine moyo?

5 Tunaweza kutia wengine moyo kwa kuwapongeza juu ya jambo fulani la muzuri lenye wamefanya. Tunaweza pia kutia wengine moyo kwa kuwaambia kama wako na sifa za muzuri na kwa kuwafariji wakati wako na huzuni ao wakati wanavunjika moyo. (1 Wathesalonike 5:14) Kwa sababu tuko pamoja na ndugu na dada zetu kila mara, tuko na nafasi nyingi za kuwaambia jambo fulani lenye kuwatia moyo. (Soma Mhubiri 4:9, 10.) Kwa hiyo, ujiulize hivi: ‘Ninaambia wengine sababu gani ninawapenda na kuwaona kuwa wa maana? Na ninafanya hivyo kila wakati inawezekana?’ Fikiria jambo hili lenye Biblia inasema: ‘Neno linalosemwa wakati unaofaa ni njema kama nini!’—Methali 15:23.

6. Sababu gani Shetani anapenda kuvunja watu wa Mungu moyo? Toa mufano wenye kuonyesha namna alijaribu kufanya hivyo.

6 Methali 24:10 inasema hivi: “Je, umejionyesha kuwa umevunjika moyo siku ya taabu? Nguvu zako zitakuwa chache [kidogo].” Shetani anajua kwamba ikiwa anatuvunja moyo, anaweza kufanya urafiki wetu pamoja na Yehova ukuwe zaifu. Alijaribu kuvunja Ayubu moyo kwa kumuletea mateso makali. Lakini, mupango mubaya sana wa Shetani ulishindwa. Ayubu alibakia mushikamanifu kwa Yehova. (Ayubu 2:3; 22:3; 27:5) Sisi pia tunaweza kupiganisha Shetani na kumuzuia apate ushindi. Ikiwa tunaendelea kutia watu wa familia yetu moyo na ndugu na dada zetu katika kutaniko, tunaweza kusaidiana ili tukuwe na furaha na tubakie karibu na Yehova.

MIFANO YENYE TUNAWEZA KUIGA

7, 8. (a) Namna gani Yehova ametia watu moyo? (b) Namna gani wazazi wanaweza kufuata mufano wa Yehova? (Ona picha kwenye mwanzo wa habari hii.)

7 Yehova anatia watu moyo. Muandikaji mumoja wa Zaburi alisema hivi: ‘Yehova yuko karibu na wale waliovunjika moyo; naye anawaokoa wale waliopondwa roho.’ (Zaburi 34:18) Wakati nabii Yeremia aliogopa na kuvunjika moyo, Yehova aliahidi kama atamusaidia. (Yeremia 1:6-10) Yehova alituma malaika mumoja ili kutia nguvu Danieli, nabii mwenye kuzeeka. Na Malaika huyo alimuita Danieli ‘mutu mwenye kutamanika sana.’ (Danieli 10:8, 11, 18, 19) Je, unaweza kutia ndugu na dada zako moyo katika njia kama hiyo, na pia mapainia na ndugu na dada wenye kuzeeka wenye hawawezi tena kufanya mengi kama zamani?

8 Hata kama Yehova na Yesu walikuwa wameishi pamoja kwa miaka mingi, Yehova alijua kama ni lazima aendelee kutia moyo Mwana wake wakati alikuwa katika dunia. Yesu alisikia Baba yake anasema kutoka mbinguni wakati alianza kazi yake ya kuhubiri na katika mwaka wa mwisho wa maisha yake hapa duniani. Katika hali hizo mbili, Yehova alisema hivi: ‘Huyu ni Mwanangu, mupendwa, ambaye nimemukubali.’ (Mathayo 3:17; 17:5) Kwa kweli, Yesu alitiwa moyo sana wakati alisikia Baba yake anasema kama anamupenda na anamufurahia. Kisha, usiku wenye ulitangulia kifo chake, Yesu alihangaika sana. Yehova alimutia moyo kwa kutuma malaika fulani ili amutie nguvu na kumufariji. (Luka 22:43) Wazazi, munaweza kuiga mufano wa Yehova kwa kutia watoto wenu moyo sikuzote. Muwapongeze wakati wanafanya muzuri jambo fulani. Na wakati wanapata majaribu kwenye masomo, mufanye yenu yote ili kuwatia nguvu na kuwasaidia wavumilie.

9. Namna Yesu alitendea mitume wake inaweza kutufundisha nini?

9 Yesu pia alituachia mufano muzuri wa kuiga. Usiku wenye ulitangulia kifo chake, Yesu alinawisha mitume wake miguu na akawaambia kama ni jambo la maana sana kuwa wanyenyekevu. Lakini walikuwa na kiburi, na walibishana juu ya nani alikuwa mukubwa kati yao, na Petro alijisifu kuwa hatamuacha Yesu hata siku moja. (Luka 22:24, 33, 34) Hata hivyo, Yesu hakukazia makosa yao. Lakini, aliwapongeza kwa sababu walibakia washikamanifu kwake. Aliwaahidi kama wangefanya mambo makubwa zaidi kuliko yeye, na aliwahakikishia kama Yehova anawapenda. (Luka 22:28; Yohana 14:12; 16:27) Tunaweza kujiuliza hivi: ‘Ninaiga mufano wa Yesu na ninapongeza wengine juu ya sifa zao za muzuri kuliko kukazia makosa yao?’

10, 11. Namna gani Paulo alitia moyo ndugu zake, na alikuwa tayari kufanya nini?

10 Mutume Paulo alisema sikuzote mambo ya muzuri juu ya ndugu zake. Alisafiri kwa miaka mingi na wamoja kati yao na aliwajua muzuri kabisa, lakini hakuandika juu ya makosa yao. Kuliko kufanya hivyo, aliwasifu. Kwa mufano, Paulo alisema kama Timotheo alikuwa ‘mutoto wake mupendwa na mwaminifu katika Bwana’ na kwamba alikuwa hakika kama Timotheo atahangaikia mahitaji ya wengine. (1 Wakorintho 4:17; Wafilipi 2:19, 20) Paulo alimupongeza Tito kwa kuambia Kutaniko la Korintho kama Tito ni ‘mushiriki pamoja nami na mufanyakazi mwenzangu kwa ajili ya faida yenu.’ (2 Wakorintho 8:23) Kwa kweli, Timotheo na Tito walitiwa moyo wakati walisikia mambo yenye mutume Paulo alisema juu yao!

11 Paulo na mwenzake Barnaba, walitia maisha yao katika hatari ili kutia moyo ndugu zao. Kwa mufano, walijua kama watu wengi katika muji wa Listra walipenda kuwaua. Lakini, walirudia huko ili kutia moyo wanafunzi wapya na kuwasaidia wabakie waaminifu kwa Yehova. (Matendo 14:19-22) Kisha, katika muji wa Efeso, Paulo alikuwa katika hatari kwa sababu ya kikundi cha watu wenye kukasirika sana, lakini alibakia huko kwa muda murefu ili kutia moyo ndugu zake. Matendo 20:1, 2 inasema hivi: “Paulo akatuma watu wawaite wanafunzi, na alipokuwa amewatia moyo na kuwaaga, akasafiri na kuingia Makedonia. Baada ya kupitia sehemu hizo na kuwatia moyo wale walio huko kwa maneno mengi, akaingia Ugiriki.”

TUTIANE MOYO

12. Sababu gani ni muzuri tuende kwenye mikutano?

12 Yehova anatutakia mambo ya muzuri sana. Ndiyo sababu anatuambia tukusanyike pamoja kwa ukawaida. Kwenye mikutano yetu, tunajifunza juu yake na tunatiana moyo. (1 Wakorintho 14:31; soma Waebrania 10:24, 25.) Cristina, mwenye kuzungumuziwa kwenye mwanzo wa habari hii, anasema hivi: “Jambo lenye kunifurahisha sana juu ya mikutano yetu, ni namna wengine wananionyesha upendo na kunitia moyo. Wakati fulani ninajisikia kuwa mwenye kuvunjika moyo wakati ninafika kwenye Jumba la Ufalme. Lakini, dada wananikaribia, wanikumbatia na wananiambia kama niko mwenye kupendeza. Wananiambia kama wananipenda na wanafurahi kuona maendeleo yangu ya kiroho. Ninajisikia muzuri zaidi wakati wananitia moyo!” Ni jambo la maana sana kila mumoja wetu atie wengine moyo!—Waroma 1:11, 12.

13. Sababu gani hata wale wenye wamemutumikia Yehova kwa miaka mingi wako na lazima ya kutiwa moyo?

13 Hata wale wenye wametumikia Yehova kwa miaka mingi wako na lazima ya kutiwa moyo. Fikiria mufano wa Yoshua. Wakati Waisraeli walikuwa karibu kuingia katika Inchi ya Ahadi, Yehova alichagua Yoshua ili awaongoze. Hata hivyo, Yehova aliambia Musa amutie moyo, hata kama Yoshua alikuwa ametumikia Yehova kwa miaka mingi. Yehova aliambia Musa hivi: ‘ Nawe umupe Yoshua utume na kumutia moyo na kumuimarisha, kwa maana yeye ndiye atakayevuka mbele ya watu hawa naye ndiye atakayewafanya wariti inchi utakayoiona.’ (Kumbukumbu la Torati 3:27, 28) Yoshua alikuwa na lazima ya kutiwa moyo kwa sababu taifa la Israeli lingepigana vita nyingi na hata wakati fulani maadui wangepata ushindi juu yao. (Yoshua 7:1-9) Leo, tunaweza kutia moyo wazee na waangalizi wa muzunguko wenye wanatumika kwa bidii ili kuhangaikia watu wa Mungu. (Soma 1 Wathesalonike 5:12, 13.) Mwangalizi mumoja wa muzunguko alisema hivi: “Wakati fulani ndugu wanatutumia barua ya kutushukuru, wanasema kama walifurahi sana wakati tuliwatembelea. Tunachunga barua hizo ili kuzisoma wakati tunavunjika moyo. Zinatutia moyo kabisa.”

Tunasaidia watoto wetu wamukaribie Yehova wakati tunawatia moyo kwa upendo (Picha hii inapatana na fungu la 14)

14. Ni mifano gani yenye kuonyesha kama ni muzuri kupongeza wengine wakati tunawatolea mashauri?

14 Siku fulani, mutume Paulo alitolea Wakorintho mashauri. Wakati walitumikisha mashauri hayo, Paulo aliwapongeza. (2 Wakorintho 7:8-11) Kwa kweli, maneno yake yaliwatia moyo waendelee kufanya mambo yenye kuwa sawa. Leo, wazee na wazazi wanaweza kufuata mufano wa Paulo. Andreas, mwenye kuwa na watoto wawili anasema hivi: “Kutia watoto moyo kunawasaidia wakomae kiroho na kiakili. Wakati tunawatia moyo, hilo linawachochea kufuata mashauri. Hata kama watoto wetu wanajua mambo yenye kuwa sawa, ili waendelee kufanya mambo hayo katika maisha yao, tunapaswa kuwatia moyo sikuzote.”

NI NINI ITAKUSAIDIA KUTIA WENGINE MOYO?

15. Ni katika njia gani moja tunaweza kutia wengine moyo?

15 Ambia ndugu na dada zako kama unafurahia bidii yao na kama unapendezwa na sifa zao za muzuri. (2 Mambo ya Nyakati 16:9; Ayubu 1:8) Kama tunafanya hivyo, tunaiga Yehova na Yesu. Wanafurahia mambo yote yenye tunawafanyia, hata kama hatuwezi kufanya tena mambo mengi kama vile tungependa kufanya. (Soma Luka 21:1-4; 2 Wakorintho 8:12.) Kwa mufano, tunajua kama ndugu na dada zetu wenye kuzeeka wanajikaza sana ili kuenda kwenye mikutano na kuhubiri kwa ukawaida. Tunawatia moyo na kuwapongeza kwa mambo yote yenye wanafanya?

16. Ni wakati gani tunaweza kutia wengine moyo?

16 Tia wengine moyo kila wakati unapata nafasi ya kufanya hivyo. Wakati wowote unaona jambo la muzuri lenye mutu alifanya, umupongeze. Wakati mutume Paulo na Barnaba walikuwa Antiokia katika Pisidia, viongozi wa sinagogi waliwaambia hivi: ‘Wanaume, akina ndugu, ikiwa kuna neno lolote la kitia moyo mulilo nalo kwa ajili ya watu, muliseme.’ Paulo alitumia nafasi hiyo ili kutia watu moyo. (Matendo 13:13-16, 42-44) Wakati tunatia wengine moyo, watu wanaweza pia kututia moyo.—Luka 6:38.

17. Unaweza kutumia njia gani ya muzuri zaidi ili kupongeza wengine?

17 Ukuwe wazi. Wakati Yesu alipongeza Wakristo wa Thiatira, alikuwa wazi na aliwaambia mambo ya muzuri yenye walikuwa wamefanya. (Soma Ufunuo 2:18, 19.) Namna gani tunaweza kumuiga? Pengine, tunaweza kupongeza mama mwenye anajikaza kulea watoto peke yake hata kama ni vigumu kwake. Ao kama uko muzazi unaweza kupongeza watoto wako kwa sababu wanajikaza kutumikia Yehova. Uwaambie mambo ya muzuri yenye umeona. Ikiwa tunataja mambo fulani waziwazi wakati tunatia wengine moyo, wataona kama mambo yenye tunasema ni ya kweli.

18, 19. Namna gani tunaweza kusaidiana kuendelea kuwa karibu na Yehova?

18 Yehova aliambia Musa atie Yoshua moyo na kumutia nguvu. Kwa kweli, Yehova hatazungumuza na sisi leo na kutuambia tutie mutu fulani moyo. Lakini anafurahi wakati anaona tunajikaza ili kutia wengine moyo. (Methali 19:17; Waebrania 12:12) Kwa mufano, wakati ndugu fulani anatoa hotuba katika kutaniko letu, tunaweza kumuambia jambo lenye tulifurahia katika hotuba yake. Pengine jambo fulani lenye alisema lilitusaidia kupiganisha magumu fulani ao kuelewa andiko fulani. Dada mumoja aliandikia ndugu mwenye alitoa hotuba, na kumuambia hivi: “Hata kama tulizungumuza kwa dakika kidogo tu, uliona moyo wangu wenye huzuni, na ulinituliza na kunitia moyo. Ninapenda ujue kama wakati ulikuwa unazungumuza kwenye jukwaa, na wakati ulizungumuza na mimi, niliona kama ilikuwa zawadi kutoka kwa Yehova.”

19 Tutasaidiana kuendelea kuwa karibu na Yehova ikiwa tunafuata shauri hili la mutume Paulo: ‘Muendelee kufarijiana na kujengana, kama vile munavyofanya.’ (1 Wathesalonike 5:11) Kama ‘Tunaendelea kuhimizana kila siku,’ tutamufurahisha sana Yehova!

^ [1] (fungu la 1) Majina fulani yamebadilishwa.