Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HABARI KUU | JE, UTAITHAMINI ZAWADI BORA ZAIDI YA MUNGU?

Jinsi ya Kuithamini Zawadi Bora ya Mungu!

Jinsi ya Kuithamini Zawadi Bora ya Mungu!

“Upendo alio nao Kristo hutulazimisha . . . Alikufa kwa ajili ya wote ili wale wanaoishi wasiishi tena kwa ajili yao wenyewe, bali kwa ajili ya yeye aliyekufa kwa ajili yao.”—2 Wakorintho 5:14, 15.

ZAWADI ya pekee inapaswa kutuchochea kushukuru. Yesu alikazia somo hilo alipowaponya wanaume kumi waliokuwa na ukoma, ugonjwa ambao haukuwa na tiba nyakati hizo. Mmoja kati ya wanaume hao “akarudi, akimtukuza Mungu kwa sauti kubwa.” Yesu akauliza: “Wale kumi walitakaswa, sivyo? Basi, wako wapi wale wengine tisa?” (Luka 17:12-17) Tunajifunza nini? Ni rahisi sana kusahau matendo ya fadhili tuliyotendewa na watu wengine!

Fidia haiwezi kulinganishwa na zawadi nyingine yoyote. Fidia ndio zawadi bora zaidi iliyowahi kutolewa. Hivyo basi, tunapaswa kufanya nini kuhusiana na kile ambacho Mungu ametufanyia?

  • Jifunze kuhusu Yule aliyetoa. Fidia inawawezesha wanadamu kupata uzima wa milele, lakini jitihada fulani zinahitajika. Yesu alisali hivi kwa Mungu: “Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.” (Yohana 17:3) Ikiwa ungeambiwa kwamba mtu fulani aliokoa uhai wako ulipokuwa mtoto, je, hungependa kumjua vizuri zaidi na kujua ni kwa nini alifanya hivyo? Yehova Mungu, ambaye alitoa zawadi ya fidia inayookoa uhai, anataka umjue na vilevile uwe na uhusiano wa karibu pamoja naye. Biblia inatuhimiza hivi: “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.”—Yakobo 4:8.

  • Uwe na imani katika fidia. “Yule anayemwamini Mwana ana uzima wa milele.” (Yohana 3:36) Kuwa na imani kunamaanisha nini? Kunamaanisha kuchukua hatua; kuamini fidia kunaonyeshwa kupitia matendo. (Yakobo 2:17) Matendo ya aina gani? Zawadi inakuwa yako unapoikubali na kuipokea. Vivyo hivyo, ni lazima uikubali fidia. Jinsi gani? Jifunze mapenzi ya Mungu, kisha, ishi na kutenda kupatana na yale unayojifunza. * Sali kwa Mungu ili akusamehe na upate dhamiri safi. Mkaribie Mungu ukiwa na uhakika kabisa kwamba kuwa na imani katika fidia kutatuwezesha tupate uzima, amani, usalama na ufanisi wakati ujao!—Waebrania 11:1.

  • Hudhuria Ukumbusho wa Kifo cha Yesu. Yesu alianzisha tukio ambalo hufanywa kila mwaka ili kutukumbusha kuhusu zawadi hiyo ya fidia. Kuhusu tukio hilo, alisema hivi: “Endeleeni kufanya hivi kwa kunikumbuka mimi.” (Luka 22:19) Mashahidi wa Yehova wataadhimisha ukumbusho wa kifo cha Yesu, Jumanne, Aprili 11, 2017, baada ya jua kutua. Programu hiyo ambayo hufanywa kwa muda wa saa moja, itatia ndani hotuba inayoelezea umuhimu wa kifo cha Yesu na jinsi tunavyonufaika sasa na hata wakati ujao. Mwaka uliopita, karibu watu milioni 20 walihudhuria Ukumbusho ulimwenguni pote. Tunakukaribisha kwa moyo wote ujiunge nasi kumshukuru Mungu kwa ajili ya zawadi yake kuu.

^ fu. 7 Njia bora ya kumjua Mungu na kumkaribia ni kujifunza Neno lake, Biblia. Ili kujua mengi zaidi, wasiliana na Mashahidi wa Yehova au tembelea tovuti yetu, www.pr418.com/sw.