Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HABARI KUU | MALAIKA​—JE, WANAHUSIKA KATIKA MAISHA YAKO?

Ukweli Kuwahusu Malaika

Ukweli Kuwahusu Malaika

Je, ungependa kujua ukweli kuwahusu malaika—wao ni nani, walitoka wapi, na wanafanya nini? Hakuna mahali pengine tunapoweza kupata majibu sahihi ya maswali hayo isipokuwa, katika Biblia, Neno la Mungu lililoongozwa na roho Yake. (2 Timotheo 3:16) Maandiko yanasema nini kuwahusu malaika?

  • Kama ambavyo Mungu ni Roho, malaika pia ni viumbe wa roho wasioonekana, nao hawana “nyama na mifupa.” Malaika washikamanifu wanaishi mbinguni nao wanatumikia mbele za Mungu.—Luka 24:39; Mathayo 18:10; Yohana 4:24.

  • Nyakati fulani malaika walikuja duniani wakiwa wamejivika miili ya kibinadamu ili kutimiza migawo waliyopewa na Mungu, na kurudia miili yao baada ya kumaliza migawo hiyo.—Waamuzi 6:11-23; 13:15-20.

  • Ingawa katika Biblia malaika wanatajwa wakiwa wa kiume na mara zote walikuja duniani na miili ya kiume, ukweli ni kwamba wao hawana jinsia ya kiume wala ya kike. Hawaoani wala kuzaliana. Kwa kuongezea, malaika hawakuwa wanadamu zamani, wakiwa watoto au watu wazima. Wao waliumbwa na Yehova; ndio sababu Biblia inawaita “wana wa Mungu wa kweli.”—Ayubu 1:6; Zaburi 148:2, 5.

  • Biblia inataja kuhusu “lugha za wanadamu na za malaika,” ikionyesha kwamba viumbe wa roho wana njia ya mawasiliano na lugha. Ingawa Mungu amewatumia malaika kuwasiliana na wanadamu, hataki tusali kwao wala kuwaabudu.—1 Wakorintho 13:1; Ufunuo 22:8, 9.

  • Kuna makumi ya maelfu ya makumi ya maelfu ya malaika, na hivyo huenda wakafikia mabilioni. *Danieli 7:10; Ufunuo 5:11.

  • Malaika wana “nguvu nyingi,” zinazopita za wanadamu, na pia wana uwezo mkubwa zaidi wa akili. Kwa kweli malaika wanaweza kusafiri kwa kasi sana, kuliko tunavyoweza kuwazia.—Zaburi 103:20, Verbum Bible; Danieli 9:20-23.

  • Licha ya kuwa na uwezo mkubwa wa akili na nguvu nyingi, malaika wana mipaka, na kuna mambo ambayo hawajui.—Mathayo 24:36; 1 Petro 1:12.

  • Malaika waliumbwa wakiwa na utu tofauti-tofauti, sifa kama za Mungu, na uhuru wa kuchagua. Hivyo, kama vile wanadamu, wanaweza kuchagua kufanya mema au mabaya. Kwa kusikitisha, baadhi ya malaika waliamua kumwasi Mungu.—Yuda 6.

^ fu. 8 Makumi ya elfu ni 10,000. Na elfu kumi mara elfu kumi ni sawa na milioni 100. Hata hivyo, kitabu cha Ufunuo kinataja kuhusu, “makumi ya maelfu ya makumi ya maelfu” ya malaika. Hiyo ni sawa na mamia ya mamilioni, au hata mabilioni ya viumbe hao wa roho!