Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Mtegemee Yehova na Ufanye Mema”

“Mtegemee Yehova na Ufanye Mema”

“Mtegemee Yehova na ufanye mema . . . na utende kwa uaminifu.ZAB. 37:3.

NYIMBO: 133, 63

1 Yehova aliwaumba wanadamu wakiwa na uwezo gani mbalimbali wa pekee?

YEHOVA aliwaumba wanadamu wakiwa na uwezo mbalimbali wa pekee. Alitupatia uwezo wa kufikiri ili tusuluhishe matatizo na kupangia wakati ujao. (Met. 2:11) Alitupatia nguvu za kutimiza mipango yetu na kutusaidia kufikia malengo yanayofaa. (Flp. 2:13) Pia, alituumba tukiwa na dhamiri, yaani, uwezo tuliozaliwa nao wa kutambua lililo sawa na lililo kosa. Uwezo huo unaweza kutusaidia kuepuka au kurekebisha makosa yetu.—Rom. 2:15.

2. Yehova anatarajia tutumie uwezo wetu jinsi gani?

2 Yehova anatarajia tutumie vizuri uwezo mbalimbali tulio nao. Kwa nini? Kwa sababu anatupenda na anajua kwamba tutaridhika tunapotumia zawadi hizo. Kupitia Neno lake, Yehova anatuhimiza mara kwa mara tutumie uwezo wetu mbalimbali kufanya mema. Kwa mfano, katika Maandiko ya Kiebrania tunasoma hivi: “Mipango ya mwenye bidii bila shaka huleta faida”; na “yote ambayo mkono wako unapata kufanya, yafanye kwa nguvu zako zote.” (Met. 21:5; Mhu. 9:10) Tunaambiwa hivi katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo: “Tukiwa na wakati unaofaa kwa ajili ya hilo, tuwatendee wote mema”; na “kwa kadiri ambayo kila mmoja amepokea zawadi, itumieni katika kuhudumiana.” (Gal. 6:10; 1 Pet. 4:10) Ni wazi kwamba Yehova anataka tufanye yote tuwezayo ili tujinufaishe na kuwanufaisha wengine.

3. Ni mambo gani ambayo wanadamu hawawezi kufanya?

3 Wakati huohuo, Yehova anatambua kwamba kuna mambo ambayo wanadamu hawawezi kufanya. Hatuwezi kamwe kuondoa kutokamilika, dhambi, na kifo kwa jitihada zetu wenyewe; wala hatuwezi kuwadhibiti watu wengine kwa sababu kila mtu ana uhuru wa kuchagua. (1 Fal. 8:46) Hata tuwe na ujuzi au uzoefu kiasi gani, sikuzote sisi ni kama watoto tunapolinganishwa na Yehova.Isa. 55:9.

Unaposhughulika na matatizo, “mtegemee Yehova na ufanye mema”

4. Tutachunguza nini katika makala hii?

4 Tunahitaji kumtegemea Yehova atuongoze katika hali zote, huku tukitumaini kwamba atatutegemeza na kutufanyia mambo tusiyoweza kufanya. Na wakati huohuo, tunapaswa kufanya yote tuwezayo kwa kuchukua hatua kusuluhisha matatizo na kuwasaidia wengine. (Soma Zaburi 37:3.) Kwa ufupi, tunahitaji ‘kumtegemea Yehova na kufanya mema’; na ‘kutenda kwa uaminifu.’ Kuhusiana na hilo, acheni tuchunguze mambo tunayoweza kujifunza kutokana na mfano wa Noa, Daudi, na watumishi wengine waaminifu wa Yehova ambao walimtegemea na kuchukua hatua inayofaa. Kama tutakavyoona, hilo lilihusisha kutofautisha kati ya mambo ambayo hawangeweza kufanya na yale ambayo wangeweza kufanya na kisha kutenda ifaavyo.

TUNAPOZUNGUKWA NA UOVU

5. Eleza hali ambayo Noa alikabili.

5 Noa aliishi katika ulimwengu ambao ‘ulijaa jeuri’ na maadili mapotovu. (Mwa. 6:4, 9-13) Alijua kwamba hatimaye Yehova angeuharibu ulimwengu huo mwovu. Ingawa hivyo, lazima Noa alihuzunishwa na uovu uliomzunguka. Alipokabili hali hiyo, Noa alitambua kwamba kuna mambo fulani ambayo hangeweza kufanya na mengine ambayo angeweza kufanya.

Kupingwa unapohubiri (Tazama fungu la 6 hadi 9)

6, 7. (a) Ni mambo gani ambayo Noa hangeweza kufanya? (b) Hali katika siku zetu inafananaje na hali katika siku za Noa?

6 Mambo ambayo Noa hangeweza kufanya: Ingawa Noa alihubiri kwa uaminifu ujumbe wa Yehova wa kuwaonya watu, hangewalazimisha watu waovu waliomzunguka wakubali ujumbe huo wala hangeweza kufanya Gharika ije haraka zaidi. Noa alihitaji kuamini kwamba Yehova angetimiza ahadi Yake ya kukomesha uovu na kwamba angefanya hivyo kwa wakati unaofaa kabisa.—Mwa. 6:17.

7 Sisi pia tunaishi katika ulimwengu uliojaa uovu, na tunajua Mungu ameahidi kwamba atauharibu. (1 Yoh. 2:17) Kwa sasa, hatuwezi kuwalazimisha watu wakubali “habari njema ya ufalme.” Na hatuwezi kufanya jambo lolote ili “dhiki kuu” ije haraka zaidi. (Mt. 24:14, 21) Kama Noa, tunahitaji imani yenye nguvu tukiamini kwamba hivi karibuni Mungu ataingilia kati. (Zab. 37:10, 11) Tunasadiki kwamba Yehova hataruhusu ulimwengu huu mwovu uendelee kuwepo kwa siku moja zaidi kuliko alivyokusudia.Hab. 2:3.

8. Noa alikaziaje fikira mambo ambayo angeweza kufanya? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

8 Mambo ambayo Noa angeweza kufanya: Badala ya kukata tamaa kwa sababu ya mambo ambayo hangeweza kufanya, Noa alikazia fikira mambo ambayo angeweza kufanya. Akiwa “mhubiri wa uadilifu,” Noa alitangaza kwa uaminifu ujumbe ambao alikuwa amekabidhiwa wa kuwaonya watu. (2 Pet. 2:5) Hakuna shaka kwamba kufanya hivyo kulimsaidia Noa aendelee kuimarisha imani yake. Zaidi ya kuhubiri, alitumia pia uwezo wake wa kimwili na kiakili kutimiza kazi aliyopewa na Mungu ya kujenga safina.Soma Waebrania 11:7.

9. Tunaweza kuigaje mfano wa Noa?

9 Kama Noa, tunajitahidi kuwa na “mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana.” (1 Kor. 15:58) Huenda kazi hiyo ikatia ndani ujenzi na udumishaji wa majumba ya ibada, kujitolea kwenye makusanyiko, au kutimiza migawo mbalimbali katika ofisi za tawi au ofisi za kutafsiri. Zaidi ya yote, tunakuwa na mengi ya kufanya katika kazi ya kuhubiri, tukijua kwamba kazi hiyo inaimarisha tumaini letu la wakati ujao. Dada mmoja mwaminifu anasema hivi: “Unapozungumza na wengine kuhusu baraka za Ufalme wa Mungu, unatambua kwamba wasikilizaji wako hawana tumaini lolote na wanafikiri kwamba matatizo yao ni ya kudumu.” Kwa kweli, kazi ya kuhubiri inatuimarisha tuwe na mtazamo mzuri kuhusu wakati ujao na kuimarisha azimio letu la kutokata tamaa katika mbio zetu za uzima.1 Kor. 9:24.

TUNAPOKOSEA

10. Eleza hali ambayo Daudi alikabili.

10 Yehova alisema kwamba Mfalme Daudi alikuwa “mtu anayekubalika kwa moyo [wake].” (Mdo. 13:22) Kwa ujumla, Daudi alikuwa mwaminifu katika maisha yake yote. Hata hivyo, pindi fulani alifanya dhambi nzito. Alifanya uzinzi na Bath-sheba. Na jambo baya hata zaidi ni kwamba alijaribu kuficha dhambi hiyo kwa kupanga Uria, mume wa Bath-sheba, auawe vitani. Daudi hata aliandika barua iliyoidhinisha kifo cha Uria na kumpa aiwasilishe! (2 Sam. 11:1-21) Mwishowe, dhambi za Daudi zilifunuliwa, jambo ambalo hangeweza kuliepuka. (Marko 4:22) Zilipofunuliwa, Daudi alitendaje?

Makosa ya zamani (Tazama fungu la 11 hadi 14)

11, 12. (a) Baada ya kutenda dhambi, ni mambo gani ambayo Daudi hangeweza kufanya? (b) Tukitubu baada ya kufanya makosa mazito, tunaweza kutumaini kwamba Yehova atatufanyia nini?

11 Mambo ambayo Daudi hangeweza kufanya: Daudi hangeweza kutangua dhambi zake. Wala hangeweza kuepuka matokeo ya makosa yake. Kwa kweli, baadhi ya matokeo ya dhambi za Daudi yangemwandama katika maisha yake yote. (2 Sam. 12:10-12, 14) Kwa hiyo, alihitaji imani. Alihitaji kuamini kwamba ikiwa angetubu kikweli, Yehova angemsamehe na kumsaidia kuvumilia matokeo ya matendo yake.

12 Kwa kuwa sisi si wakamilifu, sote hutenda dhambi. Makosa fulani ni mazito kuliko mengine. Katika visa fulani, huenda tusiweze kutangua makosa yetu. Huenda tukalazimika kuvumilia matokeo ya makosa hayo maisha yetu yote. (Gal. 6:7) Lakini tunaamini kile ambacho Mungu amesema, tukitumaini kwamba ikiwa tutatubu Yehova atatutegemeza katika kipindi hicho kigumu, hata iwe sisi wenyewe ndio tuliojisababishia hali hizo.—Soma Isaya 1:18, 19; Matendo 3:19.

13. Daudi alipataje tena nguvu za kiroho?

13 Mambo ambayo Daudi angeweza kufanya: Daudi alimruhusu Yehova amsaidie kupata tena nguvu za kiroho. Kwanza ni kwa kukubali kurekebishwa na nabii Nathani, ambaye alikuwa mwakilishi wa Yehova. (2 Sam. 12:13) Pia, Daudi alisali kwa Yehova, akakiri dhambi zake, na kueleza tamaa yake ya kupata tena kibali cha Yehova. (Zab. 51:1-17) Badala ya kulemewa na hisia za hatia, Daudi alijifunza kutokana na makosa yake. Ukweli ni kwamba hakurudia kamwe dhambi hizo nzito. Miaka mingi baadaye, alikufa akiwa mwaminifu, rekodi yake ya utimilifu ikiwa imebaki daima katika kumbukumbu ya Yehova.Ebr. 11:32-34.

14. Tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa Daudi?

14 Tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa Daudi? Tukitumbukia kwenye dhambi nzito, tunahitaji kutubu kikweli na kuomba msamaha wa Yehova. Lazima tukiri dhambi zetu mbele zake. (1 Yoh. 1:9) Pia tunahitaji kuwaona wazee, ambao wanaweza kutupatia msaada wa kiroho. (Soma Yakobo 5:14-16.) Kwa kutumia maandalizi ya Yehova, tunaonyesha kwamba tunatumaini ahadi yake ya kutuponya na kutusamehe. Baada ya kufanya hivyo, itakuwa vema tukijifunza kutokana na makosa yetu, kuendelea kumtumikia Yehova, na kuwa na uhakika kwamba tutapata wakati ujao mzuri.—Ebr. 12:12, 13.

HALI NYINGINE

Matatizo ya kiafya (Tazama fungu la 15)

15. Tunajifunza nini kutokana na mfano wa Hana?

15 Inaelekea unaweza kufikiria watumishi wengine waaminifu wa zamani ambao walimtegemea Yehova huku wakichukua hatua inayofaa. Kwa mfano, Hana hangeweza kutatua tatizo la utasa kwa nguvu zake mwenyewe. Lakini aliamini kwamba Yehova angemfariji, kwa hiyo aliendelea kumwabudu kwenye maskani na kummiminia moyo wake katika sala. (1 Sam. 1:9-11) Je, hatupaswi kuiga mfano huo? Tunaposhughulika na matatizo ya kiafya au mambo mengine tusiyoweza kudhibiti, tunamtupia Yehova mahangaiko yetu tukiamini kwamba anatujali. (1 Pet. 5:6, 7) Na tunafanya yote tuwezayo ili kunufaika na mikutano ya Kikristo na maandalizi mengine ya kiroho.Ebr. 10:24, 25.

Watoto wanapoasi (Tazama fungu la 16)

16. Wazazi wanaweza kujifunza nini kutoka kwa mwanamume mzee Samweli?

16 Namna gani wazazi waaminifu ambao watoto wao wameasi? Mwanamume mzee Samweli, hangeweza kuwalazimisha watoto wake ambao tayari walikuwa watu wazima kuendelea kuwa washikamanifu kwa viwango vya uadilifu alivyowafundisha. (1 Sam. 8:1-3) Hangeweza kufanya mengi, ila tu kumwachia Yehova mahangaiko yake. Lakini Samweli angeweza kudumisha utimilifu na kumfurahisha Baba yake wa mbinguni, Yehova. (Met. 27:11) Leo, wazazi fulani Wakristo wanakabili hali hiyohiyo. Wanaamini kwamba Yehova anatazamia kwa hamu kuwakaribisha watenda dhambi wanaotubu kama baba anayetajwa katika mfano wa mwana mpotevu. (Luka 15:20) Wakati huohuo, wazazi hao wanajitahidi kubaki washikamanifu kwa Yehova wakitumaini kwamba mfano wao utawachochea watoto kurudi kwenye kundi.

Hali ngumu za kiuchumi (Tazama fungu la 17)

17. Kwa nini mfano wa mjane maskini unatutia moyo?

17 Fikiria pia yule mjane maskini katika siku za Yesu. (Soma Luka 21:1-4.) Hangeweza kufanya chochote kuhusu mazoea ya ufisadi yaliyoendelezwa hekaluni. (Mt. 21:12, 13) Na yaelekea hangeweza kufanya chochote ili kuboresha hali yake ya kiuchumi. Hata hivyo, alitoa kwa hiari “sarafu ndogo mbili,” ambazo zilikuwa “riziki yote aliyokuwa nayo.” Mwanamke huyo mwaminifu alionyesha anamtumaini Yehova kwa moyo wote, akijua kwamba kwa kutanguliza mambo ya kiroho Mungu angemwandalia mahitaji ya kimwili. Kumtumaini Yehova kulimfanya mjane huyo aunge mkono mpango uliokuwepo kwa ajili ya ibada ya kweli. Vivyo hivyo, tunaamini kwamba tukitanguliza Ufalme, Yehova atahakikisha tunapata mahitaji yetu.Mt. 6:33.

18. Toa mfano wa mtumishi wa kisasa wa Yehova ambaye alikuwa na mtazamo unaofaa.

18 Hata katika siku zetu, wengi wa waabudu wenzetu wameonyesha kwamba wanamtumaini Yehova na wamechukua hatua inayofaa. Mfikirie ndugu anayeitwa Malcolm, ambaye alikuwa mwaminifu mpaka kifo chake mnamo 2015. Katika miaka mingi ambayo yeye na mke wake walimtumikia Yehova, walikabili changamoto nyingi. Alisema hivi: “Huwezi kutabiri mambo ya kesho, maisha yana changamoto nyingi. Lakini Yehova huwabariki wale wanaomtegemea.” Malcolm alitoa pendekezo gani? “Sali ili ushiriki kikamili katika utumishi wa Yehova kadiri unavyoweza. Kazia fikira mambo unayoweza kufanya bali si yale usiyoweza kufanya.” *

19. (a) Kwa nini andiko la mwaka 2017 linafaa? (b) Utatumia jinsi gani andiko la mwaka 2017 maishani mwako?

19 Kadiri mfumo huu unavyoendelea “kutoka ubaya mpaka ubaya zaidi,” tunaweza kutarajia kukabili hali ngumu hata zaidi. (2 Tim. 3:1, 13) Kwa hiyo, leo kuliko wakati mwingine wowote, ni muhimu tusijiruhusu kamwe kulemewa na changamoto kama hizo. Badala yake, tunahitaji kumtegemea Yehova kikamili huku tukichukua hatua inayofaa. Kwa hiyo, andiko la mwaka 2017 linafaa sana: “Mtegemee Yehova na ufanye mema”!Zab. 37:3.

Andiko la mwaka 2017: “Mtegemee Yehova na ufanye mema.”Zaburi 37:3