Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Mtume Paulo aliandika kwamba Yehova “hatawaacha ninyi mjaribiwe kupita mnavyoweza kuhimili.” (1 Kor. 10:13) Je, hilo linamaanisha kwamba Yehova huchanganua mapema kile tunachoweza kuhimili na kisha kuchagua majaribu tutakayokabili?

Fikiria matokeo ya maoni kama hayo. Ndugu mmoja ambaye mwanawe alijiua, aliuliza hivi: ‘Je, Yehova alichanganua mapema ikiwa mimi na mke wangu tungeweza kuvumilia mwana wetu atakapojiua? Je, hilo lilitukia kwa sababu Mungu alikuwa na uhakika kwamba tungevumilia?’ Je, kuna sababu nzuri ya kuamini kwamba Yehova anaelekeza matukio ya maisha yetu kwa njia hususa kama hizo?

Kuchunguza kwa kina maneno ya Paulo katika 1 Wakorintho 10:13 kunatufanya tukate kauli hivi: Hakuna sababu ya Kimaandiko ya kuamini kwamba Yehova huchanganua mapema kile tunachoweza kuhimili na kisha, kwa msingi wa uchanganuzi huo, kuamua majaribu yatakayotupata. Acheni tuchunguze sababu nne zinazotufanya tufikie mkataa huo.

Kwanza, Yehova aliwapa wanadamu zawadi ya uhuru wa kuchagua. Anataka tuamue jinsi tutakavyoishi. (Kum. 30:19, 20; Yos. 24:15) Ikiwa tutachagua njia inayofaa, tunaweza kumtegemea Yehova aongoze hatua zetu. (Met. 16:9) Lakini ikiwa tutachagua njia isiyofaa, lazima tutapatwa na matokeo mabaya. (Gal. 6:7) Ikiwa Yehova angechagua majaribu ambayo yangetupata, je, hilo halimaanishi kwamba angekuwa akiweka mipaka ya jinsi ya kutumia zawadi ya uhuru wa kuchagua?

Pili, Yehova hatulindi kutokana na “wakati na tukio lisilotazamiwa.” (Mhu. 9:11) Aksidenti mbaya inaweza kutokea kwa sababu tupo mahali pasipofaa kwa wakati usiofaa, na nyakati nyingine huenda hata kifo kikatokea. Yesu alizungumzia msiba uliohusisha watu 18 ambao walikufa mnara ulipowaangukia, na akasema kwamba kifo cha watu hao hakikusababishwa na Mungu. (Luka 13:1-5) Kwa hiyo, si jambo la busara kufikiri kwamba Mungu huamua mapema ni nani ataishi au ni nani atakufa kwa sababu ya matukio yasiyotazamiwa.

Tatu, kila mmoja wetu anahusika kibinafsi katika suala la utimilifu. Kumbuka kwamba Shetani alitilia shaka utimilifu wa wale wote wanaomtumikia Yehova, akidai kuwa hatutaendelea kuwa washikamanifu kwa Yehova tunapopatwa na majaribu. (Ayu. 1:9-11; 2:4; Ufu. 12:10) Ikiwa Yehova angezuia tusipatwe na majaribu fulani eti kwa sababu ameona kuwa hatuwezi kuyahimili, je, hilo halingeunga mkono madai ya Shetani kwamba tunamtumikia Mungu kwa sababu za kibinafsi?

Nne, Yehova hahitaji kujua mapema kila kitu kitakachotupata. Wazo la kwamba Mungu huchagua mapema majaribu tutakayokabili linaonyesha kwamba lazima awe anajua kila kitu kuhusu wakati wetu ujao. Hata hivyo, maoni hayo si ya Kimaandiko. Ni kweli kwamba Mungu anaweza kujua wakati ujao. (Isa. 46:10) Lakini Biblia inaonyesha kwamba Mungu huchagua mambo atakayojua kuhusu wakati ujao. (Mwa. 18:20, 21; 22:12) Kwa hiyo, Yehova hutumia uwezo wake wa kujua wakati ujao bila kuingilia uhuru wetu wa kuchagua. Je, hatutarajii Mungu anayeheshimu uhuru wetu na ambaye sikuzote huonyesha sifa zake kwa usawaziko afanye hivyo?​—Kum. 32:4; 2 Kor. 3:17.

Hivyo basi, tunapaswa kuelewaje maneno haya ya Paulo: “Mungu . . . hatawaacha ninyi mjaribiwe kupita mnavyoweza kuhimili”? Katika mstari huo, Paulo anaeleza kile ambacho Yehova hufanya wakati wa majaribu, si kabla ya majaribu. * Maneno ya mtume huyo yanatuhakikishia kwamba hata tupatwe na majaribu ya aina gani maishani, Yehova atatutegemeza ikiwa tutamtumaini. (Zab. 55:22) Maneno ya Paulo yenye kufariji yanategemea kweli mbili muhimu.

Kwanza, majaribu tunayokabili ni ya “kawaida kwa watu.” Kwa hiyo, majaribu yetu ni ya kawaida kwa wanadamu. Tunaweza kuhimili majaribu hayo maadamu tutamtegemea Mungu. (1 Pet. 5:8, 9) Katika muktadha wa 1 Wakorintho 10:13, Paulo anarejelea majaribu ambayo Waisraeli walikabili walipokuwa nyikani. (1 Kor. 10:6-11) Majaribu hayo yote hayakupita uwezo wa wanadamu, na Waisraeli waaminifu wangeweza kuyahimili. Mara nne Paulo alisema kwamba “baadhi yao” walikosa kutii. Kwa kuhuzunisha, baadhi ya Waisraeli walishindwa na tamaa zisizofaa kwa kuwa walikataa kumtegemea Mungu.

Pili, “Mungu ni mwaminifu.” Historia ya jinsi Mungu alivyoshughulika na watu wake imethibitisha kwamba yeye huwaonyesha upendo mshikamanifu “wale wanaompenda na wale wanaoshika amri zake.” (Kum. 7:9) Historia hiyo inaonyesha pia kwamba sikuzote Mungu hutimiza ahadi zake. (Yos. 23:14) Kwa msingi wa historia yake ya uaminifu, wale wanaompenda na kumtii wanaweza kuamini kwamba atatimiza ahadi hizi mbili zinazohusu majaribu ambayo huenda yakawapata: (1) Hataruhusu jaribu lolote lifikie hatua ambayo haitawezekana kwao kuhimili, na kwamba (2) “ataifanya . . . njia ya kutokea” kwa ajili yao.

Yehova “hutufariji katika dhiki yetu yote”

Yehova hutokezaje njia kwa ajili ya wale wanaomtegemea wanapokabili majaribu? Kwa kweli, ikiwa ni mapenzi yake, anaweza kuondoa jaribu kwa urahisi. Lakini kumbuka maneno haya ya Paulo: “[Yehova] ataifanya pia njia ya kutokea kusudi mweze kulivumilia.” Hivyo, katika visa vingi, yeye hutokeza “njia ya kutokea” kwa kuandaa kile tunachohitaji ili tuvumilie majaribu kwa mafanikio. Fikiria baadhi ya njia ambazo Yehova anaweza kutokeza njia:

  • Yeye “hutufariji katika dhiki yetu yote.” (2 Kor. 1:3, 4) Yehova anaweza kutuliza akili, moyo, na hisia zetu kupitia Neno lake, roho yake takatifu, na chakula cha kiroho kinachoandaliwa na mtumwa mwaminifu.—Mt. 24:45; Yoh. 14:16; Rom. 15:4.

  • Anaweza kutuongoza kupitia roho takatifu. (Yoh. 14:26) Tunapopatwa na majaribu, roho takatifu inaweza kutusaidia kukumbuka masimulizi na kanuni za Biblia zinazoweza kutusaidia kufahamu uamuzi wa hekima tunaopaswa kufanya.

  • Anaweza kuwatumia malaika zake kutusaidia.—Ebr. 1:14.

  • Anaweza kutusaidia kupitia waabudu wenzetu ambao kwa maneno na matendo yao wanaweza kuwa “msaada wenye [kutia] nguvu.”—Kol. 4:11.

Hivyo basi, tunaweza kukata kauli gani kuhusu maana ya maneno ya Paulo yaliyonukuliwa katika 1 Wakorintho 10:13? Yehova hachagui wala kuamua majaribu tutakayokabili. Lakini tunapokabili majaribu maishani, tunaweza kuwa na uhakika huu: Tukimtegemea Yehova kikamili, hataruhusu majaribu tunayokabili yazidi uwezo wetu wa kibinadamu; sikuzote atatokeza njia ili tuweze kuyavumilia. Hilo ni wazo lenye kufariji kwelikweli!

^ fu. 2 Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “majaribu,” pia linaweza kumaanisha “mtihani.”