Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mapainia hawa wawili, George Rollston na Arthur Willis wakiwa wamesimamisha gari lao ili kujaza maji kwenye rejeta (radiator).—Eneo la Kaskazini, 1933

HIFADHI YETU YA VITU VYA KALE

“Hakuna Barabara Isiyopitika au Ndefu Kupita Kiasi”

“Hakuna Barabara Isiyopitika au Ndefu Kupita Kiasi”

MACHI 26, 1937, wanaume wawili waliokuwa wamechoka kwa sababu ya safari waliendesha polepole gari lao lililojaa vumbi kuingia Sydney, Australia. Tangu walipoondoka kwenye jiji hilo mwaka mmoja uliotangulia, walikuwa wamesafiri zaidi ya kilomita 19,300 wakipitia maeneo ya vijijini yenye milima katika bara hilo. Wanaume hao hawakuwa wavumbuzi. Arthur Willis na Bill Newlands walikuwa mapainia wawili kati ya wengi wenye bidii waliokuwa wameazimia kuhubiri habari njema za Ufalme wa Mungu katika eneo kubwa la mashambani barani Australia.

Wanafunzi wa Biblia * walikuwa wachache nchini Australia kufikia mwishoni mwa miaka ya 1920, na walikuwa wamehubiri hasa katika miji na majiji yaliyo pwani. Eneo la bara lenye ukame lilikuwa na watu wachache, na ukubwa wake ni zaidi ya nusu ya nchi ya Marekani. Hata hivyo, ndugu hao walifahamu vema kwamba wafuasi wa Yesu walipaswa kutoa ushahidi kumhusu katika “sehemu ya mbali zaidi ya dunia,” kutia ndani maeneo ya mashambani ya Australia. (Mdo. 1:8) Lakini wangewezaje kutimiza kazi kubwa hivyo? Wakiwa na imani thabiti kwamba Yehova angebariki jitihada zao, waliazimia kufanya yote waliyoweza.

MAPAINIA WATAYARISHA NJIA

Katika 1929, makutaniko ya Queensland na ya Magharibi mwa Australia yaliboresha magari kadhaa ili yaweze kuhimili hali mbalimbali wanaposafiri katika maeneo ya bara. Magari hayo yaliendeshwa na mapainia wenye nguvu ambao wangeweza kukabili hali ngumu na kuyarekebisha yalipoharibika. Walihubiri katika maeneo mengi ambayo hayakuwahi kamwe kuhubiriwa.

Mapainia ambao hawakuwa na pesa za kutosha kununua gari, walitumia baiskeli kusafiri mashambani. Kwa mfano, katika 1932, Bennett Brickell mwenye umri wa miaka 23 aliondoka Rockhampton, Queensland, akihubiri kwa miezi mitano katika vijiji vilivyo kaskazini mwa jimbo hilo. Kwenye baiskeli yake iliyobeba vitu vingi, kulikuwa na blanketi, mavazi, chakula, na vitabu vingi. Matairi ya baiskeli yake yalipoisha, aliendelea kusafiri akiwa na uhakika kwamba Yehova angemwongoza. Kwa kilomita 320 zilizosalia, alisukuma baiskeli yake akipitia maeneo ambayo watu waliangamia kutokana na kiu. Kwa miaka 30 iliyofuata, Ndugu Brickell alisafiri mamia ya maelfu ya kilomita kotekote Australia akitumia baiskeli, pikipiki, na gari. Alikuwa wa kwanza kuwahubiria wenyeji wa asili wa Australia, alisaidia kuanzisha makutaniko mapya, naye alijulikana sana na kuheshimiwa katika maeneo yote ya mashambani.

KUSHINDA CHANGAMOTO

Australia ni kati ya nchi zenye idadi ndogo zaidi ya watu ulimwenguni, na hasa maeneo ya mashambani. Kwa hiyo, watu wa Yehova walijitahidi kutafuta watu kwenye maeneo ya mbali ya bara hilo.

Mapainia Stuart Keltie na William Torrington walionyesha jitihada kama hiyo. Mnamo 1933, walivuka jangwa la Simpson, lililofanyizwa na marundo ya mchanga, ili kuhubiri kwenye mji wa Alice Springs ulio katikati ya bara hilo. Gari lao dogo lilipoharibika na wakalazimika kuliacha, Ndugu Keltie, ambaye alikuwa na mguu bandia, aliendelea na safari yake ya kuhubiri akitumia ngamia! Jitihada za mapainia hao zilizaa matunda walipokutana na msimamizi wa hoteli iliyokuwa kwenye kituo cha gari moshi kilicho mashambani huko William Creek. Baadaye, msimamizi huyo wa hoteli anayeitwa Charles Bernhardt, alikubali kweli, akauza hoteli yake, na akawa painia kwa miaka 15 akiwa peke yake katika baadhi ya maeneo makavu na ya mbali zaidi ya Australia.

Arthur Willis akijitayarisha kwenda kuhubiri kwenye eneo la mashambani la Australia.​—Perth, Magharibi mwa Australia, 1936

Kwa hakika, mapainia hao wa mapema walihitaji ujasiri na ustahimilivu ili kushinda changamoto nyingi walizokabili. Pindi moja, walipokuwa wakihubiri katika maeneo ya mashambani ya Australia, Arthur Willis na Bill Newlands, waliotajwa mwanzoni, walisafiri kilomita 32 kwa majuma mawili na walipata matatizo makubwa kwa sababu ya mvua kubwa iliyokuwa imefanya jangwa hilo kuwa bahari ya matope. Nyakati nyingine, walisukuma gari lao kupita kwenye mchanga, mabonde yenye mawe na mito iliyokauka na yenye mchanga mwingi huku wakitokwa na jasho na kukabiliana na joto jingi. Kwa kuwa gari lao liliharibika mara nyingi, walitembea au kuendesha baiskeli kwa siku nyingi ili wafike kwenye mji ulio karibu na kisha kusubiri kwa majuma mengi ili wapate vifaa vipya vya kurekebisha gari lao. Licha ya hali hizo ngumu, walidumisha mtazamo unaofaa. Baadaye akirejelea maneno fulani yaliyonukuliwa kwenye gazeti la The Golden Age, Arthur Willis alisema hivi: “Hakuna barabara isiyopitika au ndefu kupita kiasi kwa mashahidi Wake.”

Painia wa muda mrefu, Charles Harris, alisema kwamba kuwa peke yake na kukabili hali ngumu akiwa mashambani kulimfanya amkaribie Yehova zaidi. Aliongeza hivi: “Kuwa na vitu vichache iwezekanavyo ndiyo maisha bora zaidi. Ikiwa Yesu alikuwa tayari kulala nje usiku ilipohitajika, sisi pia tunapaswa kufurahia kufanya hivyo ikiwa mgawo wetu utatulazimu.” Na hivyo ndivyo mapainia wengi walivyofanya. Kwa sababu waliendelea kujitahidi, habari njema ilipenya sehemu zote za bara hilo na kuwasaidia watu wengi kuchukua msimamo upande wa Ufalme wa Mungu.

^ fu. 4 Wanafunzi wa Biblia walianza kutumia jina Mashahidi wa Yehova mwaka 1931.​—Isa. 43:10.