Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ni Nini Kitakachoondolewa Ufalme wa Mungu Utakapokuja?

Ni Nini Kitakachoondolewa Ufalme wa Mungu Utakapokuja?

“Ulimwengu unapitilia mbali na pia tamaa yake, lakini yeye anayefanya mapenzi ya Mungu anadumu milele.”—1 YOH. 2:17.

NYIMBO: 134, 24

1, 2. (a) Mfumo huu wa mambo unalinganishwa na mhalifu aliyehukumiwa kifo kwa njia gani? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.) (b) Viumbe wenye akili watahisije ulimwengu huu mwovu utakapoharibiwa?

“MAITI INATEMBEA!” Maneno hayo yalisemwa mhalifu hatari alipokuwa akiongozwa kutoka jela. Kwa nini walinzi walisema maneno hayo? Mhalifu huyo alionekana kuwa mwenye afya; hakuonekana kama ana tatizo linaloweza kumwua. Hata hivyo, walinzi walimwongoza mpaka mahali ambapo angeuawa. Ni kana kwamba mhalifu huyo alikuwa amekufa tayari. *

2 Kwa njia fulani, mfumo wa mambo wa sasa ni kama mhalifu huyo aliyehukumiwa kifo. Ulimwengu huu mwovu umehukumiwa tayari, na kutekelezwa kwa hukumu hiyo kumekaribia sana. Biblia inasema hivi: “Ulimwengu unapitilia mbali.” (1 Yoh. 2:17) Kwa hakika, mfumo huu utaisha. Lakini kuna tofauti kubwa kati ya mwisho wa ulimwengu huu na kifo cha mhalifu aliyetajwa mwanzoni. Kuhusu mhalifu huyo, huenda baadhi ya watu wakapinga hukumu hiyo wakitilia shaka ikiwa ilikuwa ya haki au kutumaini kwamba itaahirishwa dakika za mwisho. Hata hivyo, kuhusu ulimwengu huu, hukumu yake imetolewa na Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu ambaye ni mwenye haki kabisa. (Kum. 32:4) Haitaahirishwa, na hakutakuwa na shaka yoyote kuhusu haki ya hukumu hiyo. Itakapotekelezwa, viumbe wote wenye akili ulimwenguni watakubali kwamba imetekelezwa kwa haki. Kitakuwa kitulizo kikubwa sana!

3. Tutachunguza mambo gani manne yatakayoondolewa Ufalme wa Mungu utakapokuja?

3 Hata hivyo, “ulimwengu [unaopitilia] mbali” unahusisha nini? Sehemu nyingi za mambo ambayo watu ulimwenguni huona kuwa zitadumu milele, zitaondolewa. Je, hiyo ni habari yenye kuhuzunisha? La hasha! Kwa kweli, hiyo ni sehemu muhimu ya “habari njema ya ufalme.” (Mt. 24:14) Kwa hiyo, acheni tuchunguze kile kitakachoondolewa Ufalme wa Mungu utakapokuja. Tutachunguza mambo manne makuu: watu waovu, mashirika yenye ufisadi, matendo maovu, na hali zenye kuhuzunisha. Katika visa vyote, tutachunguza (1) jinsi mambo hayo yanavyotuathiri sasa, (2) mambo ambayo Yehova atafanya kuyahusu, na (3) hali itakavyokuwa atakapoondoa mambo mabaya na kuleta mambo yaliyo mazuri kikweli.

WATU WAOVU

4. Watu waovu wanatuathirije?

4 Watu waovu wanatuathirije? Baada ya kutabiri kwamba kipindi cha sasa kingehusisha “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo,” mtume Paulo aliongozwa na roho kuandika hivi: “Watu waovu na wajanja wataendelea kutoka ubaya mpaka ubaya zaidi.” (2 Tim. 3:1-5, 13) Je, umeona maneno hayo ya kinabii yakitimia? Wengi wetu tumetendewa vibaya na watu waovu, kama vile wakandamizaji wenye jeuri, watu shupavu wenye chuki, na wahalifu sugu. Baadhi yao huonyesha waziwazi uovu wao; wengine ni walaghai, wakificha matendo yao kwa kujifanya waadilifu. Hata ikiwa sisi wenyewe hatujatendewa vibaya, watu hao waovu bado hutuathiri. Tunaumia moyoni tunaposikia kuhusu matendo yao yenye kutisha. Tunashtuka tunapoona wanavyowatendea vibaya watoto, wazee, na watu wengine dhaifu. Watu waovu huonyesha roho isiyo ya kibinadamu, ya kinyama, au hata ya roho waovu. (Yak. 3:15) Jambo la kufurahisha ni kwamba Neno la Yehova lina habari njema.

5. (a) Waovu wana fursa gani kwa sasa? (b) Watu waovu wanaokataa kubadili maisha yao watapatwa na nini?

5 Yehova atafanya nini? Kwa sasa, Yehova anawapa watu waovu fursa ya kubadili maisha yao. (Isa. 55:7) Wakiwa mtu mmojammoja, bado hawajapokea hukumu yao ya mwisho. Mfumo huu ndio umehukumiwa. Lakini ni nini kitakachowapata wale wanaokataa kubadilika au wanaoendelea kuunga mkono mfumo huu hadi dhiki kuu itakapoanza? Yehova ameahidi kuwaondoa watu waovu milele. (Soma Zaburi 37:10.) Huenda waovu wakafikiri kwamba hawatapatwa na hukumu hiyo. Wengi wao huficha matendo yao, na katika mfumo huu, ni kana kwamba wao huepuka hukumu na matokeo ya matendo yao. (Ayu. 21:7, 9) Hata hivyo, Biblia inatukumbusha hivi: “Macho [ya Mungu] yako juu ya njia za mwanadamu, naye huziona hatua zake zote. Hakuna giza wala kivuli kizito kwa ajili ya wale wanaozoea kufanya madhara kujificha humo.” (Ayu. 34:21, 22) Huwezi kujificha kutoka kwa Yehova Mungu. Hakuna mlaghai anayeweza kumdanganya; hakuna kivuli au giza zito sana hivi kwamba lizuie macho ya Mungu yenye uwezo usio na kifani kupenya na kuona moyo. Kisha, baada ya Har–Magedoni, tutaangalia mahali ambapo waovu walikuwa, lakini hatutawaona. Hawatakuwapo milele!Zab. 37:12-15.

6. Waovu watakapoondolewa, ni nani watakaobaki, na kwa nini hiyo ni habari njema?

6 Ni nani watakaobaki waovu watakapoondolewa? Yehova anatoa ahadi hii yenye kugusa moyo: “Wapole wataimiliki dunia, nao watapata furaha yao tele katika wingi wa amani.” Baadaye katika kitabu hichohicho cha zaburi, tunasoma hivi: “Waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake.” (Zab. 37:11, 29) “Wapole” na “waadilifu” ni nani? Wapole ni wale wanaokubali kwa unyenyekevu mafundisho na mwongozo wa Yehova; nao waadilifu ni wale wanaopenda kufanya yaliyo sawa machoni pa Yehova Mungu. Katika ulimwengu wa leo, waadilifu ni wachache sana kwa kulinganisha na waovu. Lakini katika ulimwengu mpya unaokuja, wapole na waadilifu hawatakuwa kikundi cha watu wachache zaidi duniani au cha watu wengi zaidi; watakuwa ndio watu pekee duniani. Kwa kweli, watu wa aina hiyo wataifanya dunia kuwa paradiso!

MASHIRIKA YENYE UFISADI

7. Mashirika yenye ufisadi yanatuathirije?

7 Mashirika yenye ufisadi yanatuathirije? Mambo mengi maovu yanayofanywa ulimwenguni leo hayasababishwi na mtu mmojammoja, bali na mashirika. Kwa mfano, fikiria mashirika ya kidini ambayo huwadanganya mamilioni ya watu kuhusu Mungu, kutegemeka kwa Biblia, wakati ujao wa dunia na wanadamu, na kuhusu mambo mengine mengi. Namna gani kuhusu serikali zinazochochea vita na machafuko ya kikabila, zinazowakandamiza maskini na walio dhaifu, na kutajirika kwa sababu ya ufisadi na upendeleo? Vipi kuhusu mashirika yenye pupa yanayochafua mazingira, kutumia vibaya rasilimali, na kuwapotosha wanunuzi ili kuwatajirisha watu wachache tu huku mamilioni ya watu wakihangaika kwa sababu ya umaskini? Bila shaka, mashirika yenye ufisadi yanalaumika kwa sababu ya matatizo mengi katika ulimwengu wa leo.

8. Kulingana na Biblia, mashirika yanayoonwa na wengi kuwa imara leo yatapatwa na nini?

8 Yehova atafanya nini? Dhiki kuu itaanza sehemu za kisiasa zitakaposhambulia mashirika yote ya dini ya uwongo ambayo yanawakilishwa na kahaba anayeitwa Babiloni Mkubwa. (Ufu. 17:1, 2, 16; 18:1-4) Mashirika hayo ya kidini yataharibiwa kabisa. Namna gani kuhusu mashirika mengine yenye ufisadi? Biblia hutumia milima au visiwa kuwakilisha mashirika na taasisi nyingi zinazoonekana imara sana machoni pa wanadamu leo. (Soma Ufunuo 6:14.) Neno la Mungu linatabiri kwamba serikali zote na mashirika yake yatabomolewa kuanzia kwenye misingi. Dhiki kuu itafikia upeo wake serikali zote za ulimwengu huu na wote wanaoziunga mkono na kupinga Ufalme wa Mungu watakapoangamizwa. (Yer. 25:31-33) Baada ya hapo, hakutakuwa tena na mashirika yenye ufisadi!

9. Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba dunia mpya itakuwa na utaratibu?

9 Ni nini kitachukua mahali pa mashirika yenye ufisadi? Je, kutakuwa na shirika lolote duniani baada ya Har–Magedoni? Biblia inatuambia hivi: “Kulingana na ahadi yake tunangojea mbingu mpya na dunia mpya, na humo uadilifu utakaa.” (2 Pet. 3:13) Mbingu na dunia za zamani, serikali zenye ufisadi na jamii ya kibinadamu inayoongozwa na serikali hizo, hazitakuwapo tena. Ni nini kitachukua mahali pake? Maneno “mbingu mpya na dunia mpya” yanamaanisha kwamba kutakuwa na serikali mpya na jamii mpya ya kibinadamu ambayo itatawaliwa na serikali hiyo. Ufalme huo utakaotawaliwa na Yesu Kristo utaonyesha kikamili utu wa Yehova Mungu, ambaye si Mungu wa machafuko. (1 Kor. 14:33) Kwa hiyo, “dunia mpya” itakuwa yenye utaratibu. Kutakuwa na wanaume wanaofaa watakaosimamia mambo. (Zab. 45:16) Wataongozwa na Kristo na watawala wenzake 144,000. Wazia wakati ambapo shirika moja, lenye umoja, na lisilo na ufisadi litakapochukua mahali pa mashirika yote yenye ufisadi!

MATENDO MAOVU

10. Ni matendo gani maovu unayoona katika eneo unaloishi, nayo hukuathirije wewe na familia yako?

10 Matendo maovu yanatuathirije? Tunaishi katika ulimwengu uliojaa matendo maovu. Maadili mapotovu, ukosefu wa unyoofu, na matendo mabaya ya jeuri yamejaa katika mfumo huu wa mambo. Kwa kawaida, wazazi hasa hujitahidi kuwalinda watoto wao kutokana na matendo hayo mabaya. Ulimwengu wa burudani unaendelea kubobea katika kutukuza mambo maovu ya aina zote, huku ukipuuza viwango vya Yehova vya mema na mabaya. (Isa. 5:20) Wakristo wa kweli hujiepusha na mambo kama hayo. Wanapambana ili kulinda utimilifu wao katika ulimwengu unaochochea mtazamo wa kutoheshimu viwango vya Yehova.

11. Tunajifunza nini kutokana na hukumu ya Yehova juu ya Sodoma na Gomora?

11 Yehova atafanya nini kuhusu matendo maovu? Fikiria kile alichofanya kuhusu matendo maovu yaliyokuwa yakifanywa katika miji ya Sodoma na Gomora. (Soma 2 Petro 2:6-8.) Mwanamume mwadilifu Loti alitaabishwa na matendo maovu yaliyomzunguka yeye na familia yake. Yehova alipoharibu miji hiyo, hakuwa tu anakomesha matendo maovu katika eneo hilo. Alikuwa “akiweka kielelezo kwa watu wasiomwogopa Mungu juu ya mambo yatakayokuja.” Kama Yehova alivyokomesha maadili mapotovu wakati huo, atakomesha matendo maovu atakapoleta hukumu dhidi ya mfumo huu wa mambo.

12. Unatazamia kufanya mambo gani mfumo huu wa mambo utakapoondolewa?

12 Ni nini kitachukua mahali pa matendo maovu? Dunia paradiso itajaa mambo yanayoleta furaha. Fikiria kazi yenye kuchangamsha ya kugeuza dunia kuwa paradiso au kujenga nyumba zetu na za wapendwa wetu. Fikiria tumaini la kuwakaribisha mamilioni watakaofufuliwa na kuwaelimisha kuhusu njia za Yehova na vilevile jinsi alivyoshughulika na wanadamu. (Isa. 65:21, 22; Mdo. 24:15) Maisha yetu yatajawa na shughuli zitakazotuletea shangwe na kumletea Yehova sifa!

HALI ZENYE KUHUZUNISHA

13. Uasi wa Shetani, Adamu, na Hawa umesababisha hali gani zenye kuhuzunisha ulimwenguni leo?

13 Hali zenye kuhuzunisha zinatuathirije? Hali zenye kuhuzunisha duniani husababishwa na watu waovu, mashirika yenye ufisadi, na matendo maovu. Ni nani anayeweza kudai kwamba hajaathiriwa na vita, umaskini, au ubaguzi? Namna gani magonjwa na kifo? Sote tunaathiriwa na hali hizo. Hali hizo zimesababishwa na uasi dhidi ya Yehova uliofanywa na viumbe watatu waovu, yaani, Shetani, Adamu, na Hawa. Hakuna mmoja wetu anayeweza kuepuka madhara ya uasi wao.

14. Yehova atafanya nini kuhusu hali zenye kuhuzunisha? Toa mfano.

14 Yehova atafanya nini kuhusu hali zenye kuhuzunisha? Chunguza mambo kadhaa. Kwanza, Yehova ameahidi kukomesha vita milele. (Soma Zaburi 46:8, 9.) Namna gani magonjwa? Atayaondoa. (Isa. 33:24) Na kifo? Yehova atakimeza milele! (Isa. 25:8) Atakomesha umaskini. (Zab. 72:12-16) Atafanya vivyo hivyo kuelekea hali nyingine zenye kuhuzunisha zinazofanya maisha yawe magumu. Ataondoa “hewa” mbaya ya ulimwengu huu, kwa kuwa roho mbaya ya Shetani na roho wake waovu itakuwa imeondolewa mwishowe.Efe. 2:2.

Wazia ulimwengu bila vita, magonjwa, au kifo! (Tazama fungu la 15)

15. Ni mambo gani yataondolewa milele baada ya Har–Magedoni?

15 Je, unaweza kuwazia ulimwengu bila vita, magonjwa, au kifo? Fikiria wakati ambapo hakutakuwa na majeshi ya nchi kavu, ya wanamaji, au ya angani! Hakutakuwa na silaha au makaburi ya watu waliofia vitani. Hakuna hospitali, madaktari, wauguzi, au bima ya afya; hakuna makaburi, vyumba vya kuhifadhia maiti, au wanaotayarisha maiti kwa ajili ya maziko! Ukosefu wa usalama utakapoondolewa, hakutakuwa na makampuni ya usalama, ving’ora, polisi, na labda hakutakuwa na makomeo au funguo! Fikiria wakati ambapo mahangaiko hayatatusumbua tena akilini na moyoni.

16, 17. (a) Watakaookoka Har–Magedoni watapata kitulizo gani? Toa mfano. (b) Tutafanya nini ili tuwe na uhakika kwamba tutabaki ulimwengu huu utakapoondolewa?

16 Maisha yatakuwaje hali zenye kuhuzunisha zitakapoondolewa? Ni vigumu kuwazia. Tumeishi katika ulimwengu huu kwa muda mrefu sana hivi kwamba huenda hatutambui tena mikazo inayotokana na hali za ulimwengu. Ni kama watu wanaoishi karibu na kituo cha gari-moshi chenye shughuli nyingi ambao huenda wasigundue kelele za kituo hicho, au wale wanaoishi karibu na jalala huenda wasitambue harufu mbaya. Lakini mambo hayo yote yatakapoondolewa tutapata kitulizo kikubwa!

17 Ni nini kitachukua mahali pa mikazo tunayohisi leo? Zaburi 37:11 inajibu hivi: “Watapata furaha yao tele katika wingi wa amani.” Je, maneno hayo hayakugusi moyo? Yehova angependa ufurahie mambo hayo. Basi, jitahidi uwezavyo kukaa karibu na Yehova Mungu na tengenezo lake katika siku hizi za mwisho zenye mikazo! Thamini tumaini lako, tafakari kulihusu, fanya liwe halisi akili na moyoni, na uwaeleze wengine kulihusu! (1 Tim. 4:15, 16; 1 Pet. 3:15) Ukifanya hivyo, unaweza kuwa na uhakika kwamba hutapitilia mbali pamoja na ulimwengu huu uliohukumiwa. Badala yake, utaendelea kuishi ukiwa na shangwe, kwa umilele wote!

^ fu. 1 Fungu hili linaeleza desturi fulani zilizofuatwa zamani katika baadhi ya magereza nchini Marekani.