Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Kile Unachoweka Nadhiri, Timiza”

“Kile Unachoweka Nadhiri, Timiza”

“Lazima umtimizie Yehova nadhiri zako.”MT. 5:33.

NYIMBO: 63, 59

1. (a) Mwamuzi Yeftha na Hana walilingana kwa njia gani? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.) (b) Tutajibu maswali gani katika makala hii?

ALIKUWA kiongozi jasiri; alikuwa mke anayejitiisha. Alikuwa shujaa wa vita; alikuwa mke wa hali ya chini wa nyumbani. Mbali na kuabudu Mungu yuleyule, je, Mwamuzi Yeftha na Hana mke wa Elkana walilingana kwa vyovyote? Wote wawili walikuwa wameweka nadhiri kwa Mungu, na wote walitimiza nadhiri hizo kwa uaminifu. Wao ni mfano bora kwa wanaume na wanawake wanaoamua kuweka nadhiri kwa Yehova leo. Hata hivyo, maswali haya ya msingi yanazuka: Nadhiri ni nini? Kuweka nadhiri kwa Mungu ni jambo zito kadiri gani? Tunajifunza nini kutoka kwa Yeftha na Hana?

2, 3. (a) Nadhiri ni nini? (b) Maandiko yanasema nini kuhusu kuweka nadhiri kwa Mungu?

2 Kama inavyotumiwa katika Biblia, nadhiri ni ahadi nzito inayotolewa kwa Mungu. Mtu anaahidi kufanya jambo, kutoa zawadi, kuanza utumishi wa aina fulani, au kujiepusha na mambo fulani. Nadhiri hutolewa kwa hiari. Hata hivyo, nadhiri ni takatifu na mtu huwajibika mbele za Mungu kwa sababu inabeba uzito wa kiapo, au ahadi ya kiapo, inayoonyesha kwamba mtu atafanya au atajiepusha na jambo fulani. (Mwa. 14:22, 23; Ebr. 6:16, 17) Maandiko yanasema nini kuhusu uzito wa kuweka nadhiri kwa Mungu?

3 Sheria ya Musa ilisema hivi: “Ikiwa mwanamume ataweka nadhiri kwa Yehova au ikiwa ataapa kiapo . . . , hapaswi kulivunja neno lake. Anapaswa kufanya kulingana na yote ambayo yametoka kinywani mwake.” (Hes. 30:2) Baadaye, Sulemani aliongozwa na roho kuandika hivi: “Wakati wowote unapoweka nadhiri kwa Mungu, usisite kuitimiza, kwa maana hapendezwi na wajinga. Kile unachoweka nadhiri, timiza.” (Mhu. 5:4) Yesu alionyesha uzito wa kuweka nadhiri aliposema hivi: “Watu wa kale waliambiwa, ‘Usiape bila kutimiza, bali lazima umtimizie Yehova nadhiri zako.’”Mt. 5:33.

4. (a) Kuweka nadhiri kwa Mungu ni jambo zito kadiri gani? (b) Tungependa kujifunza nini kutoka kwa Yeftha na Hana?

4 Hivyo basi, ni wazi kwamba ni jambo zito sana kumtolea Mungu ahadi. Uhusiano wetu na Yehova huathiriwa na jinsi tunavyotenda baada ya kuweka nadhiri. Daudi aliandika hivi: “Ni nani anayeweza kuupanda mlima wa Yehova, na ni nani anayeweza kusimama katika mahali pake patakatifu? Yeyote . . . ambaye hajaitendea nafsi Yangu [Yehova] kwa ubatili mtupu, wala kuapa kwa udanganyifu.” (Zab. 24:3, 4) Yeftha na Hana waliweka nadhiri gani, na je, ilikuwa rahisi kwao kutimiza nadhiri hiyo?

WALITIMIZA KWA UAMINIFU NADHIRI ZAO KWA MUNGU

5. Yeftha aliweka nadhiri gani, na matokeo yalikuwa nini?

5 Yeftha alitimiza kwa uaminifu ahadi aliyomtolea Yehova alipoenda kupigana na Waamoni, ambao walikuwa wakiwakandamiza watu wa Mungu. (Amu. 10:7-9) Kwa kuwa alitamani sana kupata ushindi, Yeftha aliweka nadhiri hii: “Hakika ukiwatia wana wa Amoni mkononi mwangu, itatukia pia kwamba yule atakayetoka nje, atakayetoka nje ya milango ya nyumba yangu kuja kunipokea nitakaporudi kwa amani kutoka kwa wana wa Amoni, lazima atakuwa wa Yehova.” Matokeo yalikuwa nini? Waamoni walishindwa, na binti mpendwa wa Yeftha ndiye aliyekuja kumlaki aliporudi baada ya ushindi wake. Yeye ndiye ‘angekuwa wa Yehova.’ (Amu. 11:30-34) Hilo lingebadili maisha yake jinsi gani?

6. (a) Kwa nini haikuwa rahisi kwa Yeftha na binti yake kutimiza nadhiri yao kwa Mungu? (b) Andiko la Kumbukumbu la Torati 23:21, 23 na Zaburi 15:4 linakufundisha nini kuhusu kumwekea Mungu nadhiri?

6 Ili kutimiza nadhiri ya baba yake, binti ya Yeftha alipaswa kumtumikia Yehova wakati wote katika mahali pake patakatifu. Je, Yeftha alikuwa ameweka nadhiri bila kufikiri? Hapana, kwa kuwa huenda alijua kuwa binti yake ndiye angekuja kumlaki. Hata hivyo, ilikuwa hali ngumu kihisia kwa baba na binti. Wote wawili walihitaji kujidhabihu kwelikweli. Alipomwona, Yeftha “akaanza kuyararua mavazi yake” na kusema kwamba amehuzunika. Binti yake ‘aliulilia ubikira wake.’ Kwa nini? Yeftha hakuwa na mwana, na binti yake wa pekee hangeolewa na kumzalia wajukuu. Jina na urithi wa familia haungeendelezwa. Lakini Yeftha hakukazia fikira jambo hilo. Yeftha alisema hivi: “Mimi nimemfungulia Yehova kinywa changu, nami siwezi kurudi nyuma.” Naye binti yake akajibu hivi: “Nitendee kulingana na neno lililotoka katika kinywa chako.” (Amu. 11:35-39) Yeftha na binti yake walikuwa watu washikamanifu ambao hawangefikiria kamwe kuvunja nadhiri waliyoweka kwa Mungu Aliye Juu Zaidi, haidhuru wangegharimika kadiri gani.Soma Kumbukumbu la Torati 23:21, 23; Zaburi 15:4.

7. (a) Hana alitoa nadhiri gani, na kwa nini, na matokeo yalikuwa nini? (b) Nadhiri ya Hana ilibadili maisha ya Samweli jinsi gani? (Tazama maelezo ya chini.)

7 Mfano mwingine ni Hana, ambaye alitimiza kwa uaminifu nadhiri aliyomwekea Yehova. Alitoa ahadi yake akiwa amefadhaika na akiwa na mkazo mwingi kwa kuwa alikuwa tasa na alidhihakiwa sana. (1 Sam. 1:4-7, 10, 16) Hana alimmiminia Mungu moyo wake na kutoa nadhiri hii: “Ee Yehova wa majeshi, ikiwa hakika utayaona mateso ya kijakazi wako, nawe kwa kweli unikumbuke, na ikiwa hutamsahau kijakazi wako na kwa kweli umpe kijakazi wako uzao wa kiume, mimi nitamtoa kwa Yehova siku zote za maisha yake, wala wembe hautapita juu ya kichwa chake.” * (1 Sam. 1:11) Ombi la Hana lilijibiwa, naye akamzaa mwana, mzaliwa wa kwanza. Alifurahi sana! Lakini hakusahau nadhiri aliyokuwa ameweka kwa Mungu. Alipomzaa mwanawe, alitangaza hivi: “Nimemwomba kutoka kwa Yehova.”1 Sam. 1:20.

8. (a) Kwa nini haikuwa rahisi kwa Hana kutimiza nadhiri yake? (b) Maneno ya Daudi katika Zaburi 61 yanakukumbusha nini kuhusu mtazamo mzuri wa Hana?

8 Muda mfupi baada ya Samweli mchanga kuacha kunyonya, akiwa na umri wa miaka mitatu hivi, Hana alitenda kulingana na nadhiri yake kwa Mungu. Hakufikiria hata kidogo kubadili nadhiri yake. Alimpeleka Samweli kwa Kuhani Mkuu Eli kwenye maskani huko Shilo na kusema hivi: “Ilikuwa kuhusu mvulana huyu kwamba nilisali ili Yehova anipe ombi langu nililomwomba. Na mimi nimemwazima Yehova mvulana huyu. Siku zote atakazokuwapo, yeye ni mtu aliyeombwa kwa ajili ya Yehova.” (1 Sam. 1:24-28) Akiwa huko, “mvulana Samweli akaendelea kukua akiwa na Yehova.” (1 Sam. 2:21) Lakini hilo lingemwathiri Hana jinsi gani? Alimpenda sana mwanawe mchanga, lakini sasa hangeweza kumwona kila siku akikua. Fikiria jinsi alivyotamani kumpakata, kucheza naye, kumtunza, yaani, kufurahia pindi zote nzuri ambazo mama mwenye upendo huwa nazo anapomwona mwanawe akikua. Ingawa hivyo, Hana hakujutia nadhiri yake kwa Mungu. Moyo wake ulifurahi katika Yehova.1 Sam. 2:1, 2; soma Zaburi 61:1, 5, 8.

Je, unatimiza nadhiri zako kwa Yehova?

9. Tutajibu maswali gani?

9 Kwa kuwa sasa tumeelewa uzito wa kuweka nadhiri kwa Mungu, acheni tuchunguze maswali haya: Tukiwa Wakristo tunaweza kuweka nadhiri gani? Pia, tunapaswa kuwa tumeazimia kadiri gani kutimiza nadhiri zetu?

NADHIRI YAKO YA KUJIWEKA WAKFU

Nadhiri ya kujiweka wakfu (Tazama fungu la 10)

10. Ni nadhiri gani muhimu zaidi ambayo Mkristo anaweza kuweka, na inahusisha nini?

10 Nadhiri muhimu zaidi ambayo Mkristo huweka ni kujiweka wakfu kwa Yehova. Kwa nini? Kwa sababu alipotoa sala faraghani, alimwahidi Yehova kwamba atatumia maisha yake kumtumikia milele, hata hali iweje. Kulingana na maneno ya Yesu, mtu huyo ‘anajikana mwenyewe,’ anaacha kutanguliza mapenzi yake, na kuweka nadhiri ya kutanguliza mapenzi ya Mungu maishani. (Mt. 16:24) Kuanzia siku hiyo na kuendelea, ‘yeye ni wa Yehova.’ (Rom. 14:8) Yeyote yule anayeweka nadhiri ya kujiweka wakfu anapaswa kuichukua kwa uzito sana, kama ambavyo mtunga zaburi alisema kuhusu nadhiri alizoweka kwa Mungu: “Nitamlipa Yehova nini kwa ajili ya faida zake zote kwangu? Nadhiri zangu nitamtimizia Yehova, naam, mbele ya watu wake wote.”Zab. 116:12, 14.

11. Ni nini kilichotukia katika siku yako ya ubatizo?

11 Je, umejiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa? Ikiwa ndivyo, umefanya vema sana! Kumbuka kwamba ulipobatizwa uliulizwa mbele ya mashahidi ikiwa umejiweka wakfu kwa Yehova na kuelewa kuwa “wakfu na ubatizo wako unakutambulisha kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova anayeshirikiana na tengenezo linaloongozwa na roho ya Mungu.” Kujibu maswali hayo kwa kusema “ndiyo” kulikuwa tangazo la hadharani kwamba umejiweka wakfu bila masharti na kuonyesha kwamba umestahili kubatizwa na kuwa mhudumu wa Yehova Mungu aliyewekwa rasmi. Ulimfanya Yehova afurahi sana!

12. (a) Inafaa tujiulize maswali gani? (b) Petro alisema tunapaswa kuwa na sifa zipi?

12 Hata hivyo, ubatizo ni mwanzo tu. Baada ya hapo, tungependa kuendelea kuishi kulingana na wakfu wetu na kumtumikia Mungu kwa uaminifu. Hivyo, huenda tukajiuliza hivi: ‘Nimefanya maendeleo gani ya kiroho tangu nilipobatizwa? Je, ninaendelea kumtumikia Yehova kwa moyo wote? (Kol. 3:23) Je, ninasali, kusoma Neno la Mungu, kuhudhuria mikutano, na kuhubiri mara nyingi iwezekanavyo? Au je, nimepunguza utendaji huo kwa kiasi fulani?’ Mtume Petro alieleza kwamba tunaweza kuepuka kuwa wasiotenda katika utumishi wetu ikiwa tutaongeza kwenye imani yetu ujuzi, uvumilivu, na ujitoaji-kimungu.Soma 2 Petro 1:5-8.

13. Mkristo aliyejiweka wakfu na kubatizwa anapaswa kutambua nini?

13 Hatuwezi kutangua nadhiri yetu ya wakfu ambayo tulimtolea Mungu. Mtu akichoka kumtumikia Yehova au kuishi maisha ya Kikristo, hawezi kudai kwamba hakujiweka wakfu kikamili au ubatizo wake haukuwa halali. * Kihalisi, alionyesha waziwazi kwamba amejiweka wakfu kwa Mungu kikamili. Atawajibika mbele za Yehova na kutaniko akifanya dhambi yoyote nzito. (Rom. 14:12) Kamwe isisemwe kutuhusu kuwa ‘tumeacha upendo tuliokuwa nao mwanzoni.’ Badala yake, tungependa Yesu aseme hivi kutuhusu: “Mimi nayajua matendo yako, na upendo wako na imani na huduma na uvumilivu wako, na kwamba matendo yako ya hivi karibuni yanazidi yale ya zamani.” (Ufu. 2:4, 19) Na tuendelee kuonyesha bidii tunapoishi kulingana na nadhiri yetu ya wakfu, na hivyo kumfurahisha Yehova.

NADHIRI YAKO YA NDOA

Nadhiri ya ndoa (Tazama fungu la 14)

14. Ni nadhiri gani ya pili muhimu zaidi ambayo mtu anaweza kuweka, na kwa nini?

14 Nadhiri ya pili muhimu zaidi ambayo mtu anaweza kuweka ni nadhiri ya ndoa. Kwa nini? Kwa kuwa ndoa ni takatifu. Bwana na bibi arusi wanaweka nadhiri zao za ndoa mbele ya Mungu na mashahidi. Kwa kawaida wao huahidi kupendana, kutunzana, na kuheshimiana, na kwamba watafanya hivyo “kwa muda wote ambao [wao wawili wataishi] pamoja duniani kulingana na mpango wa ndoa wa Mungu.” Huenda wengine hawakusema maneno hayohayo, lakini bado waliweka nadhiri mbele za Mungu. Kisha wanatangazwa kuwa mume na mke, na ndoa yao inakusudiwa kudumu maisha yao yote. (Mwa. 2:24; 1 Kor. 7:39) “Kwa hiyo,” kama Yesu alivyosema, “kile ambacho Mungu ameunganisha mtu yeyote asikitenganishe,” iwe mume au mke au mtu mwingine yeyote. Hivyo, mwanamume na mwanamke wanaoamua kufunga ndoa, hawapaswi kuwa na mtazamo au kufikiria uwezekano wa kutalikiana.—Marko 10:9.

15. Kwa nini Wakristo hawapaswi kuiga mtazamo wa ulimwengu kuhusu ndoa?

15 Bila shaka, hakujawahi kuwa na ndoa kamilifu. Ndoa zote huhusisha watu wawili wasio wakamilifu. Hiyo ndiyo sababu Biblia husema kwamba wenzi wa ndoa “watakuwa na dhiki” nyakati fulani. (1 Kor. 7:28) Kwa kuhuzunisha, watu wengi ulimwenguni hawachukui ndoa kwa uzito. Wanapokuwa na matatizo katika ndoa, wanakata tamaa na kuachana. Hata hivyo, hiyo si njia ya Kikristo ya kushughulikia matatizo ya ndoa. Kuvunja nadhiri ya ndoa ni sawa na kumdanganya Mungu, na Mungu anachukia waongo! (Law. 19:12; Met. 6:16-19) Mtume Paulo aliandika hivi: “Je, umefungwa kwa mke? Uache kutafuta kufunguliwa.” (1 Kor. 7:27) Paulo alisema hivyo kwa kuwa alijua kwamba Yehova anachukia watu wanaotalikiana kwa hila.Mal. 2:13-16.

16. Biblia inasema nini kuhusu talaka na kutengana?

16 Yesu alifundisha kwamba msingi pekee wa Kimaandiko wa kuvunja nadhiri ya ndoa ni mwenzi wa ndoa asiye na hatia anapoamua kutomsamehe mwenzi wake mzinzi. (Mt. 19:9; Ebr. 13:4) Vipi kuhusu kutengana na mwenzi wa ndoa? Biblia inatoa shauri lililo wazi kuhusu hilo pia. (Soma 1 Wakorintho 7:10, 11.) Hakuna sababu zozote katika Biblia zinazoruhusu wenzi wa ndoa kutengana. Hata hivyo, baadhi ya wenzi wa ndoa Wakristo wameona kuwa hali fulani zinaweza kuwa sababu ya kutengana, kama vile kuhatarisha kabisa uhai wa mtu au hali yake ya kiroho kwa kumtendea vibaya kimwili, au mwenzi kuwa mwasi-imani. *

17. Wenzi wa ndoa Wakristo wanaweza kufanya nini ili kifungo chao cha ndoa kidumu?

17 Wenzi wa ndoa wanapowafikia wazee wa kutaniko ili kupata ushauri kuhusu matatizo ya ndoa, ingefaa wazee wawaulize wenzi hao ikiwa wametazama video ya Upendo wa Kweli Ni Nini? hivi karibuni, na kujifunza pamoja broshua Unaweza Kuwa na Familia Yenye Furaha. Kwa nini? Kwa sababu vifaa hivyo hukazia kanuni za Mungu ambazo zimewasaidia wengi kuimarisha ndoa zao. Wenzi fulani wa ndoa walisema hivi: “Tangu tuanze kujifunza broshua hii, ndoa yetu imezidi kuwa na furaha.” Mke fulani alisema hivi kuhusu ndoa yao ya miaka 22 iliyokuwa karibu kuvunjika: “Sote tumebatizwa, lakini tulikuwa tofauti sana kihisia. Video hiyo ilitolewa kwa wakati unaofaa kabisa! Kwa sasa ndoa yetu inaendelea kuimarika.” Je, umefunga ndoa? Fanya juu chini kutumia kanuni za Yehova katika ndoa yako. Kufanya hivyo kutakusaidia kuishi kwa furaha unapotimiza nadhiri yako ya ndoa!

NADHIRI YA WATUMISHI WA PEKEE WA WAKATI WOTE

18, 19. (a) Wazazi wengi Wakristo wamefanya nini? (b) Watumishi wa pekee wa wakati wote wameweka nadhiri gani, na hilo linamaanisha nini?

18 Je, umetambua Yeftha na Hana walilingana katika njia gani nyingine? Binti ya Yeftha na mwana wa Hana walitolewa kwa ajili ya utumishi wa pekee na mtakatifu kwenye maskani kwa sababu ya nadhiri ambazo wazazi wao walitoa. Hayo yalikuwa maisha yenye kuridhisha kwelikweli! Leo, wazazi wengi Wakristo wamewatia moyo watoto wao waanze utumishi wa wakati wote na kutanguliza utumishi wa Mungu maishani. Wale ambao wamefanya hivyo wanastahili pongezi.—Amu. 11:40; Zab. 110:3.

Nadhiri ya utumishi wa pekee wa wakati wote (Tazama fungu la 19)

19 Kwa sasa, kuna washiriki 67,000 hivi wa Kikundi cha Ulimwenguni Pote cha Watumishi wa Pekee wa Wakati Wote cha Mashahidi wa Yehova. Baadhi yao ni Wanabetheli, wajenzi, waangalizi wa mzunguko, walimu wa shule za kitheokrasi, mapainia wa pekee, wamishonari, au wanaotunza Majumba ya Kusanyiko au majengo ya shule za Biblia. Wote wako chini ya “Nadhiri ya Utii na Umaskini,” ambapo wanakubali mgawo wowote watakaopewa ili kuendeleza masilahi ya Ufalme, kuishi maisha rahisi, na kuepuka kufanya kazi ya kimwili bila ruhusa. Kazi hiyo ndiyo inayoonwa kuwa ya pekee bali si watu. Wanatambua uzito wa kuishi kulingana na nadhiri yao kwa muda wote ambao watakuwa katika utumishi wa pekee wa wakati wote.

20. Tunapaswa kufanya nini “siku baada ya siku,” na kwa nini?

20 Kati ya nadhiri tulizozungumzia, umeweka nadhiri ngapi kwa Mungu? Moja, mbili, au zote tatu? Bila shaka, unatambua kuwa unapaswa kuchukua nadhiri zako kwa uzito. (Met. 20:25) Tukikosa kutimiza ahadi yetu kwa Yehova au kutimiza nadhiri zetu huenda tukapatwa na matokeo mabaya sana. (Mhu. 5:6) Kwa hiyo, kwa furaha acheni ‘tulipigie jina la Yehova muziki milele, ili tupate kutimiza nadhiri zetu siku baada ya siku.’Zab. 61:8.

^ fu. 7 Kulingana na nadhiri ya Hana, mtoto wake angekuwa Mnadhiri maisha yake yote. Hilo lilimaanisha kwamba angekuwa wa pekee, aliyewekwa wakfu, na kutengwa kwa ajili ya utumishi mtakatifu wa Yehova.Hes. 6:2, 5, 8.

^ fu. 13 Tunapofikiria hatua ambazo wazee huchukua ili kuhakikisha kwamba mtu anastahili kubatizwa, ni vigumu sana kwa ubatizo wa mtu yeyote kutokuwa halali.

^ fu. 16 Tazama kitabu “Jitunzeni Katika Upendo wa Mungu,” uku. 219-221”.